Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Friday 15 November 2019

Kikombe Cha Asubuhi;Isaya 56....


Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu katika yote...

Asante  Mungu wetu kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwatayari kwa majukumu yetu


Utukuzwe ee Mungu wetu,usifiwe Baba wa Mbinguni

Neema yako yatutosha  Mungu wetu..!



Kwa nguvu yako uliisimika milima mahali pake. Wewe una nguvu mno! Watuliza mshindo wa bahari na wa mawimbi yake, wakomesha ghasia za watu. Ulimwengu wote washangazwa na matendo yako. Wasababisha furaha kila mahali, toka mashariki hata magharibi.
Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,
tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako

Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea,Usitutie majaribuni Mungu wetu tunaomba utuepushe na yule mwovu na kazi zake zote,Jehovah ututakase miili yetu na akili zetu Baba wa Mbinguni tunaomba utufunike kwa  Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti,
Yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona....


Wewe waitunza nchi kwa kuinyeshea mvua, waijalia rutuba na kuistawisha; mto wako umejaa maji tele, waifanikisha nchi na kuipatia mavuno. Hivi ndivyo uitengenezavyo nchi: Mashamba wayanyeshea mvua kwa wingi, na kuyalowanisha kwa maji; ardhi wailainisha kwa manyunyu, na kuibariki mimea ichipue.
Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa 
katika utendaji
Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki ridhiki zetu
ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba ukatupe neema ya kuweza
kuwabariki wenye kuhitaji
Yahweh tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Mungu wetu ukatupe kama inavyokupendeza wewe



Jehovah tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyo vimiliki
Yahweh tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia
Baba wa Mbinguni tukawe salama rohoni
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia 
sauti yako na kuitii
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe neema ya kufuata njia zako
Yahweh tukasimamie Neno lako amri na sheria zako siku zote 
za maisha yetu

Mungu  wetu ukaonekane katika maisha yetu popote tupitapo na ikajulikane kwamba upo 

Neema zako zikawe nasi Nuru yako ikaangaze katika maisha yetu
Ukatufanye barua njema ee Mungu wetu nasi tukasomeke kama
inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi...


Wautunukia mwaka wote mema yako, kila ulipopitia pamejaa fanaka. Mbuga za majani zimejaa mifugo, milima nayo imejaa furaha. Malisho yamejaa kondoo, mabonde yamefunikwa kwa ngano. Kila kitu kinashangilia kwa furaha.
Tazama wenye shida/tabu,Mungu wetu tunaomba
 ukawaguse kila mmoja na mahitaji yake
Baba wa Mbinguni tunaomba ukawasamehe pale walipokwenda
kinyume nawe
Mungu wetu ukawape neema ya kujiombea,macho ya rohoni,masikio yakusikia sauti yako,wakafuate njia zako nazo zikawaweke huru
Mungu wetu tunaomba ukasikie kulia kwao
Baba wa Mbinguni tunomba ukawafute machozi yao
Nuru yako ikaangaze katika maisha yao
Mungu wetu tunaomba ukawatendee sawasawa na mapenzi yako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina....!!!


Wapendwa katika Kristo Yesu asanteni sana
kwakuwanami/kunisoma

Mungu Baba aendelee kuwabariki na kuwatendea
kama inavyompendeza yeye
Amani ya Bwana wetu Yesu Kristo na upendo wa Mungu Baba
ukae nanyi daima....

Nawapenda.

Wote wanakaribishwa
1Mwenyezi-Mungu asema:
“Zingatieni haki na kutenda mema,
maana nitawaokoeni hivi karibuni,
watu wataona wazi kwamba ninawakomboeni.
2Heri mtu anayezingatia kikamilifu ninayosema,
anayeshika sheria ya Sabato kwa heshima
na kuepa kutenda uovu wowote.
3“Mgeni anayenitambua mimi Mwenyezi-Mungu asifikiri:
‘Hakika Mwenyezi-Mungu atanitenga na watu wake.’
Naye towashi asiseme:
‘Mimi ni mti mkavu tu!’
4Maana mimi Mwenyezi-Mungu nasema:
Towashi ashikaye sheria zangu za Sabato,
anayefanya mambo yanayonipendeza,
na kulizingatia agano langu,
5nitampa nafasi maalumu na ya sifa
katika nyumba yangu na kuta zake;
nafasi bora kuliko kuwa na watoto wa kiume na wa kike:
Nitampa jina la kukumbukwa daima,
na ambalo halitafutwa kamwe.
6“Watu wageni watakaonikiri mimi Mwenyezi-Mungu,
watakaoniheshimu, wakapenda jina langu na kuwa watumishi wangu,
wote watakaoshika Sabato bila kuikufuru,
watu watakaozingatia agano langu,
7hao nitawaleta katika mlima wangu mtakatifu,
na kuwafurahisha katika nyumba yangu ya sala;
tambiko na sadaka zao zitakubaliwa madhabahuni pangu.
Maana nyumba yangu itaitwa:
‘Nyumba ya sala kwa ajili ya watu wote’.
8“Hii ni kauli yangu mimi Bwana Mwenyezi-Mungu
ninayewakusanya Waisraeli waliotawanyika.
Licha ya hao niliokwisha kukusanya,
nitawakusanya watu wengine wajumuike nao.”
Viongozi wa Israeli walaumiwa
9Enyi wanyama wote wakali,
nanyi wanyama wote wa mwituni,
njoni muwatafune watu wangu.
10Maana viongozi wao wote ni vipofu;
wote hawana akili yoyote.
Wote ni kama mbwa bubu wasiobweka,
hulala tu na kuota ndoto,
hupenda sana kusinzia!
11Hao ni kama mbwa wenye uchu sana,
wala hawawezi kamwe kutoshelezwa.
Wachungaji hao hawana akili yoyote;
kila mmoja hutafuta faida yake mwenyewe.
12Huambiana, “Njoni, twende kutafuta divai;
njoni tunywe tushibe pombe!
Kesho itakuwa kama leo,
tena itakuwa sikukuu kubwa zaidi.”


Isaya56;1-12

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: