Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Tuesday 7 April 2020

Kikombe Cha Asubuhi; Ezekieli 35...

Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu katika yote...

Asante  Mungu wetu kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwatayari kwa majukumu yetu


Utukuzwe ee Mungu wetu,usifiwe Baba wa Mbinguni

Neema yako yatutosha  Mungu wetu..!

Kwa sababu hiyo, nampigia magoti Baba, aliye asili ya jamaa zote duniani na mbinguni. Namwomba Mungu, kadiri ya utajiri wa utukufu wake, awajalieni kwa uwezo wa Roho wake, nguvu ya kuwa imara ndani yenu, naye Kristo akae mioyoni mwenu kwa imani. Namwomba mpate kuwa na mzizi na msingi katika mapendo
Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,
tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako

Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea,Usitutie majaribuni Mungu wetu tunaomba utuepushe na yule mwovu na kazi zake zote,Jehovah ututakase miili yetu na akili zetu Baba wa Mbinguni tunaomba utufunike kwa  Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti,
Yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona....

kusudi muweze kufahamu pamoja na watu wote wa Mungu jinsi upendo wa Kristo ueneavyo kwa mapana na marefu, kwa kimo na kina. Naam, mpate kujua upendo wa Kristo upitao elimu yote, mjazwe kabisa utimilifu wote wa Mungu.
Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa 
katika utendaji
Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki ridhiki zetu
ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba ukatupe neema ya kuweza
kuwabariki wenye kuhitaji
Yahweh tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Mungu wetu ukatupe kama inavyokupendeza wewe



Jehovah tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyo vimiliki
Yahweh tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia
Baba wa Mbinguni tukawe salama rohoni
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia 
sauti yako na kuitii
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe neema ya kufuata njia zako
Yahweh tukasimamie Neno lako amri na sheria zako siku zote 
za maisha yetu

Mungu  wetu ukaonekane katika maisha yetu popote tupitapo na ikajulikane kwamba upo 

Neema zako zikawe nasi Nuru yako ikaangaze katika maisha yetu
Ukatufanye barua njema ee Mungu wetu nasi tukasomeke kama
inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi...

Kwake yeye ambaye kwa nguvu yake ifanyayo kazi ndani yetu aweza kufanya mambo makuu zaidi ya yale tuwezayo kuomba au kufikiria; kwake Mungu uwe utukufu katika kanisa na katika Kristo Yesu, nyakati zote, milele na milele! Amina.
Tazama wenye shida/tabu,Mungu wetu tunaomba
 ukawaguse kila mmoja na mahitaji yake
Baba wa Mbinguni tunaomba ukawasamehe pale walipokwenda
kinyume nawe
Mungu wetu ukawape neema ya kujiombea,macho ya rohoni,masikio yakusikia sauti yako,wakafuate njia zako nazo zikawaweke huru
Mungu wetu tunaomba ukasikie kulia kwao
Baba wa Mbinguni tunomba ukawafute machozi yao
Nuru yako ikaangaze katika maisha yao
Mungu wetu tunaomba ukawatendee sawasawa na mapenzi yako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina....!!!


Wapendwa katika Kristo Yesu asanteni sana
kwakuwanami/kunisoma

Mungu Baba aendelee kuwabariki na kuwatendea
kama inavyompendeza yeye
Amani ya Bwana wetu Yesu Kristo na upendo wa Mungu Baba
ukae nanyi daima....

Nawapenda.

Unabii juu ya Edomu
1Neno la Mwenyezi-Mungu lilinijia: 2“Wewe mtu! Ugeukie mlima Seiri, utoe unabii juu ya wakazi wake. 3Uambie kuwa mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Mimi napambana nawe, ee mlima Seiri. Ninanyosha mkono wangu dhidi yako na kukufanya uwe jangwa na ukiwa. 4Ninaifanya miji yako kuwa magofu nawe utakuwa jangwa. Ndipo utakapotambua kuwa mimi ni Mwenyezi-Mungu. 5Ulikuwa adui wa daima wa Israeli, ukasababisha watu wake wauawe kwa upanga, wakati wa msiba wao, wakati wa adhabu yao ya mwisho. 6Kwa hiyo, kama niishivyo, nasema mimi Bwana Mwenyezi-Mungu, naapa kwamba kifo kinakungoja na hutaweza kukikwepa. Kwa kuwa unayo hatia ya mauaji, basi mauaji nayo yatakuandama. 7Nitaufanya mlima Seiri kuwa ukiwa na jangwa na yeyote apitaye huko nitamwangamiza. 8Nitajaza milima yako watu waliouawa; na katika vilima vyako na mabonde yako na magenge yako yote watakuwako waliouawa kwa upanga. 9Nitakufanya kuwa jangwa milele, na miji yako haitakaliwa tena. Ndipo utatambua kuwa mimi ni Mwenyezi-Mungu.
10“Wewe ulisema ya kwamba mataifa hayo mawili yaani Yuda na Israeli ni mali yako na kwamba utazimiliki! Ulisema hivyo ingawa humo ni makao yangu mimi Mwenyezi-Mungu. 11Kwa hiyo, mimi Bwana Mwenyezi-Mungu naapa kwa nafsi yangu kwamba nitakutenda kadiri ya hasira na wivu wako, kulingana na chuki yako kwao. Nitakapokuadhibu utatambua mimi ni nani! 12Wewe utajua ya kwamba mimi mwenyewe Mwenyezi-Mungu nimeyasikia matusi yote uliyoyatoa dhidi ya milima ya Israeli, ukisema: ‘Milima ya Israeli imefanywa kuwa jangwa! Tumepewa sisi tuinyakue!’ 13Nimesikia jinsi unavyojigamba na kusema maneno mengi dhidi yangu. 14Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Nitakapokufanya wewe Edomu kuwa jangwa, dunia yote itafurahi 15kama wewe ulivyofanya wakati nchi ya Waisraeli ilipoharibiwa. Utakuwa jangwa, ewe mlima Seiri, pamoja na nchi yote ya Edomu. Ndipo watu watakapotambua kuwa mimi ni Mwenyezi-Mungu.”



Ezekieli35;1-15

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)


"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: