Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Friday 19 July 2019

Kikombe Cha Asubuhi ; Methali 22...

Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu katika yote...

Asante  Mungu wetu kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwatayari kwa majukumu yetu


Utukuzwe ee Mungu wetu,usifiwe Baba wa Mbinguni

Neema yako yatutosha  Mungu wetu..!

Labda Onesimo aliondoka kwako kwa kitambo tu, kusudi uweze tena kuwa naye daima. Na sasa yeye si mtumwa wa kawaida, ila ni bora zaidi ya mtumwa: Yeye ni ndugu yetu mpenzi. Ni wa maana sana kwangu mimi, na kwako atakuwa wa maana zaidi, kama mtumwa na kama ndugu katika Bwana.
Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea,Usitutie majaribuni Mungu wetu tunaomba utuepushe na yule mwovu na kazi zake zote,Jehovah ututakase miili yetu na akili zetu Baba wa Mbinguni tunaomba utufunike kwa  Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti,
Yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona....

Basi, ikiwa wanitambua mimi kuwa mwenzako, mpokee tena kama vile ungenipokea mimi mwenyewe. Kama alikuwa amekukosea kitu, au alikuwa na deni lako, basi, unidai mimi. Naandika jambo hili kwa mkono wangu mwenyewe: Mimi Paulo nitalipa! (Tena sina haja ya kusema kwamba wewe unalo deni kwangu la nafsi yako). Naam, ndugu yangu, nifanyie jambo hilo kwa ajili ya jina la Bwana; burudisha moyo wangu kama ndugu katika Kristo.
Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa 
katika utendaji
Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki ridhiki zetu
ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba ukatupe neema ya kuweza
kuwabariki wenye kuhitaji
Yahweh tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Mungu wetu ukatupe kama inavyokupendeza wewe



Jehovah tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyo vimiliki
Yahweh tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia
Baba wa Mbinguni tukawe salama rohoni
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia 
sauti yako na kuitii
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe neema ya kufuata njia zako
Yahweh tukasimamie Neno lako amri na sheria zako siku zote 
za maisha yetu

Mungu  wetu ukaonekane katika maisha yetu popote tupitapo na ikajulikane kwamba upo 

Neema zako zikawe nasi Nuru yako ikaangaze katika maisha yetu
Ukatufanye barua njema ee Mungu wetu nasi tukasomeke kama
inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi...

Naandika nikitumaini kwamba utanikubalia ombi langu; tena najua kwamba utafanya hata zaidi ya haya ninayokuomba. Pamoja na hayo, nitayarishie chumba kwani natumaini kwamba kwa sala zenu, Mungu atanijalia niwatembeleeni. Epafra, mfungwa mwenzangu kwa ajili ya Kristo Yesu, anakusalimu. Nao akina Marko, Aristarko, Dema na Luka, wafanyakazi wenzangu, wanakusalimu. Nawatakieni nyinyi nyote neema ya Bwana Yesu Kristo.
Tazama wenye shida/tabu,Mungu wetu tunaomba
 ukawaguse kila mmoja na mahitaji yake
Baba wa Mbinguni tunaomba ukawasamehe pale walipokwenda
kinyume nawe
Mungu wetu ukawape neema ya kujiombea,macho ya rohoni,masikio yakusikia sauti yako,wakafuate njia zako nazo zikawaweke huru
Mungu wetu tunaomba ukasikie kulia kwao
Baba wa Mbinguni tunomba ukawafute machozi yao
Nuru yako ikaangaze katika maisha yao
Mungu wetu tunaomba ukawatendee sawasawa na mapenzi yako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina....!!!


Wapendwa katika Kristo Yesu asanteni sana
kwakuwanami/kunisoma

Mungu Baba aendelee kuwabariki na kuwatendea
kama inavyompendeza yeye
Amani ya Bwana wetu Yesu Kristo na upendo wa Mungu Baba
ukae nanyi daima....
Nawapenda.

1Afadhali kuwa na sifa nzuri kuliko mali nyingi;
wema ni bora kuliko fedha au dhahabu.
2Matajiri na maskini wana hali hii moja:
Mwenyezi-Mungu ni Muumba wao wote.
3Mtu mwangalifu huona hatari akajificha,
lakini wajinga hujitokeza mbele wakaumia.
4Ukinyenyekea na kumcha Mwenyezi-Mungu,
utapata tuzo: Fanaka, heshima na uhai.
5Njia ya waovu imejaa miiba na mitego;
anayetaka kuhifadhi maisha yake ataiepa.
6Mfunze mtoto namna ya kuishi vizuri,
naye hatasahau njia hiyo hata uzeeni.
7Tajiri humtawala maskini;
mkopaji ni mtumwa wa mkopeshaji.
8Apandaye dhuluma atavuna janga;
uwezo wake wa kutenda mabaya utavunjwa.
9Mtu mkarimu atabarikiwa,
maana chakula chake humgawia maskini.
10Mfukuze mwenye dharau na fujo itatoweka,
ugomvi na matusi vitakoma.
11Mwenye nia safi na maneno mazuri,
atakuwa rafiki wa mfalme.
12Mwenyezi-Mungu hulinda elimu ya kweli,
lakini huyavuruga maneno ya waovu.
13Mvivu husema, “Siwezi kutoka nje;
kuna simba huko, ataniua!”
14Kinywa cha mwasherati ni shimo refu;
anayechukiwa na Mwenyezi-Mungu atatumbukia humo.
15Mtoto hupenda mambo ya kijinga moyoni,
lakini fimbo ya nidhamu humwondolea hayo.
16Anayemdhulumu maskini atamfanya afaidike mwishowe,
anayewapa matajiri zawadi ataishia kuwa maskini.
Misemo thelathini ya wenye hekima
17Tega sikio usikie maneno ya wenye hekima,
elekeza moyo wako uzingatie maarifa yangu.
18Wewe utafurahi endapo utayaweka moyoni,
na kuyakariri kila wakati.
19Ninayependa kumfundisha leo ni wewe,
ili tegemeo lako liwe kwa Mwenyezi-Mungu.
20Nimekuandikia misemo thelathini,
misemo ya maonyo na maarifa,
21ili kukufundisha yaliyo sawa na kweli;
na mtu akikuuliza uweze kumpa jibu sahihi.
- 1 -
22Usimdhulumu maskini kwa kuwa ni maskini,
wala usimnyime fukara haki yake mahakamani.
23Maana Mwenyezi-Mungu atawatetea;
atawapokonya maisha yao wale watakaowadhulumu.
- 2 -
24Usifanye urafiki na mtu wa hasira,
wala usiandamane na mwenye ghadhabu,
25usije ukajifunza mwenendo wake,
ukajinasa kabisa katika mtego.
- 3 -
26Usiwe mmoja wao wenye kuweka ahadi,
watu ambao hujiweka wadhamini wa madeni.
27Ikiwa huna chochote cha kulipa,
hata kitanda unacholalia kitachukuliwa!
- 4 -
28Usiondoe alama ya mipaka ya zamani
ambayo iliwekwa na wazee wako.
- 5 -
29Je, yuko mtu mwenye maarifa kazini mwake?
Huyo atawatumikia wafalme;
hatawapa huduma yake watu wasiofaa.

Methali22;1-29

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: