Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Thursday 27 February 2020

Kikombe Cha Asubuhi; Ezekieli 7...


Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu katika yote...

Asante  Mungu wetu kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwatayari kwa majukumu yetu


Utukuzwe ee Mungu wetu,usifiwe Baba wa Mbinguni

Neema yako yatutosha  Mungu wetu..!

Maandiko Matakatifu yasema: “Kila anayemwamini hataaibishwa.” Jambo hili ni kwa wote, kwani hakuna tofauti kati ya Wayahudi na wasio Wayahudi; Bwana wa wote ni mmoja, naye ni mkarimu sana kwao wote wamwombao. Maana Maandiko Matakatifu yasema: “Kila mtu atakayeomba kwa jina la Bwana, ataokolewa.”
Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,
tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako

Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea,Usitutie majaribuni Mungu wetu tunaomba utuepushe na yule mwovu na kazi zake zote,Jehovah ututakase miili yetu na akili zetu Baba wa Mbinguni tunaomba utufunike kwa  Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti,
Yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona....


Basi, watamwombaje yeye ambaye hawamwamini? Tena, watamwaminije kama hawajapata kusikia habari zake? Na watasikiaje habari zake kama hakuna mhubiri?
Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa 
katika utendaji
Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki ridhiki zetu
ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba ukatupe neema ya kuweza
kuwabariki wenye kuhitaji
Yahweh tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Mungu wetu ukatupe kama inavyokupendeza wewe



Jehovah tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyo vimiliki
Yahweh tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia
Baba wa Mbinguni tukawe salama rohoni
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia 
sauti yako na kuitii
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe neema ya kufuata njia zako
Yahweh tukasimamie Neno lako amri na sheria zako siku zote 
za maisha yetu

Mungu  wetu ukaonekane katika maisha yetu popote tupitapo na ikajulikane kwamba upo 

Neema zako zikawe nasi Nuru yako ikaangaze katika maisha yetu
Ukatufanye barua njema ee Mungu wetu nasi tukasomeke kama
inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi...

Na watu watahubirije kama hawakutumwa? Kama yasemavyo Maandiko Matakatifu: “Ni jambo la kupendeza mno kuja kwa wale wanaohubiri Habari Njema!”
Tazama wenye shida/tabu,Mungu wetu tunaomba
 ukawaguse kila mmoja na mahitaji yake
Baba wa Mbinguni tunaomba ukawasamehe pale walipokwenda
kinyume nawe
Mungu wetu ukawape neema ya kujiombea,macho ya rohoni,masikio yakusikia sauti yako,wakafuate njia zako nazo zikawaweke huru
Mungu wetu tunaomba ukasikie kulia kwao
Baba wa Mbinguni tunomba ukawafute machozi yao
Nuru yako ikaangaze katika maisha yao
Mungu wetu tunaomba ukawatendee sawasawa na mapenzi yako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina....!!!


Wapendwa katika Kristo Yesu asanteni sana
kwakuwanami/kunisoma

Mungu Baba aendelee kuwabariki na kuwatendea
kama inavyompendeza yeye
Amani ya Bwana wetu Yesu Kristo na upendo wa Mungu Baba
ukae nanyi daima....

Nawapenda.

Mwisho wa Israeli ni karibu
1Neno la Mwenyezi-Mungu lilinijia: 2“Wewe mtu, waambie wakazi wa nchi ya Israeli kuwa mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi:
Sasa ni mwisho!
Mwisho umeifikia nchi yote kutoka pande zote nne!
3Sasa mwisho umewafikia;
sasa mtausikia ukali wa hasira yangu juu yenu.
Nitawahukumu kadiri ya mwenendo wenu.
Nitawaadhibu kwa machukizo yenu yote.
4Sitawaachia wala sitawahurumia;
nitawaadhibu kulingana na mienendo yenu,
maadamu machukizo bado yapo kati yenu.
Ndipo mtakapotambua kuwa mimi ni Mwenyezi-Mungu.
5Ninachosema mimi Bwana Mwenyezi-Mungu ni hiki:
Mtapatwa na maafa mfululizo!
6Mwisho umekuja!
Naam, mwisho umefika!
Umewafikia nyinyi!
7Enyi wakazi wa nchi hii, maangamizi yenu yamewajia!
Wakati umekuja;
naam, siku imekaribia.
Hiyo ni siku ya msukosuko
na siyo ya sauti za shangwe mlimani.7:7 aya ya 7 maana yake katika Kiebrania si dhahiri.
8Sasa mtausikia uzito wa hasira yangu juu yenu.
Nitawahukumu kulingana na mwenendo wenu;
nitawaadhibu kadiri ya machukizo yenu.
9Sitawaachilia wala sitawaonea huruma.
Nitawaadhibu kulingana na mienendo yenu
maadamu machukizo yapo bado miongoni mwenu.
Ndipo mtakapotambua kuwa ni mimi Mwenyezi-Mungu ninayewaangamiza.
10“Tazameni, siku ile inakuja!
Maangamizi yenu yamekuja.
Ukatili uko kila mahali na kiburi kimechanua.
11Ukatili unaendelea kuwa mbaya zaidi.
Hakuna hata mmoja wenu atakayebaki,
wala vitu mlivyojirundikia kwa wingi au utajiri wenu;
hatakuwako mtu mwenye heshima miongoni mwenu.
12Wakati umewadia,
naam, ile siku imekaribia.
Mnunuzi asifurahi wala mwuzaji asiomboleze;
kwa sababu ghadhabu yangu itaukumba umati wote.
13Wauzaji hawataweza kurudia mali yao waliyouza
hata kama wakibaki hai.
Kwani maono haya yahusu umati wote na hayatabatilishwa.
Kutokana na uovu huo, hakuna mtu atakayesalimisha maisha yake.
14Tarumbeta imepigwa na kuwafanya wote wawe tayari.
Lakini hakuna anayekwenda vitani,
kwani ghadhabu yangu iko juu ya umati wote.
15Nje kuna kifo kwa upanga
na ndani ya mji kuna maradhi mabaya na njaa.
Walioko shambani watakufa kwa upanga;
walio mjini njaa na maradhi mabaya yatawaangamiza.
16Wakiwapo watu watakaosalimika
watakimbilia milimani kama hua waliotishwa bondeni.
Kila mmoja wao ataomboleza kwa dhambi zake.
17Kila mtu, mikono yake itakuwa dhaifu
na magoti yake yatakuwa maji.
18Watavaa mavazi ya gunia,
hofu itawashika,
nao watakuwa na aibu,
vichwa vyao vyote vitanyolewa.
19Watatupa fedha yao barabarani
na dhahabu yao itakuwa kama kitu najisi.
Fedha na dhahabu zao hazitaweza kuwaokoa
katika siku hiyo ya ghadhabu ya Mwenyezi-Mungu;
wala hawataweza kushiba
au kuyajaza matumbo yao fedha na dhahabu waliyojirundikia;
kwani mali hiyo ndiyo chanzo cha dhambi yao.
20Kwa kuwa walijifanyia utukufu usio na maana kwa njia ya vikuku,
wakajifanyia sanamu za miungu zinazochukiza
pamoja na vitu vyao vya aibu;
vyote hivyo nitavifanya kuwa najisi kwao.
21Utajiri wao nitautia mikononi mwa mataifa mengine,
watu waovu wa dunia watauteka na kuutia najisi.
22Uso wangu nitaugeuzia mbali nao
ili walitie najisi hekalu langu.
Wanyanganyi wataingia humo ndani na kulitia najisi.
23Tengeneza mnyororo.
Kwa kuwa nchi imejaa makosa ya jinai ya umwagaji damu
na mji umejaa dhuluma kupindukia,
24nitayaleta mataifa mabaya sana
nao watazimiliki nyumba zao. Kiburi chao nitakikomesha,
na mahali pao pa ibada patatiwa unajisi.
25Uchungu mkali utakapowajia,
watatafuta amani, lakini haitapatikana.
26Watapata maafa mfululizo;
nazo habari mbaya zitafuatana.
Watamwomba nabii maono.
Makuhani hawatakuwa na sheria yoyote;
na wazee watakosa shauri la kuwapatia.
27Mfalme ataomboleza,
mkuu atakata tamaa
na watu watatetemeka kwa hofu.
Nitawatenda kadiri ya mienendo yao,
nitawahukumu kama nilivyowahukumu wengine.
Ndipo watakapotambua kuwa mimi ni Mwenyezi-Mungu.”


Ezekieli7;1-27

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: