Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Friday 27 March 2020

Kikombe Cha Asubuhi; Ezekieli 28...

Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu katika yote....

Mungu wetu Baba yetu,Muumba wetu Muumba wa Mbingu na Nchi
Muumba wa vyote vilivyomo vinavyoonekana na visivyoonekana
Mungu wa walio hai,Mungu  mwenye huruma,Mungu wa upendo
Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo...
Asante kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwatayari kwa majukumu yetu

Neema yako yatutosha ee Mungu wetu....!!

Adhabu yao itakuwa kuangamizwa milele na kutengwa mbali na utukufu wake mkuu, wakati atakapokuja siku ile kupokea utukufu kutoka kwa watu wake na heshima kutoka kwa wote wanaoamini. Nyinyi pia mtakuwa miongoni mwao, kwani mmeuamini ule ujumbe tuliowaletea.
Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,
tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako

Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote 
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba ukatupe neema
ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea
Usitutie majaribuni Mungu wetu tunaomba utuepushe
na yule mwovu na kazi zake zote
Jehovah ututakase miili yetu na akili zetu
Baba wa Mbinguni tunaomba utufunike kwa Damu
ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti
yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona....

Ndiyo maana tunawaombeeni daima. Tunamwomba Mungu wetu awawezesheni kustahili maisha aliyowaitia muyaishi. Tunamwomba, kwa uwezo wake, atimize nia yenu ya kutenda mema na kukamilisha kazi yenu ya imani.
Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa katika utendaji
Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Yahweh tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomna ukatupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji
Tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe kama inavyokupendeza wewe...


Yahweh tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyovimiliki
Yahweh tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia
Baba wa Mbinguni tukawe salama rohoni
Yahwe ukatupe akili ya kutambua mema na mabaya
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu ukatupe macho ya kuona,masikio ya kusikia sauti yako na kuitii..
Baba wa Mbinguni  tunaomba ukatupe neema ya kufuata
njia zako,tukasimamie Neno lako,amri na sheria zako
siku zote za maisha yetu...
Ukatuguse kwa mkono wako wenye nguvu,ukatufanye chombo chema
ee Mungu wetu nasi tukatumike kama inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi....

Kwa namna hiyo, jina la Bwana wetu Yesu litapata utukufu kutoka kwenu, nanyi mtapata utukufu kutoka kwake kwa neema ya Mungu wetu na ya Bwana Yesu Kristo.
Tazama watoto wako wenye shida/tabu,wote wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali
Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu
kila mmoja na mahitaji yake
Mungu wetu tunaomba ukawasamehe pale walipo kwenda kinyume nawe
Yahweh tunaomba ukawape neema ya kuweza kujiombea,kufuata njia zako nazo zikawaweke huru...
Baba wa Mbinguni tunayaweka haya yote mikononi mwako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele...
Amina...!!


Asanteni sana wapendwa katika Kristo Yesu kwakuwa nami,Baba wa Mbinguni aendelee kuwatendea sawasawa na mapenzi yake...

Nawapenda.


Unabii juu ya mfalme wa Tiro
1Neno la Mwenyezi-Mungu lilinijia: 2“Wewe mtu! Mwambie mfalme wa Tiro kuwa mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi:
Wewe una kiburi cha moyo,
na umesema kwamba wewe ni mungu,
kwamba umekalia kiti cha enzi cha miungu,
umekaa mbali huko baharini.
Lakini, wewe ni binadamu tu wala si Mungu,
ingawa wajiona kuwa una hekima kama Mungu.
3Haya! Wewe wajiona mwenye hekima kuliko Danieli,
wadhani hakuna siri yoyote usiyoijua.
4Kwa hekima na akili yako
umejipatia utajiri,
umejikusanyia dhahabu na fedha
ukaziweka katika hazina zako.
5Kwa busara yako kubwa katika biashara
umejiongezea utajiri wako,
ukawa na kiburi kwa mali zako!
6Kwa hiyo mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi:
Kwa vile unajiona mwenye hekima kama Mungu,
7basi nitakuletea watu wageni,
mataifa katili kuliko yote.
Wataharibu fahari ya hekima yako
na kuchafua uzuri wako.
8Watakutumbukiza chini shimoni,
nawe utakufa kifo cha kikatili kilindini mwa bahari.
9Je, utajiona bado kuwa mungu
mbele ya hao watakaokuua?
Mikononi mwa hao watakaokuangamiza,
utatambua kuwa wewe ni mtu tu, wala si Mungu!
10Utakufa kifo cha aibu kubwa
mikononi mwa watu wa mataifa.
Ni mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nimesema.”
Kuanguka kwa mfalme wa Tiro:
11Tena neno la Mwenyezi-Mungu lilinijia: 12“Wewe mtu! Imba wimbo wa maombolezo juu ya mfalme wa Tiro. Mwambie kuwa mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi:
Wewe mfalme wa Tiro ulikuwa upeo wa ukamilifu;28:12 makala ya Kiebrania si dhahiri.
ulijaa hekima na uzuri kamili.
13Ulikaa Edeni, bustani ya Mungu.
Ulipambwa kwa kila namna ya johari,
akiki, topazi, yaspi, zabarajadi, berili,
sardoniki, johari ya rangi ya samawati, almasi na zumaridi.
Ulikuwa na mapambo ya dhahabu.
Yote uliwekewa tayari siku ulipoumbwa.28:13 siku ulipoumbwa: Makala ya Kiebrania si dhahiri.
14Nilimteua malaika kukulinda,28:14 Nilimteua … kukulinda: Makala ya Kiebrania si dhahiri.
uliishi katika mlima wangu mtakatifu
na kutembea juu ya vito vinavyometameta.
15Uliishi maisha yasiyo na lawama,
tangu siku ile ulipoumbwa,
hadi ulipoanza kufanya uovu.
16Ufanisi wa biashara yako
ulikujaza dhuluma, ukatenda dhambi.
Kwa hiyo nilikufukuza kama kinyaa,
mbali na mlima wangu mtakatifu.
Na yule malaika aliyekulinda
akakufukuzia mbali na vito vinavyometameta.
17Ulikuwa na kiburi
kwa sababu ya uzuri wako.
Uliharibu hekima yako kwa sababu ya fahari yako.
Nilikubwaga chini udongoni,
nikakufanya kuwa kioja kwa wafalme.
18Kwa wingi wa uhalifu wako
na udanganyifu katika biashara yako
ulipachafua mahali pako pa ibada;
kwa hiyo nilizusha moto kwako, nao ukakuteketeza,
nami nikakufanya majivu juu ya nchi,
mbele ya wote waliokutazama.
19Wote wanaokufahamu kati ya mataifa
wameshikwa na mshangao juu yako.
Umeufikia mwisho wa kutisha,
na hutakuwapo tena milele.”
Unabii juu ya Sidoni
20 28:20-26 Taz Yoe 3:4-8; Zek 9:1-2; Mat 11:21-22; Luka 10:13-14 Neno la Mwenyezi-Mungu lilinijia: 21“Wewe mtu! Ugeukie mji wa Sidoni, 22utoe unabii juu yake kwamba mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi:
Mimi nitapambana nawe Sidoni,
na kuudhihirisha utukufu wangu kati yako.
Nitakapotekeleza hukumu zangu juu yako
na kukudhihirishia utakatifu wangu,
ndipo utakapotambua kuwa mimi ni Mwenyezi-Mungu.
23Nitakupelekea maradhi mabaya
na umwagaji damu utafanyika katika barabara zako.
Utashambuliwa kwa upanga toka pande zote
na watu wako watakaouawa, watakuwa wengi.
Ndipo watakapotambua kuwa mimi ni Mwenyezi-Mungu.”
Waisraeli watapata baraka
24Mungu asema, “Mataifa jirani na Waisraeli ambayo yalikuwa yanawaudhi hayataweza tena kuwaumiza Waisraeli kama vile kwa miiba na michongoma. Ndipo watakapojua ya kuwa mimi ni Bwana Mwenyezi-Mungu.
25“Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Nitawakusanya na kuwaleta Waisraeli kutoka katika mataifa yote ambamo walitawanywa. Hivyo nitawafanya watu wa mataifa waone kuwa mimi ni mtakatifu. Watu wa Israeli wataishi katika nchi yao ambayo mimi nilimpa mtumishi wangu Yakobo. 26Watakaa humo salama salimini; watajenga nyumba na kupanda mizabibu. Wataishi bila hofu maana mataifa jirani zao ambayo yaliwaudhi, mimi nitayaadhibu. Hapo watatambua kuwa mimi ni Mwenyezi-Mungu, Mungu wao.”


Ezekieli28;1-26

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: