Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Monday 3 February 2020

Kikombe Cha Asubuhi; Yeremia 46....


Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Haleluyah ni siku/wiki/mwezi mwingine tena Mungu wetu ametuchagua

na kutupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Si kwamba sisi tumetenda mema sana wala si kwa nguvu zetu
si kwa utashi wetu wala si kwa akili zetu si kwamba sisi
ni wazuri mno si kwa uwezo wetu sisi kuwa hivi tulivyo leo hii
Ni kwa rehema/neema zake ni kwa mapenzi yake Mungu wetu....

Tumshukuru Mungu wetu katika yote...

Asante Mungu wetu kwa wema na fadhili zako kwetu

Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwa tayari kwa majukumu yetu
Sifa na Utukufu tunakurudshia Mungu wetu....!!


“Sasa roho yangu imefadhaika, na niseme nini? Je, niseme: ‘Baba, usiruhusu saa hii inifikie?’ Lakini ndiyo maana nimekuja – ili nipite katika saa hii. Baba, ulitukuze jina lako.” Hapo sauti ikasema kutoka mbinguni, “Nimelitukuza, na nitalitukuza tena.”
Tazama jana imepita ee Mungu wetu leo ni siku mpya na kesho ni siku nyingine Jehovah tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako
 Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizozifanya kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea
Jehovah usitutie majaribu Mungu wetu tunaomba utuepushe na yule mwovu na kazi zake zote
Yahweh tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu
Baba wa Mbinguni utufunike kwa Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti
yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona
Kwakupigwa kwake sisi tumepata kupona....

Umati wa watu waliokuwa wamesimama hapo walisikia sauti hiyo, na baadhi yao walisema, “Ni ngurumo.” Lakini wengine wakasema, “Malaika ameongea naye!” Lakini Yesu akawaambia, “Sauti hiyo haikutokea kwa ajili yangu mimi, ila kwa ajili yenu. Sasa ndio wakati wa ulimwengu huu kuhukumiwa; sasa mtawala wa ulimwengu huu atapinduliwa. Nami nitakapoinuliwa juu ya nchi nitamvuta kila mmoja kwangu.” (Kwa kusema hivyo alionesha atakufa kifo gani).
Yahweh tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa 
katika utendaji
Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki ridhiki zetu
ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba ukatupe neema ya kuweza
kuwabariki wenye kuhitaji
Yahweh tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Mungu wetu ukatupe kama inavyokupendeza wewe

Baba wa Mbinguni tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyo vimiliki
Yahweh tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia
Baba wa Mbinguni tukawe salama rohoni
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia 
sauti yako na kuitii
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe neema ya kufuata njia zako
Yahweh tukasimamie Neno lako amri na sheria zako siku zote 
za maisha yetu
Mungu wetu ukaonekane katika maisha yetu
Neema zako zikawe nasi Nuru yako ikaangaze katika maisha yetu
ukatuguse kwa mkono wako wenye nguvu
Ukatufanye chombo chema ee Mungu wetu nasi tukatumike kama
inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi...


Basi, umati huo ukamjibu, “Sisi tunaambiwa na sheria yetu kwamba Kristo atadumu milele. Wawezaje basi, kusema ati Mwana wa Mtu anapaswa kuinuliwa? Huyo Mwana wa Mtu ni nani?” Yesu akawaambia, “Mwanga bado uko nanyi kwa muda mfupi. Tembeeni mngali mnao huo mwanga ili giza lisiwapate; maana atembeaye gizani hajui aendako. Basi, wakati mnao huo mwanga uaminini ili mpate kuwa watu wa mwanga.” Baada ya kusema maneno hayo, Yesu alikwenda zake na kujificha mbali nao.
Mungu wetu tunawaweka mikononi mwako wenye shida/tabu,wote wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali
Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu
 kila mmoja na mahitaji yake 
Mungu wetu tunaomba ukawasamehe pale walipokwenda kinyume nawe
Baba wa Mbinguni ukawape neema ya kujiombea,kufuata njia zako
wakasimamie Neno lako nalo likaweke huru
Mungu wetu tunaomba ukasikie kuomba kwetu
Mungu wetu ukawatendee sawasawa na mapenzi yako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina...!!

Asanteni sana wapendwa katika Kristo Yesu kwakuwa nami
Mungu Baba aendelee kuwabariki na kuwatendea 
kama inavyompendeza yeye....
Nawapenda.


1Neno la Mwenyezi-Mungu lililomjia Yeremia kuhusu watu wa mataifa.
Tamko la Mwenyezi-Mungu juu ya Misri
2Kuhusu Misri na jeshi la Farao Neko mfalme wa Misri, lililokuwa huko Karkemishi karibu na mto Eufrate ambalo Nebukadneza mfalme wa Babuloni alilishambulia mnamo mwaka wa nne wa utawala wa Yehoyakimu mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda:
3Tayarisheni ngao ndogo na kubwa
msonge mbele kupigana vita.
4Tandikeni farasi na kuwapanda,
Shikeni nafasi zenu na kofia za chuma mvae.
Noeni mikuki yenu,
vaeni mavazi yenu ya chuma!
5Lakini mbona nawaona wametishwa?
Wamerudi nyuma.
Mashujaa wao wamepigwa,
wamekimbia mbio,
bila hata kugeuka nyuma.
Kitisho kila upande.
Mwenyezi-Mungu amesema.
6Walio wepesi kutoroka hawawezi,
mashujaa hawawezi kukwepa;
huko kaskazini kwenye mto Eufrate
wamejikwaa na kuanguka.
7Nani huyo aliye kama mto Nili uliofurika
kama mito inayoumuka mawimbi?
8Misri ni kama mto Nili uliofurika
kama mito inayoumuka mawimbi
Ilisema: “Nitajaa, nitaifunika nchi,
nitaiharibu miji na wakazi wake.
9Songeni mbele, enyi farasi,
shambulieni enyi magari ya farasi.
Mashujaa wasonge mbele:
Watu wa Kushi na Puti washikao ngao,
watu wa Ludi, stadi wa kutumia pinde.”
10Siku hiyo ni siku ya Mwenyezi-Mungu wa majeshi,
ni siku ya kulipiza kisasi;
naam, siku ya kuwaadhibu maadui zake.
Upanga utawamaliza hao na kutosheka,
utainywa damu yao na kushiba.
Maana Mwenyezi-Mungu wa majeshi anayo kafara
huko kaskazini karibu na mto Eufrate.
11Pandeni Gileadi, enyi watu wa Misri,
mkachukue dawa ya marhamu.
Mmetumia dawa nyingi bure;
hakuna kitakachowaponya nyinyi.
12Mataifa yamesikia aibu yenu,
kilio chenu kimeenea duniani kote;
mashujaa wamegongana wenyewe kwa wenyewe,
wote pamoja wameanguka.
Misri inavamiwa
13Neno ambalo Mwenyezi-Mungu alimwambia Yeremia wakati alipofika Nebukadneza mfalme wa Babuloni kuishambulia nchi ya Misri:
14“Tangaza nchini Misri,
piga mbiu huko Migdoli,
tangaza huko Memfisi na Tahpanesi.
Waambie: ‘Kaeni tayari kabisa
maana upanga utawaangamiza kila mahali.’
15Kwa nini shujaa wako amekimbia?
Mbona fahali wako hakuweza kustahimili?
Kwa sababu mimi Mwenyezi-Mungu nilimwangusha chini!
16Wengi walijikwaa, wakaanguka,
kisha wakaambiana wao kwa wao:
‘Simameni, tuwaendee watu wetu,
turudi katika nchi yetu,
tuukimbie upanga wa adui.’
17“Naye Farao, mfalme wa Misri, mpangeni jina hili:
‘Kishindo kitupu!’
18Mimi naapa kwa uhai wangu
nasema mimi mfalme niitwaye Mwenyezi-Mungu wa majeshi,
kweli adui anakuja kuwashambulieni:
Ni hakika kama Tabori ulivyo mlima
kama mlima Karmeli uonekanavyo kutoka baharini.
19Enyi wakazi wa Misri
jitayarisheni na mizigo kwenda uhamishoni!
Maana mji wa Memfisi utaharibiwa kabisa,
utakuwa magofu yasiyokaliwa na watu.
20Misri ni kama mtamba mzuri wa ng'ombe,
lakini kipanga kutoka kaskazini amemvamia.
21Hata askari wake wa kukodiwa ni kama ndama wanono;
nao pia wamegeuka, wakakimbia pamoja,
wala hawakuweza kustahimili,
kwa maana siku yao ya kuangamizwa imefika,
wakati wao wa kuadhibiwa umewadia.
22Misri anatoa sauti kama nyoka anayekimbia;
maana maadui zake wanamjia kwa nguvu,
wanamjia kwa mashoka kama wakata-miti.
23Wataukata kabisa msitu wake, ingawa haupenyeki,
nasema mimi Mwenyezi-Mungu,
maana wao ni wengi kuliko nzige wasiohesabika.
24Watu wa Misri wataaibishwa,
watatiwa mikononi mwa watu kutoka kaskazini.”
25Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, alisema: “Tazama, mimi nitamwadhibu Amoni mungu wa Thebesi, nitaiadhibu Misri na miungu yake na wafalme wake, nitamwadhibu Farao na wote wanaomtegemea. 26Nitawatia mikononi mwa wale wanaotaka kuyaangamiza maisha yao, yaani Nebukadneza mfalme wa Babuloni na maofisa wake. Baadaye, nchi ya Misri itakaliwa na watu kama ilivyokuwa hapo zamani. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
Mwenyezi-Mungu atawaokoa watu wake
27“Lakini wewe usiogope, ee Yakobo mtumishi wangu,
usifadhaike, ee Israeli;
maana, kutoka mbali nitakuokoa,
nitakuja kuwaokoa wazawa wako
kutoka nchi walimohamishwa.
Yakobo utarudi na kutulia na kustarehe,
wala hakuna yeyote atakayekutia hofu.
28Usiogope, ee Yakobo mtumishi wangu,
kwa maana mimi niko pamoja nawe.
Nitayaangamiza kabisa mataifa yote
ambayo nimekutawanya kati yao,
lakini wewe sitakuangamiza.
Nitakuchapa kadiri unavyostahili,
sitakuacha bila kukuadhibu.”

Yeremia46;1-28

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: