Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Wednesday 30 October 2019

Kikombe Cha Asubuhi;Isaya 44....


Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu katika yote...

Asante  Mungu wetu kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwatayari kwa majukumu yetu


Utukuzwe ee Mungu wetu,usifiwe Baba wa Mbinguni

Neema yako yatutosha  Mungu wetu..!

Namlilia Mungu kwa sauti, kwa sauti namlilia Mungu anisikie. Wakati wa taabu namwomba Bwana; namnyoshea mikono yangu usiku bila kuchoka, lakini sipati faraja yoyote kwa mtu. Ninamfikiria Mungu na kusononeka; ninatafakari na kufa moyo. Wanizuia hata kupata lepe la usingizi, nina mahangaiko hata kusema siwezi.
Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,
tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako

Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea,Usitutie majaribuni Mungu wetu tunaomba utuepushe na yule mwovu na kazi zake zote,Jehovah ututakase miili yetu na akili zetu Baba wa Mbinguni tunaomba utufunike kwa  Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti,
Yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona....

Nafikiria siku za zamani; nakumbuka miaka ya hapo kale. Usiku nawaza na kuwazua moyoni; natafakari na kujiuliza rohoni: “Je, Bwana ametuacha kabisa? Je, hatatuonesha tena hisani yake? Je fadhili zake zimekoma kabisa? Je, hatatimiza tena ahadi zake? Je, Mungu amesahau kuwa na huruma? Je, hasira yake imeuondoa upole wake?”
Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa 
katika utendaji
Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki ridhiki zetu
ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba ukatupe neema ya kuweza
kuwabariki wenye kuhitaji
Yahweh tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Mungu wetu ukatupe kama inavyokupendeza wewe



Jehovah tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyo vimiliki
Yahweh tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia
Baba wa Mbinguni tukawe salama rohoni
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia 
sauti yako na kuitii
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe neema ya kufuata njia zako
Yahweh tukasimamie Neno lako amri na sheria zako siku zote 
za maisha yetu

Mungu  wetu ukaonekane katika maisha yetu popote tupitapo na ikajulikane kwamba upo 

Neema zako zikawe nasi Nuru yako ikaangaze katika maisha yetu
Ukatufanye barua njema ee Mungu wetu nasi tukasomeke kama
inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi...

Kisha nikasema, “Kinachonichoma zaidi ni kwamba, Mungu Mkuu hatendi tena kitu kwa ajili yetu!” Nitayakumbuka matendo yako, ee Mwenyezi-Mungu, naam, nitayafikiria maajabu yako ya hapo kale.
Tazama wenye shida/tabu,Mungu wetu tunaomba
 ukawaguse kila mmoja na mahitaji yake
Baba wa Mbinguni tunaomba ukawasamehe pale walipokwenda
kinyume nawe
Mungu wetu ukawape neema ya kujiombea,macho ya rohoni,masikio yakusikia sauti yako,wakafuate njia zako nazo zikawaweke huru
Mungu wetu tunaomba ukasikie kulia kwao
Baba wa Mbinguni tunomba ukawafute machozi yao
Nuru yako ikaangaze katika maisha yao
Mungu wetu tunaomba ukawatendee sawasawa na mapenzi yako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina....!!!


Wapendwa katika Kristo Yesu asanteni sana
kwakuwanami/kunisoma

Mungu Baba aendelee kuwabariki na kuwatendea
kama inavyompendeza yeye
Amani ya Bwana wetu Yesu Kristo na upendo wa Mungu Baba
ukae nanyi daima....

Nawapenda.

Mwenyezi-Mungu ndiye Mungu pekee
1“Sikiliza ewe taifa Israeli mtumishi wangu;
sikiliza ewe kizazi cha Yakobo mteule wangu.
2Mimi, Mwenyezi-Mungu Muumba wako,
niliyekufanya tangu tumboni mwa mama yako,
nimekuja kukusaidia wewe.
Mimi Mwenyezi-Mungu nasema:
Usiogope, ewe taifa la Yakobo, mtumishi wangu,
naam, usiogope ewe Yeshuruni mteule wangu.
3“Nitaimwagilia maji nchi iliyokauka,
na kutiririsha mto katika nchi kame.
Nitawamiminia roho yangu wazawa wako,
nitawamwagia watoto wako baraka yangu.
4Watachipua kama nyasi penye maji mengi,
kama majani kandokando ya vijito.
5“Mmoja atasema: ‘Mimi ni wa Mwenyezi-Mungu’,
mwingine atajiita kwa jina la Yakobo,
mwingine ataandika mkononi mwake, ‘Wa Mwenyezi-Mungu’,
na kujitambulisha kwa jina la Israeli.”
6Mwenyezi-Mungu, Mfalme na Mkombozi wa Israeli,
naam, Mwenyezi-Mungu wa majeshi asema hivi:
“Mimi ni wa kwanza na wa mwisho;
hakuna Mungu mwingine ila mimi.
7Ni nani Mungu aliye kama mimi?
Mwache atangaze na kusema wazi mbele yangu.
Nani alitangaza hapo kale mambo ambayo yatatukia?
Na watuambie yale ambayo bado kutokea.44:7 aya ya 7 Kiebrania si dhahiri.
8Enyi watu wangu, msiogope wala msiwe na hofu,
Je, sikuwaambia tangu zamani mambo yatakayotokea?
Nyinyi ni mashahidi wangu.
Je, yuko Mungu mwingine ila mimi?
Je, kuna mwenye nguvu mwingine?
Huyo simjui!”
Upumbavu wa kuabudu sanamu
9Watu wote wanaotengeneza sanamu za miungu ni bure kabisa; na vitu hivyo wanavyovifurahia haviwafai chochote. Wanaoshuhudia hiyo miungu ya uongo ni vipofu na wajinga. Kwa hiyo hao wataaibishwa! 10Ajabu ya mtu kutengeneza sanamu au kinyago cha mungu ambaye hawezi kumsaidia chochote! 11Hakika wote wanaomheshimu wataaibishwa, tena hao mafundi wa sanamu ni binadamu tu. Basi, wakutane wote, wajitokeze, nao watatishika na kuaibishwa.
12Mfuachuma huchukua madini, akayayeyusha motoni na kufua sanamu. Huigongagonga kwa nyundo ili kuipa umbo kwa mikono yake yenye nguvu. Wakati wote huo yeye huona njaa na kuchoka; huona kiu na nguvu kumwishia. 13Kadhalika naye seremala hupima kipande cha mbao, akakitia alama kwa kalamu yake, kisha kwa vifaa vyake hukichonga na kukipa umbo la binadamu na sura ya kupendeza; kisha akaiweka sanamu hiyo ya mungu mahali pake pa pekee. 14Mtu hukata mti wa mwerezi ili autumie, au huchagua mberoshi au mwaloni. Huuacha ukue kati ya miti ya msituni. Au hupanda mwerezi na mvua huustawisha. 15Sehemu ya mti huo itatumiwa kama kuni; mtu huota moto wake na kuoka mikate yake juu yake. Sehemu nyingine ya mti huohuo, mtu hujichongea sanamu ya mungu, akainakshi, halafu akaiabudu. 16Kisha huchukua kuni zake akaoka nazo moto, akachoma nyama juu yake, akala, akashiba. Halafu hukaa hapo akiota moto na kusema, “Naam! Ama kweli nimepata joto! Huo ndio moto!” 17Sehemu iliyobaki ya mti huohuo, hujichongea sanamu ya mungu, kinyago chake, kisha huisujudia na kuiabudu. Huiomba akisema, “Wewe ni mungu wangu, niokoe!”
18Watu hao hawajui wala hawaelewi kitu chochote. Wamefumbwa macho wasiweze kuona; kadhalika na akili zao wasiweze kufahamu. 19Hakuna awezaye kutafakari; au kuwa na akili na kufikiri na kusema: “Nusu ya mti huo niliwashia moto; tena nikaoka mikate juu ya makaa yake, nikachoma nyama, nikala. Je, sehemu iliyobaki nitatengeneza sanamu ambayo ni chukizo na kukisujudia hicho kipande cha mti?”
20La! Fikira zake zimeambatana na hicho ambacho ni majivu tu! Mtu huyo amepotoka hata hawezi kujiokoa mwenyewe na kusema: “Kweli ninachoshika mkononi ni udanganyifu mtupu!”
Mwenyezi-Mungu, hatawasahau Waisraeli
21Mwenyezi-Mungu asema hivi:
“Ewe taifa la Yakobo kumbuka;
naam, kumbuka ewe Israeli:
Wewe ni mtumishi wangu.
Nilikuumba ili uwe mtumishi wangu,
nami kamwe sitakusahau.
22Nimeyafagilia mbali makosa yako kama wingu,
nimezifanya dhambi zako zitoweke kama ukungu.
Rudi kwangu maana mimi nimekukomboa.”
23Imbeni kwa furaha enyi mbingu,
kwa sababu ya hayo aliyotenda Mwenyezi-Mungu.
Pazeni sauti enyi vilindi vya dunia!
Imbeni kwa furaha enyi milima!
Enyi misitu na miti yote iliyomo, imbeni.
Maana Mwenyezi-Mungu amewakomboa wazawa wa Yakobo,
naye atatukuka katika nchi ya Israeli.
24Mwenyezi-Mungu, Mkombozi wako,
aliyekuumba tangu tumboni mwa mama yako, asema:
“Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu niliyeumba vitu vyote.
Mimi peke yangu nilizitandaza mbingu,
niliiumba dunia kwa nguvu yangu mwenyewe!
25 44:25 Taz 1Kor 1:20 Mimi huzivuruga ishara za watabiri waongo
na kuwapumbaza waaguzi.
Mimi huyakanusha maneno ya wenye hekima
na kufanya ujuzi wao kuwa upumbavu.
26Lakini huuthibitisha ujumbe wa mtumishi wangu,
na kukamilisha maaguzi ya wajumbe wangu.
Mimi ndimi niuambiaye mji wa Yerusalemu:
Wewe Yerusalemu, utakaliwa tena na watu.
Na miji ya Yuda:
Nyinyi mtajengeka tena:
Magofu yenu nitayarekebisha tena.
27Mimi ndimi ninayeviamuru vilindi:
Kaukeni.
28Ndimi nimwambiaye Koreshi:
Wewe utawachunga watu kwa niaba yangu.
Wewe utatekeleza mipango yangu yote.
Ndimi ninayesema kuhusu Yerusalemu:
Wewe Yerusalemu utajengwa tena upya;
na juu ya hekalu: Msingi wako utawekwa tena.”

Isaya44;1-28

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: