Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Wednesday 1 April 2020

Kikombe Cha Asubuhi; Ezekieli 31...



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu katika yote....

Mungu wetu Baba yetu,Muumba wetu Muumba wa Mbingu na Nchi
Muumba wa vyote vilivyomo vinavyoonekana na visivyoonekana
Mungu wa walio hai,Mungu  mwenye huruma,Mungu wa upendo
Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo...
Asante kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwatayari kwa majukumu yetu

Neema yako yatutosha ee Mungu wetu....!!



“Mkinipenda mtazishika amri zangu. Nami nitamwomba Baba naye atawapeni Msaidizi mwingine, atakayekaa nanyi milele. Yeye ni Roho wa ukweli. Ulimwengu hauwezi kumpokea kwa sababu hauwezi kumwona wala kumjua. Lakini nyinyi mnamjua kwa sababu anabaki nanyi na yu ndani yenu.
Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako,
Tukijinyenyekeza,tukijiachilia mikononi mwako
Mungu wetu tunamomba utusamehe dhambi zetu
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba ukatupe neema
 ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea

Usitutie majaribuni Mungu wetu tunaomba utuepushe
na yule mwovu na kazi zake zote
Jehovah ututakase miili yetu na akili zetu
Baba wa Mbinguni tunaomba utufunike kwa Damu
ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti
yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona....

“Sitawaacha nyinyi yatima; nitakuja tena kwenu. Bado kidogo nao ulimwengu hautaniona tena, lakini nyinyi mtaniona; na kwa kuwa mimi ni hai, nanyi pia mtakuwa hai.
Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa katika utendaji
Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Yahweh tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomna ukatupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji
Tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe kama inavyokupendeza wewe...


Yahweh tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyovimiliki
Yahweh tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia
Baba wa Mbinguni tukawe salama rohoni
Yahwe ukatupe akili ya kutambua mema na mabaya
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu ukatupe macho ya kuona,masikio ya kusikia sauti yako na kuitii..
Baba wa Mbinguni  tunaomba ukatupe neema ya kufuata
njia zako,tukasimamie Neno lako,amri na sheria zako
siku zote za maisha yetu...
Ukatuguse kwa mkono wako wenye nguvu,ukatufanye chombo chema
ee Mungu wetu nasi tukatumike kama inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi....

Siku ile itakapofika mtajua kwamba mimi niko ndani ya Baba, nanyi mko ndani yangu, nami ndani yenu. Azipokeaye amri zangu na kuzishika, yeye ndiye anipendaye. Naye anipendaye mimi atapendwa na Baba yangu, nami nitampenda na kujidhihirisha kwake.”
Tazama watoto wako wenye shida/tabu,wote wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali
Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu
kila mmoja na mahitaji yake
Mungu wetu tunaomba ukawasamehe pale walipo kwenda kinyume nawe
Yahweh tunaomba ukawape neema ya kuweza kujiombea,kufuata njia zako nazo zikawaweke huru...
Baba wa Mbinguni tunayaweka haya yote mikononi mwako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele...
Amina...!!


Asanteni sana wapendwa katika Kristo Yesu kwakuwa nami,Baba wa Mbinguni aendelee kuwatendea sawasawa na mapenzi yake...

Nawapenda.

Misri inalinganishwa na mwerezi
1Mnamo siku ya kwanza ya mwezi wa tatu, mwaka wa kumi na moja tangu uhamisho wetu, neno la Mwenyezi-Mungu lilinijia: 2“Wewe mtu! Mwambie hivi Farao mfalme wa Misri na watu wake wote:
Wewe wafanana na nini kwa ukuu wako?
3Wewe ni kama mwerezi wa Lebanoni31:3 kama … Lebanoni: Au unalingana na Ashuru.
wenye matawi mazuri na majani mengi na shina refu.
Kilele chake kinafika hata mawinguni.
4Maji yaliustawisha,
vilindi vya maji viliulisha.
Mito ilibubujika mahali ulipoota,
ikapeleka vijito kwenye miti yote ya msituni.
5“Kwa hiyo, ulirefuka sana
kupita miti yote msituni;
matawi yake yalizidi kuwa mengi na makubwa,
kutokana na maji mengi mizizini mwake.
6Ndege wote waliweka viota matawini mwake,
chini yake wanyama walizaliwa,
mataifa yote makubwa yaliburudika kivulini mwake.
7Ulikuwa mzuri kwa ukubwa wake,
na kwa urefu wa matawi yake.
Mizizi yake ilipenya chini
mpaka penye maji mengi.
8 31:8 Taz Mwa 2:9 Miongoni mwa mierezi ya bustanini mwa Mungu,
hakuna mti uliolingana nao,
wala misonobari haikulingana na matawi yake,
mibambakofi haikuwa na matawi kama yake,
hata mti wowote wa bustani ya Mungu
haukulingana nao kwa uzuri.
9Mimi niliufanya kuwa mzuri
kwa matawi yake mengi;
ulionewa wivu na miti yote ya Edeni
iliyokuwa katika bustani ya Mungu.
10“Kwa hiyo, mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Kwa sababu wewe ulirefusha31:10 Kwa … ulirefusha: Au Kwa sababu wewe ulirefusha. kimo chake na kukiinua kilele chake kati ya matawi makubwa, ukajivunia urefu wake, 11nitautia mikononi mwa mkuu kati ya mataifa. Yeye, atauadhibu. Nimeutupilia mbali kadiri ya uovu wake. 12Watu wa mataifa mengine katili kupindukia, wataukata na kuubwaga chini na kuuacha. Matawi yake yataanguka chini mlimani na kila mahali mabondeni; yatavunjika na kutapakaa chini katika magenge yote. Watu wote wataondoka kivulini mwake na kuuacha. 13Ndege wote watatua juu ya mabaki yake na wanyama wote wa porini watakanyaga matawi yake. 14Hayo yameupata ili mti wowote ulio mahali penye maji usiweze kurefuka tena kiasi hicho wala kukifikisha kilele chake mawinguni. Mti wowote unaonyweshwa maji usiweze tena kufikia urefu huo. Kwa maana kila kitu mwisho wake ni kifo; hali kadhalika na watu. Wote watashiriki hali yao washukao shimoni kwa wafu.
15“Kwa hiyo mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Siku ileile mwerezi ulipofika kuzimu nilitandaza giza nene juu yake nikaufunika; mito yake niliikausha na mtiririko wa maji yake mengi nikaukomesha. Nayo Lebanoni niliiweka gizani kwa ajili yake, na miti yote msituni ikazirai kwa ajili yake. 16Niliyafanya mataifa yatetemeke kwa sauti ya kuanguka kwake, naam, wakati nilipouangusha chini kuzimu pamoja nao washukao shimoni kwa wafu nayo miti yote ya Edeni, miti mizuri na ya pekee ya Lebanoni ambayo ilimwagiliwa maji ilifarijiwa huko chini kwa wafu. 17Hiyo nayo ilishuka huko kuzimu pamoja nao, ikajiunga na wale waliofungamana nao na ambao waliburudika chini ya kivuli chake.
18“Kwa uzuri na ukuu wa mti huo, hamna mti wowote bustanini Edeni ambao uliweza kulinganishwa nao. Sasa, mti huo ni wewe mfalme Farao. Wewe utatupwa chini kwa wafu pamoja na miti ya Edeni. Utalala karibu na wale wasiomjua Mungu na wale waliouawa kwa upanga. Hiyo itakuwa hali yako ewe Farao, wewe na watu wako. Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nimesema.”


Ezekieli31;1-18

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)


"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: