Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Wednesday 7 February 2018

Kikombe Cha Asubuhi ; 2 Samueli 7...



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Haleluyah Mungu wetu yu mwema sana..

Tumshukuru Mungu wetu katika yote..

Asante Mungu wetu kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako wakati wote kwetu
Asante kwakutuchagua tena na kutupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwa tayari kwa majukumu yetu
Utukuzwe ee Mungu wetu, Mungu mwenye nguvu,Mungu wa Wajane,Baba wa Yatima,Mungu wa walio hai,Mungu mwenye huruma,Mungu unayeponya,Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo..
Neema yako yatutosha ee Mungu wetu..!!

Enyi watu wote, pigeni makofi! Msifuni Mungu kwa sauti za shangwe! Maana Mwenyezi-Mungu, Mungu Mkuu, anatisha. Yeye ni Mfalme mkuu wa ulimwengu wote. Ametuwezesha kuwashinda watu wa mataifa, ameyaweka mataifa chini ya mamlaka yetu. Ametuchagulia nchi hii iwe urithi wetu, ambayo ni fahari ya Yakobo anayempenda. Mungu amepanda juu na vigelegele, Mwenyezi-Mungu na sauti ya tarumbeta. Mwimbieni Mungu sifa, mwimbieni! Mwimbieni mfalme wetu sifa, mwimbieni! Mwimbieni Mungu sifa kwa tenzi; maana yeye ni mfalme wa ulimwengu wote. Mungu anayatawala mataifa yote; amekaa katika kiti chake cha enzi kitakatifu. Viongozi wa watu wa mataifa wanakusanyika, wanajiunga na watu wa Mungu wa Abrahamu, maana nguvu zote duniani ni zake Mungu, yeye ametukuka sana.

Yahweh tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako
Jehovah tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizozifanya
Kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua
Baba wa mbinguni tunaomba nasi utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea
Yahweh utuepushe katika majaribu Mungu wetu utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote..
Nguvu za giza,nguvu za mapepo,nguvu za mizimu,nguvu za mpinga Kristo zishindwe katika jina la Bwana wetu Yesu Kristo..
Jehovah ututakase miili yetu na akili zetu Yahweh utufunike kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo wa Nazareti yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona..

Mwenyezi-Mungu wa majeshi asema, “Tazama, namtuma mjumbe wangu anitangulie kunitayarishia njia. Bwana mnayemtafuta atalijia hekalu lake ghafla. Mjumbe mnayemtazamia kwa hamu kubwa atakuja na kutangaza agano langu.” Lakini ni nani atakayestahimili siku hiyo atakapokuja? Ni nani atakayesimama kustahimili atakapotokea? Yeye ni kama moto mkali usafishao chuma; ni kama sabuni ya dobi. Yeye atakuja kuhukumu kama mtu asafishaye na kutakasa fedha. Atawasafisha wazawa wa Lawi, kama mtu afuavyo dhahabu au fedha, mpaka wamtolee Mwenyezi-Mungu tambiko zinazokubalika. Hivyo, tambiko za watu wa Yuda na wa Yerusalemu zitampendeza Mwenyezi-Mungu kama za watu wa kale; kama katika miaka ya zamani. Mwenyezi-Mungu wa majeshi asema: “Kisha nitawakaribia ili kuwahukumu. Sitasita kutoa ushahidi dhidi ya wachawi, wazinzi, watoa ushahidi wa uongo, wanaowapunja waajiriwa, wanaowadhulumu wageni na wale wasionicha mimi.

Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Jehovah tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa katika utendaji
Yahweh tukatende sawasawa na mapenzi yako..
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Jehovah tunaomba nasi utupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji,Yahweh tusipungukiwe kwenye mahitaji yetu Baba wa Mbinguni ukatupe kama inavyokupendeza wewe..

“Mimi ni Mwenyezi-Mungu, mimi sibadiliki. Lakini nyinyi, nyinyi wazawa wa Yakobo hamjatoweka bado. Tangu wakati wa wazee wenu, mmezidharau kanuni zangu wala hamkuzifuata. Basi, mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu Mkuu nasema: Nirudieni, nami nitawageukieni. Lakini nyinyi mnauliza, ‘Tutakurudia namna gani?’ Nami nawaulizeni, Je, ni sawa mtu kumdanganya Mungu? La! Lakini nyinyi mnanidanganya! Walakini nyinyi mwauliza: ‘Tunakudanganya kwa namna gani?’ Naam! Mnanidanganya kuhusu zaka na tambiko zenu. Nyinyi na taifa lenu lote mmelaaniwa kwa sababu ya kunidanganya. Leteni ghalani mwangu zaka yote, ili nyumbani mwangu kuwe na chakula cha kutosha. Kisha mwaweza kunijaribu. Nijaribuni namna hiyo nanyi mtaona kama sitayafungua madirisha ya mbinguni na kuwatiririshia baraka tele. Wadudu waharibifu nitawakemea wasiyaharibu tena mazao yenu. Mizabibu yenu mashambani haitaacha kuzaa matunda. Mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi nimesema. Ndipo mataifa yote yatawaita nyinyi watu waliobarikiwa, maana nchi yenu itakuwa nchi ya furaha. Mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu Mkuu nimesema.”


Mfalme wa amani tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Yahweh amani yako ikatawale katika nyumba/ndoa zetu
Mungu wetu ukabariki watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka..
Baba wa Mbinguni tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyomiliki,Yahweh tunaomba ukatamalaki na kutuatamia
Mungu wetu ukatubariki tuingiapo/tutokapo Yahweh ukabariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia Jehovah ukavitakase  na kuvifunika kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo..
Baba wa Mbinguni tunaomba uwepo wako Yahweh ukatuguse kwa mkono wako wenye nguvu Mungu wetu tukawe salama moyoni Baba wa Mbinguni ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia sauti yako na kuitii,Mungu wetu ukatupe neema ya kufuata njia zako Yahweh tukasimamie Neno lako amri na sheria zako siku zote za maisha yetu
Tukawe Barua njema Mungu wetu popote tupitapo tukasomeke kama inavyokupendeza wewe..
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi..


Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Maneno yenu yamekuwa mzigo kwangu. Hata hivyo mnasema, ‘Tumesema nini dhidi yako?’ Nyinyi mmesema, ‘Kumtumikia Mungu hakuna faida. Kuna faida gani kuyatii maagizo ya Mwenyezi-Mungu wa majeshi, au kujaribu kumwonesha kuwa tumekosa mbele yake kwa kutembea kama watu wanaoomboleza? Tuonavyo sisi, ni kwamba, wenye kiburi ndio wenye furaha daima. Watu waovu, licha ya kustawi, hata wanapomjaribu Mungu, hawapati adhabu.’” Ndipo watu wanaomcha Mwenyezi-Mungu walipozungumza wao kwa wao, naye Mwenyezi-Mungu akasikia mazungumzo yao. Mbele yake kikawekwa kitabu ambamo iliandikwa kumbukumbu ya wale wanaomcha na kumheshimu. Iliandikwa hivi: Mwenyezi-Mungu asema: “Hao watakuwa watu wangu. Watakuwa urithi wangu maalumu siku ile nitakapoinuka kufanya ninalokusudia. Sitawadhuru kama vile baba asivyomdhuru mwanawe anayemtumikia. Hapo ndipo mtakapotambua tena tofauti iliyopo kati ya waadilifu na waovu; naam, kati ya mtu anayemtumikia Mungu na asiyemtumikia.”


Yahweh tunaomba uponyaji wako kwa wote wali wagonjwa,wanaopitia magumu/majaribu,wenye njaa,waliokata tamaa,waliokataliwa,walio katika vifungo vya yule mwovu,walio magerezani pasipo na hatia,wenye hofu na mashaka,wafiwa ukawe mfariji wao,Wanaotafuta watoto,Baba wa Mbinguni tunaomba ukawafungue matumbo yao,Mungu wetu ukawaokoe na kuwabariki,Baba wa Mbinguni ukawasamehe,Yahweh ukawape neema ya kujiombea na kufuata njia zako,Nuru yako ikaangaze katika maisha yao
Baba wa Mbinguni ukawape macho ya rohoni,ukawaponye kimwili na kiroho,Yahweh ukawape masikio ya kusikia sauti yako,Mungu wetu ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu na neema yako ikawe nao
Mungu wetu tunaomba ukasikie kulia kwao Baba wa Mbinguni ukawatendee sawasawa na mapenzi yako..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina..!!

Asanteni sana wapendwa katika Kristo Yesu kwakuwa nami
Baba wa Mbinguni akawalinde na kuwaongoza msipungukiwe katika mahitaji yenu Mungu Baba akawape kinacho wafaa..
Nawapenda.

Unabii wa Nathani kwa Daudi

(1Nya 17:1-15)

1Wakati mfalme Daudi alipokuwa akikaa katika ikulu, naye Mwenyezi-Mungu amemuwezesha kuwa na amani na adui zake kila upande, 2mfalme Daudi akamwambia nabii Nathani, “Hebu tazama; mimi ninakaa katika nyumba iliyojengwa kwa mierezi, lakini sanduku la Mungu linakaa hemani.” 3Nathani akamwambia mfalme, “Nenda ufanye chochote unachofikiria moyoni mwako, kwa kuwa Mwenyezi-Mungu yu pamoja nawe.” 4Lakini usiku uleule neno la Mwenyezi-Mungu lilimjia Nathani, 5“Nenda ukamwambie mtumishi wangu Daudi, ‘Mwenyezi-Mungu asema hivi: Je, wewe utanijengea nyumba ya kukaa? 6Tangu siku ile nilipowatoa Waisraeli nchini Misri mpaka hivi leo sijaishi kwenye nyumba. Nimetembea kila mahali nikiwa ninakaa hemani. 7Je, kila mahali ambako nimekwenda na Waisraeli wote nimemwuliza mtu yeyote wa Israeli ambaye nilimwamuru awachunge watu wa Israeli: Kwa nini hajanijengea nyumba ya mierezi? 8Kwa hiyo basi, mwambie mtumishi wangu Daudi: Mwenyezi-Mungu wa majeshi anasema hivi: Nilikutoa malishoni ulikokuwa unawachunga kondoo, ili uwe mkuu wa watu wangu Israeli. 9Tangu wakati huo nimekuwa pamoja nawe kokote ulikokwenda na nimewaangamiza adui zako wote mbele yako. Nitakufanya kuwa maarufu kama wakuu wengine duniani. 10Nami nitawachagulia watu wangu wa Israeli mahali pa kuishi, niwapandikize, ili waishi mahali pao wenyewe, wasisumbuliwe tena. Nao watu wakatili wanaotumia nguvu hawatawatesa tena kama hapo awali, 11tangu wakati nilipowateua waamuzi juu ya watu wangu Israeli, nami nitakulinda kutokana na adui zako wote. Zaidi ya yote, mimi Mwenyezi-Mungu nakutangazia kuwa nitakujengea nyumba. 12Siku zako zitakapotimia na utakapofariki na kujiunga na babu zako, nitamfanya mmoja wa watoto wako wewe mwenyewe awe mfalme, nami nitauimarisha ufalme wake. 13Yeye ndiye atakayejenga nyumba kwa ajili ya jina langu na kiti chake cha enzi cha ufalme wake nitakiimarisha milele. 14Mimi nitakuwa baba yake, naye atakuwa mwanangu. Akifanya maovu, nitamrudi kama wanadamu wanavyowarudi wana wao kwa fimbo. 15Lakini sitamwondolea fadhili zangu kama vile nilivyoziondoa kwa Shauli, niliyemwondoa mbele yako. 16Ukoo wako na ufalme wako vitadumu imara daima. Kiti chako cha enzi kitakuwa imara milele.’” 17Nathani alimweleza Daudi kila kitu ambacho alioneshwa katika maono hayo na Mungu.

Sala ya Daudi ya shukrani

(1Nya 17:16-27)

18Kisha mfalme Daudi akaingia ndani na kuketi mbele ya Mwenyezi-Mungu; halafu akaomba, “Mimi ni nani ee Bwana Mungu, na jamaa yangu ni nini hata ukaniinua mpaka hapa nilipo leo! 19Tena jambo hili lilikuwa dogo machoni pako, Bwana Mungu; zaidi ya hayo umeiahidi jamaa yangu mambo makubwa katika miaka mingi ijayo; na kwamba umenijalia kuona hayo,7:19 kuona hayo: Au vijavyo: Makala ya Kiebrania: Hii ndiyo Sheria ya mtu. Ee Bwana Mungu. 20Nikuambie nini zaidi, mimi Daudi, mtumishi wako? Kwani wewe unanijua mimi mtumishi wako, ee Bwana Mungu! 21Kutokana na ahadi yako na kulingana na moyo wako, umetenda makuu hayo yote ili unijulishe mimi mtumishi wako. 22Kutokana na yale tuliyosikia, wewe Mwenyezi-Mungu ni mkuu; hakuna aliye kama wewe, na hakuna Mungu mwingine ila wewe. 23Tena ni watu gani duniani ambao wanaweza kufananishwa na watu wako7:23 watu … wako: Makala ya Kiebrania: Mbele ya watu wako, ambao uliwakomboa kwa ajili yako kutoka Misri, mataifa na miungu. wa Israeli, ambao Mungu wake alikwenda kuwakomboa ili wawe watu wake? Wewe ee Mungu ulijifanyia jina na kujitendea mambo makubwa na ya ajabu kwa ajili ya nchi yako mbele ya watu wako ambao kwa ajili yako mwenyewe uliwaokoa kutoka Misri, ukayafukuza mataifa na miungu yake mbele yao? 24Hata umewaimarisha watu wako wa Israeli kwa ajili yako mwenyewe, ili wawe watu wako milele; nawe ee Mwenyezi-Mungu umekuwa Mungu wao. 25Basi, sasa, ee Mwenyezi-Mungu, ikamilishe ile ahadi uliyosema kuhusu mimi mtumishi wako na kuhusu jamaa yangu kama ulivyoahidi. 26Nalo jina lako litatukuzwa milele, nao watu watasema, ‘Mwenyezi-Mungu wa majeshi ni Mungu juu ya Israeli!’ Na jamaa yangu, mimi Daudi mtumishi wako, itaimarika mbele yako. 27Maana wewe, ee Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, umenifunulia mimi mtumishi wako, ukisema ‘Nitakujengea nyumba;’ ndio maana nina ujasiri kutoa ombi hili mbele yako. 28Sasa, ee Bwana Mungu, wewe ndiwe Mungu, na maneno yako ni kweli na umeniahidi mimi mtumishi wako jambo hili jema; 29kwa hiyo, nakuomba nyumba yangu mimi mtumishi wako ipate kudumu milele mbele yako; kwani wewe umesema hivyo, pia kwa baraka zako nyumba yangu itabarikiwa milele.”


2Samweli7;1-29

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: