Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Thursday 19 December 2019

Kikombe Cha Asubuhi; Yeremia 14....


Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu katika yote...

Asante  Mungu wetu kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwatayari kwa majukumu yetu


Utukuzwe ee Mungu wetu,usifiwe Baba wa Mbinguni

Neema yako yatutosha  Mungu wetu..!


Mwisho wa vitu vyote umekaribia. Kwa hiyo mnapaswa kuwa na utaratibu na kukesha ili muweze kusali. Zaidi ya yote pendaneni kwa moyo wote, maana upendo hufunika dhambi nyingi.
Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,
tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako

Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea,Usitutie majaribuni Mungu wetu tunaomba utuepushe na yule mwovu na kazi zake zote,Jehovah ututakase miili yetu na akili zetu Baba wa Mbinguni tunaomba utufunike kwa  Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti,
Yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona....

Muwe na ukarimu nyinyi kwa nyinyi bila kunung'unika. Kila mmoja anapaswa kutumia kipaji alichojaliwa na Mungu kwa faida ya wengine kama wakili mwema wa zawadi mbalimbali za Mungu.
Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa 
katika utendaji
Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki ridhiki zetu
ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba ukatupe neema ya kuweza
kuwabariki wenye kuhitaji
Yahweh tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Mungu wetu ukatupe kama inavyokupendeza wewe



Jehovah tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyo vimiliki
Yahweh tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia
Baba wa Mbinguni tukawe salama rohoni
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia 
sauti yako na kuitii
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe neema ya kufuata njia zako
Yahweh tukasimamie Neno lako amri na sheria zako siku zote 
za maisha yetu

Mungu  wetu ukaonekane katika maisha yetu popote tupitapo na ikajulikane kwamba upo 

Neema zako zikawe nasi Nuru yako ikaangaze katika maisha yetu
Ukatufanye barua njema ee Mungu wetu nasi tukasomeke kama
inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi...


Anayesema kitu, maneno yake na yawe kama maneno ya Mungu; anayetumikia anapaswa kutumikia kwa nguvu anayojaliwa na Mungu, ili katika mambo yote, Mungu atukuzwe kwa njia ya Yesu Kristo ambaye utukufu na nguvu ni vyake milele na milele! Amina.
Tazama wenye shida/tabu,Mungu wetu tunaomba
 ukawaguse kila mmoja na mahitaji yake
Baba wa Mbinguni tunaomba ukawasamehe pale walipokwenda
kinyume nawe
Mungu wetu ukawape neema ya kujiombea,macho ya rohoni,masikio yakusikia sauti yako,wakafuate njia zako nazo zikawaweke huru
Mungu wetu tunaomba ukasikie kulia kwao
Baba wa Mbinguni tunomba ukawafute machozi yao
Nuru yako ikaangaze katika maisha yao
Mungu wetu tunaomba ukawatendee sawasawa na mapenzi yako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina....!!!


Wapendwa katika Kristo Yesu asanteni sana
kwakuwanami/kunisoma

Mungu Baba aendelee kuwabariki na kuwatendea
kama inavyompendeza yeye
Amani ya Bwana wetu Yesu Kristo na upendo wa Mungu Baba
ukae nanyi daima....

Nawapenda.


Ukame wa kutisha
1Neno la Mwenyezi-Mungu lilimjia Yeremia kuhusu ule ukame:
2“Watu wa Yuda wanaomboleza,
na malango yao yanalegea.
Watu wake wanaomboleza udongoni
na kilio cha Yerusalemu kinapanda juu.
3Wakuu wake wanawatuma watumishi wao maji;
watumishi wanakwenda visimani,
lakini maji hawapati;
wanarudi na vyombo vitupu.
Kwa aibu na fadhaa wanafunika vichwa vyao.
4Wakulima wanahuzunika na kufunika vichwa vyao
kwa kuona jinsi ardhi ilivyonyauka.
5Hata kulungu porini anamwacha mtoto wake mchanga,
kwa sababu hakuna nyasi.
6Pundamwitu wanasimama juu ya vilele vikavu,
wanatweta kwa kukosa hewa kama mbweha;
macho yao yanafifia kwa kukosa chakula.
7“Nao watu wanasema:
Ingawa dhambi zetu zashuhudia dhidi yetu,
utusaidie ee Mwenyezi-Mungu kwa heshima ya jina lako.
Maasi yetu ni mengi,
tumetenda dhambi dhidi yako.
8Ewe uliye tumaini la Israeli,
mwokozi wetu wakati wa taabu,
utakuwaje kama mgeni nchini mwetu,
kama msafiri alalaye usiku mmoja?
9Utakuwaje kama mtu uliyechanganyikiwa,
kama shujaa asiyeweza kusaidia mtu?
Lakini wewe ee Mwenyezi-Mungu, u pamoja nasi;
sisi twaitwa kwa jina lako, usituache.”
10Mwenyezi-Mungu asema hivi juu ya watu hawa:
“Kweli wamependa sana kutangatanga,
wala hawakujizuia;
kwa hiyo mimi Mwenyezi-Mungu siwapokei.
Sasa nitayakumbuka makosa yao,
na kuwaadhibu kwa dhambi zao.”
11Mwenyezi-Mungu aliniambia hivi: “Usiwaombee watu hawa fanaka. 12Hata wakifunga, sitayasikiliza maombi yao, na hata wakinitolea sadaka za kuteketeza na za nafaka, mimi sitazikubali. Bali nitawaangamiza kwa upanga, njaa na tauni.”
13Kisha mimi nikasema, “Tazama, ee Bwana Mwenyezi-Mungu! Manabii wanawaambia watu hawa kwamba hapatakuwa na vita wala njaa, kwa sababu umeahidi kuwa patakuwa na amani tu katika nchi yetu.”
14Naye Mwenyezi-Mungu, akaniambia: “Hao manabii wanatoa unabii wa uongo kwa jina langu. Mimi sikuwatuma, wala sikuwaamuru, wala sikusema nao. Wanawatabiria maono ya uongo, maaguzi yasiyo na maana yoyote, uongo wanaojitungia wenyewe. 15Kwa hiyo, mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi kuhusu hao manabii wanaotabiri kwa jina langu, ingawa mimi sikuwatuma, na wanaosema kwamba hapatakuwa na vita wala njaa katika nchi hii: Manabii hao wataangamia kwa upanga na kwa njaa. 16Na hao ambao waliwatabiria mambo hayo, watatupwa nje katika barabara za Yerusalemu wakiwa wamekufa kwa njaa na vita, wala hapatakuwa na mtu wa kuwazika. Hayo yatawapata wao wenyewe, wake zao, watoto wao wa kike na wa kiume; maana mimi nitawamwagia uovu wao wenyewe.
17Hivi ndivyo utakavyowaambia:
Laiti macho yangetoa machozi kutwa kucha,
wala yasikome kububujika,
maana, watu wangu wamejeruhiwa vibaya,
wamepata pigo kubwa sana.
18Nikienda nje mashambani,
naiona miili ya waliouawa vitani;
nikiingia ndani ya mji,
naona tu waliokufa kwa njaa!
Manabii na makuhani wanashughulikia mambo yao nchini,
wala hawajui wanalofanya.”14:18 Manabii … wanalofanya: Au Manabii na makuhani wameburutwa hadi katika nchi wasiyoifahamu kabisa.
Watu wanamsihi Mungu
19Ee Mwenyezi-Mungu, je, umemkataa Yuda kabisa?
Je, moyo wako umechukizwa na Siyoni?
Kwa nini umetupiga vibaya,
hata hatuwezi kupona tena?
Tulitazamia amani, lakini hatukupata jema lolote;
tulitazamia wakati wa kuponywa, badala yake tukapata vitisho.
20Tunakiri uovu wetu, ee Mwenyezi-Mungu,
tunakiri uovu wa wazee wetu,
maana, tumekukosea wewe.
21Usitutupe, kwa heshima ya jina lako;
usikidharau kiti chako cha enzi kitukufu.
Ukumbuke agano ulilofanya nasi, wala usilivunje.
22Je miungu ya uongo ya mataifa
yaweza kuleta mvua?
Au, je, mbingu zaweza kutoa manyunyu?
Je, si wewe ee Mwenyezi-Mungu uliye Mungu wetu?
Tunakuwekea wewe tumaini letu,
maana wewe unayafanya haya yote.


Yeremia14;1-22

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: