Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Friday 8 March 2019

Kikombe Cha Asubuhi ;Zaburi 77...


Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu katika yote...

Asante  Mungu wetu kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwatayari kwa majukumu yetu


Utukuzwe ee Mungu wetu,usifiwe Baba wa Mbinguni

Neema yako yatutosha  Mungu wetu..!

Wakimtii Mungu na kumtumikia, hufanikiwa katika siku zao zote; miaka yao yote huwa ya furaha. Lakini wasipomtii, huangamia kwa upanga, na kufa kwa kukosa akili. “Wasiomcha Mungu hupenda kukasirika, hawamlilii msaada anapowabana. Hufa wangali bado vijana, maisha yao huisha kama ya walawiti.
Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea,Usitutie majaribuni Mungu wetu tunaomba utuepushe na yule mwovu na kazi zake zote,Jehovah ututakase miili yetu na akili zetu Baba wa Mbinguni tunaomba utufunike kwa  Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti,
Yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona....

Lakini Mungu huwaokoa wanyonge kwa unyonge wao hutumia shida zao kuwafumbua macho. Mungu alikuvuta akakutoa taabuni, akakuweka mahali pa wasaa pasipo shida, na mezani pako akakuandalia vinono.
Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa 
katika utendaji
Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki ridhiki zetu
ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba ukatupe neema ya kuweza
kuwabariki wenye kuhitaji
Yahweh tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Mungu wetu ukatupe kama inavyokupendeza wewe



Jehovah tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyo vimiliki
Yahweh tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia
Baba wa Mbinguni tukawe salama rohoni
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia 
sauti yako na kuitii
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe neema ya kufuata njia zako
Yahweh tukasimamie Neno lako amri na sheria zako siku zote 
za maisha yetu

Mungu wetu tunaomba ukatupe akili ya kutambua mema na mabaya Baba wa Mbinguni ukaonekane katika maisha yetu popote tupitapo na ikajulikane kwamba upo Mungu wetu

Neema zako zikawe nasi Nuru yako ikaangaze katika maisha yetu
ukatuguse kwa mkono wako wenye nguvu
Ukatufanye barua njema ee Mungu wetu nasi tukasomeke kama
inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi...

“Lakini sasa umehukumiwa kama mwovu, hukumu ya haki imekukumba. Jihadhari ghadhabu isije ikakufanya ukadhihaki, au ukubwa wa mali za kukukomboa ukakupotosha. Je, kilio chako kitafaa kukutoa taabuni, au nguvu zako zote zitakusaidia?
Tazama wenye shida/tabu,watoto wako wanaokutafuta kwa bidii na imani
Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu
Yahweh tunaomba  ukawaguse kila mmoja na mahitaji yake
Mungu wetu  unajua haja za mioyo ya kila mmoja
Baba wa Mbinguni tunaomba ukawasamehe pale walipokwenda
kinyume nawe
Mungu wetu ukawape neema ya kujiombea,macho ya rohoni,masikio yakusikia sauti yako,wakafuate njia zako nazo zikawaweke huru
Mungu wetu tunaomba ukasikie kulia kwao
Baba wa Mbinguni tunomba ukawafute machozi yao
Jehovah ukaonekane katika maisha yao
Nuru yako ikaangaze katika maisha yao
Mungu wetu tunaomba ukawatendee sawasawa na mapenzi yako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina....!!!


Wapendwa katika Kristo Yesu asanteni sana
kwakuwanami/kunisoma

Mungu Baba aendelee kuwabariki na kuwatendea
kama inavyompendeza yeye
Amani ya Bwana wetu Yesu Kristo na upendo wa Mungu Baba
ukae nanyi daima....
Nawapenda.


Faraja wakati wa shida
(Kwa Mwimbishaji: Mtindo wa Yeduthuni. Zaburi ya Asafu)
1Namlilia Mungu kwa sauti,
kwa sauti namlilia Mungu anisikie.
2Wakati wa taabu namwomba Bwana;
namnyoshea mikono yangu usiku bila kuchoka,
lakini sipati faraja yoyote kwa mtu.
3Ninamfikiria Mungu na kusononeka;
ninatafakari na kufa moyo.
4Wanizuia hata kupata lepe la usingizi,
nina mahangaiko hata kusema siwezi.
5Nafikiria siku za zamani;
nakumbuka miaka ya hapo kale.
6Usiku nawaza na kuwazua moyoni;
natafakari na kujiuliza rohoni:
7“Je, Bwana ametuacha kabisa?
Je, hatatuonesha tena hisani yake?
8Je fadhili zake zimekoma kabisa?
Je, hatatimiza tena ahadi zake?
9Je, Mungu amesahau kuwa na huruma?
Je, hasira yake imeuondoa upole wake?”
10Kisha nikasema, “Kinachonichoma zaidi ni kwamba,
Mungu Mkuu hatendi tena kitu kwa ajili yetu!”
11Nitayakumbuka matendo yako, ee Mwenyezi-Mungu,
naam, nitayafikiria maajabu yako ya hapo kale.
12Nitatafakari juu ya kazi zako,
na kuwaza juu ya matendo yako makuu.
13Kila ufanyacho ee Mungu, ni kitakatifu.
Ni mungu gani aliye mkuu kama Mungu wetu?
14Wewe ni Mungu unayetenda maajabu;
wewe umeyaonesha mataifa uwezo wako.
15Kwa mkono wako wa nguvu uliwakomboa watu wako;
uliwakomboa wazawa wa Yakobo na Yosefu.
16Maji yalipokuona, ee Mungu,
maji yalipokuona, yaliogopa mno;
naam, bahari ilitetemeka hata vilindini.
17Mawingu yalichuruzika maji,
ngurumo zikavuma angani,
mishale ya umeme ikaangaza kila upande.
18Kishindo cha ngurumo yako kilitokea katika kimbunga,
umeme wako ukauangaza ulimwengu;
dunia ikatikisika na kutetemeka.
19Wewe uliweka njia yako juu ya bahari;
ulitembea juu ya maji yale mengi,
lakini nyayo zako hazikuonekana.
20Uliwaongoza watu wako kama kondoo,
chini ya uongozi wa Mose na Aroni.

Zaburi77;1-20

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: