Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Friday 9 March 2018

Kikombe Cha Asubuhi ;1 Wafalme 5....




Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Ni siku nyingine tena Mungu wetu ametuchagua na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona leo hii..
Si kwamba sisi tumetenda mema sana,wala si kwamba sisi
ni wazuri mno,si kwa uwezo wetu wala nguvu zetu,
si kwa akili zetu sisi kuwa hivi tulivyo leo hii ni 
kwa neema/rehema zake ni kwa mapenzi yake Mungu wetu.....

Tumshukuru Mungu wetu katika yote...

Asante Baba wa Mbinguni kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwa tayari kwa majukumu yetu
Utukuzwe ee Mungu wetu,Muumba wetu Muumba wa vyote vilivyomo
vinavyoonekana na visivyoonekana,Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo
Mungu mwenye nguvu,Mungu wa walio hai,Mungu mwenye huruma,
Mungu wenye kusamehe,hakuna kama wewe,hakuna lililogumu mbele zako
wewe ni mwanzo na wewe ni mwisho,Alfa na Omega....!!

Habari Njema ya Yesu Kristo, Mwana wa Mungu. Ilianza kama ilivyoandikwa katika kitabu cha nabii Isaya: “Mungu alisema, ‘Namtuma mjumbe wangu akutangulie, ambaye atakutayarishia njia yako.’ Sauti ya mtu anaita jangwani: ‘Mtayarishieni Bwana njia yake, nyosheni barabara zake.’” Yohane Mbatizaji alitokea jangwani, akahubiri kwamba watu watubu na kubatizwa ili Mungu awasamehe dhambi zao. Watu kutoka sehemu zote za Yudea na wenyeji wote wa Yerusalemu walimwendea, wakaziungama dhambi zao, naye akawabatiza katika mto Yordani. Yohane alikuwa amevaa vazi lililofumwa kwa manyoya ya ngamia, na ukanda wa ngozi kiunoni mwake. Chakula chake kilikuwa nzige na asali ya mwituni. Naye alihubiri akisema, “Baada yangu anakuja mwenye nguvu zaidi kuliko mimi, ambaye mimi sistahili hata kuinama na kufungua kamba za viatu vyake. Mimi ninawabatiza kwa maji, lakini yeye atawabatiza kwa Roho Mtakatifu.”


Tunakuja mbele zako Baba wa Mbinguni tukijinyenyekeza,tukijishusha
na kujiachilia mikononi mwako Mungu wetu
Yahweh tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizozifanya
kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua
Jehovah nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale
wote waliotukosea
Mungu wetu usitutie katika majaribu Baba wa Mbinguni utuokoe na
yule mwovu na kazi zake zote..
Yahweh tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu
Baba wa Mbinguni utufunike kwa Damu ya Bwana na Mwokozi wetu
Yesu Kristo wa Nazareti yeye alitesekakwanza ili sisi tupate kupona...

Siku hizo, Yesu alifika kutoka Nazareti, mji wa Galilaya, akabatizwa na Yohane katika mto Yordani. Mara tu alipotoka majini, aliona mbingu zimefunguliwa, na Roho akishuka juu yake kama njiwa. Sauti ikasikika kutoka mbinguni: “Wewe ni Mwanangu mpendwa, nimependezwa nawe.” Mara akaongozwa na Roho kwenda jangwani, akakaa huko siku arubaini akijaribiwa na Shetani. Alikuwa huko pamoja na wanyama wa porini, nao malaika wakawa wanamhudumia.

Jehovah tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Yahweh tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa katika utendaji
Mungu wetu nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwabariki
wenye kuhitaji
Jehovah tusipungukiwe katika mahitaji yetu baba wa Mbinguni
ukatupe sawasawa na mapenzi yako...


Mungu wetu tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu
Yahweh tunaomba ukabariki watoto,wazazi wetu,familia/ndugu
na wote wanaotuzunguka
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyovimiliki
vilivyo ndani na vilivyo nje Baba wa Mbinguni ukatubariki 
tuingiapo/tutokapo Yahweh  ukatamalaki na kutuatamia
Mungu wetu tukawe salama moyoni Mfalme wa amani
amani yako ikatawale katika maisha yetu,Neema na Nuru
yako ikaangaze katika maisha yetu,Yahweh ukatupe neema ya 
kufuata njia zako Mungu wetu tukasimamiE Neno lako
amri na sheria zako siku zote za maisha yetu...
Jehovah ukatupe macho ya kuona na amasikio ya kusikia
sauti yako na kuitii Mungu wetu ukaonekane popote
tupitapo na ikajulikane kwamba upo Baba wa Mbinguni
Yahweh ukatufanye chombo chema Mungu wetu nasi tukatumike
 kama inavyokupendeza wewe..
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi....


Yohane alipokwisha fungwa gerezani, Yesu alikwenda Galilaya, akahubiri Habari Njema ya Mungu, akisema, “Wakati umetimia, na ufalme wa Mungu umekaribia. Tubuni na kuiamini Habari Njema!” Alipokuwa anapita kando ya ziwa Galilaya, aliwaona wavuvi wawili: Simoni na Andrea ndugu yake wakivua samaki kwa wavu. Yesu akawaambia, “Nifuateni nami nitawafanya nyinyi kuwa wavuvi wa watu.” Mara wakaziacha nyavu zao, wakamfuata. Alipokwenda mbele kidogo, aliwaona Yakobo na Yohane, wana wa Zebedayo. Nao pia walikuwa ndani ya mashua yao wakizitengeneza nyavu zao. Yesu akawaita mara, nao wakamwacha baba yao Zebedayo katika mashua pamoja na wafanyakazi, wakamfuata.

Baba wa Mbinguni tazama watoto wako wanaokutafuta/
kukuhitaji kwa bidii na imani,Mungu wetu tunaomba
ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu
Yahweh kila mmoja kwa mahitaji/maombi yake... Mungu wetu
ukaonekane katika maisha yao Jehovah ukawape neeema
ya kujiombea,Mungu wetu ukawape neema ya kufuata njia
zako na kusimamia Neno lako Yahweh wakasikie sauti yako
Mungu wetu ukawape macho ya  rohoni Yahweh ukawaponye
kimwili na kiroho pia.....


Wakafika mjini Kafarnaumu, na mara ilipofika Sabato, Yesu akaingia katika sunagogi, akaanza kufundisha. Watu wote waliomsikia walishangazwa na mafundisho yake, maana hakuwa anafundisha kama waalimu wao wa sheria, bali kama mtu mwenye mamlaka. Mara akatokea mle ndani ya sunagogi mtu mmoja mwenye pepo mchafu, akapaza sauti, “Una nini nasi, wewe Yesu wa Nazareti? Je, umekuja kutuangamiza? Najua wewe ni nani: Wewe ni Mtakatifu wa Mungu!” Yesu akamkemea huyo pepo akisema, “Nyamaza! Mtoke mtu huyu.” Basi, huyo pepo mchafu akamtikisatikisa mtu huyo, kisha akalia kwa sauti kubwa, akamtoka. Watu wote wakashangaa, wakaulizana, “Ni mambo gani haya? Je, ni mafundisho mapya? Mtu huyu anayo mamlaka ya kuamuru hata pepo wachafu, nao wanamtii!” Habari za Yesu zikaenea upesi kila mahali katika eneo la Galilaya.

 Baba wa Mbinguni ukawasamehe
pale walipokwenda kinyume nawe Yahweh ukawasimamishe
na kuwaongoza Mungu wetu Nuru yako ikaangaze katika
maisha yao ee Baba tunaomba ukasikie na ukapokee
sala/maombi yetu Mungu wetu tunaomba ukatende
sawaswa na mapenzi yako...
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina..!!


Wapendwa/waungwana asanteni sana kwakuwa nami/kunisoma
Mungu aendelee kuwabariki na kuwatendea kama inavyompendeza
yeye,
Baraka na amani vikatawale katika maisha yenu
Nawapenda.

Solomoni ajitayarisha kujenga hekalu

(2Nya 2:1-18)

1 5:1 Kiebrania ni 5:15. Naye mfalme Hiramu wa Tiro, aliyekuwa rafiki ya Daudi, alipopata habari kwamba Solomoni amekuwa mfalme mahali pa baba yake, alituma watumishi kwake. 2Ndipo Solomoni akampelekea Hiramu ujumbe huu: 3“Wajua kwamba baba yangu Daudi hakuweza kumjengea Mwenyezi-Mungu, Mungu wake, hekalu la kumwabudia, kwa sababu ya kukumbana na vita vingi dhidi ya maadui wa nchi jirani mpaka hapo Mwenyezi-Mungu alipompatia ushindi. 4Lakini sasa, Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu, amenijalia amani pande zote. Sina adui wala taabu. 5Basi, nimeamua kumjengea Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu, nyumba ya kumwabudia. Na hii ni sawa kabisa kama Mwenyezi-Mungu alivyomwahidi baba yangu akisema: ‘Mwanao ambaye nitamfanya aketi katika kiti chako cha enzi, atanijengea nyumba!’ 6Sasa basi, uwaamuru watu wako wanikatie mierezi ya Lebanoni. Watu wangu watajiunga na watu wako katika kazi hiyo, nami nitawalipa watumishi wako kadiri utakavyosema; kwani kama ujuavyo, hakuna yeyote mwenye ujuzi wa kukata miti kama nyinyi Wasidoni.”
7Hiramu alifurahi sana alipopata ujumbe huu wa Solomoni, akasema, “Mwenyezi-Mungu asifiwe wakati huu, kwa kumpa Daudi mwana mwenye hekima atawale taifa hili kubwa.” 8Kisha, Hiramu alimpelekea Solomoni ujumbe, akisema, “Nimepokea ujumbe wako, nami niko tayari kutimiza mahitaji yako kuhusu mbao za mierezi na za miberoshi. 9Watu wangu watasomba magogo na kuyateremsha kutoka Lebanoni mpaka baharini na kuyafunga mafungumafungu yaelee juu ya maji mpaka mahali utakaponielekeza. Huko, yatafunguliwa, nawe utayapokea. Kwa upande wako, wewe utanipa chakula kwa ajili ya watu wa nyumbani mwangu.”
10Basi, Hiramu alimpa Solomoni mbao zote za aina ya mierezi na miberoshi alizohitaji, 11naye Solomoni akampa Hiramu ngano madebe 240,000, na mafuta safi madebe 200 kila mwaka, kwa ajili ya watu wa nyumbani mwake.
12Basi, Mwenyezi-Mungu akampa Solomoni hekima kama alivyomwahidi. Kukawa na amani kati ya Solomoni na Hiramu; wakafanya mkataba kati yao.
13Mfalme Solomoni alikusanya watu 30,000 kutoka kila mahali nchini Israeli, wafanye kazi za kulazimishwa, 14akamweka Adoniramu awe msimamizi wao. Aliwagawa watu hao katika makundi matatu ya watu 10,000 kila moja, akayapeleka makundi hayo kwa zamu, mwezi mmoja Lebanoni na miezi miwili nyumbani. 15Solomoni alikuwa pia na wachukuzi wa mizigo 70,000, na wachongaji mawe milimani 80,000, 16mbali na maofisa wakuu 3,300 waliosimamia kazi hiyo na wafanyakazi wote. 17Kwa amri ya mfalme, walichimbua mawe makubwa na ya thamani, ili yachongwe kwa ajili ya kujengea msingi wa nyumba. 18Basi, hivyo ndivyo wajenzi wa Solomoni na Hiramu na watu wa mji wa Gebali walivyotayarisha mawe na mbao za kujengea nyumba hiyo.




1Wafalme5;1-18


Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: