Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Tuesday 6 November 2018

Kikombe Cha Asubuhi ;Yobu 31...


Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu katika yote....

Mungu wetu Baba yetu,Muumba wetu Muumba wa Mbingu na Nchi
Muumba wa vyote vilivyomo vinavyoonekana na visivyoonekana
Mungu wa walio hai,Mungu  mwenye huruma,Mungu wa upendo
Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo..
Yahweh..!Jehovah..! Adonai..!Elohim..!El Olam..!El Qanna..!
El Elyon..!El shaddai..!Emanueli...!-Mungu pamoja nasi...
Unastahili sifa Mungu wetu,Unastahili kuabudiwa Jehovah,
Unastahili kuhimidiwa Yahweh,Unastahili Kutukuzwa Baba wa Mbinguni....!



Asante kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwatayari kwa majukumu yetu

Neema yako yatutosha ee Mungu wetu....!!

Basi, ikiwa mmefufuka pamoja na Kristo, panieni mambo ya juu, kule Kristo aliko, ameketi upande wa kulia wa Mungu. Muwe na hamu ya mambo ya huko juu, na siyo mambo ya hapa duniani. Maana nyinyi mmekufa na uhai wenu umefichwa pamoja na Kristo katika Mungu. Uhai wenu halisi ni Kristo, na wakati atakapotokea ndipo nanyi pia mtakapotokea pamoja naye katika utukufu.

Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizo zifanya
Kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba ukatupe neema
ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea
Usitutie majaribu Mungu wetu tunaomba utuepushe
na yule mwovu na kazi zake zote
Jehovah ututakase miili yetu na akili zetu
Baba wa Mbinguni tunaomba utufunike kwa Damu
ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazaretiyeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona....


Basi, ueni chochote kilicho ndani yenu ambacho ni cha kidunia: Uasherati, uchafu, shauku, tamaa mbaya na uchu (ambao ni sawa na kuabudu sanamu). Kwa sababu ya mambo hayo hasira ya Mungu huwajia wote wanaomwasi. Wakati mmoja nyinyi pia mliishi kufuatana na mambo hayo, mlipotawaliwa nayo. Lakini sasa mnapaswa kuachana na mambo haya yote: Hasira, tamaa na uovu; kufuru au maneno yasiyofaa yasitoke kamwe vinywani mwenu. Msiambiane uongo, kwani nyinyi mmekwisha vua ule utu wa kale pamoja na matendo yake yote, mkavaa utu mpya. Huu unaendelea kurekebishwa na Mungu, Muumba wake, kadiri ya mfano wake, ili mpate kumjua Mungu kwa ukamilifu.

Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa katika utendaji

Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Yahweh tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba ukatupe neema ya kuweza
kuwabariki wenye kuhitaji
Tusipungukiwe katika mahitaji yetu Baba wa Mbinguni
tunaomba ukatupe kama inavyokupendeza wewe....



Yahweh  tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyo vimiliki
Yahweh tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia
Baba wa Mbinguni tukawe salama rohoni

Yahweh ukatupe akili ya kutambua mema na mabaya
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia 
sauti yako na kuitii
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe neema ya kufuata njia zako
Yahweh tukasimamie Neno lako amri na sheria zako siku zote 
za maisha yetu
Mungu wetu ukaonekane katika maisha yetu
Baba wa Mbinguni tukanene yaliyo yako
Neema zako zikawe nasi Nuru yako ikaangaze katika maisha yetu
ukatuguse kwa mkono wako wenye nguvu
Ukatufanye chombo chema ee Mungu wetu nasi tukatumike kama
inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi...



Katika hali hii, hakuna tena tofauti kati ya Mgiriki na Myahudi, aliyetahiriwa na asiyetahiriwa, msomi na asiye msomi, mtumwa na mtu aliye huru. Kristo ni kila kitu, na yumo katika yote.

Tazama watoto wako wanaokutafuta/kukuomba kwa bidii na imani, Mungu wetu tunawaweka mikononi mwako wenye shida/tabu,
wote wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali
Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu
kila mmoja na mahitaji yake
Baba wa Mbinguni tunaomba ukaonekane katika maisha yao
Mungu wetu tunaomba ukawasamehe pale walipokwenda
kinyume nawe Yahweh tunaomba ukawape neema ya kujiombea
Kufuata njia zako nazo zikawaweke huru
Ukawape macho ya rohoni ee Mungu wetu na masikio ya kusikia
sauti yako,Ukawaokoe na kuwalinda,ukawaponye kimwili na kiroho
Nuru yako ikaangaze katika maisha yao,Amani ikatawale katika maisha yao,Upendo ukadumu kati yao
 

Baba wa Mbinguni tunayaweke haya yote mikono mwako
tukiamini Mungu wetu utawatendea sawasawa na mapenzi yako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina...!!



Asanteni sana wapendwa katika Kristo Yesu
kwakuwanami/kunisoma Mungu Baba aendelee
kuwabariki na kuwatendea kama inavyompendeza yeye
Amani ya Bwana wetu Yesu Kristo na Upendo wa Mungu Baba
ukae nanyi daima
Nawapenda. 


1“Nimejifunga rasmi mimi mwenyewe,
macho yangu yasimtazame msichana kwa tamaa.
2Au je, nangojea nini kutoka kwa Mungu aliye juu?
Mungu Mwenye Nguvu ameniwekea kitu gani?
3Je, maafa hayawapati watu waovu
na maangamizi wale watendao mabaya?
4Je, Mungu haoni njia zangu,
na kujua hatua zangu zote?
5“Kama nimeishi kwa kufuata uongo,
kama nimekuwa mbioni kudanganya watu,
6Mungu na anipime katika mizani ya haki,
naye ataona kwamba sina hatia.
7Kama hatua zangu zimepotoka,
moyo wangu ukafuata tamaa za macho yangu;
kama mikono yangu imechafuliwa na dhambi,
8jasho langu na liliwe na mtu mwingine,
mazao yangu shambani na yangolewe.
9“Kama moyo wangu umevutwa kwa mke wa mtu,
kama nimenyemelea mlangoni kwa jirani yangu,
10basi, mke wangu na ampikie mume mwingine,
na wanaume wengine wamtumie.
11Jambo hilo ni kosa kuu la jinai,
uovu ambao hakimu lazima atoe adhabu.
12Kosa langu lingekuwa kama moto,
wa kuniteketeza na kuangamiza,
na kuchoma kabisa mapato yangu yote.
13Kama nimekataa kesi ya mtumishi wangu
wa kiume au wa kike,
waliponiletea malalamiko yao,
14nitafanya nini basi Mungu atakaponikabili?
Je, akinichunguza nitamjibu nini?
15Maana Mungu ndiye aliyeniumba mimi na mtumishi wangu;
yeye ndiye aliyetuumba sisi wote.
16 Taz Yobu 4:7-11,16 “Je, nimepata kumnyima maskini mahitaji yake
au kuwafanya wajane watumaini bure?
17Je, nimekula chakula changu peke yangu,
bila kuwaachia yatima nao wapate chochote?
18La! Tangu ujana wangu nimekuwa mlezi wao,
tangu utoto wangu nimewaongoza wajane.
19Je, nilimwona mtu anakufa kwa kukosa nguo,
au maskini ambaye hana nguo ya kuvaa,
20bila kumpa joto kwa mavazi ya manyoya ya kondoo wangu
naye akanitakia baraka za shukrani ya moyo?
21Kama nimenyosha mkono mahakamani dhidi ya yatima,
nikijua nitapendelewa na mahakimu,
22basi, bega langu na lingoke,
mkono wangu na ukwanyuke kiwikoni mwake.
23Maana maafa kutoka kwa Mungu ni kitisho kwangu;
mimi siwezi kuukabili ukuu wake.
24 Taz Sir 31:5-10 “Je, tumaini langu nimeliweka katika dhahabu,
au, nimeiambia dhahabu safi, ‘Wewe ni usalama wangu?’
25Je, nimepata kufurahia wingi wa utajiri wangu
au kujivunia mapato ya mikono yangu?
26Kama nimeliangalia jua likiangaza,
na mwezi ukipita katika uzuri wake,
27na moyo wangu ukashawishika kuviabudu,
nami nikaibusu mikono yangu kwa heshima yake,
28huo pia ungekuwa uovu wa kuadhibiwa na mahakimu
maana ningekuwa mwongo mbele ya Mungu aliye juu.
29“Je, nimefurahia kuangamia kwa adui yangu,
au kufurahi alipopatwa na maafa?
30La! Sikuruhusu kinywa changu kumtakia mabaya,
kwa kumlaani ili afe.
31Watumishi wangu wote wanasema wazi
kila mgeni amekaribishwa nyumbani mwangu.
32Msafiri hakulala nje ya nyumba yangu,
nilimfungulia mlango mpita njia.
33Je nimeficha makosa yangu kama wengine?
Je nimekataa kukiri dhambi zangu?
34Sijaogopa kusimama mbele ya umati wa watu,
wala kukaa kimya au kujifungia ndani,
eti kwa kuogopa kutishwa na dharau zao.
35Laiti angekuwapo mtu wa kunisikiliza!
Naweza kutia sahihi yangu katika kila nilichosema.
Namwambia Mungu Mwenye Nguvu anijibu!
Laiti mashtaka wanayonitolea maadui zangu yangeandikwa!
36Ningeyavaa kwa maringo mabegani
na kujivisha kichwani kama taji.
37Ningemhesabia Mungu kila kitu nilichofanya,
ningemwendea kama mwana wa mfalme.
38Kama nimeiiba ardhi ninayoilima,
nikasababisha mifereji yake iomboleze,
39kwa kufaidika na mazao yake bila kulipa
na kusababisha kifo cha wenyewe,
40basi miiba na iote humo badala ya ngano,
na magugu badala ya shayiri.”
Mwisho wa hoja za Yobu.



Yobu31;1-40

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: