Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Monday 13 July 2020

Kikombe Cha Asubuhi; Habakuki 3...

Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Haleluyah ni siku/wiki nyingine tena Mungu wetu ametuchagua

na kutupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Si kwamba sisi tumetenda mema sana wala si kwa nguvu zetu
si kwa utashi wetu wala si kwa akili zetu si kwamba sisi
ni wazuri mno si kwa uwezo wetu sisi kuwa hivi tulivyo leo hii
Ni kwa rehema/neema zake ni kwa mapenzi yake Mungu wetu....

Tumshukuru Mungu wetu katika yote...
Asante Mungu wetu kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwa tayari kwa majukumu yetu
Sifa na Utukufu tunakurudshia Mungu wetu....!!

Neno lako, ee Mwenyezi-Mungu, ladumu milele; limethibitika juu mbinguni. Uaminifu wako wadumu vizazi vyote, umeiweka dunia mahali pake nayo yadumu.
Tazama jana imepita ee Mungu wetu leo ni siku mpya na kesho ni siku nyingine Jehovah tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako
 Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizozifanya kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea
Jehovah usitutie majaribuni Mungu wetu tunaomba utuepushe na yule mwovu na kazi zake zote
Yahweh tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu
Baba wa Mbinguni utufunike kwa Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti
yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona

Kwakupigwa kwake sisi tumepata kupona....

Kwa amri yako viumbe vyote vipo leo, maana vitu vyote ni watumishi wako. Kama sheria yako isingekuwa furaha yangu, ningalikwisha angamia kwa taabu zangu. Sitasahau kamwe kanuni zako, maana kwa hizo umenipa uhai.
Yahweh tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu

Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa 
katika utendaji
Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki ridhiki zetu
ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba ukatupe neema ya kuweza
kuwabariki wenye kuhitaji
Yahweh tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Mungu wetu ukatupe kama inavyokupendeza wewe

Baba wa Mbinguni tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyo vimiliki
Yahweh tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia
Baba wa Mbinguni tukawe salama rohoni
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia 
sauti yako na kuitii
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe neema ya kufuata njia zako
Yahweh tukasimamie Neno lako amri na sheria zako siku zote 
za maisha yetu
Mungu wetu ukaonekane katika maisha yetu
Neema zako zikawe nasi Nuru yako ikaangaze katika maisha yetu
ukatuguse kwa mkono wako wenye nguvu
Ukatufanye chombo chema ee Mungu wetu nasi tukatumike kama
inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi...


Mimi ni wako, uniokoe, maana nimejitahidi kuzishika kanuni zako. Waovu wanivizia wapate kuniua; lakini mimi natafakari masharti yako. Nimetambua kila kitu hufikia kikomo, lakini amri yako ni kamilifu.
Mungu wetu tunawaweka mikononi mwako wenye shida/tabu,wote wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali
Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu
 kila mmoja na mahitaji yake 
Mungu wetu tunaomba ukawasamehe pale walipokwenda kinyume nawe
Baba wa Mbinguni ukawape neema ya kujiombea,kufuata njia zako
wakasimamie Neno lako nalo likawaweke huru
Mungu wetu tunaomba ukasikie kuomba kwetu
Mungu wetu ukawatendee sawasawa na mapenzi yako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina...!!


Asanteni sana wapendwa katika Kristo Yesu kwakuwa nami
Mungu Baba aendelee kuwabariki na kuwatendea 
kama inavyompendeza yeye....
Nawapenda.

Sala ya Habakuki
1Sala ya nabii Habakuki:
2Ee Mwenyezi-Mungu, nimesikia juu ya fahari yako,
juu ya matendo yako, nami naogopa.
Uyafanye tena mambo hayo wakati wetu;
uyafanye yajulikane wakati huu wetu.
Ukasirikapo tafadhali ukumbuke huruma yako!
3Mungu amekuja kutoka Temani,
Mungu mtakatifu kutoka mlima Parani.
Utukufu wake umetanda pote mbinguni,
nayo dunia imejaa sifa zake.
4Mng'ao wake ni kama wa jua;
miali imetoka mkononi mwake
ambamo nguvu yake yadhihirishwa.
5Maradhi yanatangulia mbele yake,
nyuma yake yanafuata maafa.
6Akisimama dunia hutikisika;
akiyatupia jicho mataifa, hayo hutetemeka.
Milima ya milele inavunjwavunjwa,
vilima vya kudumu vinadidimia;
humo zimo njia zake za kale na kale.
7Niliwaona watu wa Kushani wakiteseka,
na watu wa Midiani wakitetemeka.
8Ee Mwenyezi-Mungu, je, umeikasirikia mito?
Je, umeyakasirikia maji ya bahari,
hata ukaendesha farasi wako,
na magari ya vita kupata ushindi?
9Uliuweka tayari uta wako,
ukaweka mishale yako kwenye kamba.
Uliipasua ardhi kwa mito.
10Milima ilikuona, ikanyauka;
mafuriko ya maji yakapita humo.
Vilindi vya bahari vilinguruma,
na kurusha juu mawimbi yake.
11Jua na mwezi vilikaa kimya katika makazi yao,
vilipoona miali ya mishale yako ikienda kasi,
naam, vilipouona mkuki wako ukimetameta.
12Kwa ghadhabu ulipita juu ya nchi,
uliyakanyaga mataifa kwa hasira yako.
13Ulitoka kwenda kuwaokoa watu wako,
kumwokoa yule uliyemweka wakfu kwa mafuta.
Ulimponda kiongozi wa jamii ya waovu,
ukawaangamiza kabisa wafuasi wake.
14Amiri jeshi ulimchoma mishale yako,
jeshi lilipokuja kama kimbunga kututawanya,
wakijigamba kuwaangamiza maskini mafichoni mwao.
15Kwa farasi wako ulitembea juu ya bahari,
bahari inayosukwasukwa na mawimbi.
16Nasikia hayo nami ninashtuka mwilini,
midomo yangu inatetemeka kwa hofu;
mifupa yangu inateguka,
miguu yangu inatetemeka.
Ninangojea kwa utulivu siku ile ya maafa,
ambayo inawajia wale wanaotushambulia.
17Hata kama mitini isipochanua maua,
wala mizabibu kuzaa zabibu;
hata kama mizeituni isipozaa zeituni,
na mashamba yasipotoa chakula;
hata kama kondoo wakitoweka zizini,
na mifugo kukosekana mazizini,
18mimi nitaendelea kumfurahia Mwenyezi-Mungu
nitamshangilia Mungu anayeniokoa.
19Bwana, Mwenyezi-Mungu ndiye nguvu yangu,
huiimarisha miguu yangu kama ya paa,
huniwezesha kupita juu milimani.



Habakuki3;1-19

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe

No comments: