Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Wednesday 21 March 2018

Kikombe Cha Asubuhi ;1 Wafalme 13...




Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Mungu wetu yu mwema sana Tumshukuru katika yote

Asante Mungu wetu kwa wema na fadhili zako
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa kibali cha kuendelea
kuiona leo hii
Asante kwa Pumzi/uzima,afya na kuwa tayari kwa majukumu yetu
Si kwamba sisi tumetenda mema sana,wala si kwa nguvu zetu
utashi wetu,Si kwa uwezo wetu na akili zetu sisi kuwa hivi 
tulivyo leo hii ni kwa rehema/neema zako ni kwa mapenzi
yako Mungu wetu sisi kuwa hivi tulivyo leo hii
Utukuzwe eeMungu wetu,usifiwe Baba wa Mbinguni,Uabudiwe Jehovah,
Uhimidiwe Yahweh,Matendo yako ni makuu sana,Matendo yako ni ya ajabu,Matendo yako yanatisha...
Neema yako yatutosha ee Mungu nwetu...!!

Yesu aliposhuka mlimani, makundi mengi ya watu yalimfuata. Basi, akaja mtu mmoja mwenye ukoma, akamsujudia na kusema, “Bwana, ukitaka, waweza kunitakasa!” Yesu akanyosha mkono, akamgusa na kusema, “Nataka! Takasika.” Mara huyo mtu akapona ukoma wake. Kisha Yesu akamwambia, “Angalia, usimwambie mtu yeyote, ila nenda ukajioneshe kwa kuhani, na kutoa sadaka iliyoamriwa na Mose kuwathibitishia kwamba umepona.”

Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha
na kujiachilia mikononi mwako..
Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizozifanya
kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua
Jehovah nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale
wote waliotukosea
Mungu wetu usitutie katika majaribu Baba wa Mbinguni tunaomba
utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote
Nguvu za giza,nguvu za mapepo,nguvu za mizimu,nguvu za mapinga Kristo
zishindwe katika jina lililokuu jina la Bwana wetu Yesu Kristo
Yahweh tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu
Baba wa Mbinguni utufunike kwa Damu ya Bwana na Mwokozi wetu
Yesu Kristo wa Nazareti yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona...


Yesu alipokuwa anaingia mjini Kafarnaumu, jemadari mmoja alimwendea, akamsihi akisema, “Bwana, mtumishi wangu amelala nyumbani, mgonjwa wa kupooza na anaumwa sana.” Yesu akamwambia, “Nitakuja kumponya.” Huyo jemadari akamwambia, “Bwana, sistahili uingie nyumbani mwangu. Lakini sema tu neno, na mtumishi wangu atapona. Maana, hata mimi niliye mtu chini ya mamlaka ya wengine, ninao askari chini yangu. Namwambia mmoja, ‘Nenda!’ Naye huenda; na mwingine, ‘Njoo!’ Naye huja; na mtumishi wangu, ‘Fanya kitu hiki!’ Naye hufanya.” Yesu aliposikia hayo, alistaajabu, akawaambia watu waliokuwa wanamfuata, “Kweli nawaambieni, sijapata kumwona mtu yeyote katika Israeli mwenye imani kama hii. Basi, nawaambieni kwamba watu wengi watakuja kutoka mashariki na magharibi, nao wataketi karamuni pamoja na Abrahamu, Isaka na Yakobo katika ufalme wa mbinguni. Lakini wale ambao ufalme huo ni wao watatupwa nje, gizani, ambako watalia na kusaga meno.” Kisha Yesu akamwambia huyo jemadari Mroma, “Nenda nyumbani; na iwe kama ulivyoamini.” Na mtumishi wake akapona saa ileile.

Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa katika
utendaji Yahweh nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Jehovah tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwabariki
wenye kuhitaji
Jehovah tunaomba tusipungukiwe katika mahitaji yetu Mungu wetu
tunaomba ukatupe kama inavyokupendeza wewe...

Mfalme wa amani tunaomba amani yako ikatawale katika nyumba/ndoa
zetu,Mungu wetu tunaomba ukabariki watoto,wazazi wetu,familia/ndugu
na wote wanaotuzunguka,Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa
vyote tunavyovimiliki,Mungu wetu tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki vyote
tunavyoenda kugusa/kutumia Jehovah tunaomba ukavitakase na 
kuvifunika kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Yahweh tunaomba ukatamalaki na kutuatamia Mungu wetu tukawe
salama rohoni Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe macho ya kuona
na masikio ya kusikia sauti yako na kuitii
Mungu wetu ukaonekane katika maisha yetu Yahweh popote tupitapo
na ikajulikane kwamba upo Baba wa Mbinguni,Jehovah ukatupe neema
ya kutambua mema na mabaya,Mungu wetu ukatupe neema ya kufuata
njia zako Yahweh tukasimamie Neno lako amri na sheria zako siku
zote za maisha yetu...
Mungu wetu ukatufanye chombo chema Jehovah nasi tukatumike
kama inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi....


Yesu alifika nyumbani kwa Petro, akamkuta mama mkwe wa Petro amelala kitandani, ana homa kali. Basi, Yesu akamgusa huyo mama mkono, na homa ikamwacha; akasimama, akamtumikia. Ilipokuwa jioni, walimletea watu wengi waliokuwa wamepagawa na pepo; naye, kwa kusema neno tu, akawafukuza hao pepo. Aliwaponya pia watu wote waliokuwa wagonjwa. Alifanya hivyo ili yale aliyosema nabii Isaya yatimie: “Yeye mwenyewe ameuchukua udhaifu wetu, ameyabeba magonjwa yetu.”

Mungu wetu tazama wenye shida/tabu Yahweh tunaomba ukawaguse
kwa mkono wako wenye nguvu Mungu wetu tunaomba ukawaponye wagonjwa na ukawape tumaini,imani  wanao wauguza Jehovah ukawaponye kimwili na kiroho pia...
Wenye njaa baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki mashamba/vyanzo
vyao wakapate chakula cha kutosha kuweka akiba na kubariki wengine
Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wote wanaopitia
magumu/majaribu mbalimbali waliokata tamaa,walio kataliwa,
wenye hofu na mashaka Mungu wetu ukawe tumaini lao
Tazama walio katika vifungo vya yule mwovu walio magerezani
pasipo na hatia Mungu wetu tunaomba ukawafungue na kuwaweka huru
Baba wa Mbinguni haki ikatendeke
Yahweh tunaomba ukawasamehe wale wote waliokwenda kinyume
nawe,Mungu wetu tunaomba ukawape neema ya kujiombea,kufuata
njia zako nazo zikawaweke huru
Baba wa Mbinguni ukaonekane katika maisha ya watoto wako
wanaokutafuta kwa bidii na imani Mungu wetu ukasikie kulia kwao
Baba wa Mbiguni tunaomba ukawafute machozi yao...
Mungu wetu ukawape neema ya kukujua wewe wale wote
wasio amani Mungu wetu ukawape ufahamu na kujitambua
Yahweh ukawahurumie  na kuwaokoa Jehovah ukawatue mizigo
waliyoibeba,Nuru yako ikaangaze katika maisha yao,amani ikatawale
Jehovah tunaomba ukasikie na ukapokee sala/maombi yetu
Mungu nwetu ukawatendee sawasawa na mapenzi yako
Kwakuwa Ufalme ni wako nguvu na Utukufu hata Milele...
Amina....!!

Wapendwa katika Kristo Yesu asanteni sana kwakuwanami/kunisoma
Mungu Baba akawabariki na kuwatendea kama inavyompendeza yeye
Amani ya Bwana wetu Yesu Kristo na upendo wa Mungu Baba
vikawe nanyi Daima...
Nawapenda.


Nabii alaani ibada huko Betheli

1Siku moja Yeroboamu alikuwa amesimama kando ya madhabahu ili afukize ubani. Basi, mtu wa Mungu kutoka Yuda akawasili hapo Betheli na ujumbe wa Mwenyezi-Mungu. 2Mtu huyo akailaani ile madhabahu akisema, “Ee madhabahu! Mwenyezi-Mungu asema hivi: ‘Atazaliwa mtoto katika ukoo wa Daudi, jina lake Yosia. Huyo atawatwaa makuhani wanaohudumu mahali pa ibada na kufukiza ubani juu yako, na kutambika juu yako; naam, mifupa ya watu itateketezwa juu yako!’” 3Mtu huyo akatoa ishara siku ileile, akasema: “Hii ndiyo ishara aliyotamka Mwenyezi-Mungu: ‘Madhabahu itabomoka, na majivu yaliyo juu yake yatamwagika.’”
4Mfalme Yeroboamu aliposikia maneno hayo ya mtu wa Mungu dhidi ya madhabahu huko Betheli, alinyosha mkono akasema, “Mkamateni huyo!” Na mara huo mkono wake aliounyosha, ukakauka, asiweze tena kuukunja. 5Madhabahu nayo ikabomoka, na majivu yake yakamwagika chini, kama ishara ile aliyoitoa huyo mtu wa Mungu na ujumbe wa Mwenyezi-Mungu. 6Basi, mfalme Yeroboamu akamwambia nabii, “Tafadhali, umsihi Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, uniombee mkono wangu upate kupona.” Naye nabii akamwomba Mwenyezi-Mungu, na mkono wa mfalme ukapona, ukarudia hali yake ya hapo awali. 7Ndipo mfalme akamwambia mtu wa Mungu, “Karibu nyumbani kwangu kula chakula, nami nikupe zawadi.” 8Lakini mtu wa Mungu akamwambia, “Hata kama ukinipa nusu ya milki yako, sitakwenda pamoja nawe. Sitakula wala kunywa maji mahali hapa, 9kwani Mwenyezi-Mungu aliniamuru nisile chakula au kunywa maji, wala nisirudi kwa njia ileile niliyoifuata kuja hapa.” 10Basi, mtu huyo akaenda zake, wala hakurudi kwa njia ile aliyoijia Betheli.

Nabii mzee wa Betheli

11Wakati huo, palikuwa na nabii mmoja mzee huko Betheli. Wanawe wakamwendea, wakamweleza mambo yote aliyotenda yule mtu wa Mungu siku hiyo, huko Betheli; wakamwambia pia yale maneno yule mtu aliyomwambia mfalme Yeroboamu. 12Baba yao akawauliza, “Amefuata njia ipi?” Nao wakamwonesha njia aliyoifuata huyo mtu wa Mungu kutoka Yuda. 13Naye akawaambia watoto wake, “Nitandikieni huyo punda.” Nao wakamtandikia punda, na mzee akapanda juu yake. 14Akamfuata yule mtu wa Mungu, akamkuta ameketi chini ya mti wa mwaloni. Basi, akamwuliza, “Je, wewe ndiwe yule mtu wa Mungu kutoka Yuda?” Naye akamjibu, “Naam! Mimi ndiye.” 15Huyo mzee akamwambia, “Karibu nyumbani kwangu, ukale chakula.” 16Lakini yeye akamwambia, “Siwezi kurudi pamoja nawe, wala kuingia nyumbani kwako. Siwezi kula chakula au kunywa maji mahali hapa, 17maana, Mwenyezi-Mungu aliniamuru nisile chakula au kunywa maji mahali hapa, wala nisirudi kwa njia niliyoijia.” 18Huyo mzee wa Betheli akamwambia, “Mimi pia ni nabii kama wewe, na Mwenyezi-Mungu amenena nami kwa njia ya malaika akisema, ‘Mrudishe nyumbani kwako, ale chakula na kunywa maji.’” Lakini huyo nabii mzee alikuwa anamdanganya tu. 19Basi, mtu wa Mungu akarudi pamoja naye, akala chakula na kunywa maji kwa huyo mzee.
20Walipokuwa mezani, neno la Mwenyezi-Mungu likamjia huyo nabii mzee, 21naye akamwambia kwa sauti huyo mtu wa Mungu kutoka Yuda: “Mwenyezi-Mungu asema hivi: ‘Wewe umeacha kutii ujumbe wa Mwenyezi-Mungu; wewe hukufuata amri aliyokupa Mwenyezi-Mungu, Mungu wako. 22Badala yake, umerudi hapa, ukala chakula na kunywa maji mahali hapa ambapo uliambiwa usile chakula wala kunywa maji. Basi, mwili wako hautazikwa kwenye kaburi la babu zako.’” 23Walipomaliza kula, huyo nabii mzee akamtandikia punda huyo mtu wa Mungu, naye akaondoka.
24Alipokuwa anakwenda zake, simba akakutana naye njiani, akamuua; mwili wake ukawa umetupwa hapo barabarani; punda wake na huyo simba wakawa wamesimama kando yake. 25Watu waliopitia hapo na kuiona maiti barabarani, na simba amesimama karibu nayo, wakaenda mpaka mjini alimokuwa anakaa yule nabii, wakawaambia watu. 26Nabii yule ambaye alikuwa amemkaribisha nyumbani kwake aliposikia habari hiyo, akasema, “Huyo ni yuleyule mtu wa Mungu aliyekataa kutii neno la Mwenyezi-Mungu! Mwenyezi-Mungu amemtuma simba, akamshambulia na kumwua kama alivyokuwa amemwambia.” 27Hapo akawaambia wanawe “Nitandikie punda.” Nao wakamtandikia. 28Mzee akaenda, akaikuta maiti ya mtu wa Mungu barabarani, simba na punda wake kando yake; huyo simba hakuila maiti wala hakumshambulia punda. 29Basi, huyo nabii mzee akaitwaa maiti ya mtu wa Mungu, akaiweka juu ya punda wake, akairudisha mjini Betheli, kuomboleza kifo chake na kumzika. 30Basi, akamzika katika kaburi lake, naye pamoja na wanawe wakaomboleza kifo chake wakisema, “Aa! Ndugu yangu!” 31Baada ya mazishi, nabii huyo akawaambia wanawe, “Nikifa, nizikeni katika kaburi hilihili alimozikwa mtu wa Mungu; mifupa yangu kando ya mifupa yake. 32Mambo yote aliyoagizwa na Mwenyezi-Mungu dhidi ya madhabahu ya Betheli, na mahali pote pa kutambikia vilimani Samaria, hakika yatatimia.”
33Yeroboamu hakuuacha upotovu wake; aliendelea kuteua watu wa kawaida kuwa makuhani, wahudumie mahali pa kutambikia vilimani. Mtu yeyote aliyejitolea, alimweka wakfu kuwa kuhani wa mahali pa kutambikia huko vilimani. 34Tendo hili likawa dhambi ambayo ilisababisha ukoo wa Yeroboamu ufutiliwe mbali na kuangamizwa.




1Wafalme13;1-34


Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: