Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Tuesday 3 December 2019

Kikombe Cha Asubuhi; Yeremia 2....


Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu katika yote....

Mungu wetu Baba yetu,Muumba wetu Muumba wa Mbingu na Nchi
Muumba wa vyote vilivyomo vinavyoonekana na visivyoonekana
Mungu wa walio hai,Mungu  mwenye huruma,Mungu wa upendo
Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo...
Asante kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwatayari kwa majukumu yetu

Neema yako yatutosha ee Mungu wetu....!!

Yesu akamjibu, “Kama tu ungalijua zawadi ya Mungu na ni nani anayekuambia: ‘Nipatie maji ninywe,’ ungalikwisha mwomba, naye angekupa maji yenye uhai.” Huyo mama akasema, “Bwana, wewe huna chombo cha kutekea maji, nacho kisima ni kirefu; utapata wapi maji yenye uhai? Au, labda wewe wajifanya mkuu zaidi kuliko baba yetu Yakobo? Yeye alitupa sisi kisima hiki; na yeye mwenyewe, watoto wake na mifugo wake walikunywa maji ya kisima hiki.”
Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote 
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba ukatupe neema
ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea
Usitutie majaribuni Mungu wetu tunaomba utuepushe
na yule mwovu na kazi zake zote
Jehovah ututakase miili yetu na akili zetu
Baba wa Mbinguni tunaomba utufunike kwa Damu
ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti
yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona....

Yesu akamjibu, “Kila anayekunywa maji haya ataona kiu tena. Lakini atakayekunywa maji nitakayompa mimi, hataona kiu milele. Maji nitakayompa yatakuwa ndani yake chemchemi ya maji ya uhai na kumpatia uhai wa milele.”
Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa katika utendaji
Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Yahweh tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomna ukatupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji
Tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe kama inavyokupendeza wewe...


Yahweh tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyovimiliki
Yahweh tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia
Baba wa Mbinguni tukawe salama rohoni
Yahwe ukatupe akili ya kutambua mema na mabaya
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu ukatupe macho ya kuona,masikio ya kusikia sauti yako na kuitii..
Baba wa Mbinguni  tunaomba ukatupe neema ya kufuata
njia zako,tukasimamie Neno lako,amri na sheria zako
siku zote za maisha yetu...
Ukatuguse kwa mkono wako wenye nguvu,ukatufanye chombo chema
ee Mungu wetu nasi tukatumike kama inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi....


Huyo mwanamke akamwambia, “Bwana, nipe maji hayo ili nisione kiu tena; na, nisije tena mpaka hapa kuteka maji.” Yesu akamwambia, “Nenda ukamwite mumeo, uje naye hapa.”
Tazama watoto wako wenye shida/tabu,wote wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali
Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu
kila mmoja na mahitaji yake
Mungu wetu tunaomba ukawasamehe pale walipo kwenda kinyume nawe
Yahweh tunaomba ukawape neema ya kuweza kujiombea,kufuata njia zako nazo zikawaweke huru...
Baba wa Mbinguni tunayaweka haya yote mikononi mwako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele...
Amina...!!


Asanteni sana wapendwa katika Kristo Yesu kwakuwa nami,Baba wa Mbinguni aendelee kuwatendea sawasawa na mapenzi yake...
Nawapenda.


Mungu awalinda Waisraeli
1Neno la Mwenyezi-Mungu likanijia: 2“Nenda ukawatangazie waziwazi wakazi wote wa Yerusalemu kuwa mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi:
Naukumbuka uaminifu wako ulipokuwa kijana,
jinsi ulivyonipenda kama mchumba wako,
ulivyonifuata jangwani
kwenye nchi ambayo haikupandwa kitu.
3Israeli, wewe ulikuwa mtakatifu kwangu,
ulikuwa matunda ya kwanza ya mavuno yangu.
Wote waliokudhuru walikuwa na hatia,
wakapatwa na maafa.
Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
Dhambi ya wazee wa Israeli
4Sikilizeni neno la Mwenyezi-Mungu, enyi wazawa wa Yakobo. Sikilizeni enyi jamaa zote za wazawa wa Israeli.
5Mwenyezi-Mungu asema hivi:
“Wazee wenu waliona kosa gani kwangu
hata wakanigeuka na kuniacha,
wakakimbilia miungu duni,
hata nao wakawa watu duni?
6Hawakujiuliza:
‘Yuko wapi Mwenyezi-Mungu aliyetutoa nchini Misri,
aliyetuongoza nyikani
katika nchi ya jangwa na makorongo,
nchi kame na yenye giza nene,
nchi isiyopitiwa na mtu yeyote,
wala kukaliwa na binadamu?’
7Niliwaleta katika nchi yenye rutuba,
muyafurahie mazao yake na mema yake mengine.
Lakini mlipofika tu mliichafua nchi yangu,
mkaifanya chukizo nchi niliyowapa iwe yenu.
8Nao makuhani hawakujiuliza: ‘Yuko wapi Mwenyezi-Mungu?’
Wataalamu wa sheria hawakunijua,
viongozi2:8 viongozi: Kiebrania: Wachungaji. wa watu waliniasi;
manabii nao walitabiri kwa jina la Baali
na kuabudu sanamu zisizo na faida yoyote.”
Mashtaka ya Mwenyezi-Mungu dhidi ya watu wake
9Mwenyezi-Mungu asema,
“Kwa hiyo, mimi nitawalaumu nyinyi,
na nitawalaumu wazawa wenu.
10Haya, vukeni bahari hadi Kupro2:10 Kupro: Au Mwambao wa nchi za Ugiriki na Italia. mkaone,
au tumeni watu huko Kedari2:10 Kedari: Makazi ya Mabedui katika jangwa la Suria na Arabia. wakachunguze,
kama jambo kama hili limewahi kutokea:
11Kwamba kuna taifa lililowahi kubadilisha miungu yake
ingawa miungu hiyo si miungu!
Lakini watu wangu wameniacha mimi, utukufu wao,
wakafuata miungu isiyofaa kitu.
12Shangaeni enyi mbingu, juu ya jambo hili,
mkastaajabu na kufadhaika kabisa.
Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
13Maana, watu wangu wametenda maovu mawili;
wameniacha mimi niliye chemchemi ya maji ya uhai,
wakajichimbia visima vyao wenyewe,
visima vyenye nyufa, visivyoweza kuhifadhi maji.
Matokeo ya utovu wa imani ya Israeli
14“Je, Israeli ni mtumwa,
ama amezaliwa utumwani?
Mbona basi amekuwa kama mawindo?
15Simba wanamngurumia,
wananguruma kwa sauti kubwa.
Nchi yake wameifanya jangwa,
miji yake imekuwa magofu, haina watu.
16Isitoshe, watu wa Memfisi na Tahpanesi,
wameuvunja utosi wake.2:16 wameuvunja … wake: Kitendo kinachomaanisha angamizo kubwa.
17Israeli, je, hayo yote si umejiletea mwenyewe,
kwa kuniacha mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wako,
niliyekuwa ninakuongoza njiani?
18Na sasa itakufaa nini kwenda Misri,
kunywa maji ya mto Nili?
Au itakufaa nini kwenda Ashuru,
kunywa maji ya mto Eufrate?
19Uovu wako utakuadhibu;
na uasi wako utakuhukumu.
Ujue na kutambua kuwa ni vibaya mno
kuniacha mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wako,
na kuondoa uchaji wangu ndani yako.
Mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi nimesema.
Israeli yakataa kumwabudu Mwenyezi-Mungu
20“Tangu zamani wewe ulivunja nira yako,
ukaikatilia mbali minyororo yako,
ukasema, ‘Sitakutumikia’.
Juu ya kila kilima kirefu
na chini ya kila mti wa majani mabichi,
uliinamia miungu ya rutuba kama kahaba.2:20 Katika Israeli kuabudu miungu mingine kulifananishwa na ukahaba.
21Lakini mimi nilikupanda kama mzabibu mteule,
mzabibu wenye afya na wa mbegu safi;
mbona basi umeharibika,
ukageuka kuwa mzabibu mwitu?
22Hata ukijiosha kwa magadi,
na kutumia sabuni nyingi,
madoa ya uovu wako bado yatabaki mbele yangu.
Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
23“Unawezaje kusema, ‘Mimi si najisi;
sijawafuata Mabaali?’
Tazama ulivyotenda dhambi kule bondeni;
angalia ulivyofanya huko!
Wewe ni kama mtamba wa ngamia,
akimbiaye huko na huko;
24kama pundamwitu aliyezoea jangwani.
Katika tamaa yake hunusanusa upepo;
nani awezaye kuizuia hamu yake?
Amtakaye hana haja ya kujisumbua;
wakati wake ufikapo watampata tu.
25Israeli, usiichakaze miguu yako
wala usilikaushe koo lako.
Lakini wewe wasema: ‘Hakuna tumaini lolote.
Nimeipenda miungu ya kigeni,
hiyo ndiyo nitakayoifuata.’
Israeli astahili kuadhibiwa
26“Kama vile mwizi aonavyo aibu akishikwa,
ndivyo Waisraeli watakavyoona aibu;
wao wenyewe, wafalme wao, wakuu wao,
makuhani wao na manabii wao.
27Hao huuambia mti: ‘Wewe u baba yangu,’
na jiwe: ‘Wewe ndiwe uliyenizaa;’
kwa maana wamenipa kisogo,
wala hawakunielekezea nyuso zao.
Lakini wakati wa shida husema: ‘Inuka utuokoe!’
28“Lakini iko wapi miungu yako uliyojifanyia?
Iinuke basi, kama inaweza kukusaidia,
wakati unapokuwa katika shida.
Ee Yuda, idadi ya miungu yako
ni sawa na idadi ya miji yako!
29Mbona mnanilalamikia?
Nyinyi nyote mmeniasi.
Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
30Niliwaadhibu watu wako bila kufanikiwa,
wao wenyewe walikataa kukosolewa.
Upanga wako uliwamaliza manabii wako
kama simba mwenye uchu.
31Enyi watu! Sikilizeni ninachosema mimi Mwenyezi-Mungu:
Je, nimekuwa jangwa kwa Israeli
au nchi yenye giza nene?
Kwa nini basi watu wangu waseme:
‘Sisi tu watu huru;
hatutakuja kwako tena!’
32Kijana msichana aweza kusahau mapambo yake
au bibi arusi mavazi yake?
Lakini watu wangu wamenisahau
kwa muda wa siku zisizohesabika.
33Kweli wewe ni bingwa wa kutafuta wapenzi!
Hata wanawake wabaya huwafundisha njia zako.
34Nguo zako zina damu ya maskini wasio na hatia,
japo hukuwakuta wakivunja nyumba yako.
“Lakini licha ya hayo yote,
35wewe wasema: ‘Mimi sina hatia;
hakika hasira yake imegeuka mbali nami.’
Lakini mimi nitakuhukumu kwa sababu unasema:
‘Sikutenda dhambi.’
36Kwa nini unajirahisisha hivi,
ukibadilibadili mwenendo wako?
Utaaibishwa na Misri,
kama ulivyoaibishwa na Ashuru.
37Na huko pia utatoka,
mikono kichwani kwa aibu.
Mimi Mwenyezi-Mungu nimewakataa wale uliowategemea,
wala hutafanikiwa kwa msaada wao.


Yeremia2;1-37

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: