Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Monday 15 October 2018

Kikombe Cha Asubuhi ;Yobu 15...



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Haleluyah ni siku/wiki nyingine tena Mungu wetu ametuchagua
na kutupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Si kwamba sisi tumetenda mema sana wala si kwa nguvu zetu
si kwa utashi wetu wala si kwa akili zetu si kwamba sisi
ni wazuri mno si kwa uwezo wetu sisi kuwa hivi tulivyo leo hii
Ni kwa rehema/neema zake ni kwa mapenzi yake Mungu wetu....

Tumshukuru Mungu wetu katika yote...

Asante Mungu wetu kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwa tayari kwa majukumu yetu
Sifa na Utukufu tunakurudshia Mungu wetu....!!

Tunapomshukuru Mungu kwa kikombe kile cha baraka, je, huwa hatushiriki damu ya Kristo? Na tunapoumega mkate, je, huwa hatushiriki mwili wa Kristo? Kwa kuwa mkate huo ni mmoja, sisi, ingawa ni wengi, tu mwili mmoja; maana sote twashiriki mkate huohuo. Angalieni kwa mfano Wayahudi wenyewe: Wale wanaokula tambiko wanaungana na hiyo madhabahu. Nataka kusema nini, basi? Kwamba chakula kilichotambikiwa sanamu ni kitu zaidi ya chakula? Na hizo sanamu, je, ni kitu kweli zaidi ya sanamu?



Tazama jana imepita ee Mungu wetu leo ni siku mpya na kesho ni siku nyingine
Jehovah tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako
 Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizozifanya kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea
Jehovah usitutie majaribu Mungu wetu tunaomba utuepushe na yule mwovu na kazi zake zote
Yahweh tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu
Baba wa Mbinguni utufunike kwa Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti
yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona
Kwakupigwa kwake sisi tumepata kupona...

Hata kidogo! Ninachosema ni kwamba tambiko wanazotoa watu wasiomjua Mungu wanawatolea pepo, sio Mungu. Sipendi kamwe nyinyi muwe na ushirika na pepo. Hamwezi kunywa kikombe cha Bwana na kikombe cha pepo; hamwezi kushiriki katika Karamu ya Bwana na katika meza ya pepo. Au je, tunataka kumfanya Bwana awe na wivu? Mnadhani tuna nguvu zaidi kuliko yeye?

Yahweh tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa 
katika utendaji
Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki ridhiki zetu
ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba ukatupe neema ya kuweza
kuwabariki wenye kuhitaji
Yahweh tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Mungu wetu ukatupe kama inavyokupendeza wewe

Baba wa Mbinguni tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyo vimiliki
Yahweh tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia
Baba wa Mbinguni tukawe salama rohoni
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia 
sauti yako na kuitii
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe neema ya kufuata njia zako
Yahweh tukasimamie Neno lako amri na sheria zako siku zote 
za maisha yetu
Mungu wetu ukaonekane katika maisha yetu
Neema zako zikawe nasi Nuru yako ikaangaze katika maisha yetu
ukatuguse kwa mkono wako wenye nguvu
Ukatufanye chombo chema ee Mungu wetu nasi tukatumike kama
inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi...


Vitu vyote ni halali, lakini si vyote vinafaa. Vitu vyote ni halali lakini si vyote vinajenga. Mtu asitafute faida yake mwenyewe, ila faida ya mwenzake. Kuleni chochote kile kiuzwacho sokoni bila ya kuulizauliza kwa sababu ya dhamiri zenu; maana Maandiko yasema: “Dunia na vyote vilivyomo ni mali ya Bwana.” Kama mtu ambaye si mwaamini akiwaalikeni nanyi mkakubali kwenda, basi, kuleni vyote atakavyowaandalieni bila kuulizauliza kwa sababu ya dhamiri zenu. Lakini mtu akiwaambieni: “Chakula hiki kimetambikiwa sanamu,” basi, kwa ajili ya huyo aliyewaambieni hivyo na kwa ajili ya dhamiri, msile. Nasema, “kwa ajili ya dhamiri,” si dhamiri yenu, bali dhamiri yake huyo aliyewaambieni. Mtaniuliza: “Kwa nini uhuru wangu utegemee dhamiri ya mtu mwingine? Ikiwa mimi nashiriki chakula hicho huku namshukuru Mungu, kwa nini nilaumiwe kwa chakula ambacho kwa ajili yake nimemshukuru Mungu?” Basi, chochote mfanyacho iwe ni kula au kunywa, fanyeni yote kwa ajili ya utukufu wa Mungu. Msiwe kikwazo kwa Wayahudi au kwa Wagiriki au kwa kanisa la Mungu. Muwe kama mimi; najaribu kuwapendeza wote kwa kila njia, bila kutafuta faida yangu mwenyewe ila faida ya wote, wapate kuokolewa.

Mungu wetu tunawaweka mikononi mwako wenye shida/tabu,wote wanaopotia magumu/majaribu mbalimbali
watoto wako wanaokuomba kwa bidii na imani
Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu
 kila mmoja na mahitaji yake 
Yahweh tunaomba ukaonekane katika maisha yao
Jehovah tunaomba ukawaokoe,ukawavushe salama na  kuwalinda
Mungu wetu tunaomba ukawasamehe pale walipokwenda kinyume nawe
Baba wa Mbinguni ukawape neema ya kujiombea,kufuata njia zako
wakasimaie Neno lako nalo likaweke huru
Mungu wetu tunaomba ukasikie kuomba kwetu
Baba wa Mbinguni ukapokee sala/maombi yetu
Mungu wetu ukawatendee sawasawa na mapenzi yako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina...!!

Asanteni sana wapendwa katika Kristo Yesu kwakuwa nami
Mungu Baba aendelee kuwabariki na kuwatendea 
kama inavyompendeza yeye....
Nawapenda.



Hoja ya pili ya Elifazi

(15:1–21:34)

1Kisha Elifazi, Mtemani, akajibu:
2“Je, mtu wa hekima hujibu kwa maneno ya upuuzi?
Je, mtu huyo amejaa maneno matupu?
3Je, mwenye hekima hujitetea kwa maneno yasiyofaa,
au kwa maneno yasiyo na maana?
4Lakini wewe unapuuza uchaji wa Mungu;
na kuzuia kutafakari mbele ya Mungu.
5Uovu wako ndio unaokifundisha kinywa chako,
nawe wachagua kusema kama wadanganyifu.
6Maneno yako mwenyewe yanakuhukumu, sio mimi;
matamshi yako yashuhudia dhidi yako.
7Je, wewe ni mtu wa kwanza kuzaliwa?
Je, wewe ulizaliwa kabla ya kuweko vilima?
8Je, ulipata kuweko katika halmashauri ya Mungu?
au, wewe ndiwe peke yako mwenye hekima?
9Unajua kitu gani tusichokijua sisi?
Unafahamu kitu gani tusichokifahamu sisi?
10Miongoni mwetu wapo wazee wenye hekima,
wenye miaka mingi kuliko baba yako.
11Je, faraja anazokupa Mungu ni ndogo mno?
Au je, neno lake la upole kwako si kitu?
12Mbona moyo unakusukuma kukasirika
na kutoa macho makali,
13hata kumwasi Mungu
na kusema maneno mabaya kama hayo?
14 Taz Yobu 25:4-6 Mtu ni nini hata aweze kuwa mwadilifu?
au yule aliyezaliwa na mwanamke hata aweze kuwa mwema?
15Ikiwa Mungu hawaamini hata watakatifu wake,
nazo mbingu si safi mbele yake,
16sembuse binadamu aliye kinyaa na mpotovu
binadamu atendaye uovu kama kunywa maji!
17“Sasa nisikilize, nami nitakuonesha,
nitakuambia yale niliyoyaona,
18mafundisho ya wenye hekima,
mambo ambayo wazee wao hawakuyaficha,
19ambao Mungu aliwapa hiyo nchi peke yao,
wala hakuna mgeni aliyepita miongoni mwao.
20Mwovu atateseka kwa maumivu siku zote,
miaka yote waliyopangiwa wakatili.
21Sauti za vitisho zitampigia kelele masikioni,
anapodhani amestawi mwangamizi atamvamia.
22Mwovu hana tumaini la kutoka gizani;
mwisho wake ni kufa kwa upanga.
23Hutangatanga kutafuta chakula,
akisema, ‘Kiko wapi?’
Ajua kwamba siku ya giza inamkaribia.
24Taabu na uchungu, vyamtisha;
vyamkabili kama jeshi la mfalme anayeshambulia.
25Kwa sababu amenyosha mkono wake dhidi ya Mungu;
akadiriki kumpinga huyo Mungu mwenye nguvu;
26alikimbia kwa kiburi kumshambulia,
huku ana ngao yenye mafundo makubwa.
27Uso wake ameunenepesha kwa mafuta,
na kiuno chake kimejaa mafuta.
28Ameishi katika miji iliyoachwa tupu,
katika nyumba zisizokaliwa na mtu;
nyumba zilizotakiwa ziwe lundo la uharibifu.
29Mtu huyo kamwe hatakuwa tajiri;
wala utajiri wake hautadumu duniani.
30Hatalikwepa giza la kifo.
Ndimi za moto zitakausha chipukizi zake,
maua yake yatapeperushwa na upepo.
31Heri aache kutumainia upuuzi na kujidanganya,
maana upuuzi ndio utakaokuwa tuzo lake.
32Atalipwa kikamilifu kabla ya kufa kwake,
na wazawa wake hawatadumu.
33Atakuwa kama mzabibu unaopukutisha zabibu mbichi,
kama mzeituni unaoangusha maua yake.
34Wote wasiomcha Mungu hawatapata watoto,
moto utateketeza mahema ya wala rushwa.
35Wanatunga udanganyifu na kuzaa uovu.
Mioyo yao hupanga udanganyifu.”



Yobu15;1-35

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: