Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Friday 25 May 2018

Kikombe Cha Asubuhi ; 1Mambo ya Nyakati 12...



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Haleluyah Mungu wetu yu mwema sana..
Tumshukuru Mungu wetu katika yote....

Mungu wetu Baba yetu,Muumba wetu Muumba wa Mbingu na Nchi
Mungu mwenye nguvu,Mungu mwenye huruma,Mungu mwenye upendo
Mungu wa walio hai,Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo
Mungu wa baraka,Mungu unaye jibu,Mungu unayesikia,Mungu wetu
ni Mungu wa haki.....
Unatosha ee Baba wa Mbinguni,Utukuzwe ee Mungu  wetu
Hakuna kama wewe Jehovah Jireh..!Jehovah Nissi..!Jehovah Raah..!
Jehovah Rapha..!Jehovah Shammah..!Jehovah Shalom...!
Emanuel-Mungu pamoja nasi...!!!

Asante kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwatayari kwa majukumu yetu
Sifa na Utukufu tunakurudishia ee Baba wa Mbinguni....!!


Mwanamke mwenye hekima huijenga nyumba yake, lakini mpumbavu huibomoa kwa mikono yake mwenyewe. Mwenye mwenendo mnyofu humcha Mwenyezi-Mungu, lakini mpotovu humdharau Mungu. Mpumbavu hujiadhibu mwenyewe kwa kuropoka kwake, lakini mwenye hekima hulindwa na maneno yake. Bila ng'ombe wa kulima ghala za mtu ni tupu, mavuno mengi hupatikana kwa nguvu ya ng'ombe wa kulima. Shahidi mwaminifu hasemi uongo, lakini asiyeaminika hububujika uongo. Mwenye dharau hutafuta hekima bure, lakini mwenye busara hupata maarifa kwa urahisi. Ondoka mahali alipo mpumbavu, maana hapo alipo hamna maneno ya hekima. Hekima ya mwenye busara humwonesha njia yake, lakini upumbavu wa wapumbavu huwadanganya wenyewe. Wapumbavu huchekelea dhambi, bali wanyofu hupata fadhili kwa Mungu.

Yahweh tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha
na kujiachilia mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizo zifanya
Kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba ukatupe neema
ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea
Usitutie majaribu Mungu wetu tunaomba utuepushe
na yule mwovu na kazi zake zote
Jehovah ututakase miili yetu na akili zetu
Baba wa Mbinguni tunaomba utufunike kwa Damu
ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti
yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona....




Moyo waujua uchungu wake wenyewe, wala mgeni hawezi kushiriki furaha yake. Nyumba ya mtu mwovu itabomolewa, lakini hema ya wanyofu itaimarishwa. Njia unayodhani kuwa ni sawa, mwishoni yaweza kukuongoza kwenye kifo. Huzuni yaweza kufichika katika kicheko; baada ya furaha huja majonzi. Mtu mpotovu atavuna matunda ya mwenendo wake, naye mtu mwema atapata tuzo la matendo yake. Mjinga huamini kila kitu anachoambiwa, lakini mwenye busara huwa na tahadhari. Mwenye hekima ni mwangalifu na huepa uovu, lakini mpumbavu hajizuii wala hana uangalifu. Mwenye kuwaka hasira haraka hutenda kipumbavu, lakini mwenye busara ana uvumilivu. Wajinga hurithi upumbavu, lakini wenye busara hutuzwa taji ya maarifa. Waovu watapiga magoti mbele ya watu wema, watu wabaya mlangoni mwa waadilifu. Maskini huchukiwa hata na jirani yake, lakini tajiri ana marafiki wengi. Anayemdharau jirani yake ni mwenye dhambi, bali ana heri aliye mwema kwa maskini. Anayepanga maovu kweli anakosea! Wanaopanga kutenda mema hufadhiliwa.

Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa katika utendaji
Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Yahweh tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba ukatupe neema ya kuweza
kuwabariki wenye kuhitaji
Tusipungukiwe katika mahitaji yetu Baba wa Mbinguni
ukatupe kama inavyokupendeza wewe....

Mfalme wa amani tunaomba amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,watoto,wazazi wetu,
Familia/ndugu na wote wanaotuzunguka
Jehovah tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Yahweh tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase na kuvifunika kwa Damu ya
Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu tunaomba ulinzi wako kwetu na kwavyote tunavyo vimiliki
Baba wa Mbinguni ukatamalaki na kutuatamia
Mungu wetu tukawe salama rohoni
Baba wa Mbinguni ukaonekane katika maisha yetu
popote tupitapo na ikajulikane kwamba upo Baba wa Mbinguni
Ukatupe akili ya kutambua mema na mabaya
Ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia sauti yako na kuitii
Ukatupe neema ya kufuata njia zako Baba wa Mbinguni
tukasimamie Neno lako amri na sheria zako siku zote za maisha yetu
Neema zako zikawe nasi Nuru yako ikaangaze katika maisha yetu
Ukatufanye chombo chema ee Mungu wetu nasi tukatumike
kama inavyokupendeza wewe
Roho Matakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi...





Bidii katika kila kazi huleta faida, lakini maneno matupu huleta umaskini. Mali ni taji ya fahari ya wenye hekima, lakini ujinga ni shada la wapumbavu. Shahidi wa kweli huokoa maisha, lakini msema uongo ni msaliti. Amchaye Mwenyezi-Mungu ana tumaini imara, na watoto wake watapata kimbilio salama. Kumcha Mwenyezi-Mungu ni chemchemi ya uhai; humwezesha mtu kuepa mitego ya kifo. Fahari ya mfalme ni wingi wa watu wake, lakini bila watu mtawala huangamia. Mtu asiye mwepesi wa hasira ana busara kubwa, lakini akasirikaye upesi hukuza upumbavu. Amani rohoni humpa mtu afya, lakini tamaa huozesha mifupa. Anayemdhulumu maskini anamtukana Muumba wake, lakini amwoneaye huruma mhitaji anamtukuza Mungu. Mwovu huangamizwa kwa matendo yake maovu, lakini mwadilifu hupata usalama kwa unyofu wake. Hekima imo moyoni mwa mtu mwenye busara; haipatikani kamwe mioyoni mwa wapumbavu. Uadilifu hukuza taifa, lakini dhambi ni balaa kwa taifa lolote. Mfalme humfadhili mtumishi atendaye kwa hekima, lakini hasira yake huwakumba watendao yasiyofaa.


Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu
wote wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali
wenye shida/tabu,wagonjwa,wenye njaa na kila mmoja
na mahitaji yake..
Baba wa Mbinguni tunaomba ukaonekane katika maisha yao
Mungu wetu tunaomba ukawaokoe na kuwavusha salama
Yahweh tunaomba ukawasamehe pale walipokwenda kinyume nawe
Mungu wetu tunaomba ukawape neema ya kujiombea,kufuata njia zako
Baba wa Mbinguni ukawape macho ya rohoni na masikio ya kusikia sauti yako na kuitii
Nuru yako ikaangaze katika maisha yao,amani ikatawale..
Ee Baba tunaomba ukasikie kuomba kwetu
Mungu wetu tunaomba ukawatendee sawasawa na mapenzi yako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina...!!

Wapendwa katika Kristo Yesu asanteni sana
kwakuwanami/kunisoma
Mungu Baba aendelee kuwabariki na kuwatendea
kama inavyompendeza yeye
Amani ya Bwana wetu Yesu Kristo na upendo wa Mungu Baba
ukae nanyi daima....
Nawapenda.


Wafuasi wa kwanza wa Daudi kutoka Benyamini

1Hawa ni wanaume ambao walijiunga na Daudi huko Siklagi, alipokuwa hana uhuru wowote wa kutembea kwa sababu ya mfalme Shauli mwana wa Kishi; walikuwa miongoni mwa askari mashujaa waliomsaidia vitani. 2Hao walikuwa watu wa kabila la Benyamini kama alivyokuwa Shauli. Walikuwa wapiga upinde hodari, na warusha mawe kwa kombeo kwa kutumia mikono yote, wa kulia na kushoto. 3Kiongozi wao alikuwa Ahiezeri, aliyesaidiwa na Yoashi, wote wana wa Shemaa kutoka Gibea; wengineo ni: Yezieli na Peleti, wana wa Azmawethi, Beraka, Yehu kutoka Anathothi, 4Ishmaya kutoka Gibeoni, mtu shujaa miongoni mwa wale thelathini na kiongozi wao pia pamoja na Yeremia, Yahazieli, Yohanani, Yozabadi kutoka Gedera, 5Eluzai, Yeremothi, Bealia, Shemaria, Shefatia, Mharufi, 6Elkana, Ishia, Azareli, Yoezeri, Yashobeamu kutoka ukoo wa Kora 7na Yoela na Zebadia, wana wa Yerohamu, kutoka Gedori.

Wafuasi wa Daudi kutoka kabila la Gadi

8Tena, watu kutoka kabila la Gadi walijiunga na Daudi akiwa ngomeni kule nyikani. Hawa walikuwa askari wenye nguvu na uzoefu, hodari wa kutumia ngao na mkuki; wenye nyuso za kutisha kama simba na wepesi kama swala milimani. 9Kiongozi wao mkuu alikuwa Ezeri, wa pili Obadia, wa tatu Eliabu, 10wa nne Mishmana, wa tano Yeremia, 11wa sita Atai, wa saba Elieli, 12wa nane Yohanani, wa tisa Elsabadi, 13wa kumi Yeremia, na wa kumi na moja Makbanai. 14Wagadi hao, walikuwa maofisa wa jeshi. Kulingana na vyeo vyao, mdogo alisimamia kikosi cha wanajeshi 100, na mkubwa alisimamia kikosi cha wanajeshi 1,000. 15Hawa ndio watu waliovuka mto Yordani mnamo mwezi wa kwanza, mto ulipokuwa umefurika pande zote na kuwatawanya watu mashariki na magharibi ya mto.

Wafuasi kutoka Benyamini na Yuda

16Baadhi ya watu kutoka makabila ya Benyamini na Yuda walifika ngomeni alipokuwa Daudi. 17Daudi akatoka nje kuwalaki, akawaambia, “Ikiwa mmekuja kwangu kama marafiki ili kunisaidia basi nawapokea kwa moyo wote, lakini kama mmekuja ili kunisaliti kwa maadui zangu, ingawa sijatenda ovu lolote, Mungu wa baba zetu awaone na awakemee.” 18Hapo Roho akamjia Abishai, mkuu wa hao watu thelathini, naye akasema,
“Sisi tu watu wako, ee Daudi,
tuko upande wako, ee mwana wa Yese!
Amani, amani iwe kwako,
na amani iwe kwa yeyote akusaidiaye!
Maana akusaidiaye ndiye Mungu wako.”
Ndipo Daudi akawapokea na kuwafanya maofisa katika jeshi lake.

Wafuasi toka Manase

19Askari wengine wa kabila la Manase, walitoroka na kujiunga na Daudi, wakati alipoondoka pamoja na Wafilisti kwenda kupigana na mfalme Shauli. (Lakini hata hivyo, hakuwasaidia maana watawala wa Wafilisti walifanya shauri wamfukuze arudi Siklagi wakisema, “Tutayahatarisha maisha yetu kwa sababu atatutoroka arudi kwa bwana wake Shauli.”) 20Basi, Daudi alipokuwa Siklagi, watu wafuatao wa kabila la Manase walimwendea: Adna, Yozabadi, Yediaeli, Mikaeli, Yozabadi, Elihu na Silethai. Kila mmoja wao alikuwa kiongozi wa kikosi cha watu 1,000 katika kabila la Manase. 21Walimsaidia Daudi kupigana na magenge ya washambuliaji,12:21 kupigana … washambuliaji: Au Kama maofisa wa jeshi lake. kwani wote walikuwa askari mashujaa na makamanda jeshini. 22Siku hata siku, watu walijiunga na Daudi kumsaidia, hatimaye akawa na jeshi kubwa sana, kama jeshi la Mungu.

Orodha ya majeshi ya Daudi

23Hii ndio idadi ya vikosi vya askari wenye silaha waliojiunga na Daudi huko Hebroni ili kumtwalia ufalme kutoka kwa Shauli, kulingana na neno la Mwenyezi-Mungu: 24Watu wa kabila la Yuda waliokuwa na mikuki na ngao, walikuwa 6,800. Wote walikuwa na silaha zao. 25Kutoka kabila la Simeoni, watu 7,100 mashujaa na wenye ujuzi mwingi wa vita. 26Kutoka kabila la Lawi: Watu 4,600. 27Yehoyada, wa uzao wa Aroni na wenzake: Watu 3,700. 28Jamaa ya Sadoki, kijana hodari vitani, yeye pamoja na makamanda ishirini na wawili kutoka ukoo wa baba yake mwenyewe. 29Kutoka kabila la Benyamini, (kabila la Shauli): Watu 3,000. Wengi wao walibaki waaminifu kwa jamaa ya Shauli; 30Kutoka kabila la Efraimu: Watu 20,800, watu mashujaa sana tena mashuhuri katika koo zao; 31Kutoka nusu ya kabila la Manase: Watu 18,000, waliotajwa majina ili waje kumtawaza Daudi awe mfalme. 32Kutoka kabila la Isakari: Wakuu 200 pamoja na ndugu zao wote waliokuwa chini ya amri yao. Wakuu hao walikuwa na elimu ya kujua mambo ya nyakati na walijua kilichowapasa Waisraeli kufanya. 33Kutoka kabila la Zebuluni: Watu 50,000; waaminifu na wazoefu wa vita. Walijiandaa na zana za vita za kila namna, lengo lao likiwa ni kumsaidia Daudi tu. 34Kutoka kabila la Naftali: Makamanda 1,000 pamoja na watu 37,000 wenye ngao na mikuki. 35Kutoka kabila la Dani: Watu 28,600 wenye silaha tayari kwa vita. 36Kutoka kabila la Asheri: Watu 40,000 wazoefu wa vita, tayari kwa mapigano. 37Kutoka kabila la Wareubeni, Wagadi na nusu ya kabila la Manase kutoka ngambo ya mto Yordani: Watu 120,000 wenye kila aina ya silaha za vita.
38Wanajeshi hao wote, waliojiandaa tayari kabisa kwa vita, walikwenda Hebroni na nia yao kubwa ikiwa ni kumtawaza Daudi awe mfalme wa Israeli yote. Nao watu wote wa Israeli, pia waliungana wakiwa na nia moja ya kumtawaza Daudi awe mfalme.
39Basi, walikaa na Daudi kwa muda wa siku tatu, wakila na kunywa kwani ndugu zao walikuwa wamekwisha waandalia vyakula. 40Zaidi ya hayo, majirani zao wa karibu na hata wa mbali kama huko Isakari, Zebuluni na Naftali, waliwaletea vyakula walivyobeba kwa punda, ngamia, nyumbu na ng'ombe. Waliwaletea unga, mikate ya tini, vichala vya zabibu kavu, divai na mafuta, ng'ombe na kondoo wengi, kukawa na vyakula tele, kwani kulikuwa na furaha katika Israeli.



1Mambo ya Nyakati12;1-40


Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: