Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Wednesday 16 May 2018

Kikombe Cha Asubuhi ; 1Mambo ya Nyakati 5...




Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Haleluyah Mungu wetu yu mwema sana..
Tumshukuru Mungu wetu katika  yote...

Asante Mungu wetu kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa kibali cha kundelea
kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwa tayari kwa majukumu yetu
Utukuzwe ee mungu wetu,Usifiwe Baba wa Mbinguni,Uhimidiwe Jehovah,
Uabudiwe Yahweh,Matendo yako ni makuu mno,Mtaendo yako ni ya ajabu
Matendo yako yanatisha...
Neema yako yatutosha ee Mungu wetu...


Anayekaa chini ya ulinzi wa Mungu Mkuu, anayeishi chini ya kivuli cha Mungu Mwenye Nguvu, ataweza kumwambia Mwenyezi-Mungu: “Wewe ni kimbilio langu na ngome yangu; Mungu wangu, ninayekutumainia!” Hakika Mungu atakuokoa katika mtego; atakukinga na maradhi mabaya. Atakufunika kwa mabawa yake, utapata usalama kwake; mkono wake utakulinda na kukukinga.

Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha
na kujiachilia mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba utusamehe makosa yetu yote tuliyoyafanya
Kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua
Jehovah nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale
wote waliotukosea
Yahweh tunaomba utuepushe katika majaribu Mungu wetu utuokoe
na yule mwovu na kazi zake zote
Baba wa Mbinguni tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu
Jehovah utufunike na Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo
wa Nazareti yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona..


Huna haja ya kuogopa vitisho vya usiku, wala shambulio la ghafla mchana; huna haja ya kuogopa baa lizukalo usiku, wala maafa yanayotokea mchana. Hata watu elfu wakianguka karibu nawe, naam, elfu kumi kuliani mwako, lakini wewe baa halitakukaribia. Kwa macho yako mwenyewe utaangalia, na kuona jinsi watu waovu wanavyoadhibiwa. Wewe umemfanya Mwenyezi-Mungu kuwa kimbilio lako; naam, Mungu aliye juu kuwa kinga yako. Kwa hiyo, hutapatwa na maafa yoyote; nyumba yako haitakaribiwa na baa lolote.

Mungu wetu tunaomba  ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa katika utendaji
Yahweh nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Jehovah tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba ukatupe neema ya kuweza kuwabariki
wenye kuhitaji
Baba wa Mbinguni tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Mungu wetu ukatupe kama inavyokupendeza wewe..

Yahweh tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Jehovah tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,watoto,wazazi wetu
Familia/ndugu na wote wanaotuzunguka
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatamalaki na kutuatamia
Mungu wetu tukawe salama rohoni
Yahweh tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyo vimiliki
Jehovah tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukabariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Jehovah ukavitakase na kuvifunika kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mfalme wa amani tunaomba amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu tunaomba ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia
sauti yako na kuitii
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe  neema ya kufuata njia zako
Mungu wetu tukasimamie Neno lako amri na sheria zako siku zote za maisha yetu
Yahweh ukaonekane katika maisha yetu Mungu wetu ukatuguse
 kwa mkono wako wenye nguvu
Neema zako zitufuate  na Nuru yako ikaangaze katika maisha yetu
Mungu wetu ukatufanye chombo chema Yahweh nasi  tukatumike
kama inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi

Maana Mungu atawaamuru malaika zake, wakulinde popote uendapo. Watakuchukua mikononi mwao, usije ukajikwaa kwenye jiwe. Utakanyaga simba na nyoka, utawaponda wana simba na majoka. Mungu asema: “Nitamwokoa yule anipendaye; nitamlinda anayenitambua! Akiniita, mimi nitamwitikia; akiwa taabuni nitakuwa naye; nitamwokoa na kumpa heshima. Nitamridhisha kwa maisha marefu, nitamjalia wokovu wangu.”

Mungu wetu tazamna watoto wako wanaokutafuta/kukuomba
kwa bidii na imani
Baba wa Mbinguni tunaomba ukawaguse kila mmoja na mahita yake
Yahweh tunaomba ukaonekane katika maisha yao
Mungu wetu tunaomba ukasikie kulia kwao Baba wa Mbinguni
tunaomba ukawafute machozi yao
Jehovah tunaomba ukawasamehe pale walipokwenda kinyume nawe
Mungu wetu tunaomba ukawape neema ya kujiombea,kufuata njia
zako na kusimamia Neno lako nalo likawaweke huru
Yahweh tunaomba ukawape macho ya rohoni na masikio ya kusikia
sauti yako
Mungu wetu tunaomba ukasikie kuomba kwetu Baba wa Mbinguni
tunaomba ukapokee sala/maombi yetu
Jehovah ukawajibu na kuwatendea sawasawa na mapenzi yako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina..!!

Wapendwa katika Kristo Yesu asanteni sana kwa kuwa nami
Mungu Baba aendelee kuwabariki na kuwatendea sawasawa na mapenzi yake
Amani ya Bwana wetu Yesu Kristo na upendo wa Mungu Baba
ukawe nanyi daima...
Nawapenda.


Wazawa wa Reubeni

1Hawa ndio wazawa wa Reubeni, mzaliwa wa kwanza wa Israeli. (Ingawa Reubeni alikuwa mzaliwa wa kwanza haki yake ya mzaliwa wa kwanza ilipewa Yosefu nduguye kwa sababu Reubeni alilala na suria wa baba yake. Hivyo, yeye hakutiwa katika orodha ya ukoo kulingana na haki yake ya mzaliwa wa kwanza. 2Ingawa kabila la Yuda ndilo lililokuja kuwa lenye nguvu zaidi kuliko mengine, na watawala walitoka humo, haki ya mzaliwa wa kwanza ilikuwa ya Yosefu). 3Wana wa Reubeni, mzaliwa wa kwanza wa Israeli, walikuwa Henoki, Palu, Hesroni na Karmi.
4Wazawa wa Yoeli toka kizazi hadi kizazi walikuwa Shemaya, Gogi, Shimei, 5Mika, Reaya, Baali, 6na Beera, ambaye mfalme Tiglath-pileseri wa Ashuru, alimchukua mateka ingawa alikuwa kiongozi wa Wareubeni, akampeleka uhamishoni.
7Wakuu wa koo wafuatao waliandikishwa katika orodha ya kumbukumbu ya kabila la Reubeni, Yeieli, Zekaria, 8Bela, mwana wa Azazi na mjukuu wa Shema, wa ukoo wa Yoeli, uliokuwa ukiishi Aroeri na katika eneo lote la kaskazini hadi Bela na Baal-meoni. 9Pia, kwa maana mifugo yao iliongezeka kwa wingi sana, walisambaa upande wa mashariki hadi kwenye maingilio ya jangwa lililoenea hadi mto Eufrate.
10Katika siku za mfalme Shauli, kabila la Reubeni lilizusha vita dhidi ya Wahajiri, wakawaua vitani na kuitwaa ardhi yao yote mashariki mwa Gileadi, wakaishi humo.

Wazawa wa Gadi

11Kabila la Gadi lilipakana na kabila la Reubeni upande wa kaskazini, katika nchi ya Bashani iliyoenea mashariki hadi Saleka. 12Yoeli ndiye aliyekuwa mwanzilishi wa ukoo ulioongoza, wa pili Shafamu. Yanai na Shefati walikuwa waanzilishi wa koo nyingine huko Bashani. 13Ndugu zao kulingana na koo zao walikuwa saba: Mikaeli, Meshulamu, Sheba, Yorai, Yaakani, Zia na Eberi. 14Wote hawa walikuwa wana wa Abihaili, aliyekuwa mwana wa Huri, mwana wa Yaroa, mwana wa Yeshishai, mwana wa Yado, mwana wa Buzi. 15Ahi, aliyekuwa mwana wa Abdieli na mjukuu wa Guni, alikuwa mkuu katika koo hizi. 16Waliishi katika sehemu ya Gileadi, katika Bashani na miji yake na katika malisho yote ya Sharoni, hadi mipakani. 17Watu hao wote waliandikishwa katika koo, katika siku za Yothamu, mfalme wa Yuda, na Yeroboamu, mfalme wa Israeli.

Majeshi ya makabila ya mashariki

18Makabila ya Reubeni, Gadi na Manase ya mashariki, yalikuwa na wanajeshi shupavu wapatao 44,760, wenye ngao na mapanga, wavuta pinde stadi vitani. 19Walipigana vita na makabila ya Wahajiri, Yeturi, Nafishi na Nodabu. 20Waliweka tumaini lao kwa Mungu na wakamwomba awasaidie, naye akaitikia ombi lao na kuwatia mikononi mwao Wahajiri pamoja na marafiki zao. 21Waliteka nyara ngamia 50,000, kondoo 250,000, punda 2,000 na mateka hai 100,000. 22Waliua maadui wengi sana kwa sababu vita hivyo vilikuwa ni vita vya Mungu. Nao waliendelea kuishi katika nchi hiyo, mpaka wakati wa uhamisho.

Watu wa Manase ya mashariki

23Watu wa Manase ya mashariki waliishi katika nchi ya Bashani. Idadi yao iliongezeka kwa wingi sana, wakasambaa upande wa kaskazini hadi Baal-hermoni, Seniri na mlima Hermoni. 24Wafuatao ndio waliokuwa wakuu wa koo za kabila hilo: Eferi, Ishi, Elieli, Azrieli, Yeremia, Hodavia na Yadieli. Wote walikuwa askari shujaa, watu mashuhuri sana na viongozi katika koo hizo.

Makabila ya mashariki yatekwa

25Lakini watu walimwasi Mungu wa babu zao, wakafanya uzinzi kwa kuabudu miungu ya wakazi wa nchi hizo ambazo Mungu aliziangamiza mbele yao. 26Basi, Mungu wa Israeli akamfanya Pulu, mfalme wa Ashuru, (ambaye pia alijulikana kama Tiglath-pileseri), aivamie nchi yao na kuwachukua mateka hao Wareubeni, Wagadi na nusu Manase ya mashariki mpaka uhamishoni huko Hala, Habori na Hara, kando ya mto Gozani, ambako wamekaa mpaka leo.



1Mambo ya Nyakati5;1-26


Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: