Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Wednesday 5 February 2020

Kikombe Cha Asubuhi; Yeremia 48....


Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu katika yote....

Mungu wetu Baba yetu,Muumba wetu Muumba wa Mbingu na Nchi
Muumba wa vyote vilivyomo vinavyoonekana na visivyoonekana
Mungu wa walio hai,Mungu  mwenye huruma,Mungu wa upendo
Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo...
Asante kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwatayari kwa majukumu yetu

Neema yako yatutosha ee Mungu wetu....!!

Kisha Yesu akasema kwa sauti kubwa, “Mtu anayeniamini, haniamini mimi tu, ila anamwamini pia yule aliyenituma. Anayeniona mimi anamwona pia yule aliyenituma.
Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote 
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba ukatupe neema
ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea
Usitutie majaribuni Mungu wetu tunaomba utuepushe
na yule mwovu na kazi zake zote
Jehovah ututakase miili yetu na akili zetu
Baba wa Mbinguni tunaomba utufunike kwa Damu
ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti
yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona....


Mimi ni mwanga, nami nimekuja ulimwenguni ili wote wanaoniamini wasibaki gizani. Anayeyasikia maneno yangu lakini hayashiki, mimi sitamhukumu; maana sikuja kuuhukumu ulimwengu bali kuuokoa. Asiyeyashika maneno yangu anaye wa kumhukumu: Neno lile nililosema ni hakimu wake siku ya mwisho.
Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa katika utendaji
Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Yahweh tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomna ukatupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji
Tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe kama inavyokupendeza wewe...


Yahweh tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyovimiliki
Yahweh tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia
Baba wa Mbinguni tukawe salama rohoni
Yahwe ukatupe akili ya kutambua mema na mabaya
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu ukatupe macho ya kuona,masikio ya kusikia sauti yako na kuitii..
Baba wa Mbinguni  tunaomba ukatupe neema ya kufuata
njia zako,tukasimamie Neno lako,amri na sheria zako
siku zote za maisha yetu...
Ukatuguse kwa mkono wako wenye nguvu,ukatufanye chombo chema
ee Mungu wetu nasi tukatumike kama inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi....


Mimi sikunena kwa mamlaka yangu mwenyewe, ila Baba aliyenituma ndiye aliyeniamuru niseme nini na niongee nini. Nami najua kuwa amri yake huleta uhai wa milele. Basi, mimi nasema tu yale Baba aliyoniagiza niyaseme.”
Tazama watoto wako wenye shida/tabu,wote wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali
Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu
kila mmoja na mahitaji yake
Mungu wetu tunaomba ukawasamehe pale walipo kwenda kinyume nawe
Yahweh tunaomba ukawape neema ya kuweza kujiombea,kufuata njia zako nazo zikawaweke huru...
Baba wa Mbinguni tunayaweka haya yote mikononi mwako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele...
Amina...!!


Asanteni sana wapendwa katika Kristo Yesu kwakuwa nami,Baba wa Mbinguni aendelee kuwatendea sawasawa na mapenzi yake...
Nawapenda.

Moabu
1Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi:
“Ole watu wa Nebo, maana mji wake umeharibiwa!
Kiriathaimu umeaibishwa, umetekwa,
ngome yake imebomolewa mbali;
2fahari ya Moabu imetoweka.
Mpango ulifanywa huko Heshboni dhidi yake:
‘Haya! Tuwaangamize wasiwe tena taifa!’
Nawe Madmeni utanyamazishwa,
upanga utakufuatia.
3Sikiliza! Kilio kutoka Horonaimu:
‘Maangamizi na uharibifu mkubwa!’
4Moabu tayari imeangamizwa
kilio chake chasikika mpaka Soari.
5Walionusurika wanapanda kwenda Luhithi
huku wanalia kwa sauti.
Wanapoteremka kwenda Horonaimu,
wanasikia kilio cha uharibifu.
6Kimbieni! Jiokoeni wenyewe!
Kimbieni kama pundamwitu jangwani!
7“Moabu, ulitumainia ngome na hazina zako,
lakini sasa wewe pia utatekwa;
mungu wako Kemoshi atapelekwa uhamishoni
pamoja na makuhani na watumishi wake.
8Mwangamizi atapita katika kila mji,
hakuna mji utakaomwepa;
kila kitu mabondeni kitaangamia
nyanda za juu zitaharibiwa,
kama alivyosema Mwenyezi-Mungu.
9Mchimbieni Moabu kaburi,
maana kuangamia kwake ni hakika;
miji yake itakuwa tupu,
bila mkazi hata mmoja.
10Na alaaniwe mtu afanyaye kazi ya Mwenyezi-Mungu kwa ulegevu; alaaniwe anayezuia upanga wake usimwage damu!
11Moabu amestarehe tangu ujana wake,
ametulia kama divai katika gudulia.
Hajamiminiwa toka chombo hata chombo,
hajapata kuchukuliwa uhamishoni.
Kwa hiyo yungali na ladha yake,
harufu yake nzuri haijabadilika kamwe.
12“Kwa hiyo, wakati waja, nasema mimi Mwenyezi-Mungu ambapo nitampelekea wamiminaji ambao wataimimina divai yake. Wataimwaga yote kutoka vyombo vyake na kuvivunja vipandevipande. 13Hapo Wamoabu watamwonea aibu mungu wao Kemoshi, kama vile watu wa Israeli walivyomwonea aibu Betheli, mungu waliyemtegemea.
14Mwawezaje kusema: ‘Sisi ni mashujaa,
na watu wenye nguvu nyingi za vita?’
15Mwangamizi wa Moabu na miji yake amewasili
vijana wake wazuri wamechinjwa.
Nimesema mimi mfalme
niitwaye Mwenyezi-Mungu wa Majeshi.
16Janga la Moabu limekaribia,
maangamizi yake yanawasili haraka.
17Mwomboleezeni Moabu, enyi jirani zake wote,
na nyote mnaomjua vizuri
semeni: ‘Jinsi gani fimbo ya nguvu ilivyovunjwa,
naam fimbo ile ya fahari!’
18Enyi wenyeji wa Diboni:
Shukeni kutoka mahali penu pa fahari,
mkaketi katika ardhi isiyo na maji.
Maana mwangamizi wa Moabu,
amefika kuwashambulia;
amekwisha haribu ngome zenu.
19Enyi wakazi wa Aroeri,
simameni kando ya njia mtazame!
Mwulizeni anayekimbia na anayetoroka:
‘Kumetokea nini?’
20Moabu imeaibishwa maana imevunjwa;
ombolezeni na kulia.
Tangazeni kando ya mto Arnoni,
kwamba Moabu imeharibiwa kabisa.
21“Hukumu imeifikia miji iliyo nyanda za juu: Holoni, Yasa, Mefaathi, 22Diboni, Nebo, Beth-diblathaimu, 23Kiriathaimu, Beth-gamuli, Beth-meoni, 24Keriothi na Bosra. Naam, hukumu imeifikia miji yote ya Moabu mbali na karibu. 25Nguvu za Moabu zimevunjiliwa mbali na uwezo wake umevunjwa. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
26“Mlewesheni Moabu kwa sababu alijikuza dhidi yangu mimi Mwenyezi-Mungu. Moabu atagaagaa katika matapishi yake na watu watamcheka. 27Kumbuka Moabu ulivyomcheka Israeli. Je, alikamatwa pamoja na wezi, hata ukawa unatikisa kichwa chako kila ulipoongea juu yake?
28“Enyi wenyeji wa Moabu,
tokeni mijini, mkakae mapangoni!
Mwigeni njiwa ajengaye kiota penye genge.
29Tumesikia juu ya kiburi cha Moabu;
Moabu ana majivuno sana.
Tumesikia juu ya kujiona, kiburi na majivuno yake;
tumesikia jinsi anavyojigamba moyoni.
30“Nami Mwenyezi-Mungu nasema:
Najua ufidhuli wake;
Majivuno yake ni ya bure,
na matendo yake si kitu.
31Kwa hiyo ninaomboleza juu ya Moabu,
ninalia kwa ajili ya Wamoabu wote,
naomboleza juu ya watu wa Kir-heresi.
32Nakulilia wewe bustani ya Sibma
kuliko hata watu wa Yazeri.
Matawi yako yametanda
mpaka ngambo ya bahari ya Chumvi
yakafika hata mpaka Yazeri.
Lakini mwangamizi ameyakumba
matunda yako ya kiangazi na zabibu zako.
33Furaha na shangwe zimeondolewa
kutoka nchi ya Moabu yenye rutuba.
Nimeikomesha divai kutoka mashinikizo
hakuna mtu anayekamua zabibu kwa shangwe;
kelele zinazosikika si za shangwe.
34“Kilio cha watu wa Heshboni chasikika huko Eleale mpaka Yahazi; kinaenea kutoka Soari mpaka Horonaimu na hata Eglath-shelishiya. Hata maji ya kijito Nimrimu yamekauka. 35Nami nitamfutilia mbali kila mtu katika Moabu ambaye anatambikia vilimani na kumfukizia ubani mungu wake.
36“Kwa hiyo, moyo wangu unaomboleza juu ya watu wa Moabu na watu wa Kir-heresi, kama mpiga zumari mazishini; maana hata mali yote waliyojipatia imeangamia. 37Kila mtu amenyoa upara na ndevu zake. Wote wamejikatakata mikononi na viunoni wamevaa mavazi ya gunia. 38Juu ya nyumba za Moabu na katika viwanja vyao hakuna kinachosikika ila tu maombolezo. Mimi nimemvunja Moabu kama chombo kisichotakiwa na mtu. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema. 39Tazama alivyovunjika! Tazama wanavyoomboleza! Ajabu jinsi Moabu alivyorudi nyuma kwa aibu! Moabu amekuwa kichekesho na kioja kwa jirani zake wote.”
40Mwenyezi-Mungu asema hivi:
“Tazama, taifa litaruka kasi kuivamia Moabu,
kama tai aliyekunjua mabawa yake.
41Miji yake itatekwa,
ngome zitachukuliwa.
Siku hiyo mioyo ya wanajeshi wa Moabu,
itaogopa kama mwanamke anayejifungua.
42Wamoabu wataangamizwa, wasiwe tena taifa,
kwa sababu walijikweza dhidi ya Mwenyezi-Mungu.
43Kitisho, mashimo na mtego,
vinawasubiri enyi watu wa Moabu.
Nasema mimi Mwenyezi-Mungu.
44Atakayetoroka kitisho
atatumbukia shimoni;
atakayetoka shimoni
atanaswa mtegoni.
Kwa maana nitaleta mambo hayo juu ya Moabu,
katika mwaka wao wa adhabu.
Nasema mimi Mwenyezi-Mungu.
45Wakimbizi wachovu wanatua Heshboni kutaka usalama,
maana moto umezuka huko mjini;
mwali wa moto toka ikulu ya mfalme Sihoni;
umeteketeza mipaka48:45 mipaka: Kiebrania: Uso. ya Moabu,
umeunguza milima48:45 milima: Kiebrania: Utosi. yao hao watukutu.
46Ole wenu watu wa Moabu!
Watu wa Kemoshi sasa mmeangamizwa,
wana wenu wamechukuliwa mateka,
binti zenu wamepelekwa uhamishoni.
47Lakini siku zijazo
nitamstawisha tena Moabu.
Nasema mimi Mwenyezi-Mungu.
Hii ndiyo hukumu juu ya Moabu.”


Yeremia48;1-47

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: