Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Friday 31 July 2020

Kikombe Cha Asubuhi; Zekaria 9...

Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu katika yote....

Mungu wetu Baba yetu,Muumba wetu Muumba wa Mbingu na Nchi
Muumba wa vyote vilivyomo vinavyoonekana na visivyoonekana
Mungu wa walio hai,Mungu  mwenye huruma,Mungu wa upendo
Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo...
Asante kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwatayari kwa majukumu yetu

Neema yako yatutosha ee Mungu wetu....!!


Majeshi ya mbinguni yalimfuata yakiwa yamepanda farasi weupe na yamevaa mavazi ya kitani, meupe na safi.

Ufunuo 19:14

Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako,
Tukijinyenyekeza,tukijiachilia mikononi mwako
Mungu wetu tunamomba utusamehe dhambi zetu
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba ukatupe neema
 ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea

Usitutie majaribuni Mungu wetu tunaomba utuepushe
na yule mwovu na kazi zake zote
Jehovah ututakase miili yetu na akili zetu
Baba wa Mbinguni tunaomba utufunike kwa Damu
ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti
yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona....


Upanga mkali hutoka kinywani mwake, na kwa upanga huo atawashinda watu wa mataifa. Yeye ndiye atakayetawala kwa fimbo ya chuma na kuikamua divai katika chombo cha kukamulia zabibu za ghadhabu kuu ya Mungu Mwenye Nguvu.

Ufunuo 19:15

Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa katika utendaji
Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Yahweh tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomna ukatupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji
Tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe kama inavyokupendeza wewe...


Yahweh tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyovimiliki
Yahweh tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia
Baba wa Mbinguni tukawe salama rohoni
Yahwe ukatupe akili ya kutambua mema na mabaya
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu ukatupe macho ya kuona,masikio ya kusikia sauti yako na kuitii..
Baba wa Mbinguni  tunaomba ukatupe neema ya kufuata
njia zako,tukasimamie Neno lako,amri na sheria zako
siku zote za maisha yetu...
Ukatuguse kwa mkono wako wenye nguvu,ukatufanye chombo chema
ee Mungu wetu nasi tukatumike kama inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi....


Juu ya vazi lake, na juu ya paja lake, alikuwa ameandikwa jina: “Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana.”

Ufunuo 19:16

Tazama watoto wako wenye shida/tabu,wote wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali
Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu
kila mmoja na mahitaji yake
Mungu wetu tunaomba ukawasamehe pale walipo kwenda kinyume nawe
Yahweh tunaomba ukawape neema ya kuweza kujiombea,kufuata njia zako nazo zikawaweke huru...
Baba wa Mbinguni tunayaweka haya yote mikononi mwako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele...
Amina...!!


Asanteni sana wapendwa katika Kristo Yesu kwakuwa nami,Baba wa Mbinguni aendelee kuwatendea sawasawa na mapenzi yake...

Nawapenda.

Hukumu juu ya mataifa jirani
1Kauli ya Mwenyezi-Mungu:
Mwenyezi-Mungu ametamka siyo tu dhidi ya nchi ya Hadraki
bali pia dhidi ya Damasko.
Maana nchi ya Aramu ni mali ya Mwenyezi-Mungu,
kama vile yalivyo makabila yote ya Israeli.
2Hali kadhalika mji wa Hamathi unaopakana na Hadraki;
na hata miji ya Tiro na Sidoni
ingawaje yajiona kuwa na hekima sana.
3Mji wa Tiro umejijengea ngome kumbwa,
umejirundikia fedha kama vumbi,
na dhahabu kama takataka barabarani.
4Lakini Bwana ataichukua mali yake yote,
utajiri wake atautumbukiza baharini,
na kuuteketeza mji huo kwa moto.
5Mji wa Ashkeloni utaona hayo na kuogopa,
nao mji wa Gaza utagaagaa kwa uchungu;
hata Ekroni, maana tumaini lake litatoweka.
Mji wa Gaza utapoteza mfalme wake,
nao Ashkeloni hautakaliwa na watu.
6Mji wa Ashdodi utakaliwa na machotara.
Mwenyezi-Mungu asema hivi:
“Kiburi cha Filistia nitakikomesha.
7Nitawakomesha kula nyama yenye damu,
na chakula ambacho ni chukizo.
Mabaki watakuwa mali yangu,
kama ukoo mmoja katika Yuda.
Watu wa Ekroni watakuwa kama Wayebusi.
8Mimi mwenyewe nitailinda nchi yangu,
nitazuia majeshi yasipitepite humo.
Hakuna mtu atakayewadhulumu tena watu wangu,
maana, kwa macho yangu mwenyewe,
nimeona jinsi walivyoteseka.”
Mfalme wa amani
9Shangilieni sana enyi watu wa Siyoni!
Paazeni sauti, enyi watu wa Yerusalemu!
Tazama, mfalme wenu anawajieni,
anakuja kwa shangwe na ushindi!
Ni mpole, amepanda punda,
mwanapunda, mtoto wa punda.
10Atatokomeza magari ya vita nchini Efraimu,
na farasi wa vita kutoka mjini Yerusalemu;
pinde za vita zitavunjiliwa mbali.
Naye ataleta amani miongoni mwa mataifa;
utawala wake utaenea toka bahari hata bahari,
toka mto Eufrate hata miisho ya dunia.
Kurudishwa kwa watu wa Mungu
11Mwenyezi-Mungu asema hivi:
“Kwa sababu ya agano langu nanyi,
agano lililothibitishwa kwa damu,
nitawakomboa wafungwa wenu
walio kama wamefungwa katika shimo tupu.
12Enyi wafungwa wenye tumaini;
rudini kwenye ngome yenu.
Sasa mimi ninawatangazieni:
Nitawarudishieni mema maradufu.
13Yuda nitamtumia kama uta wangu;
Efraimu nimemfanya mshale wangu.
Ee Siyoni! Watu wako nitawatumia kama upanga
kuwashambulia watu wa Ugiriki;
watakuwa kama upanga wa shujaa.”
14Mwenyezi-Mungu atawatokea watu wake;
atafyatua mishale yake kama umeme.
Bwana Mwenyezi-Mungu atapiga tarumbeta;
atafika pamoja na kimbunga cha kusini.
15Mwenyezi-Mungu wa majeshi atawalinda watu wake,
nao watawaangamiza maadui zao.
Watapiga kelele vitani kama walevi
wataimwaga damu ya maadui zao.
Itatiririka kama damu ya tambiko
iliyomiminwa madhabahuni kutoka bakulini.9:15 maana ya aya hii katika Kiebrania si dhahiri.
16Wakati huo, Mwenyezi-Mungu, Mungu wao, atawaokoa,
maana wao ni kundi lake;
nao watang'aa katika nchi yake
kama mawe ya thamani katika taji.
17Jinsi gani uzuri na urembo wake ulivyo!
Wavulana na wasichana watanawiri
kwa wingi wa nafaka na divai mpya.

Zekaria9;1-17

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe

No comments: