Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Wednesday 11 April 2018

Kikombe Cha Asubuhi ; 2 Wafalme 5......



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Haleluyah Mungu wetu yu mwema sana ..
Tumshukuru Mungu wetu katika yote.....

Asante Baba wa Mbinguni kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa kibali cha kuendelea 
kuiona leo hii
Asante kwa uwepo wako,uzima/pumzi,afya na kuwa tayari
kwa majukumu yetu...
Utukuzwe ee Mungu wetu,Mungu mwenye nguvu,Mungu mwenye
huruma,Mungu wa walio hai,Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo
Mungu unayeponya,Mungu unayesamehe,Mungu wa Upendo,
Matendo yako ni makuu mno,Mtaendo yako ni ya ajabu,matendo yako
yanatisha,Neema yako yatutosha ee mungu wetu..
Sifa na Utukufu tunakurudisha Baba wa Mbinguni...!!



Ndugu, nataka mjue kwamba babu zetu wote walikuwa chini ya ulinzi wa lile wingu, na kwamba wote walivuka salama ile bahari. Wote walibatizwa katika umoja na Mose katika lile wingu na katika ile bahari. Wote walikula chakula kilekile cha kiroho, wakanywa pia kinywaji kilekile cha kiroho, maana walikunywa kutoka ule mwamba wa kiroho uliowafuata; mwamba huo ulikuwa Kristo mwenyewe. Hata hivyo, wengi wao hawakumpendeza Mungu, na maiti zao zilisambazwa jangwani.
Yahweh tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha na kujiachilia
mikononi mwako ...
Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizozifanya
Kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua
Jehovah nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote
waliotukosea
Baba wa Mbinguni usitutie majaribu Mungu wetu tunaomba utuokoe
na yule mwovu na kazi zake zote
Yahweh tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu Jehovah utufunike kwa Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti
yeye akliteseka kwanza ili sisi tupate kupona....




Sasa, mambo hayo yote ni mfano tu kwetu; yanatuonya sisi tusitamani ubaya kama wao walivyotamani. Msiwe waabudu sanamu kama baadhi yao walivyokuwa; kama yasemavyo Maandiko: “Watu waliketi kula na kunywa, wakasimama kucheza.” Wala tusizini kama baadhi yao walivyozini, wakaangamia siku moja watu 23,000. Tusimjaribu Bwana kama baadhi yao walivyomjaribu, wakauawa na nyoka. Wala msinungunike kama baadhi yao walivyonungunika, wakaangamizwa na Mwangamizi! Basi, mambo hayo yaliyowapata wao ni kielelezo kwa wengine, na yaliandikwa ili kutuonya sisi ambao mwisho wa nyakati unatukabili. Anayedhani amesimama imara ajihadhari asianguke. Majaribu mliyokwisha pata ni ya kawaida kwa binadamu. Mungu ni mwaminifu, naye hataruhusu mjaribiwe kupita nguvu zenu, ila pamoja na majaribu, yeye atawapeni pia nguvu ya kustahimili na njia ya kutoka humo salama.

Jehovah tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
 Mungu wetu tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa  katika utendaji
Yahweh nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba ukatupe neema ya kuweza kuwabariki wenye
kuhitaji Yahweh tusipungukiwe katika mahitaji yetu Jehovah ukatupe
kama inavyokupendeza wewe....

Mungu wetu tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Jehovah tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,watoto,wazazi wetu,
Familia/ndugu na wote wanaotuzunguka
Yahweh tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyovimiliki
Jehovah tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Yahweh ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Mungu wetu tunaomba ukavitakase na kuvifunika kwa Damu ya Bwana
wetu Yesu Kristo...
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatamalaki na kutuatamia
Jehovah tukawe salama rohoni Mungu wetu tunaomba ukatupe
macho ya kuona na masikio ya kusikia sauti yako na kuitii
Yahweh tunaomba ukatupe neema ya kutambua mema na mabaya
Mungu wetu ukatupe neema ya kufuata njia zako Jehovah tukasimamie
Neno lako amri na sheria zako siku zote za maisha yetu
Mungu wetu ukaonekane katika maisha yetu ..
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu upendo ukadumu kati yetu,ukatupe hekima na busara
katika maamuzi yetu 
Yahweh ukatufanye chombo chema Mungu wetu nasi tukatumike
kama inavyokupendeza wewe...
Roho Mtakatifu  akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi...



Kwa hiyo, wapenzi wangu, epeni ibada za sanamu. Naongea nanyi, watu wenye busara; jiamulieni wenyewe hayo nisemayo. Tunapomshukuru Mungu kwa kikombe kile cha baraka, je, huwa hatushiriki damu ya Kristo? Na tunapoumega mkate, je, huwa hatushiriki mwili wa Kristo? Kwa kuwa mkate huo ni mmoja, sisi, ingawa ni wengi, tu mwili mmoja; maana sote twashiriki mkate huohuo. Angalieni kwa mfano Wayahudi wenyewe: Wale wanaokula tambiko wanaungana na hiyo madhabahu. Nataka kusema nini, basi? Kwamba chakula kilichotambikiwa sanamu ni kitu zaidi ya chakula? Na hizo sanamu, je, ni kitu kweli zaidi ya sanamu? Hata kidogo! Ninachosema ni kwamba tambiko wanazotoa watu wasiomjua Mungu wanawatolea pepo, sio Mungu. Sipendi kamwe nyinyi muwe na ushirika na pepo. Hamwezi kunywa kikombe cha Bwana na kikombe cha pepo; hamwezi kushiriki katika Karamu ya Bwana na katika meza ya pepo. Au je, tunataka kumfanya Bwana awe na wivu? Mnadhani tuna nguvu zaidi kuliko yeye?

Yahweh tunawaweka mikononi mwako wote wanaokutafuta/kukuomba
kwa bidii na imani Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako
wenye nguvu,Baba wa Mbinguni tunaomba ukawatendee kila mmoja
na mahitaji yake,Jehovah tunaomba ukaonekane katika shida/tabu
zao Mungu wetu ukasikie kulia kwao Baba wa Mbinguni tunaomba
ukawafute machozi yao Mungu wetu tunaomba ukawasamehe pale
walipokwenda kinyume nawe Jehovah tunaomba ukawape neema
ya kujiombea,kufuata njia zako,kusimamia Neno lako nalo liwaweke
huru..Mungu wetu tunaomba ukasikie na ukapokee sala/maombi yetu
Baba wa Mbinguni ukawatendee sawasawa mapenzi yako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina...!!
Asanteni sana wapendwa katika Kristo Yesu kwakuwa nami
Mungu wetu aendelee kuwabariki na kuwalinda 
msipungukiwe katika mahitaji yenu Baba wa Mbinguni akawape 
kama inavyompendeza yeye...
Nawapenda.




Naamani aponywa

1Naamani, kamanda wa jeshi la mfalme wa Aramu alikuwa mtu mashuhuri aliyependwa sana na bwana wake, kwani kwa njia yake Mwenyezi-Mungu aliiletea nchi ya Aramu ushindi. Alikuwa askari hodari, lakini alikuwa na ugonjwa wa ukoma. 2Katika vita walivyokuwa wakipigana na Israeli, Waaramu walikuwa wamemchukua msichana mmoja mdogo kutoka Israeli, naye akawa anamtumikia mke wa Naamani. 3Siku moja akamwambia bibi yake, mke wa Naamani, “Laiti bwana wangu angekwenda na kumwona yule nabii aliyeko Samaria! Angemponya ugonjwa wake.” 4Naamani alipopata habari hizi, akaenda kwa mfalme na kumweleza habari za mtoto huyu. 5Mfalme wa Aramu akamwambia, “Chukua barua hii umpelekee mfalme wa Israeli.”
Hivyo Naamani akaondoka, huku amechukua vipande 30,000 vya fedha, vipande 6,000 vya dhahabu na mavazi kumi ya sikukuu. 6Barua yenyewe iliandikwa hivi,
“Barua hii ni ya kumtambulisha kwako ofisa wangu Naamani. Nataka umtibu huu ugonjwa wake.”
7Mfalme wa Israeli aliposoma barua hii alirarua mavazi yake na kusema, “Mbona mfalme wa Aramu anataka nimtibu mtu huyu ukoma wake? Kwani anafikiri mimi ni Mungu aliye na uwezo wa kuua au kufufua? Fahamuni basi, mwone ya kwamba mtu huyu anataka kuniletea mzozo.”
8Elisha, nabii wa Mungu, alipopata habari kwamba mfalme wa Israeli ameyararua mavazi yake, alituma ujumbe kwa mfalme, akamwuliza, “Mbona umeyararua mavazi yako? Mlete mtu huyo kwangu, ili apate kujua kwamba kuna nabii katika Israeli?”
9Naamani akaenda na farasi wake na gari lake mpaka mlangoni mwa Elisha. 10Elisha akamtuma mtumishi wake amwambie, “Nenda ukaoge mara saba mtoni Yordani, nawe utapona kabisa.” 11Lakini Naamani alikasirika sana, akaenda zake akisema, “Nilidhani kwamba hakika atanijia na kumwomba Mwenyezi-Mungu, Mungu wake, apitishe mikono yake juu ya mahali ninapougua5:11 mahali ninapougua: Mahali hapa. na kuniponya! 12Isitoshe, je, mito Abana na Farpari ya huko Damasko si bora kuliko mito yote ya Israeli? Je, nisingeweza kuoga humo na kupona?” Akaondoka na kurudi nyumbani, huku amekasirika sana.
13Watumishi wake wakamwendea na kumwambia, “Baba yetu kama nabii angekuambia ufanye jambo fulani gumu, je, hungelifanya? Sasa, aliyokuambia tu ni: ‘Jioshe, ili upone!’” 14Basi, Naamani akateremka mtoni Yordani akajitumbukiza humo mara saba, kama alivyoagizwa na Elisha mtu wa Mungu, naye akapona kabisa. Ngozi yake ikawa imara na yenye afya kama ya mtoto mdogo. 15Ndipo akarudi kwa mtu wa Mungu pamoja na watu wake, akasema, “Sasa najua kwamba hakuna Mungu yeyote ila tu Mungu wa Israeli; kwa hiyo, tafadhali sasa upokee zawadi za mtumishi wako.”
16Elisha akajibu, “Naapa kwa Mwenyezi-Mungu aliye hai ambaye ninamtumikia, kwamba sitapokea zawadi yoyote.”
Naamani akamsihi, lakini Elisha akakataa kabisa. 17Naamani akasema, “Ikiwa hutapokea zawadi zangu, basi tafadhali umpatie mtumishi wako udongo unaoweza kubebwa na nyumbu wawili, kwani toka leo mimi mtumishi wako sitatoa sadaka za kuteketezwa wala tambiko kwa miungu mingine ila tu kwa Mwenyezi-Mungu. 18Naye Mwenyezi-Mungu na anisamehe ninapofuatana na mfalme wangu kwenda kuabudu katika hekalu la Rimoni mungu wa Aramu. Naomba Mwenyezi-Mungu anisamehe!” 19Elisha akamwambia, “Nenda kwa amani.” Naamani akaenda zake.
Alipokuwa bado hajaenda mbali, 20Gehazi, mtumishi wa Elisha mtu wa Mungu, akasema, “Tazama, bwana wangu amemwachilia Naamani Mwaramu aende bila kupokea chochote alicholeta. Kama Mwenyezi-Mungu aishivyo nitamfuata ili nipate kitu kutoka kwake.” 21Hapo akaondoka kumfuata Naamani. Naamani alipotazama na kuona mtu anamfuata mbio, akashuka garini mwake akaenda kukutana naye. Basi, akamwuliza, “Je, kuna usalama?” 22Gehazi akajibu, “Mambo yote ni sawa ila tu bwana wangu amenituma nikuambie kwamba sasa hivi amepokea watu wawili wa kundi la manabii katika nchi ya milima ya Efraimu, naye angependa uwape vipande 3,000 vya fedha na mavazi mawili ya sikukuu.”
23Naamani akasema, “Tafadhali chukua vipande 6,000 vya fedha.” Akamsihi, kisha akamfungia mafungu mawili na kumpa mavazi mawili ya sikukuu, akawapa watumishi wake wawili na kuwaagiza wafuatane na Gehazi. 24Walipofika mlimani alipoishi Elisha, Gehazi akachukua mafungu ya fedha kutoka kwa watumishi wa Naamani na kuyapeleka ndani, nyumbani mwake. Kisha akawaruhusu wale watumishi waende zao, nao wakaondoka.
25Halafu Gehazi akaingia nyumbani kwa Elisha na kuanza kumhudumia. Elisha akamwuliza, “Ulikwenda wapi?” Gehazi akajibu, “Sikuenda mahali popote.” 26Lakini Elisha akamwambia, “Kwani roho yangu haikuwa pamoja nawe wakati mtu yule alipotoka garini mwake na kuja kukutana nawe? Je, huu ndio wakati wa kupokea fedha na mavazi, mashamba ya mizeituni na mizabibu, kondoo na ng'ombe au watumishi wa kiume na wa kike? 27Kwa hiyo ukoma wa Naamani utakushika wewe, na wazawa wako milele.” Basi, Gehazi aliondoka akiwa tayari ameshikwa na ukoma, na ngozi yake ilikuwa nyeupe kama theluji.





2Wafalme5;1-27


Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: