Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Thursday 16 January 2020

Kikombe Cha Asubuhi; Yeremia 34....


Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu katika yote...

Asante  Mungu wetu kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwatayari kwa majukumu yetu


Utukuzwe ee Mungu wetu,usifiwe Baba wa Mbinguni

Neema yako yatutosha  Mungu wetu..!


Siku zile, tangazo rasmi lilitolewa na Kaisari Augusto kuwataka watu wote nchini kote wahesabiwe. Sensa hiyo ilikuwa mara ya kwanza, wakati Kurenio alipokuwa mkuu wa mkoa wa Siria. Basi, wote waliohusika walikwenda kuhesabiwa kila mtu katika mji wake.
Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,
tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako

Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea,Usitutie majaribuni Mungu wetu tunaomba utuepushe na yule mwovu na kazi zake zote,Jehovah ututakase miili yetu na akili zetu Baba wa Mbinguni tunaomba utufunike kwa  Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti,
Yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona....


Yosefu pia alifanya safari kutoka mjini Nazareti mkoani Galilaya, na kwa vile alikuwa wa jamaa na ukoo wa Daudi, alikwenda mjini Bethlehemu mkoani Yudea, alikozaliwa mfalme Daudi. Alikwenda kuhesabiwa pamoja na mchumba wake Maria ambaye alikuwa mjamzito.
Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa 
katika utendaji
Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki ridhiki zetu
ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba ukatupe neema ya kuweza
kuwabariki wenye kuhitaji
Yahweh tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Mungu wetu ukatupe kama inavyokupendeza wewe



Jehovah tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyo vimiliki
Yahweh tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia
Baba wa Mbinguni tukawe salama rohoni
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia 
sauti yako na kuitii
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe neema ya kufuata njia zako
Yahweh tukasimamie Neno lako amri na sheria zako siku zote 
za maisha yetu

Mungu  wetu ukaonekane katika maisha yetu popote tupitapo na ikajulikane kwamba upo 

Neema zako zikawe nasi Nuru yako ikaangaze katika maisha yetu
Ukatufanye barua njema ee Mungu wetu nasi tukasomeke kama
inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi...


Walipokuwa huko, siku yake ya kujifungua ikawadia, akajifungua mtoto wake wa kwanza wa kiume, akamvika nguo za kitoto, akamlaza horini kwa sababu hawakupata nafasi katika nyumba ya wageni.
Tazama wenye shida/tabu,Mungu wetu tunaomba
 ukawaguse kila mmoja na mahitaji yake
Baba wa Mbinguni tunaomba ukawasamehe pale walipokwenda
kinyume nawe
Mungu wetu ukawape neema ya kujiombea,macho ya rohoni,masikio yakusikia sauti yako,wakafuate njia zako nazo zikawaweke huru
Mungu wetu tunaomba ukasikie kulia kwao
Baba wa Mbinguni tunomba ukawafute machozi yao
Nuru yako ikaangaze katika maisha yao
Mungu wetu tunaomba ukawatendee sawasawa na mapenzi yako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina....!!!


Wapendwa katika Kristo Yesu asanteni sana
kwakuwanami/kunisoma

Mungu Baba aendelee kuwabariki na kuwatendea
kama inavyompendeza yeye
Amani ya Bwana wetu Yesu Kristo na upendo wa Mungu Baba
ukae nanyi daima....

Nawapenda.

Ujumbe kwa Sedekia
1Neno la Mwenyezi-Mungu lilimjia Yeremia wakati Nebukadneza, mfalme wa Babuloni, pamoja na jeshi lake lote na falme zote za dunia zilizokuwa chini yake, kadhalika na watu wote walipokuwa wakiushambulia mji wa Yerusalemu na miji mingine yote ya kandokando yake: 2“Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli asema hivi: Nenda ukaongee na Sedekia, mfalme wa Yuda. Mwambie kwamba mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Nimeutia mji huu mikononi mwa mfalme wa Babuloni, naye atauteketeza kwa moto. 3Nawe hutatoroka mikononi mwake, bali kwa hakika utatekwa na kupelekwa kwake; utaonana na mfalme wa Babuloni macho kwa macho, na kuongea naye ana kwa ana; kisha, utakwenda Babuloni. 4Lakini, ewe Sedekia, mfalme wa Yuda, mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi juu yako: Wewe hutauawa kwa upanga vitani. 5Utakufa kwa amani. Na, kama vile watu walivyochoma ubani walipowazika wazee wako waliokuwa wafalme, ndivyo watakavyokuchomea ubani na kuomboleza wakisema, ‘Maskini! Mfalme wetu amefariki!’ Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
6Kisha, nabii Yeremia akamweleza Sedekia, mfalme wa Yuda, maneno hayo yote huko Yerusalemu, 7wakati jeshi la mfalme wa Babuloni lilipokuwa linaushambulia mji wa Yerusalemu na pia miji ya Lakishi na Azeka, ambayo ilikuwa miji pekee iliyosalia yenye ngome.
Uhuru wa bandia kwa watumwa
8Hili ndilo neno lililomjia Yeremia kutoka kwa Mwenyezi-Mungu baada ya mfalme Sedekia kufanya agano na watu wote wa Yerusalemu kuwaachia huru 9watumwa wao wa Kiebrania wa kiume na wa kike, ili mtu yeyote asimfanye Myahudi mwenzake mtumwa. 10Viongozi wote na watu wote waliofanya agano hilo walikubaliana wote wawaachie huru watumwa wao wa kiume na wa kike, na mtu yeyote asiwafanye tena kuwa watumwa. Walikubaliana, wakawaacha huru. 11Lakini baadaye walibadili nia zao, wakawashika tena watumwa hao wa kiume na wa kike ambao walikuwa wamewaacha huru, wakawafanya watumwa.
12Hapo neno la Mwenyezi-Mungu likamjia Yeremia: 13“Mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, nasema hivi: Nilifanya agano na wazee wenu nilipowatoa nchini Misri ambako walikuwa watumwa, nikawaambia: 14‘Kila mwaka wa saba, kila mmoja wenu atamwacha huru ndugu yake Myahudi aliyeuzwa akawa mtumwa kwa muda wa miaka sita. Mnapaswa kuwaacha huru, wasiwatumikie tena.’ Lakini wazee wenu hawakunisikiliza wala kunitegea sikio. 15Hivi karibuni nyinyi mlitubu, mkafanya mambo yaliyo sawa mbele yangu, mkawaacha huru Waisraeli wenzenu na kufanya agano mbele yangu katika nyumba yangu. 16Lakini baadaye mligeuka, mkalitia unajisi jina langu, wakati mlipowachukua tena watumwa walewale wa kiume na wa kike ambao mlikuwa mmewaachia kama walivyotaka, mkawalazimisha kuwa watumwa tena. 17Kwa hiyo, mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Nyinyi hamkunitii kuhusu kuwapatia uhuru ndugu zenu Waisraeli. Basi, nami pia nitawapatieni uhuru; uhuru wa kuuawa kwa upanga vitani, kuuawa kwa maradhi na kwa njaa. Nitawafanya muwe kioja kwa falme zote duniani. 18Watu waliovunja agano langu na kukataa kufuata masharti ya agano walilofanya mbele yangu, nitawafanya kama yule ndama waliyemkata sehemu mbili na kupita katikati yake. 19Watu hao ndio hao maofisa wa Yuda, maofisa wa mji wa Yerusalemu, matowashi, makuhani, pamoja na wananchi wote waliopita katikati ya sehemu mbili za yule ndama. 20Watatiwa mikononi mwa maadui zao, na mikononi mwa watu wanaotaka kuwaua. Maiti zao zitaliwa na ndege wa angani na wanyama wa porini. 21Naye Sedekia, mfalme wa Yuda, pamoja na viongozi wake, nitawatia mikononi mwa maadui zao, na mikononi mwa watu wanaotaka kuwaua; yaani mikononi mwa jeshi la mfalme wa Babuloni ambalo limeondoka na kuacha kuwashambulia. 22Mimi Mwenyezi-Mungu nasema: Nitawaamuru nao wataurudia mji huu. Wataushambulia, watauteka na kuuteketeza kwa moto. Nitaifanya miji ya Yuda kuwa ukiwa bila wakazi.”


Yeremia34;1-22

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: