Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Thursday 16 July 2020

Kikombe Cha Asubuhi; Sefania 3...

Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu katika yote....

Mungu wetu Baba yetu,Muumba wetu Muumba wa Mbingu na Nchi
Muumba wa vyote vilivyomo vinavyoonekana na visivyoonekana
Mungu wa walio hai,Mungu  mwenye huruma,Mungu wa upendo
Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo...
Asante kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwatayari kwa majukumu yetu

Neema yako yatutosha ee Mungu wetu....!!

Nawachukia watu wanafiki, lakini naipenda sheria yako. Wewe ni ngao yangu, kwako napata usalama; naweka tumaini langu katika neno lako.
Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako,
Tukijinyenyekeza,tukijiachilia mikononi mwako
Mungu wetu tunamomba utusamehe dhambi zetu
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba ukatupe neema
 ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea

Usitutie majaribuni Mungu wetu tunaomba utuepushe
na yule mwovu na kazi zake zote
Jehovah ututakase miili yetu na akili zetu
Baba wa Mbinguni tunaomba utufunike kwa Damu
ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti
yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona....

Ondokeni kwangu, enyi waovu, ili nipate kushika amri za Mungu wangu. Uniimarishe ulivyoahidi, nami nitaishi; usikubali niaibike katika tumaini langu. Unitegemeze, niwe salama; niwe daima msikivu kwa masharti yako.
Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa katika utendaji
Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Yahweh tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomna ukatupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji
Tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe kama inavyokupendeza wewe...


Yahweh tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyovimiliki
Yahweh tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia
Baba wa Mbinguni tukawe salama rohoni
Yahwe ukatupe akili ya kutambua mema na mabaya
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu ukatupe macho ya kuona,masikio ya kusikia sauti yako na kuitii..
Baba wa Mbinguni  tunaomba ukatupe neema ya kufuata
njia zako,tukasimamie Neno lako,amri na sheria zako
siku zote za maisha yetu...
Ukatuguse kwa mkono wako wenye nguvu,ukatufanye chombo chema
ee Mungu wetu nasi tukatumike kama inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi....

Unawakataa wote wanaokiuka masharti yako; mawazo yao maovu ni ya bure. Waovu wote wawaona kuwa takataka, kwa hiyo mimi napenda maamuzi yako. Natetemeka kwa kukuogopa wewe; nimejaa hofu kwa sababu ya hukumu zako.
Tazama watoto wako wenye shida/tabu,wote wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali
Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu
kila mmoja na mahitaji yake
Mungu wetu tunaomba ukawasamehe pale walipo kwenda kinyume nawe
Yahweh tunaomba ukawape neema ya kuweza kujiombea,kufuata njia zako nazo zikawaweke huru...
Baba wa Mbinguni tunayaweka haya yote mikononi mwako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele...
Amina...!!


Asanteni sana wapendwa katika Kristo Yesu kwakuwa nami,Baba wa Mbinguni aendelee kuwatendea sawasawa na mapenzi yake...

Nawapenda.

Hukumu ya Yerusalemu
1Ole wake mji wa Yerusalemu,
mji mchafu, najisi na mdhalimu.
2Hausikilizi onyo lolote,
wala haukubali kukosolewa.
Haukumtegemea Mwenyezi-Mungu kamwe,
wala kumkaribia Mungu wake.
3Viongozi wake ni simba wangurumao,
mahakimu wake ni mbwamwitu wenye njaa jioni
wasioacha chochote mpaka asubuhi.
4Manabii wake ni watu wasiojali na wadanganyifu.
Makuhani wake wamevitia unajisi vitu vitakatifu
na kuihalifu sheria kwa nguvu.
5Lakini Mwenyezi-Mungu aliye mjini humo ni mwadilifu,
yeye hatendi jambo lolote baya.
Kila siku asubuhi hudhihirisha kauli yake,
naam, kila kunapopambazuka huitekeleza.
Lakini wahalifu hawana aibu hata kidogo.
6Mwenyezi-Mungu asema:
“Nimeyafutilia mbali mataifa;
kuta zao za kujikinga ni magofu.
Barabara zao nimeziharibu,
na hamna apitaye humo.
Miji yao imekuwa mitupu,
bila watu, na bila wakazi.
7Nilisema, ‘Hakika mji huu watanicha
na kukubali kukosolewa;
hautaacha kukumbuka mara hizo zote nilizowaadhibu.’
Lakini watu wake walizidisha tamaa zao
za kufanya matendo yao kuwa upotovu.
8“Kwa hiyo ningojeni mimi Mwenyezi-Mungu,
ngoja siku nitakapoinuka kutoa mashtaka.
Nimeamua kuyakusanya mataifa na falme,
kuyamwagia ghadhabu yangu,
kadhalika na ukali wa hasira yangu.
Dunia yote itateketezwa
kwa moto wa ghadhabu yangu.
9“Wakati huo nitaibadili lugha ya watu,
nitawawezesha kusema lugha adili
ili waniite mimi Mwenyezi-Mungu,
na kuniabudu kwa moyo mmoja.
10Kutoka ng'ambo ya mito ya Kushi
watu wangu wanaoniomba ambao wametawanyika,
wataniletea sadaka yangu.
11“Siku hiyo, haitakulazimu kuona aibu,
kutokana na matendo yako ya kuniasi,
maana nitawaondoa miongoni mwako
wale wanaojigamba na kujitukuza
nawe hutakuwa na kiburi tena katika mlima wangu mtakatifu.
12Nitakuachia watu wapole na wanyenyekevu
ambao watakimbilia usalama kwangu mimi Mwenyezi-Mungu.
13Waisraeli watakaobaki,
hawatatenda mabaya wala hawatasema uongo;
wala kwao hatapatikana mdanganyifu yeyote.
Watapata malisho na kulala
wala hakuna mtu atakayewatisha.”
Wimbo wa furaha
14Imba kwa sauti, ewe Siyoni,
paza sauti ee Israeli.
Furahi na kushangilia kwa moyo wote, ewe Yerusalemu!
15Mwenyezi-Mungu amekuondolea hukumu iliyokukabili,
amewageuzia mbali adui zako.
Mwenyezi-Mungu, mfalme wa Israeli yuko pamoja nawe
hutaogopa tena maafa.
16Siku hiyo, mji wa Yerusalemu utaambiwa:
“Usiogope, ee Siyoni,
usilegee mikono.
17Mwenyezi-Mungu, Mungu wako yu pamoja nawe
yeye ni shujaa anayekuletea ushindi.
Yeye atakufurahia kwa furaha kuu,
kwa upendo wake atakujalia uhai mpya.
Atakufurahia kwa wimbo wa sauti kubwa,
18kama vile katika siku ya sikukuu.”
Mwenyezi-Mungu asema:
“Nitakuondolea maafa yako,
nawe hutahitaji kuona aibu kwa ajili yake.
19Wakati huo, nitawaadhibu wote wanaokukandamiza.
Nitawaokoa vilema na kuwakusanya waliotupwa,
na kubadili aibu yao kuwa sifa
na fahari duniani kote.
20Wakati huo nitawakusanya,
na kuwafanya mjulikane na kusifiwa,
miongoni mwa watu wote duniani
nitakapowarudishia hali yenu njema
nanyi muone kwa macho yenu wenyewe.
Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”

Sefania3;1-20

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe

No comments: