Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Friday 26 May 2017

Kikombe Cha Asubuhi;Mambo Ya Walawi..1.

Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje Wapendwa/Waungwana?

Haleluyahh..!!Mungu wetu yu mwema sana..Yeye anaweza yote,Yeye ni Mungu wetu na Baba yetu, Yeye ni Mwanzo na Yeye ni Mwisho,Yeye atosha..!!


Ni siku nyingine tena Mungu ametupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii..
Si kwamba sisi ni wema sana zaidi ya wengine waliotangulia/fariki sasa hivi, usiku au walio hoi vitandani kwa Magonjwa mbalimbali..
Wengine hawawezi hata kutamka Neno la Mungu wala kuomba au Kutubu..
Tumempa nini Mungu ?
Si kwanguvu zetu wala uwezo wetu..ni kwa Neema/Rehema zake Mungu wetu..
Basi Wapendwa/Waungwana tuitumie nafasi hii vizuri na Tumshukuru Mungu kwa wema na fadhili zake kwetu..
Asante Mungu wetu Babayetu,Muumba wetu,Muumba wa Mbingu na Nchi, Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo..
Asante kwa ulinzi wako usiku wote na wakati wote umekuwa nasi Jehovah..
Asante kwa kutuchagua tena kuendelea na kuwa hai na wenye Afya..


Tunakuja mbele zako Baba wa Mbinguni tukijinyenyekeza tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako Mfalme wa Amani..
Tunaomba utusamehe pale tulipokwenda kinyume nawe Baba wa Mbinguni..Kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua..
Mungu wetu tunaomba nasi utupe Neema ya kuweza kuwasamehe waliotukosea..
Roho Mtakatifu akatuongoze katika kunena na kutenda Baba tukawe na kiasi..


Baba wa Mbinguni utuepushe na Majaribu na utuokoe na yule mwovu na kazi zake..

Mfalme wa Amani tunaiweka siku hii na maisha yetu mikononi mwako..
Baba ukatubariki katika yote tunayoenda kufanya,Baba tusipungukiwe na mahitaji yetu..lakini utupe sawasawa na mapezni yako..

Asante Mungu wetu kwa kuanza Neno hili[Kitabu hiki cha Walawi]
Mungu wetu ukatuongoze na tukapate  kulielewa Neno hili..Baba wa mbinguni tukapate kukuona na kusikia na  yote uliyoyaweka humu yakawe Faida na Tukapande Mbegu  nzuri kwetu na kwa wengine..
Tukapate msukumo/Shauku zaidi  ya kutaka kukujua zaidi..
Nasi tukalitumie vyema Neno Lako Mungu wetu..Sifa na utukufu
tunakurudishia wewe Baba wa Mbinguni..



Neno lako ni taa ya kuniongoza, na mwanga katika njia yangu.


Maana, kama Habari Njema tunayohubiri imefichika, imefichika tu kwa wale wanaopotea. Hao hawaamini kwa sababu yule mungu wa ulimwengu huu amezitia giza akili zao wasipate kuuona wazi mwanga wa Habari Njema ya utukufu wa Kristo, ambaye ni mfano kamili wa Mungu. Maana hatujitangazi sisi wenyewe, ila tunamhubiri Yesu Kristo aliye Bwana, sisi wenyewe tukiwa watumishi wenu kwa ajili ya Yesu. Mungu ambaye alisema, “Mwanga na uangaze kutoka gizani,” ndiye mwenye kuiangaza mioyo yetu, na kutupatia mwanga wa ujuzi wa utukufu wa Mungu uangazao katika uso wa Kristo. Basi, sisi tulio na hazina hii tuko tu kama vyombo vya udongo, ili ionekane wazi kwamba nguvu hiyo kuu yatoka kwa Mungu wala si kwetu sisi wenyewe. Daima twapata taabu, lakini hatugandamizwi; twapata mashaka, lakini hatukati tamaa; twateseka, lakini hatuachwi bila msaada; na ingawa tumeangushwa chini, hatukuangamizwa. Kila wakati tumekuwa tukichukua mwilini mwetu kifo cha Kristo, ili uhai wake Yesu pia udhihirike katika miili yetu. Naam, muda tuishipo tunakabiliwa na kifo daima kwa ajili ya Yesu, ili uhai wake Yesu udhihirike katika miili yetu inayokufa. Hii ina maana kwamba ndani yetu kifo kinafanya kazi, lakini ndani yenu uhai unafanya kazi. Maandiko Matakatifu yasema: “Niliamini, ndiyo maana nilinena.” Nasi pia, tukiwa na moyo huohuo wa imani, tunaamini, na kwa sababu hiyo twanena. Tunajua kwamba yule aliyemfufua Bwana Yesu atatufufua sisi pia pamoja na Yesu na kutuweka mbele yake pamoja nanyi. Yote haya ni kwa faida yenu, hata neema ya Mungu inapowafikia watu wengi zaidi na zaidi, shukrani nazo ziongezeke zaidi, kwa utukufu wa Mungu.
Tunayaweka haya yote mikononi mwako kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na utukufu hata milele..
Amina..!
Asanteni sana wote kwakutembela hapa..
Mungu aendele kuwabariki katika yote..
Nawapenda.

Sadaka za kuteketezwa
1Mwenyezi-Mungu alimwita Mose na kuongea naye katika hema la mkutano, akamwambia, 2“Waambie Waisraeli kwamba kama mtu anapenda kumtolea Mwenyezi-Mungu sadaka ya mnyama, mnyama huyo atamchagua kutoka kundi lake la ng'ombe, kondoo au mbuzi.
3“Kama sadaka anayotoa mtu ni ya kuteketezwa, atamchagua mnyama dume asiye na dosari kutoka kundi lake, atamtolea mbele ya mlango wa hema la mkutano ili apate fadhili ya Mwenyezi-Mungu; 4ataweka mkono wake juu ya kichwa cha mnyama wa sadaka ya kuteketezwa, ambayo itakubaliwa kwa ajili ya kumfanyia huyo mtu upatanisho. 5Kisha, atamchinja huyo ng'ombe mbele ya Mwenyezi-Mungu. Nao makuhani, wazawa wa Aroni, wataichukua damu na kuinyunyizia madhabahu mlangoni mwa hema la mkutano, pande zake zote. 6Huyo mtu atamchuna huyo mnyama wa sadaka ya kuteketezwa na kumkata vipandevipande. 7Hao makuhani wazawa wa Aroni watazipanga kuni juu ya madhabahu na kuwasha moto. 8Kisha makuhani hao watachukua vile vipande vya nyama, kichwa na mafuta, na kuviweka juu ya kuni juu ya madhabahu. 9Lakini matumbo na miguu ya mnyama huyo mtu ataviosha kwa maji. Kuhani ataiteketeza sadaka yote juu ya madhabahu. Hiyo ni sadaka ya kuteketezwa kwa moto yenye harufu nzuri ya kumpendeza Mwenyezi-Mungu.
10“Kama sadaka yake ya kuteketezwa ataitoa katika kundi la kondoo au mbuzi, basi, atachagua dume asiye na dosari. 11Atamchinjia upande wa kaskazini wa madhabahu, mbele ya Mwenyezi-Mungu, hao makuhani, wazawa wa Aroni watainyunyizia madhabahu damu pande zake zote. 12Kisha huyo mtu atamkata vipandevipande, akivitenga kichwa pamoja na mafuta yake, na kuhani ataviweka kwenye moto juu ya madhabahu. 13Lakini matumbo na miguu yake ataviosha kwa maji. Kuhani ataiteketeza yote juu ya madhabahu. Hiyo ni sadaka ya kuteketezwa kwa moto yenye harufu nzuri ya kumpendeza Mwenyezi-Mungu.
14“Ikiwa anamtolea Mwenyezi-Mungu sadaka ya kuteketezwa ya ndege, basi, ataleta sadaka yake ya hua au kinda la njiwa. 15Kuhani atamleta ndege huyo kwenye madhabahu, atamkongonyoa kichwa chake na kukiteketeza juu ya madhabahu. Damu yake itanyunyiziwa ubavuni mwa madhabahu. 16Kibofu chake pamoja na uchafu wake ataviondoa na kutupa upande wa mashariki wa madhabahu ambako majivu huwekwa. 17Atamshika mabawa na kumpasua, lakini asimkate vipande viwili. Kisha, kuhani atamteketeza kwenye madhabahu, juu ya kuni. Hiyo ni sadaka ya kuteketezwa kwa moto yenye harufu nzuri ya kumpendeza Mwenyezi-Mungu.”

Mambo Ya Walawi 1;1-17

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: