Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Friday 11 January 2019

Kikombe Cha Asubuhi ;Zaburi 37...



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu katika yote....

Mungu wetu Baba yetu,Muumba wetu Muumba wa Mbingu na Nchi
Muumba wa vyote vilivyomo vinavyoonekana na visivyoonekana
Mungu wa walio hai,Mungu  mwenye huruma,Mungu wa upendo
Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo...
Asante kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwatayari kwa majukumu yetu

Neema yako yatutosha ee Mungu wetu....!!

Wakaendelea na safari, wakafika pwani ya nchi ya Wagerase inayokabiliana na Galilaya, ngambo ya ziwa. Alipokuwa anashuka pwani, mtu mmoja aliyekuwa amepagawa na pepo alimjia kutoka mjini. Kwa muda mrefu mtu huyo hakuwa anavaa nguo, wala hakuwa anaishi nyumbani bali makaburini. Alipomwona Yesu, alijitupa chini mbele yake na kusema kwa sauti kubwa, “We, Yesu Mwana wa Mungu Mkuu, una shauri gani nami? Ninakusihi usinitese!”
Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizo zifanya
Kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba ukatupe neema
ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea
Usitutie majaribu Mungu wetu tunaomba utuepushe
na yule mwovu na kazi zake zote
Jehovah ututakase miili yetu na akili zetu
Baba wa Mbinguni tunaomba utufunike kwa Damu
ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti
yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona....

Alisema hivyo kwa kuwa Yesu alikuwa amemwambia huyo pepo mchafu amtoke mtu huyo. Pepo huyo mchafu alikuwa anamvamia mtu huyo mara nyingi, na ingawa watu walimweka ndani na kumfunga kwa minyororo na pingu, lakini kila mara alivivunja vifungo hivyo, akakimbizwa na pepo huyo mchafu hadi jangwani. Basi, Yesu akamwuliza, “Jina lako nani?” Yeye akajibu, “Jina langu ni ‘Jeshi’” – kwa sababu pepo wengi walikuwa wamempagaa. Hao pepo wakamsihi asiwapeleke kwenye shimo kuu. Mahali hapo kulikuwa na kundi kubwa la nguruwe wakilisha mlimani. Basi, hao pepo wakamsihi awaruhusu wawaingie. Naye Yesu akawapa ruhusa. Kwa hiyo pepo hao wakamtoka yule mtu, wakawaingia wale nguruwe, nao wakaporomoka kwenye ule mteremko mkali, wakatumbukia ziwani, wakafa maji.

Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa katika utendaji

Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Yahweh tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba ukatupe neema ya kuweza
kuwabariki wenye kuhitaji
Tusipungukiwe katika mahitaji yetu Baba wa Mbinguni
tunaomba ukatupe kama inavyokupendeza wewe....



Yahweh  tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyo vimiliki
Yahweh tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia
Baba wa Mbinguni tukawe salama rohoni

Yahweh ukatupe akili ya kutambua mema na mabaya
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia 
sauti yako na kuitii
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe neema ya kufuata njia zako
Yahweh tukasimamie Neno lako amri na sheria zako siku zote 
za maisha yetu
Mungu wetu ukaonekane katika maisha yetuBaba wa Mbinguni tukanene yaliyo yako
Neema zako zikawe nasi Nuru yako ikaangaze katika maisha yetu
ukatuguse kwa mkono wako wenye nguvu
Ukatufanye chombo chema ee Mungu wetu nasi tukatumike kama
inavyokupendeza wewe

Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi....
Wale wachungaji walipoona yote yaliyotokea walikimbia, wakaenda kuwapa watu habari mjini na mashambani. Watu wakaja kuona yaliyotokea. Wakamwendea Yesu, wakamwona yule mtu aliyetokwa na pepo ameketi karibu na Yesu, amevaa nguo, ana akili zake, wakaogopa. Wale watu walioshuhudia tukio hilo waliwaeleza hao jinsi yule mtu alivyoponywa. Wakazi wa nchi ya Gerase walishikwa na hofu kubwa. Kwa hiyo wakamwomba Yesu aondoke, aende zake. Hivyo Yesu alipanda tena mashua, akaondoka. Yule mtu aliyetokwa na wale pepo akamsihi aende pamoja naye. Lakini Yesu hakumruhusu, bali akamwambia, “Rudi nyumbani ukaeleze yote Mungu aliyokutendea.” Basi, yule mtu akaenda akitangaza kila mahali katika mji ule mambo yote Yesu aliyomtendea.


Tazama watoto wako wanaokutafuta/kukuomba kwa bidii na imani, Mungu wetu tunawaweka mikononi mwako wenye shida/tabu,
wote wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali
Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu
kila mmoja na mahitaji yake
Baba wa Mbinguni tunaomba ukaonekane katika maisha yao
Mungu wetu tunaomba ukawasamehe pale walipokwenda
kinyume nawe Yahweh tunaomba ukawape neema ya kujiombea
Kufuata njia zako nazo zikawaweke huru
Ukawape macho ya rohoni ee Mungu wetu na masikio ya kusikia
sauti yako,Ukawaokoe na kuwalinda,ukawaponye kimwili na kiroho
Nuru yako ikaangaze katika maisha yao,Amani ikatawale katika maisha yao,Upendo ukadumu kati yao

Baba wa Mbinguni tunayaweka haya yote mikononi mikononi mwako,Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele 
Amina!!
Asanteni sana wapendwa katika Kristo Yesu kwakuwa nami,Mungu Baba aendelee kuwatendea sawasawa na mapezni yake
Nawapenda.


Kufanikiwa kwa waovu kusikufadhaishe
(Zaburi ya Daudi)
1Usihangaike kwa sababu ya waovu;
usiwaonee wivu watendao mabaya.
2Maana hao watatoweka mara kama nyasi;
watanyauka kama mimea mibichi.
3Mtumainie Mwenyezi-Mungu na kutenda mema,
upate kuishi katika nchi na kuwa salama.
4Uitafute furaha yako kwa Mwenyezi-Mungu,
naye atakujalia unayotamani moyoni.
5Mkabidhi Mwenyezi-Mungu maisha yako;
mtumainie yeye naye atafanya kitu.
6Ataufanya wema wako ungae kama mwanga,
na uadilifu wako kama jua la adhuhuri.
7Tulia mbele ya Mwenyezi-Mungu, mngojee kwa saburi;
usihangaike juu ya wale wanaofanikiwa,
watu wanaofaulu katika mipango yao mibaya.
8Epuka hasira wala usiwe na ghadhabu;
usihangaike maana hiyo huzidisha ubaya.
9Watu watendao mabaya wataangamizwa,
bali wanaomtumaini Mwenyezi-Mungu wataimiliki nchi.
10Bado kitambo kidogo, naye mwovu atatoweka;
utamtafuta pale alipokuwa, wala hutamwona.
11 Taz Mat 5:5 Lakini wapole wataimiliki nchi,
hao watafurahia wingi wa fanaka.
12Mwovu hula njama dhidi ya mwadilifu,
na kumsagia meno kwa chuki.
13Lakini Mwenyezi-Mungu humcheka mwovu,
kwani ajua mwisho wake u karibu.
14Waovu huchomoa panga na kuvuta pinde zao,
wapate kuwaua maskini na fukara;
wawachinje watu waishio kwa unyofu.
15Lakini panga zao zitawapenya wao wenyewe,
na pinde zao zitavunjwavunjwa.
16Afadhali mali kidogo ya mtu mwadilifu
kuliko utajiri wa watu waovu wengi.
17Maana nguvu za waovu zitavunjwa,
lakini Mwenyezi-Mungu huwategemeza waadilifu.
18Mwenyezi-Mungu hutunza maisha ya watu waaminifu,
na urithi wao utadumu milele.
19Hawataaibika zikifika nyakati mbaya;
siku za njaa watakuwa na chakula tele.
20Lakini waovu wataangamia,
maadui za Mwenyezi-Mungu watanyauka kama maua nyikani;
naam, watatoweka kama moshi.
21Mtu mwovu hukopa bila kurudisha;
lakini mwadilifu hutoa kwa ukarimu.
22Waliobarikiwa na Mwenyezi-Mungu wataimiliki nchi,
lakini waliolaaniwa naye watafutiliwa mbali.
23Mwenyezi-Mungu huziongoza nyayo za mtu,
humlinda yule ampendezaye.
24Ajapoanguka, haanguki akabaki chini,
kwa sababu Mwenyezi-Mungu humtegemeza.
25Nilikuwa kijana na sasa ni mzee;
kamwe sijaona mwadilifu ameachwa na Mungu,
au watoto wake wakiombaomba chakula.
26Daima huwapa wengine kwa furaha na kukopesha,
na watoto wake ni baraka.
27Achana na uovu, utende mema,
nawe utaishi nchini daima;
28maana Mwenyezi-Mungu hupenda uadilifu,
wala hawaachi waaminifu wake.
Huwalinda hao milele;
lakini wazawa wa waovu wataangamizwa.
29Waadilifu wataimiliki nchi,
na wataishi humo milele.
30Mtu mwadilifu husema maneno ya hekima,
kwa ulimi wake hunena yaliyo ya haki.
31Huizingatia moyoni mwake sheria ya Mungu wake;
naye hatetereki katika mwenendo wake.
32Mtu mwovu humvizia mtu mwema na kujaribu kumuua;
33lakini Mwenyezi-Mungu hatamtia mtu mwema makuchani mwake,
wala kumwacha apatilizwe akishtakiwa.
34Mtumainie Mwenyezi-Mungu na kushika njia yake,
naye atakukuza uimiliki nchi,
na kuwaona waovu wakiangamizwa.
35Nilimwona mwovu mdhalimu sana,
alijiweka juu ya wote kama mierezi ya Lebanoni!
36Baadaye nikapita hapo, naye hakuwapo tena;
nikamtafuta, lakini hakuonekana tena.
37Mwangalie mtu mwema, mtu mwadilifu;
mtu anayependa amani hujaliwa wazawa.
38Lakini wakosefu wote wataangamizwa;
na wazawa wao watafutiliwa mbali.
39Mwenyezi-Mungu huwaokoa waadilifu,
na kuwalinda wakati wa taabu.
40Mwenyezi-Mungu huwasaidia na kuwaokoa;
huwatoa makuchani mwa waovu na kuwaokoa,
maana wanakimbilia usalama kwake.



Zaburi37;1-40

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: