Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Wednesday 31 July 2019

Kikombe Cha Asubuhi ; Methali 30...

Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu katika yote...

Asante  Mungu wetu kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwatayari kwa majukumu yetu


Utukuzwe ee Mungu wetu,usifiwe Baba wa Mbinguni

Neema yako yatutosha  Mungu wetu..!

Kwanza kabisa, nawasihi muombe dua, msali na kumshukuru Mungu kwa ajili ya watu wote, kwa ajili ya wafalme na wote wenye mamlaka, ili tupate kuishi maisha ya utulivu na amani pamoja na uchaji wa Mungu na mwenendo mwema.
Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea,Usitutie majaribuni Mungu wetu tunaomba utuepushe na yule mwovu na kazi zake zote,Jehovah ututakase miili yetu na akili zetu Baba wa Mbinguni tunaomba utufunike kwa  Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti,
Yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona....

Jambo hili ni jema na lampendeza Mungu Mwokozi wetu, ambaye anataka watu wote waokolewe na wapate kuujua ukweli. Maana yuko Mungu mmoja, na pia yuko mmoja anayewapatanisha watu na Mungu, binadamu Kristo Yesu,
Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa 
katika utendaji
Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki ridhiki zetu
ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba ukatupe neema ya kuweza
kuwabariki wenye kuhitaji
Yahweh tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Mungu wetu ukatupe kama inavyokupendeza wewe

Jehovah tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyo vimiliki
Yahweh tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia
Baba wa Mbinguni tukawe salama rohoni
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia 
sauti yako na kuitii
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe neema ya kufuata njia zako
Yahweh tukasimamie Neno lako amri na sheria zako siku zote 
za maisha yetu

Mungu  wetu ukaonekane katika maisha yetu popote tupitapo na ikajulikane kwamba upo 

Neema zako zikawe nasi Nuru yako ikaangaze katika maisha yetu
Ukatufanye barua njema ee Mungu wetu nasi tukasomeke kama
inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi...

ambaye alijitoa mwenyewe kuwakomboa watu wote. Huo ulikuwa uthibitisho, wakati ufaao ulipowadia, kwamba Mungu anataka kuwaokoa watu wote. Kwa sababu hiyo mimi nilitumwa niwe mtume na mwalimu wa watu wa mataifa, niutangaze ujumbe wa imani na ukweli. Nasema ukweli; sisemi uongo!
Tazama wenye shida/tabu,Mungu wetu tunaomba
 ukawaguse kila mmoja na mahitaji yake
Baba wa Mbinguni tunaomba ukawasamehe pale walipokwenda
kinyume nawe
Mungu wetu ukawape neema ya kujiombea,macho ya rohoni,masikio yakusikia sauti yako,wakafuate njia zako nazo zikawaweke huru
Mungu wetu tunaomba ukasikie kulia kwao
Baba wa Mbinguni tunomba ukawafute machozi yao
Nuru yako ikaangaze katika maisha yao
Mungu wetu tunaomba ukawatendee sawasawa na mapenzi yako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina....!!!


Wapendwa katika Kristo Yesu asanteni sana
kwakuwanami/kunisoma

Mungu Baba aendelee kuwabariki na kuwatendea
kama inavyompendeza yeye
Amani ya Bwana wetu Yesu Kristo na upendo wa Mungu Baba
ukae nanyi daima....

Nawapenda.

Mawaidha ya Aguri
1Maneno ya Aguri, mwana wa Yake. Mawaidha ambayo mtu huyu alimwambia Ithieli, naam, Ithieli na Ukali.30:1 Ithieli, Ukali: Majina hayo yaweza kumaanisha Nimechoka ee Mungu; nimechoka na sina nguvu.
2Mimi ni mpumbavu mno, wala si mtu;
nayo akili ya binadamu sina.
3Sijajifunza hekima,
wala sijui kitu juu ya Mungu Mtakatifu.
4Ni nani aliyepanda juu mbinguni akashuka chini?
Ni nani aliyekamata upepo mkononi?
Ni nani aliyefunga maji katika kitambaa?
Ni nani aliyeiweka mipaka yote ya dunia?
Jina lake ni nani? Na ni nani jina la mwanawe?
Niambie kama wajua!
5Maneno yote ya Mungu ni ya kuaminika;
yeye ni ngao yao wote wanaomkimbilia.
6Usiongeze neno katika maneno yake,
asije akakukemea, nawe ukaonekana mwongo.
7Mambo haya mawili nakuomba ee Mungu,
wala usinikatalie kabla sijafa:
8Uniondolee uongo na udanganyifu;
usinipe umaskini wala utajiri;
unipatie chakula ninachohitaji,
9nisije nikashiba nikakukana;
nikasema, “Mwenyezi-Mungu ni nani?”
Au nisije nikawa maskini nikaiba,
na kulikufuru jina lako ee Mungu wangu.
10Usimchongee mtumwa kwa bwana wake,
asije akakulaani, ukaonekana una hatia.
11Kuna watu ambao huwalaani baba zao,
wala hawana shukrani kwa mama zao.
12Kuna watu ambao hujiona kuwa wema,
kumbe bado hawajatakaswa uchafu wao.
13Kuna na wengine – kiburi ajabu!
Hudharau kila kitu wanachokiona.
14Kuna watu ambao meno yao ni kama upanga,
na magego yao ni kama visu.
Wako tayari kuwatafuna maskini wa nchi,
na wanyonge walio miongoni mwa watu!30:14 Picha tunayopewa hapa yahusu jinsi watu wengine wanavyowakandamiza maskini; Taz pia 12:18; Zab 55:22; 59:8.
Methali za kialfabeti
15Mruba anao binti wawili wasemao, “Nipe, nipe!”
Kuna vitu vitatu ambavyo kamwe havishibi,
naam, vitu vinne visivyosema, “Imetosha!”
16Kuzimu,
tumbo la mwanamke lisilozaa,
ardhi isiyoshiba maji,
na moto usiosema, “Imetosha!”
17Kama mtu akimdhihaki baba yake,
na kudharau utii kwa mama yake,
kunguru wa bondeni watamdonoa macho,
na kuliwa na tai.
18Kuna mambo matatu yaliyo ya ajabu kwangu,
naam, mambo manne nisiyoyaelewa:
19Njia ya tai angani,
njia ya nyoka mwambani,
njia ya meli baharini,
na kinachomvuta mwanamume kwa mwanamke.
20Mwenendo wa mwanamke mwasherati ni hivi:
Yeye hula, akajipangusa mdomo,
na kusema, “Sijafanya kosa lolote!”
21Kuna mambo matatu ambayo huitetemesha dunia,
naam, mambo manne ambayo haiwezi kuyastahimili:
22Mtumwa anayekuwa mfalme;
mpumbavu anayeshiba chakula;
23mwanamke asiyependwa anayeolewa;
na mjakazi achukuapo nafasi ya bibi yake.
24Kuna viumbe vinne vidogo sana duniani,
lakini vina akili sana:
25Sisimizi: Wadudu wasio na nguvu,
lakini hujihifadhia chakula wakati wa kiangazi;
26pelele: Wanyama wasio na uwezo,
lakini hujitengenezea makao miambani;
27nzige: Hawana mfalme,
lakini wote huenda pamoja kwa vikosi;
28mjusi: Waweza kumshika mkononi,
lakini huingia katika ikulu.
29Kuna viumbe vitatu vyenye mwendo wa kupendeza,
naam, kuna viumbe vinne vyenye mwendo mzuri;
30simba: Mnyama mwenye nguvu kuliko wote,
wala hamwogopi mnyama mwingine yeyote;
31jogoo aendaye kwa maringo;
tena beberu;
na mfalme mbele ya watu wake.
32Kama umekuwa mpumbavu hata ukajisifu,
au kama umekuwa unapanga maovu,
chunga mdomo wako.
33Maana ukisukasuka maziwa utapata siagi,
ukimpiga mtu pua atatoka damu;
kadhalika kuchochea hasira huleta ugomvi.

Methali30;1-33

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: