Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Wednesday 11 March 2020

Kikombe Cha Asubuhi; Ezekieli 16...


Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu katika yote....

Mungu wetu Baba yetu,Muumba wetu Muumba wa Mbingu na Nchi
Muumba wa vyote vilivyomo vinavyoonekana na visivyoonekana
Mungu wa walio hai,Mungu  mwenye huruma,Mungu wa upendo
Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo...
Asante kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwatayari kwa majukumu yetu

Neema yako yatutosha ee Mungu wetu....!!

Kama vile mwili ulivyo mmoja wenye viungo vingi, na viungo hivyo vyote – ingawaje ni vingi – hufanya mwili mmoja, ndivyo ilivyo pia kwa Kristo. Maana sisi, tukiwa Wayahudi au watu wa mataifa mengine, watumwa au watu huru, sote tumebatizwa kwa Roho mmoja katika mwili huo mmoja; na sote tukanyweshwa Roho huyo mmoja.
Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,
tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako

Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote 
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba ukatupe neema
ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea
Usitutie majaribuni Mungu wetu tunaomba utuepushe
na yule mwovu na kazi zake zote
Jehovah ututakase miili yetu na akili zetu
Baba wa Mbinguni tunaomba utufunike kwa Damu
ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti
yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona....

Mwili hauna kiungo kimoja tu, bali una viungo vingi. Kama mguu ungejisemea: “Kwa kuwa mimi si mkono, basi mimi si mali ya mwili,” je, ungekoma kuwa sehemu ya mwili? La hasha!
Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa katika utendaji
Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Yahweh tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomna ukatupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji
Tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe kama inavyokupendeza wewe...


Yahweh tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyovimiliki
Yahweh tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia
Baba wa Mbinguni tukawe salama rohoni
Yahwe ukatupe akili ya kutambua mema na mabaya
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu ukatupe macho ya kuona,masikio ya kusikia sauti yako na kuitii..
Baba wa Mbinguni  tunaomba ukatupe neema ya kufuata
njia zako,tukasimamie Neno lako,amri na sheria zako
siku zote za maisha yetu...
Ukatuguse kwa mkono wako wenye nguvu,ukatufanye chombo chema
ee Mungu wetu nasi tukatumike kama inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi....

Kama sikio lingejisemea: “Kwa vile mimi si jicho, basi mimi si mali ya mwili,” je, kwa hoja hiyo lingekoma kuwa sehemu ya mwili? La! Kama mwili wote ungekuwa jicho, sikio lingekuwa wapi? Na kama mwili wote ungekuwa sikio, mtu angewezaje kunusa?
Tazama watoto wako wenye shida/tabu,wote wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali
Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu
kila mmoja na mahitaji yake
Mungu wetu tunaomba ukawasamehe pale walipo kwenda kinyume nawe
Yahweh tunaomba ukawape neema ya kuweza kujiombea,kufuata njia zako nazo zikawaweke huru...
Baba wa Mbinguni tunayaweka haya yote mikononi mwako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele...
Amina...!!


Asanteni sana wapendwa katika Kristo Yesu kwakuwa nami,Baba wa Mbinguni aendelee kuwatendea sawasawa na mapenzi yake...

Nawapenda.

Mji wa Yerusalemu si mwaminifu
1Neno la Mwenyezi-Mungu lilinijia: 2“Wewe mtu, ujulishe mji wa Yerusalemu machukizo yake. 3Uuambie kuwa, mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nauambia Yerusalemu: Kwa asili wewe ulizaliwa katika nchi ya Kanaani. Baba yako alikuwa Mwamori, na mama yako alikuwa Mhiti. 4Siku ile ulipozaliwa, kitovu chako hakikukatwa wala hukuoshwa kwa maji; hukusuguliwa kwa chumvi wala hukuvishwa nguo za kitoto. 5Hakuna aliyekuonea huruma na kukufanyia mambo hayo. Hakuna aliyekupenda. Bali, siku ile ulipozaliwa, ulitupwa huko mashambani kwa sababu siku ulipozaliwa ulichukiza sana.
6“Mimi nilipopita karibu nawe, nikakuona ukigaagaa katika damu yako, nilikuambia, 7‘Ishi, na ukue kama mmea shambani.’ Nawe ukakua na kurefuka hata ukawa msichana. Matiti yako yakakua na nywele zako nazo zikakua. Lakini ulikuwa uchi kabisa.
8“Nilipopita tena karibu nawe, nikakuona. Wakati huu, ulikuwa umefikia umri wa kupendwa kama msichana. Nikalitandaza vazi langu juu yako na kuufunika uchi wako. Nikafanya nawe agano la ndoa, nawe ukawa wangu. Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nimesema.
9“Kisha nikachukua maji, nikakuosha damu uliyokuwa nayo, nikakupaka mafuta. 10Nilikuvika pia vazi lililonakshiwa na viatu vya ngozi. Nikakuzungushia kitambaa cha kitani safi na mtandio wa hariri. 11Nikakupamba kwa vito, nikakuvika bangili mikononi mwako na mkufu shingoni. 12Nikakutia hazama puani mwako, vipuli masikioni mwako na kichwani mwako nikakupamba kwa taji nzuri. 13Basi, ukapambika kwa dhahabu na fedha. Vazi lako likawa la kitani safi na hariri, nalo lilikuwa limenakshiwa. Ulitumia unga safi, asali na mafuta kwa chakula chako. Ukawa mzuri kupindukia, ukaifikia hali ya kifalme. 14Sifa zako zikaenea kati ya mataifa kutokana na uzuri wako, kwani uzuri wako ulikamilika kwa sababu ya fahari niliyokujalia. Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nimesema.
15“Lakini, ulitegemea uzuri wako, ukatumia sifa yako kwa kufanya uzinzi, ukifanya umalaya na mtu yeyote apitaye. 16Ulitwaa baadhi ya mavazi yako, ukayatumia kupambia mahali pako pa ibada na hapo ndipo ukafanyia uzinzi wako. Jambo la namna hiyo halijapata kutokea wala halitatokea kamwe! 17Vito vyako vizuri vya dhahabu na fedha nilivyokupa, ulivitwaa, ukajifanyia sanamu za wanaume upate kufanya uzinzi nazo. 18Ukatwaa mavazi niliyokupa yaliyotiwa nakshi na kuzifunika zile sanamu, na mafuta yangu na ubani wangu, ukazitolea sanamu hizo. 19Chakula changu nilichokupa, ulikitoa kwa sanamu hizo kuwa harufu ya kupendeza kwani nilikulisha kwa unga safi, mafuta na asali. Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nimesema!
20“Tena, watoto wako wa kiume na wa kike ulionizalia uliwatwaa, ukazitambikia sanamu zako kwa kuwateketeza. Je, unadhani uzinzi wako ulikuwa ni jambo dogo? 21Je, jambo hili la kuwachinja watoto wangu ili wawe tambiko ya kuteketeza kwa ajili ya sanamu zako ni jambo dogo? 22Katika machukizo yako yote pamoja na uzinzi wako hukuzikumbuka siku za utoto wako, wakati ulipokuwa uchi kabisa, bila kitu, ukigaagaa katika damu yako!
23“Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nakuambia: Ole wako, ole wako Yerusalemu! Baada ya kufanya hayo yote 24ulijijengea majukwaa ya ibada na mahali pa juu kila mahali. 25Mwanzoni mwa kila barabara ulijijengea mahali pa juu, ukautumia urembo wako kufanya uzinzi ukijitoa kwa kila mpita njia na kuongeza uzinzi wako. 26Tena ulifanya uzinzi na jirani zako Wamisri waliojaa tamaa, ukaongeza uzinzi wako na kuichochea hasira yangu. 27Basi, niliunyosha mkono wangu kukuadhibu. Nilipunguza chakula chako, nikakuacha kwa maadui zako, binti za Wafilisti ambao waliona aibu mno juu ya tabia yako chafu mno.
28“Kwa kuwa hukutosheka, ulifanya tena uzinzi na Waashuru. Na hiyo pia haikukutosheleza. 29Ulijitoa wewe mwenyewe utumiwe na Wababuloni, watu wafanyao biashara! Hata hivyo hukutosheka.
30“Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema, kweli wewe ni mgonjwa wa mapenzi. Unafanya uzinzi bila kuona haya hata kidogo. 31Umejijengea jukwaa lako mwanzoni mwa kila barabara na kujijengea mahali pa juu katika kila mtaa. Tena wewe hukuwa kama malaya kwani ulikataa kulipwa. 32Ulikuwa mke mzinzi akaribishaye wageni badala ya mumewe. 33Kwa kawaida wanaume huwalipa malaya, lakini wewe umewalipa wapenzi wako wote, ukiwahonga waje kwako toka pande zote upate kuzini nao. 34Katika umalaya wako hukufanya kama wanawake wengine: Hakuna aliyekubembeleza ili uzini naye bali wewe ulilipa fedha badala ya kulipwa.
Hukumu ya Mungu juu ya Yerusalemu
35“Sasa basi, ewe malaya, lisikie neno langu, mimi Mwenyezi-Mungu. 36Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nakuambia kwamba, wewe umetapanya fedha, umefunua uchi wako ili kuzini na wapenzi wako, umeziabudu sanamu zako zote za miungu na kuzitolea damu ya watoto wako. 37Basi, mimi nitawakusanya wapenzi wako wote uliojifurahisha nao, wote uliowapenda na wote uliowachukia. Nitawakusanya toka pande zote wakushambulie. Nitawafunulia uchi wako wapate kuuona. 38Nitakuhukumu kama wanavyohukumiwa wanawake wanaovunja ahadi ya ndoa au wauaji; nitakuhukumu kwa adhabu ya kifo kwa hasira na kwa ajili ya wivu. 39Nitakutia mikononi mwa wapenzi wako, nao watabomoa jukwaa lako na mahali pako pa ibada. Watakuvua mavazi yako na kukunyanganya vito vyako, wakuache uchi, bila kitu. 40Watakuletea jeshi kukushambulia; watakuua kwa kukupiga mawe na kisha watakukatakata kwa mapanga yao. 41Nyumba zako watazichoma moto na kuwafanya wanawake wengi waone adhabu yako. Utakoma kujitoa kwa mtu yeyote afanye uzinzi nawe. 42Hivyo, nitaitosheleza ghadhabu yangu juu yako, wivu niliokuwa nao juu yako utakwisha; nitatulia na wala sitaona hasira tena. 43Wewe umesahau yale ambayo mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nilikufanyia ulipokuwa kijana. Wewe umenichukiza mno kwa mambo hayo yote. Basi, nitakulipiza kisasi kuhusu kila kitu ulichotenda. Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nimesema. Je, hukuongeza uchafu juu ya machukizo yako yote?
Mtoto kama mama
44“Ewe Yerusalemu! Mtu akitaka kutumia methali juu yako atasema: ‘Kama mama alivyo ndivyo alivyo binti yake.’ 45Kweli wewe ni mtoto wa mama aliyemchukia mumewe na watoto wake; wewe ni sawa na dada zako waliowachukia waume zao na watoto wao. Mama yako alikuwa Mhiti na baba yako alikuwa Mwamori. 46Dada yako mkubwa ni Samaria, aliyekaa upande wako wa kaskazini mwako pamoja na binti zake. Dada yako mdogo ni Sodoma, aliyekaa upande wako wa kusini pamoja na binti zake. 47Lakini wewe hukutosheka kufuata mienendo yao au kutenda sawa na machukizo yao. Kwa muda mfupi tu ulipotoka kuliko walivyopotoka wao katika mienendo yako yote. 48Kweli naapa kwa nafsi yangu, mimi Bwana Mwenyezi-Mungu kuwa, dada yako Sodoma na binti zake, hawakufanya maovu kama yale uliyotenda wewe na binti zako. 49Kosa la dada yako Sodoma, lilikuwa hili: Yeye pamoja na binti zake walipokuwa na chakula na fanaka tele, walianza kujivuna, wakaacha kuwasaidia maskini na fukara. 50Walijivuna, wakafanya machukizo mbele yangu. Kwa hiyo niliwaangamiza mara tu nilipoyaona hayo. 51Naye Samaria kwa kweli hakutenda hata nusu ya dhambi zako. Wewe umefanya machukizo mengi kuliko wao. Ukilinganisha maovu yako na ya dada zako, maovu yao si kitu! 52Wewe utaibeba aibu yako kabisa! Dhambi zako ni mbaya zaidi kuliko za dada zako, kiasi cha kuwafanya dada zako na dhambi zao waonekane hawana hatia. Basi, ona aibu na kubeba fedheha yako, maana umewafanya dada zako waonekane hawana hatia.
Sodoma na Samaria itajengwa upya
53“Nitawarudishia Sodoma na Samaria pamoja na binti zao fanaka yao ya awali. Nawe pia nitakufanikisha miongoni mwao, 54ili ubebe aibu yako na kuona haya, kwa sababu ya mambo yote uliyotenda, ndipo kwa hali yako hiyo dada zako watajiona kwamba wao ni afadhali. 55Dada zako, Sodoma na Samaria, pamoja na binti zao watairudia hali yao ya hapo awali. Hata wewe na binti zako mtairudia hali yenu. 56Kwa majivuno yako ulimdharau dada yako Sodoma. 57Je, hukufanya hivyo kabla uovu wako haujafichuliwa? Sasa umekuwa kama Sodoma. Umekuwa kitu cha dhihaka mbele ya binti za Edomu16:57 Edomu: Hati nyingine: Shamu. na jirani zake wote, na binti za Wafilisti jirani zako ambao walikuchukia. 58Adhabu ya uchafu wa tabia na machukizo yako utaibeba wewe mwenyewe. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
59“Naam! Mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Nitakutenda wewe Yerusalemu kama unavyostahili. Wewe umekidharau kiapo chako, ukavunja na lile agano. 60Lakini mimi nitalikumbuka agano langu nililoagana nawe katika siku za ujana wako. Nitafanya nawe agano la milele. 61Nawe utakumbuka mienendo yako na kuona aibu wakati nitakapokupa dada zako, mkubwa na mdogo, kama binti zako, ingawa si kwa sababu ya agano kati yangu na wewe. 62Mimi nitafanya agano nawe, nawe utatambua kwamba mimi ni Mwenyezi-Mungu. 63Nitakusamehe kila kitu ulichotenda. Nawe utakapokumbuka hayo yote uliyotenda utashangaa na kunyamaza kwa aibu wala hutathubutu kusema tena. Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nimesema.”

Ezekieli16;1-63

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: