Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Friday 14 July 2017

Kikombe Cha Asubuhi;kitabu cha Hesabu..9



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu kwa wema na fadhili zake kwetu..
Asante Mungu wetu,Baba yetu,Muumba wetu,Muumba wa Mbingu na Nchi..
Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo..
Yahweh..!Jehovah..!El shaddai..!Elohim..!El Olam..!Adonai..!
Emanueli[Mungu pamoja nasi]
Kuzaliwa kwa Yesu
(Luka 2:1-7)
Basi, hivi ndivyo Yesu Kristo alivyozaliwa: Maria, mama yake, alikuwa ameposwa na Yosefu. Lakini kabla hawajakaa pamoja kama mume na mke, alionekana kuwa mjamzito kwa uwezo wa Roho Mtakatifu. Yosefu, mumewe, kwa vile alikuwa mwadilifu, hakutaka kumwaibisha hadharani; hivyo alikusudia kumwacha kwa siri. Alipokuwa bado anawaza jambo hilo, malaika wa Bwana alimtokea katika ndoto, akamwambia, “Yosefu, mwana wa Daudi, usiogope kumchukua Maria awe mke wako, maana amekuwa mjamzito kwa uwezo wa Roho Mtakatifu. Atajifungua mtoto wa kiume, nawe utampa jina Yesu, kwa kuwa yeye ndiye atakayewaokoa watu wake katika dhambi zao.” Basi, haya yote yalitukia ili litimie lile neno Bwana alilosema kwa njia ya nabii: “Bikira atachukua mimba, atamzaa mtoto wa kiume, nao watampa jina Emanueli” (maana yake, “Mungu yuko nasi”). Hivyo, Yosefu alipoamka usingizini alifanya kama malaika huyo alivyomwambia, akamchukua mke wake nyumbani. Lakini hakulala naye hata Maria alipojifungua mtoto wa kiume. Naye Yosefu akampa jina Yesu.
Asante Mungu Baba  kwa ulinzi wako wakati wote..
Tazama Jana imepita Mungu wetu Leo ni Siku mpya na Kesho ni siku nyinge..
Mfalme wa Amani tunashuka mbele zako tukijinyenyekeza na kujiachilia mikononi mwako..
Tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizozifanya..
Kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua..
Baba wa Mbinguni tunaomba nasi utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale waliotukosea..
Utuepushe katika majaribu na utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote..
Ututakase Miili yetu na Akili zetu kwa Damu ya Mwanao Mpendwa Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona...

Siku moja, Yesu alikuwa mahali fulani akisali. Alipomaliza kusali, mmoja wa wanafunzi wake akamwambia, “Bwana, tunakuomba utufundishe kusali kama Yohane Mbatizaji alivyowafundisha wanafunzi wake.” Yesu akawaambia, “Mnaposali, semeni: ‘Baba! Jina lako litukuzwe; ufalme wako ufike. Utupe daima chakula chetu cha kila siku. Utusamehe dhambi zetu, maana sisi tunawasamehe wote waliotukosea; wala usitutie katika majaribu.’” Kisha akawaambia, “Tuseme mmoja wenu anaye rafiki, akaenda kwake usiku wa manane, akamwambia: ‘Rafiki, tafadhali niazime mikate mitatu, kwa kuwa rafiki yangu amepitia kwangu akiwa safarini nami sina cha kumpa.’ Naye, akiwa ndani angemjibu: ‘Usinisumbue! Nimekwisha funga mlango. Mimi na watoto wangu tumelala; siwezi kuamka nikupe!’ Hakika, ingawa hataamka ampe kwa sababu yeye ni rafiki yake, lakini, kwa sababu ya huyo mtu kuendelea kumwomba, ataamka ampe chochote anachohitaji. Kwa hiyo, ombeni nanyi mtapewa; tafuteni nanyi mtapata; bisheni mlango nanyi mtafunguliwa. Maana yeyote aombaye hupewa, atafutaye hupata na abishaye mlango hufunguliwa. Mtoto akimwomba baba yake samaki, je, atampa nyoka badala ya samaki? Na kama akimwomba yai, je, atampa nge? Kama nyinyi, ingawa ni waovu, mnajua kuwapa watoto wenu vitu vizuri, hakika baba yenu wa mbinguni atafanya zaidi; atawapa Roho Mtakatifu wale wanaomwomba.”
Roho Mtakatifu akatuongoze na tukapate kutambua/kujitambua na tukawe na kiasi
Baba wa Mbinguni tunaomba utubariki na ukabariki yote tunayoenda kufanya/kutenda na tukatende kama inavyokupendeza wewe..

Tunakushuru na kukusifu Daima..
Tunayaweka haya yote mikononi mwako tuliyoyanena na tusiyoyanena Baba wa Mbinguni unayajua na kutujua vyema kuliko tujijuavyo sisi..
Sifa na Utukufu tunakurudishia wewe Mungu..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina..!

Asanteni sana kwakunitembelea/kunisoma..
Mungu aendelee kuwabariki katika yote..
Mungu akaonekane katika maisha yenu..
nanyi msipungukiwe katika mahitaji yenu..
Mungu akawape sawasawa na mapenzi yake..
Nawapenda.


Pasaka ya pili

1Kisha mnamo mwezi wa kwanza wa mwaka wa pili baada ya Waisraeli kutoka Misri, Mwenyezi-Mungu aliongea na Mose katika jangwa la Sinai. Alimwambia: 2“Waisraeli sharti waiadhimishe sikukuu ya Pasaka wakati uliopangwa. 3Hii itakuwa siku ya kumi na nne ya mwezi huu; wakati wa jioni watafanya hivyo kufuatana na masharti na maagizo yake yote.” 4Kwa hiyo, Mose akawaambia watu kwamba wanapaswa kuiadhimisha sikukuu ya Pasaka. 5Basi, wakaiadhimisha Pasaka jioni, siku ya kumi na nne ya mwezi wa kwanza, katika jangwa la Sinai. Waisraeli walifanya yote kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose.
6Lakini, baadhi ya watu waliokuwapo walikuwa hawawezi kuiadhimisha sikukuu hiyo ya Pasaka kwa sababu walikuwa wamegusa maiti, wakawa najisi. Hao waliwaendea Mose na Aroni, 7wakawaambia, “Sisi tu najisi kwa kuwa tumegusa maiti, lakini kwa nini tukatazwe kumtolea Mwenyezi-Mungu sadaka zake kwa wakati uliopangwa pamoja na Waisraeli wengine?”
8Mose akawajibu, “Ngojeni mpaka hapo nitakapopata maagizo juu yenu kutoka kwa Mwenyezi-Mungu.”
9Naye Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose, 10“Mmoja wenu au mmoja wa wazawa wenu akiwa najisi kwa sababu amegusa maiti au akiwa mbali safarini, lakini akiwa anataka kuiadhimisha sikukuu ya Pasaka, 11mtu kama huyo anaruhusiwa kufanya hivyo mwezi mmoja baadaye, jioni ya siku ya kumi na nne ya mwezi wa pili. Ataiadhimisha kwa kula mikate isiyotiwa chachu na mboga chungu. 12Wasibakize chakula chochote hadi asubuhi, wala wasivunje hata mfupa mmoja wa wanyama wa Pasaka. Wataiadhimisha sikukuu hii ya Pasaka kulingana na kanuni zake zote. 13Lakini mtu yeyote ambaye ni safi au hayumo safarini, asipoiadhimisha sikukuu ya Pasaka, atatengwa na watu wake kwa kuwa hakunitolea sadaka kwa wakati uliopangwa. Ni lazima aadhibiwe kwa ajili ya dhambi yake.
14“Ikiwa kuna mgeni anayeishi pamoja nanyi na anapenda kuiadhimisha sikukuu ya Pasaka, mtu huyo sharti afanye hivyo kulingana na masharti na maagizo yote ya Pasaka. Kila mtu atafuata masharti yaleyale, akiwa mgeni au mwenyeji.”

Wingu la moto

(Kut 40:34-38)

15Siku ambayo hema takatifu lilisimikwa, wingu lilishuka na kulifunika hema la maamuzi. Wakati wa usiku wingu hilo lilionekana kama moto mpaka asubuhi. 16Hivyo ndivyo ilivyokuwa kila siku; wingu lililifunika hema mchana, na usiku lilionekana kama moto. 17Kila mara wingu hilo lilipoinuliwa juu ya hema, Waisraeli walivunja kambi na kupiga kambi tena mahali wingu hilo lilipotua. 18Walisafiri kwa amri ya Mwenyezi-Mungu, na kupiga kambi tena kwa amri yake. Muda wote wingu hilo lilipokuwa juu ya hema, watu walikaa katika kambi hiyo. 19Hata kama wingu hilo lilikaa juu ya hema kwa muda wa siku nyingi, Waisraeli walimtii Mwenyezi-Mungu, nao hawakuondoka. 20Wakati mwingine wingu hilo lilikaa juu ya hema kwa muda wa siku chache tu; lakini kila wakati Waisraeli walibaki kambini; walihama kama Mwenyezi-Mungu alivyowaamuru. 21Wakati mwingine wingu lilikaa juu ya hema tangu jioni mpaka asubuhi tu; na mara tu lilipoinuliwa, hao watu pia walifunga safari. Na ikiwa lilikaa juu ya hema mchana kutwa na usiku kucha, wao waliondoka tu wingu lilipoinuliwa. 22Ikiwa ni siku mbili, mwezi, mwaka au zaidi, muda wote wingu hilo lilipokuwa juu ya hema, Waisraeli hawakuhama; lakini lilipoinuliwa, nao pia walihama. 23Kwa agizo la Mwenyezi-Mungu walipiga kambi na kwa agizo la Mwenyezi-Mungu walisafiri. Walishika agizo la Mwenyezi-Mungu kama alivyotoa amri yake kwa njia ya Mose.

Hesabu9;1-23


Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)
"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: