Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Friday 13 December 2019

Kikombe Cha Asubuhi; Yeremia 10....


Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu katika yote...

Asante  Mungu wetu kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwatayari kwa majukumu yetu


Utukuzwe ee Mungu wetu,usifiwe Baba wa Mbinguni

Neema yako yatutosha  Mungu wetu..!

Kutoka Mileto Paulo alituma ujumbe kwa wazee wa Efeso wakutane naye. Walipofika kwake aliwaambia, “Mnajua jinsi nilivyokaa nanyi siku zote tangu siku ile ya kwanza nilipofika Asia.
Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,
tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako

Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea,Usitutie majaribuni Mungu wetu tunaomba utuepushe na yule mwovu na kazi zake zote,Jehovah ututakase miili yetu na akili zetu Baba wa Mbinguni tunaomba utufunike kwa  Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti,
Yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona....


Mnajua jinsi nilivyomtumikia Bwana kwa unyenyekevu wote, kwa machozi na matatizo yaliyonipata kutokana na mipango ya hila ya Wayahudi. Mnajua kwamba sikusita hata kidogo kuwahubiria hadharani na nyumbani mwenu na kuwafundisha chochote ambacho kingewasaidieni.
Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa 
katika utendaji
Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki ridhiki zetu
ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba ukatupe neema ya kuweza
kuwabariki wenye kuhitaji
Yahweh tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Mungu wetu ukatupe kama inavyokupendeza wewe



Jehovah tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyo vimiliki
Yahweh tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia
Baba wa Mbinguni tukawe salama rohoni
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia 
sauti yako na kuitii
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe neema ya kufuata njia zako
Yahweh tukasimamie Neno lako amri na sheria zako siku zote 
za maisha yetu

Mungu  wetu ukaonekane katika maisha yetu popote tupitapo na ikajulikane kwamba upo 

Neema zako zikawe nasi Nuru yako ikaangaze katika maisha yetu
Ukatufanye barua njema ee Mungu wetu nasi tukasomeke kama
inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi...

Niliwaonya wote – Wayahudi, kadhalika na watu wa mataifa, wamgeukie Mungu na kumwamini Bwana wetu Yesu. Sasa, sikilizeni! Mimi, nikiwa ninamtii Roho, nakwenda Yerusalemu bila kufahamu yatakayonipata huko. Ninachojua tu ni kwamba Roho Mtakatifu ananithibitishia katika kila mji kwamba vifungo na mateso ndivyo vinavyoningojea. Lakini, siuthamini uhai wangu kuwa kitu sana kwangu mradi tu nikamilishe ule utume wangu na ile kazi aliyonipa Bwana Yesu niifanye, yaani nishuhudie Habari Njema ya neema ya Mungu.
Tazama wenye shida/tabu,Mungu wetu tunaomba
 ukawaguse kila mmoja na mahitaji yake
Baba wa Mbinguni tunaomba ukawasamehe pale walipokwenda
kinyume nawe
Mungu wetu ukawape neema ya kujiombea,macho ya rohoni,masikio yakusikia sauti yako,wakafuate njia zako nazo zikawaweke huru
Mungu wetu tunaomba ukasikie kulia kwao
Baba wa Mbinguni tunomba ukawafute machozi yao
Nuru yako ikaangaze katika maisha yao
Mungu wetu tunaomba ukawatendee sawasawa na mapenzi yako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina....!!!


Wapendwa katika Kristo Yesu asanteni sana
kwakuwanami/kunisoma

Mungu Baba aendelee kuwabariki na kuwatendea
kama inavyompendeza yeye
Amani ya Bwana wetu Yesu Kristo na upendo wa Mungu Baba
ukae nanyi daima....

Nawapenda.

Ibada za sanamu na ibada za kweli
1Sikilizeni neno analowaambieni Mwenyezi-Mungu,
enyi Waisraeli!
2Mwenyezi-Mungu asema hivi:
“Msijifunze mienendo ya mataifa mengine,
wala msishangazwe na ishara za mbinguni;
yaacheni mataifa mengine yashangazwe nazo.
3Maana, mila za dini za watu hawa ni za uongo.
Mtu hukata mti msituni
fundi akachonga kinyago cha mungu kwa shoka.
4Kisha watu hukipamba kwa fedha na dhahabu
wakakipigilia misumari kwa nyundo
ili kisije kikaanguka.
5Vinyago vyao ni kama vinyago vya kutishia ndege
katika shamba la matango,
havina uwezo wa kuongea;
ni lazima vibebwe
maana haviwezi kutembea.
Msiviogope vinyago hivyo,
maana haviwezi kudhuru,
wala haviwezi kutenda lolote jema.”
6Ee Mwenyezi-Mungu, hakuna aliye kama wewe;
wewe ni mkuu na nguvu yako yajulikana.
7Nani asiyekuogopa wewe, ee mfalme wa mataifa?
Wewe wastahili kuheshimiwa.
Miongoni mwa wenye hekima wote wa mataifa,
na katika falme zao zote,
hakuna hata mmoja aliye kama wewe.
8Wote ni wajinga na wapumbavu
mafunzo ya vinyago ni upuuzi mtupu!
9Vinyago hivyo hupambwa kwa fedha kutoka Tarshishi,
na dhahabu kutoka Ofiri;
kazi ya mafundi stadi na wafua dhahabu.
Zimevishwa nguo za samawati na zambarau,
zilizofumwa na wafumaji stadi.
10Lakini Mwenyezi-Mungu ni Mungu wa kweli;
Mungu aliye hai, mfalme wa milele.
Akikasirika, dunia hutetemeka,
mataifa hayawezi kustahimili hasira yake.
11Basi, utawaambia hivi: “Miungu ambayo haikuumba mbingu na dunia, itaangamia. Itatoweka kabisa duniani na chini ya mbingu.”
Wimbo wa kumsifu Mungu
12Mwenyezi-Mungu aliiumba dunia kwa nguvu zake;
kwa hekima yake aliuimarisha ulimwengu,
kwa akili yake alizitandaza mbingu.
13Anapotoa sauti yake, maji hunguruma mbinguni,
huzusha ukungu kutoka mipaka ya dunia.
Huufanya umeme umulike wakati wa mvua,
na kuutoa upepo katika ghala zake.
14Binadamu ni mjinga na mpumbavu;
kila mfua dhahabu huaibishwa na vinyago vyake;
maana, vinyago hivyo ni uongo mtupu.
Havina uhai wowote ndani yao.
15Havina thamani, ni udanganyifu mtupu;
wakati vitakapoadhibiwa vyote vitaangamia.
16Lakini Mungu wa Yakobo si kama vinyago hivyo,
maana, yeye ndiye aliyeumba vitu vyote,
na Israeli ni taifa lililo mali yake;
Mwenyezi-Mungu wa majeshi ndilo jina lake.
Uhamisho unakaribia
17Kusanyeni vitu vyenu enyi watu mliozingirwa.
18Maana Mwenyezi-Mungu asema hivi:
“Wakati huo nitawatupa nje ya nchi hii,
nitawataabisha asibaki mtu yeyote.”
19Ole wangu mimi Yerusalemu maana nimejeruhiwa!
Jeraha langu ni baya sana!
Lakini nilisema: “Hakika haya ni mateso,
na sina budi kuyavumilia.”
20Lakini hema langu limebomolewa,
kamba zake zote zimekatika;
watoto wangu wameniacha, na kwenda zao,
wala hawapo tena;
hakuna wa kunisimikia tena hema langu,
wala wa kunitundikia mapazia yangu.
21Nami Yeremia nikasema:
Wachungaji wamekuwa wajinga,
hawakuomba shauri kwa Mwenyezi-Mungu;
kwa sababu hiyo, hawakufanikiwa,
na kondoo wao wote wametawanyika.
22Sikilizeni sauti! Habari zinatufikia.
Kuna kishindo kutoka kaskazini.
Taifa kutoka kaskazini linakuja,
kuifanya miji ya Yuda kuwa jangwa
ambamo kutakuwa na mapango ya mbweha!
23Najua, ee Mwenyezi-Mungu,
binadamu hana uwezo na maisha yake;
hakuna mtu awezaye kuyaongoza maisha yake.
24Utukosoe, ee Mwenyezi-Mungu, lakini si kwa ghadhabu,
wala kwa hasira yako, tusije tukaangamia.
25Imwage hasira yako juu ya mataifa yasiyokuabudu,
na juu ya watu ambao hawakutambui.
Maana, wamewaua wazawa wa Yakobo;
wamewaua na kuwaangamiza kabisa,
na nchi yao wameiacha magofu.


Yeremia10;1-25

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: