Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Friday 5 January 2018

Kikombe Cha Asubuhi ;1Samueli15...



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Mungu wetu yu mwema tumshukuru katika yote..

Asante Mungu wetu Baba yetu kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote..
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwa tayari kwa majukumu yetu..
Utukuzwe ee Mungu wetu,Mungu mwenye nguvu,Mungu mwenye huruma..
Mungu wa walio hai,Mungu wa upendo,wewe ukisema ndiyo hakuna wakupinga..
Neema yako yatutosha Mfalme wa Amani..!!!



Basi, ikiwa mmefufuka pamoja na Kristo, panieni mambo ya juu, kule Kristo aliko, ameketi upande wa kulia wa Mungu. Muwe na hamu ya mambo ya huko juu, na siyo mambo ya hapa duniani. Maana nyinyi mmekufa na uhai wenu umefichwa pamoja na Kristo katika Mungu. Uhai wenu halisi ni Kristo, na wakati atakapotokea ndipo nanyi pia mtakapotokea pamoja naye katika utukufu.

Mungu wetu tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako..
Yahweh tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizozifanya
kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua..
Jehovah nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea..
Baba wa Mbinguni tunaomba utuepushe katika majaribu Mungu wetu
tunaomba utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote..
Nguvu za giza,nguvu za mapepo,nguvu za mizimu,nguvu za mpinga Kristo
zishindwe katika jina la Yesu..
Jehovah  tunaomba  ututakase miili yetu na akili zetu
Yahweh utufunike kwa Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona..




Basi, ueni chochote kilicho ndani yenu ambacho ni cha kidunia: Uasherati, uchafu, shauku, tamaa mbaya na uchu (ambao ni sawa na kuabudu sanamu). Kwa sababu ya mambo hayo hasira ya Mungu huwajia wote wanaomwasi. Wakati mmoja nyinyi pia mliishi kufuatana na mambo hayo, mlipotawaliwa nayo. Lakini sasa mnapaswa kuachana na mambo haya yote: Hasira, tamaa na uovu; kufuru au maneno yasiyofaa yasitoke kamwe vinywani mwenu. Msiambiane uongo, kwani nyinyi mmekwisha vua ule utu wa kale pamoja na matendo yake yote, mkavaa utu mpya. Huu unaendelea kurekebishwa na Mungu, Muumba wake, kadiri ya mfano wake, ili mpate kumjua Mungu kwa ukamilifu. Katika hali hii, hakuna tena tofauti kati ya Mgiriki na Myahudi, aliyetahiriwa na asiyetahiriwa, msomi na asiye msomi, mtumwa na mtu aliye huru. Kristo ni kila kitu, na yumo katika yote. Nyinyi ni watu wake Mungu; yeye aliwapenda na kuwateua. Kwa hiyo, basi, vaeni moyo wa huruma, wema, unyenyekevu, upole na uvumilivu. Vumilianeni na kusameheana iwapo mmoja wenu analo jambo lolote dhidi ya mwenzake. Mnapaswa kusameheana kama Bwana alivyowasamehe nyinyi. Zaidi ya hayo yote, zingatieni upendo, kwani upendo huunganisha kila kitu katika umoja ulio kamili. Nayo amani ya Kristo itawale mioyoni mwenu; maana kwa ajili hiyo nyinyi mmeitwa katika mwili huo mmoja. Tena muwe na shukrani! Ujumbe wa Kristo na ukae ndani yenu pamoja na utajiri wake wote. Fundishaneni na kushauriana kwa hekima yote. Imbeni Zaburi, nyimbo na tenzi za kiroho; mwimbieni Mungu mioyoni mwenu kwa shukrani. Na, kila mfanyacho kwa neno au tendo, fanyeni vyote kwa jina la Bwana Yesu na kumshukuru Mungu Baba kwa njia yake.




Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Yahweh tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa katika ufanyaji/utendaji
Mungu Baba nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako..
Yahweh tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo Jehovah
nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji
Mungu wetu tusipungukiwe katika mahitaji yetu Baba wa Mbinguni ukatupe kama inavyokupendeza wewe..

Mfalme wa amani tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Yahweh tunaomba amani yako itawale katika nyumba/ndoa zetu
Baba wa Mbingu tunaomba ukabariki watoto,wazazi wetu,Familia/ndugu na wote wanaotuzunguka..
yahweh ukawe mlinzi wetu kwetu na kwa vyote tunavyovimiliki
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia,Yahweh ukawe nasi tuingiapo/tutokapo..
Jehovah ukatupe macho ya rohoni Yahweh masikio ya kusikia sauti yako na kuitii..
Mungu wengu tukawe salama moyoni ,Yahweh tukanene yaliyo yako
Mungu wetu ukatupe neema ya kufuata njia zako Baba wa Mbinguni tukasimamie Neno lako amri na sheria zako siku zote za maisha yetu..
Mungu wetu ukaonekane popote tupitapo Yahweh na ikajulikane kwamba upo Baba wa Mbinguni..
Jehovah ukatufanye chombo chema Yahweh nasi tukatumike kama inavyokupendeza wewe..
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi..


Enyi wake, watiini waume zenu, kwani ndivyo apendavyo Bwana. Nanyi waume, wapendeni wake zenu, na msiwe wakali kwao. Enyi watoto, watiini wazazi wenu daima maana hiyo humpendeza Bwana. Nanyi wazazi, msiwachukize watoto wenu, la sivyo watakata tamaa. Enyi watumwa, watiini wakuu wenu wa kidunia katika mambo yote, na si tu wakati wanapowatazama kwa kuwa mnataka kujipendekeza kwao; ila fanyeni hivyo kwa moyo wote, kwa sababu ya kumcha Bwana. Kila mfanyacho, fanyeni kwa moyo wote, kwa sababu ya Bwana na si kwa ajili ya mtu. Kumbukeni kwamba atawapeni tuzo lile alilowawekea watu wake. Mtumikieni Kristo Bwana! Atendaye mabaya atalipwa kufuatana na ubaya wake; Mungu hana ubaguzi.



Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu 
wenye shida/tabu,Baba wa Mbinguni tunaomba ukawavushe salama na ukawaokoe wale wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali..
Yahweh tunaomba uponyaji wako kwa wagonjwa Jehovah ukawape uvumilivu wale wanaowauguza..
Mfalme wa amani ukatawale na ukawe tumaini kwa wote walio kata tamaa,waliokataliwa,wenye hofu na mashaka..
Mungu Baba tunaomba ukawape chakula wenye njaa ukabariki mashamba/vyanzo vyao..
Yahweh tunatuomba ukawafungue walio katika vifungo vya yule mwovu
Baba wa Mbinguni na walio magerezani pasipo na hatia haki ikatendeke
Mungu wetu ukawasamehe wale wote waliokwenda kinyume nawe
Mungu Baba ukawarudishe na kuwasimamisha tena wale walioanguka
Mungu wetu ukawape neema ya kujiombea na kufuata njia zako
nazo zikawaweke huru,Nuru yako ikaangaze katika maisha yao
Baba wa Mbinguni ukawatendee sawasawa na mapenzi yako..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina..!!

Asanteni sana Wapendwa katika Kristo Yesu kwakuwa nami
Mungu wetu  mwenye nguvu, huruma,uponyaji,amani na upendo
akawaguse kwa mkono wake wenye nguvu...
Amani ya Kristo Yesu ikawe nayi daima..
Nawapenda.


Vita dhidi ya Waamaleki
1Samueli alimwambia Shauli, “Mwenyezi-Mungu alinituma kukupaka mafuta uwe mfalme wa watu wake wa Israeli. Sasa sikiliza maneno ya Mwenyezi-Mungu. 2Mwenyezi-Mungu wa majeshi asema hivi: ‘Nitawaadhibu Waamaleki kwa sababu waliwapiga Waisraeli walipokuwa wanatoka Misri. 3Sasa, nenda ukawashambulie na kuangamiza vitu vyote walivyo navyo. Usiwaache hai, ila uwaue wote: Wanaume kwa wanawake, watoto wachanga na wanyonyao, ng'ombe, kondoo, ngamia na punda.’”
4Shauli akaliita jeshi lake, akalikagua huko Telaimu. Kulikuwa na askari wa miguu 200,000 kutoka Israeli na 10,000 kutoka Yuda. 5Halafu yeye na watu wake wakaenda kwenye mji wa Amaleki, wakawa wakivizia kwenye bonde. 6Shauli akawaambia Wakeni, “Nendeni! Ondokeni! Tokeni miongoni mwa Waamaleki, la sivyo, nitawaangamiza pamoja nao. Ondokeni kwa sababu nyinyi mliwatendea wema Waisraeli walipotoka Misri.” Basi, Wakeni wakaondoka miongoni mwa Waamaleki.
7Shauli aliwashinda Waamaleki kuanzia Havila hadi Shuri, mashariki ya Misri. 8Alimteka mfalme Agagi wa Waamaleki akiwa hai. Akawaua watu kwa makali ya upanga. 9Lakini Shauli na watu wake hawakumuua Agagi, wala kondoo bora kabisa, ng'ombe wazuri, ndama, wanakondoo15:9 ndama … kondoo: Makala ya Kiebrania si dhahiri. na chochote kile kilichokuwa kizuri hawakukiangamiza. Lakini vitu vyote vibaya na visivyo na thamani15:9 vibaya … thamani: Makala ya Kiebrania si dhahiri. waliviangamiza.
10Mwenyezi-Mungu akamwambia Samueli, 11“Ninajuta kwamba nimemfanya Shauli kuwa mfalme. Yeye ameacha kunifuata mimi na hajatimiza amri zangu.” Samueli alikasirika, akamlilia Mwenyezi-Mungu usiku kucha. 12Samueli alisikia kuwa Shauli alikuwa amekuja huko Karmeli na amesimamisha mnara wa ukumbusho wake, na kwamba amekwenda Gilgali. Hivyo, kesho yake, Samueli aliamka asubuhi na mapema akaenda kukutana na Shauli. 13Samueli alipomfikia Shauli, Shauli akamwambia Samueli, “Mwenyezi-Mungu na akubariki! Nimetekeleza amri ya Mwenyezi-Mungu.”
14Samueli akamwambia, “Mbona nasikia mlio wa kondoo na ng'ombe?” 15Shauli akajibu, “Watu waliwaacha hai kondoo na ng'ombe bora kabisa ili kumtambikia Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, lakini wengine wote tumewaangamiza.” 16Samueli akamkatiza Shauli, “Nyamaza! Nitakuambia jambo aliloniambia Mwenyezi-Mungu leo usiku.” Shauli akasema, “Niambie.”
17Samueli akamwambia, “Ingawa unajiona kuwa wewe si maarufu, je, wewe si kiongozi wa makabila ya Israeli? Mwenyezi-Mungu alikupaka mafuta uwe mfalme juu ya Israeli. 18Mwenyezi-Mungu alipokutuma alikuambia, ‘Nenda ukawaangamize kabisa wale Waamaleki wenye dhambi, upigane nao hadi umewaua wote!’ 19Kwa nini basi, hukuitii sauti ya Mwenyezi-Mungu? Kwa nini mkakimbilia nyara na hivyo kutenda jambo ovu mbele ya Mwenyezi-Mungu?”
20Shauli akajibu, “Nimetii sauti ya Mwenyezi-Mungu. Nilikwenda kule alikonituma Mwenyezi-Mungu; nimemleta Agagi mfalme wa Waamaleki, na nimewaangamiza kabisa Waamaleki. 21Lakini watu walichukua nyara: Kondoo, ng'ombe na vitu vyote bora vilivyotolewa viangamizwe ili kumtambikia Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, huko Gilgali.”
22Ndipo Samueli akamwambia,
“Je, Mwenyezi-Mungu anapendelea zaidi
dhabihu za kuteketezwa na matambiko,
kuliko kuitii sauti yake?
Tazama, kumtii yeye ni bora kuliko matambiko
na kumsikiliza kuliko kumtambikia mafuta ya beberu.
23Uasi ni sawa na dhambi ya kupiga ramli,
na kiburi ni sawa na uovu na kuabudu vinyago.
Kwa sababu umeikataa amri ya Mwenyezi-Mungu,
naye amekukataa kuwa mfalme.”
24Shauli akamwambia Samueli, “Nimetenda dhambi. Nimeasi amri ya Mwenyezi-Mungu na amri yako, kwa sababu niliwaogopa watu, nikawatii wao. 25Lakini sasa nakuomba, unisamehe dhambi yangu. Niruhusu nirudi pamoja nawe ili niweze kumwabudu Mwenyezi-Mungu.” 26Samueli akamjibu: “Kamwe, siwezi kurudi pamoja nawe. Wewe umeikataa amri ya Mwenyezi-Mungu, naye amekukataa kuwa mfalme juu ya Israeli.” 27Samueli alipogeuka ili aende zake, Shauli akashika pindo la vazi lake, nalo likapasuka. 28Ndipo Samueli alipomwambia Shauli, “Tangu leo Mwenyezi-Mungu ameurarua ufalme wa Israeli kutoka kwako na atampa mtu mwingine miongoni mwa jirani zako aliye bora kuliko wewe. 29Na Mungu ambaye ni utukufu wa Israeli hadanganyi, wala habadili wazo lake. Yeye si binadamu hata abadili mawazo.” 30Shauli akajibu, “Nimefanya dhambi. Hata hivyo, unistahi sasa mbele ya wazee wa watu wangu na Waisraeli. Niruhusu nirudi pamoja nawe ili nikamwabudu Mwenyezi-Mungu, Mungu wako.”
31Basi, Samueli akarudi pamoja naye mpaka Gilgali na Shauli akamwabudu Mwenyezi-Mungu. 32Kisha Samueli akasema, “Nileteeni hapa Agagi mfalme wa Waamaleki.” Agagi akamwendea Samueli akiwa mwenye furaha15:32 mwenye furaha: Au akitetemeka kwa hofu. Neno la Kiebrania halieleweki. kwani alifikiri, “Uchungu wa kifo umepita.”15:32 uchungu … umepita: Au jinsi gani kufa kulivyo kuchungu. 33Samueli akasema, “Kwa kuwa upanga wako umewafanya akina mama wengi wasiwe na watoto, ndivyo na mama yako atakavyokuwa bila mtoto miongoni mwa akina mama.” Akamkatakata Agagi vipandevipande mbele ya Mwenyezi-Mungu huko Gilgali. 34Kisha, Samueli akaenda Rama; na mfalme Shauli akarudi nyumbani kwake huko Gibea. 35Tangu siku hiyo, Samueli hakumwona tena Shauli, mpaka siku alipofariki. Hata hivyo Samueli alimlilia Shauli. Naye Mwenyezi-Mungu alisikitika kwamba alikuwa amemtawaza Shauli mfalme juu ya Israeli.


1Samweli15;1-35

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: