Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Tuesday 26 February 2019

Kikombe Cha Asubuhi ;Zaburi 69...


Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu katika yote...

Asante kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante

 kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwatayari kwa majukumu yetu


Utukuzwe ee Mungu wetu,usifiwe Baba wa Mbinguni

Jehovah  Jireh..!Jehovah Nissi..!Jehovah Raah..!
Jehovah Rapha..!Jehovah Shammah..!Jehovah Shamlom..!
Emanuel-Mungu pamohja nasi..!!
Neema yako yatutosha Baba wa Mbinguni..!

Ndugu, nawasihini kwa jina la Bwana wetu Yesu Kristo: Pataneni nyote katika kila jambo msemalo; yasiweko mafarakano kati yenu; muwe na fikira moja na nia moja. Ndugu zangu, habari nilizopata kutoka kwa watu kadhaa wa jamaa ya Kloe, zaonesha wazi kwamba kuna kutoelewana kati yenu.

Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea,Usitutie majaribuni Mungu wetu tunaomba utuepushe na yule mwovu na kazi zake zote,Jehovah ututakase miili yetu na akili zetu Baba wa Mbinguni tunaomba utufunike kwa  Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti,
Yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona.....

Nataka kusema hivi: Kila mmoja anasema chake: Mmoja husema, “Mimi ni wa Paulo”, mwingine: “Mimi ni wa Apolo”, mwingine: “Mimi ni wa Kefa,” na mwingine: “Mimi ni wa Kristo.” Je, Kristo amegawanyika? Je, Paulo ndiye aliyesulubiwa kwa ajili yenu? Au je, mlibatizwa kwa jina la Paulo? Namshukuru Mungu kwamba sikumbatiza mtu yeyote miongoni mwenu isipokuwa tu Krispo na Gayo.

Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa 
katika utendaji
Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki ridhiki zetu
ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba ukatupe neema ya kuweza
kuwabariki wenye kuhitaji
Yahweh tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Mungu wetu ukatupe kama inavyokupendeza wewe



Jehovah tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyo vimiliki
Yahweh tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia
Baba wa Mbinguni tukawe salama rohoni
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia 
sauti yako na kuitii
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe neema ya kufuata njia zako
Yahweh tukasimamie Neno lako amri na sheria zako siku zote 
za maisha yetu

Mungu wetu tunaomba ukatupe akili ya kutambua mema na mabaya Baba wa Mbinguni ukaonekane katika maisha yetu popote tupitapo na ikajulikane kwamba upo Mungu wetu

Neema zako zikawe nasi Nuru yako ikaangaze katika maisha yetu
ukatuguse kwa mkono wako wenye nguvu
Ukatufanye barua njema ee Mungu wetu nasi tukasomeke kama
inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi...

Kwa hiyo hakuna awezaye kusema amebatizwa kwa jina langu. ( Samahani, nilibatiza pia jamaa ya Stefana; lakini zaidi ya hawa, sidhani kama nilimbatiza mtu mwingine yeyote). Kristo hakunituma kubatiza, bali kuhubiri Habari Njema; tena, niihubiri bila kutegemea maarifa ya hotuba za watu, kusudi nguvu ya kifo cha Kristo msalabani isibatilishwe.
Tazama wenye shida/tabu,watoto wako wanaokutafuta kwa bidii na imani
Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu
Yahweh tunaomba  ukawaguse kila mmoja na mahitaji yake
Mungu wetu  unajua haja za mioyo ya kila mmoja
Baba wa Mbinguni tunaomba ukawasamehe pale walipokwenda
kinyume nawe
Mungu wetu ukawape neema ya kujiombea,macho ya rohoni,masikio yakusikia sauti yako,wakafuate njia zako nazo zikawaweke huru
Mungu wetu tunaomba ukasikie kulia kwao
Baba wa Mbinguni tunomba ukawafute machozi yao
Jehovah ukaonekane katika maisha yao
Nuru yako ikaangaze katika maisha yao
Mungu wetu tunaomba ukawatendee sawasawa na mapenzi yako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina....!!!


Wapendwa katika Kristo Yesu asanteni sana
kwakuwanami/kunisoma

Mungu Baba aendelee kuwabariki na kuwatendea
kama inavyompendeza yeye
Amani ya Bwana wetu Yesu Kristo na upendo wa Mungu Baba
ukae nanyi daima....
Nawapenda.

Maombolezo
(Kwa Mwimbishaji: Mtindo wa Yungiyungi. Zaburi ya Daudi)
1Uniokoe, ee Mungu;
maji yamenifika shingoni.
2Ninazama ndani ya matope makuu,
hamna hata mahali pa kuweka miguu.
Nimetumbukia kwenye kilindi cha maji,
nachukuliwa na mawimbi.
3Niko hoi kwa kupiga yowe,
na koo langu limekauka.
Macho yangu yamefifia,
nikikungojea ewe Mungu wangu.
4 Taz Zab 35:19; Yoh 15:25 Watu wengi kuliko nywele zangu ndio wanichukiao bure.
Wana nguvu sana hao wanaotaka kuniua,
hao wanaonishambulia kwa mambo ya uongo.
Je, nirudishe kitu ambacho sikuiba?
5Ee Mungu, waujua upumbavu wangu;
makosa yangu hayakufichika kwako.
6Wanaokutumainia wasiaibishwe kwa sababu yangu,
ee Bwana Mwenyezi-Mungu wa majeshi;
wanaokutafuta, wasione fedheha kwa sababu yangu
ee Mungu wa Israeli.
7Kwa ajili yako nimefedheheshwa,
aibu imefunika uso wangu.
8Nimekuwa mgeni kwa ndugu zangu,
kaka na dada zangu hawanitambui.
9 Taz Yoh 2:17; Rom 15:3 Upendo wangu kwa nyumba yako unanimaliza.
Kashfa zote wanazokutolea wewe zimenipata mimi.
10Nilipojinyenyekesha kwa kufunga,
watu walinilaumu.
11Nilipovaa vazi la gunia kuomboleza,
wao walinidharau.
12Watu wananisengenya mabarabarani;
walevi wanatunga nyimbo juu yangu.
13Lakini mimi nakuomba wewe, ee Mwenyezi-Mungu;
nikubalie ombi langu wakati unaopenda, ee Mungu.
Kwa wingi wa fadhili zako unijibu.
Wewe ni mkombozi wa kuaminika.
14Kwa msaada wako amini uniokoe
nisizame katika matope;
uniokoe na hao wanaonichukia,
unisalimishe kutoka vilindi vya maji.
15Usiniache nikumbwe na mkondo wa maji,
au nizame kwenye kilindi
au nimezwe na kifo.
16Unijibu, ee Mwenyezi-Mungu,
kwa wema na fadhili zako;
unielekee kwa wingi wa huruma yako.
17Usimfiche mtumishi wako uso wako;
unijibu haraka, maana niko hatarini.
18Unijie karibu na kunikomboa,
uniokoe na maadui zangu wengi.
19Wewe wajua ninavyotukanwa,
wajua aibu na kashfa ninazopata;
na maadui zangu wote wewe wawajua.
20Kashfa zimeuvunja moyo wangu,
nami nimekata tamaa.
Nimetafuta kitulizo lakini sikupata,
wa kunifariji lakini sikumpata.
21 Taz Mat 27:48; Marko 15:36; Luka 23:36; Yoh 19:28-29 Walinipa sumu kuwa chakula,
na nilipokuwa na kiu wakanipa siki.
22 Taz Rom 11:9-10 Karamu zao na ziwe mtego kwao,
na sikukuu zao za sadaka ziwanase.
23Macho yao yatiwe giza wasiweze kuona,
uitetemeshe daima migongo yao.
24Uwamwagie hasira yako,
ghadhabu yako iwakumbe.
25 Taz Mate 1:20 Kambi zao ziachwe mahame,
asiishi yeyote katika mahema yao.
26Maana wanawatesa wale uliowaadhibu,
wanawaongezea majeraha wale uliowajeruhi.
27Uwaadhibu kwa kila uovu wao;
uwakatalie kabisa msamaha wako.
28 Taz Ufu 3:5; 13:8; 17:8 Uwafute katika kitabu cha walio hai,
wasiwemo katika orodha ya waadilifu.
29Lakini mimi mnyonge na mgonjwa;
uniinue juu, ee Mungu, uniokoe.
30Kwa wimbo nitalisifu jina la Mungu,
nitamtukuza kwa shukrani.
31Jambo hili litampendeza Mwenyezi-Mungu zaidi,
kuliko kumtolea tambiko ya ng'ombe,
kuliko kumtolea fahali mzimamzima.
32Wanyonge wataona hayo na kufurahi;
wanaomheshimu Mungu watapata moyo.
33Mwenyezi-Mungu huwasikiliza fukara;
hatawasahau kamwe watu wake wafungwa.
34Enyi mbingu na dunia msifuni Mungu;
bahari na vyote vilivyomo, msifuni.
35Maana Mungu atauokoa mji Siyoni,
na kuijenga tena miji ya Yuda.
Watu wake wataishi humo na kuimiliki;
36wazawa wa watumishi wake watairithi,
wale wanaopenda jina lake wataishi humo.

Zaburi69;1-36

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: