Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Thursday 11 January 2018

Kikombe Cha Asubuhi ;1Samueli19...



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Haleluyah Mungu wetu yu mwema sana....
Tumshukuru Mungu katika yote....

Asante Baba wa Mbinguni kwa wema na fadhili zako kwetu.
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwa tayari kwa majukumu yetu
Utukuzwe ee Mungu wetu,Usifiwe Baba wa mbinguni..
Matendo yako ni makuu sana,Matendo yako ni ya ajabu,
Hakuna kama wewe ee Mungu wetu,Neema yako yatutosha 
Unastahili kuabudiwa,Unastahili Kuhimidiwa..
Hakuna lililo gumu mbele zako..
Sifa na Utukufu tunakurudishia Mungu wetu..

Mimi Paulo na Timotheo, watumishi wa Yesu Kristo, tunawaandikia nyinyi watu wa Mungu huko Filipi ambao mmeunganishwa na Kristo Yesu, pamoja na viongozi na wasaidizi wa kanisa. Tunawatakieni neema na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu na kutoka kwa Bwana Yesu Kristo.

Tunakuja mbele zako Mungu Baba tukijinyenyekeza,tukijushusha na kujiachilia mikononi mwako Yahweh..
Baba wa Mbinguni tunaomba utusamehe dhambi zetu zote
tulizozifanya kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua
Mungu wetu nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea..
Yahweh tunaomba utuepushe katika majaribu Jehovah utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote..
Baba wa Mbinguni tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu
Jehovah utufunike kwa Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona..


Namshukuru Mungu wangu kila ninapowakumbukeni; na kila ninapowaombeeni nyote, nasali kwa furaha, kwa sababu ya jinsi mlivyonisaidia katika kazi ya Injili tangu siku ile ya kwanza mpaka leo. Basi, nina hakika kwamba Mungu aliyeanza kazi hii njema ndani yenu, ataiendeleza mpaka ikamilike katika siku ile ya Kristo Yesu. Hivyo ndivyo ninavyopaswa kuwafikirieni, kwani nawakumbukeni daima moyoni mwangu. Kwa maana nyinyi nyote mmeshiriki katika fadhili aliyonijalia Mungu ya kutetea na kuithibitisha Injili, sasa niwapo kifungoni na pia pale awali nilipokuwa huru. Mungu anajua kuwa ninasema ukweli ninaposisitiza kwamba, kwa upendo uleule wa Yesu Kristo, natamani sana kuwaoneni. Sala yangu ni hii: Naomba upendo wenu uzidi kuongezeka zaidi na zaidi pamoja na ujuzi wa kweli na busara ya kila namna, ili muweze kuchagua jambo lililo bora. Hapo ndipo mtakuwa safi na bila lawama yoyote ile katika siku ile ya Kristo. Maisha yenu yatajazwa mambo yote yaliyo kweli bora, ambayo Yesu Kristo mwenyewe anaweza kuwajalieni, kwa ajili ya utukufu na sifa ya Mungu.
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu Jehovah ukatupe ubunifu na maarifa katika ufanyaji/utendaji Yahweh nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako..
Mungu wetu tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Yahweh nasi tunaomba ukatupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji..

Mfalme wa amani tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Mungu Baba tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka..
Mungu wwetu tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyovimiliki..
Mungu wetu ukatulinde na kutuongoza tuingiapo/tutokapo na vyote tunavyoenda kugusa/kutumia Yahweh tunaomba ukavibariki na kuvitakasa kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo..
Mungu Baba tunaomba ukatupe neema ya unyenyekevu,utuwema,fadhili,hekima,busara,tukanene yaliyo yako na yote yanayokupendeza wewe..
Baba wa Mbinguni ukatuepushe na kiburi,majivuno,kujisifu,choyo,chuki,uchonganishi,makwazo kwa wengine na yote yanayokwenda kinyume nawe.
Yahweh tukawe salama moyoni,Mungu wetu ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia sauti yako na kuitii..
Jehovah tunaomba utupe neema ya kufuata njia zako Yahweh kusimamia Neno lako amri na sheria zako siku zote za maisha yetu..
Mungu wetu ukaonekane popote tupitapo na ikajulikane kwamba upo Baba wa Mbinguni..
Yahweh tukawe barua njema nasi tukasomeke kama inavyokupendeza wewe..
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi..


Ndugu zangu, napenda mfahamu kwamba mambo yote yaliyonipata yamesaidia sana kuieneza Injili. Kutokana na hayo, walinzi wote wa ikulu pamoja na wengine wote hapa wanafahamu kwamba niko kifungoni kwa sababu mimi namtumikia Kristo. Na huku kuweko kwangu kifungoni kumewafanya ndugu wengi kuwa na imani kwa Bwana, hata wanazidi kuwa hodari katika kuutangaza ujumbe wa Mungu bila hofu. Kweli, baadhi yao wanamhubiri Kristo kwa sababu wana wivu na ni watu wagomvi; lakini wengine wanamhubiri Kristo kwa nia nzuri. Hawa wanafanya hivyo kwa upendo, kwani wanajua kwamba Mungu amenipa jukumu hili la kuitetea Injili. Hao wengine wanamtangaza Kristo kwa mashindano na si kwa moyo mnyofu, wakidhani kwamba wataniongezea mateso yangu kifungoni. Haidhuru! Mimi nafurahi ikiwa tu watu wanamhubiri Kristo kwa kila njia, iwe ni kwa nia nzuri au kwa nia mbaya. Tena nitaendelea kufurahi, kwani najua kwamba kwa sala zenu na kwa msaada wa Roho wa Yesu Kristo, nitakombolewa. Hamu yangu kubwa na tumaini langu ni kwamba kwa vyovyote sitashindwa katika kutimiza wajibu wangu, bali nitakuwa na moyo thabiti kila wakati na hasa wakati huu, ili kwa maisha yangu yote, niwapo hai au nikifa, nimpatie Kristo heshima. Kwangu, kuishi ni Kristo, na kufa ni faida zaidi. Lakini, kama kwa kuishi nitaweza kufanya kazi yenye faida zaidi, basi, sijui nichague lipi! Nakabiliwa na haya mawili yaliyo sawa. Natamani kuyaacha maisha haya nikakae pamoja na Kristo, jambo ambalo ni bora zaidi; lakini ni jambo la maana zaidi kwenu kama nikiendelea kuishi. Nina hakika ya jambo hili, na hivyo najua kwamba nitaendelea kuishi pamoja nanyi nyote, ili nipate kuongeza maendeleo yenu na furaha katika imani. Basi, nitakapokuwa nanyi tena mtakuwa na sababu ya kuona fahari juu yangu katika kuungana na Kristo Yesu. Basi, jambo muhimu ni kwamba mwenendo wenu uambatane na matakwa ya Injili ya Kristo, ili kama nikiweza kuja kwenu au nisipoweza, nipate walau kusikia kwamba mnasimama imara mkiwa na lengo moja, na kwamba mnapigana vita kwa pamoja na mnayo nia moja kwa ajili ya imani ya Injili. Msiwaogope maadui zenu, bali muwe hodari daima, na hiyo itawathibitishia kwamba wao watashindwa, nanyi mtashinda kwani Mungu mwenyewe ndiye anayewapeni ushindi. Maana nyinyi mmepewa fadhili ya kumtumikia Kristo si tu kwa kumwamini bali pia kwa kuteswa kwa ajili yake. Sasa mwaweza kushirikiana nami katika kupigana vita. Vita hivi ni vile mlivyoona nikipigana pale awali na ambavyo bado napigana sasa kama mnavyosikia.

Asante kwa uponyaji wako Mungu wetu,Asante kwa uwepo wako katika shida zetu,Mungu wetu tulikuita nawe ukaitika,Yahweh umetutendea mengi ya ajabu,mkono wako umetugusa na tumevuka salama...
Kwako Mungu hakuna linaloshindikana Yahweh umetutendea..!!

Baba kama ulivyowaponya watoto ,ndugu,jamaa,watu wako  tunaomba ukatende miujiza kwa wengine wanaohitaji uponyaji wako..
Yahweh ukawaongoze waganga,wauguzi na wahudumu wote
Mungu wetu ukawape macho na mkono wako wenye nguvu ukawaguse wagonjwa,wenye shida/tabu Baba wa Mbinguni ukawape nguvu/uvumili na imani wanaowauguza,Yahweh ukawe tumaini kwa waliokata tamaa,waliokataliwa,wenye hofu na mashaka Mungu wetu ukawavushe salama wale walio katika magumu/majaribu mbalimbali Mungu wetu ukawaokoe na kuwaweka huru wale walio katika vifungo vya yule mwovu
na walio magerezani pasipo na hatia Mungu wetu tunaomba haki ikatendeke,Yahweh ukawalishe wenye njaa Mungu wetu ukawasamehe wale walikwenda kinyume nawe..
Baba wa Mbinguni ukawape neema ya kujiombea na kufuata njia zako nazo ziwaweke huru..
Mungu wetu ukasikie kulia kwao Yahweh ukawafute machozi ya watoto wako wanaokuomba kwa bidii na imani..
Mungu wetu ukawatendee sawasawa na mapenzi yako..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina..!!

Asanteni sana wapendwa katika Kristo Yesu kwakuwa nami
Mungu wetu aendelee kuwabariki na kuwatendea sawasawa na mapenzi yake..
Nawapenda.

Shauli anamwandama Daudi

1Shauli alimweleza mwanawe Yonathani na maofisa wake juu ya mpango wake wa kumwua Daudi. Lakini Yonathani, mwanawe Shauli, alimpenda sana Daudi. 2Kwa hiyo, akamwambia, “Baba yangu anakusudia kukuua. Hivyo, jihadhari. Kesho asubuhi, jifiche mahali pa siri, ukae hapo. 3Mimi nitakuja na kusimama karibu na baba yangu huko shambani mahali utakapokuwa. Hapo nitaongea naye juu yako, na kitu chochote nitakachogundua kutoka kwake, nitakueleza.”
4Yonathani alimsifu Daudi mbele ya baba yake, akamwambia, “Usitende dhambi dhidi ya mtumishi wako Daudi kwani yeye hajatenda dhambi yoyote dhidi yako; matendo yake yote anapokutumikia daima yamekuwa mema kwako. 5Alipomuua yule Mfilisti Goliathi, alihatarisha maisha yake, naye Mwenyezi-Mungu aliwapa Waisraeli ushindi mkubwa. Wewe ulipoona jambo lile ulifurahi. Kwa nini unataka kutenda dhambi kwa kumwaga damu isiyo na hatia kwa kumwua Daudi bila sababu?”
6Shauli alimsikiliza Yonathani, kisha akaapa, “Naapa kwa Mwenyezi-Mungu aliye hai, sitamuua Daudi.” 7Hivyo, Yonathani akamwita Daudi na kumweleza mambo hayo yote. Yonathani akampeleka Daudi kwa Shauli, na Daudi akamtumikia Shauli kama hapo awali.
8Baadaye kulikuwa na vita tena kati ya Wafilisti na Waisraeli. Daudi alitoka akapigana na Wafilisti, akawaua Wafilisti wengi na waliosalia wakamkimbia. 9Kisha, roho mbaya kutoka kwa Mwenyezi-Mungu alimjia Shauli alipokuwa amekaa nyumbani kwake akiwa ameshika mkuki mkononi, wakati ambapo Daudi alikuwa akipiga kinubi. 10Shauli alijaribu kumchoma Daudi kwa mkuki huo, Lakini Daudi alikwepa mkuki wa Shauli na mkuki ukapiga ukuta. Daudi akakimbia na kutoroka.
11Usiku huo, Shauli alituma watu nyumbani kwa Daudi wamwangalie kama yuko ili apate kumwua asubuhi. Lakini Mikali, mke wa Daudi akamwambia Daudi, “Kama huyasalimishi maisha yako usiku huu kesho utauawa.” 12Hivyo Mikali akamteremsha Daudi kupitia dirishani, naye akatoka na kutoroka. 13Mikali akachukua kinyago, akakilaza kitandani na kichwani pake akaweka mto wa manyoya ya mbuzi. Kisha akakifunika kwa nguo. 14Shauli alipotuma watu kumshika Daudi, Mikali akawaambia kuwa Daudi ni mgonjwa. 15Kisha Shauli aliwatuma warudi huko tena, akawaagiza akisema, “Mlete kwangu Daudi hata akiwa kitandani ili auawe.” 16Wale watu walipoingia nyumbani kwa Daudi na kukiangalia kitanda waliona kuna kinyago na mto wa manyoya ya mbuzi kichwani. 17Halafu Shauli akamwuliza Mikali, “Kwa nini umenidanganya? Umemwacha adui yangu atoroke?” Naye Mikali akamjibu Shauli, “Aliniambia, ‘Niache niende nisije nikakuua.’”
18Daudi alipotoroka, alikwenda Rama kwa Samueli. Alimweleza Samueli mambo yote aliyomfanyia Shauli. Basi, Daudi na Samueli walikwenda na kukaa huko Nayothi. 19Baadaye Shauli aliambiwa kuwa Daudi alikuwa huko Nayothi katika Rama. 20Ndipo Shauli alipopeleka watu wakamkamate. Lakini walipolikuta19:20 walipolikuta: Makala ya Kiebrania alipolikuta. kundi la manabii likitabiri na Samueli akiliongoza, roho ya Mungu iliwajia wale watumishi wa Shauli, nao pia wakaanza kutabiri. 21Shauli alipoambiwa habari hizo, alituma watumishi wengine, nao pia wakaanza kutabiri. Shauli alipotuma watumishi wengine kwa mara ya tatu, nao pia wakaanza kutabiri. 22Ndipo yeye mwenyewe akaenda Rama. Alipofika kwenye kisima kikubwa kilichoko huko Seku, alimkuta mtu fulani ambaye alimwuliza, “Samueli na Daudi wako wapi?” Huyo mtu alimjibu, “Wako Nayothi, katika Rama.” 23Naye Shauli akaenda huko Nayothi katika Rama. Alipofika huko, roho ya Mungu ilimjia, naye alianza kutabiri akiwa njiani mpaka alipofika Nayothi katika Rama.
24Alivua mavazi yake akawa anatabiri mbele ya Samueli. Alibaki uchi kwa siku moja, mchana na usiku. Kwa hiyo watu walianza kujiuliza, “Je, Shauli naye pia amekuwa mmoja wa manabii?”


1Samweli19;1-24
Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: