Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Tuesday 17 April 2018

Kikombe Cha Asubuhi ; 2 Wafalme 9......



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu katika yote...
Mungu wetu Baba yetu,Muumba wetu Muumba wa Mbingu na Nchi
Muumba wa vyote vilivyomo vinavyoonekana na visivyoonekana
Mungu wa walio hai,Mungu mwenye nguvu,Mungu mwenye huruma
,Mungu mwenye kuponya,Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo..
Muweza wa yote Alfa na Omega...!!

Asante Baba wa Mbinguni kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa kibali cha kuendelea
kuiona leo hii
Asante kwa uwepo wako,pumzi/uzima,afya na kuwa tayari 
kwa majukumu yetu
Neema yako yatutosha ee Mungu wetu...!!


Sisi tulio imara katika imani tunapaswa kuwasaidia wale walio dhaifu wayakabili matatizo yao. Tusijipendelee sisi wenyewe tu. Kila mmoja wetu anapaswa kumpendeza jirani yake kwa wema ili huyo apate kujijenga katika imani. Maana Kristo hakujipendelea mwenyewe; ila alikuwa kama yasemavyo Maandiko: “Kashfa zote walizokutolea wewe zimenipata mimi.” Maana, yote yaliyoandikwa yameandikwa kwa ajili ya kutufundisha sisi ili kutokana na saburi na faraja tupewayo na hayo Maandiko Matakatifu tupate kuwa na matumaini. Mungu aliye msingi wa saburi na faraja yote, awajalieni nyinyi kuwa na msimamo mmoja kufuatana na mfano wake Kristo Yesu, ili nyinyi nyote, kwa nia moja na sauti moja, mumtukuze Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo.

Tazama jana imepita  ee Mungu wetu leo ni siku mpya Baba wa Mbinguni
na kesho ni siku nyingine Jehovah....
Mungu wetu tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha na 
kujiachilia mikononi mwako
Baba wa Mbinguni tunaomba utusamehe makosa yetu yote tuliyoyafanya
Kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua
Yahweh nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote
waliotukosea
Jehovah usitutie majaribuni Mungu wetu utuokoe na yule mwovu na kazi
zake zote
Baba wa Mbinguni tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu
Yahweh tunaomba utufunike kwa Damu ya Bwana na Mwokozi wetu
Yesu Kristo wa Nazareti yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona....


Basi, karibishaneni kwa ajili ya utukufu wa Mungu kama naye Kristo alivyowakaribisheni. Maana, nawaambieni Kristo aliwatumikia Wayahudi apate kuonesha uaminifu wa Mungu, na zile ahadi Mungu alizowapa babu zetu zipate kutimia; ili nao watu wa mataifa mengine wapate kumtukuza Mungu kwa sababu ya huruma yake. Kama yasemavyo Maandiko Matakatifu: “Kwa hiyo nitakusifu miongoni mwa watu wa mataifa. Nitaziimba sifa za jina lako.” Tena Maandiko yasema: “Furahini, enyi watu wa mataifa; furahini pamoja na watu wake.” Na tena: “Enyi mataifa yote, msifuni Bwana; enyi watu wote, msifuni.” Tena Isaya asema: “Atatokea chipukizi katika ukoo wa Yese, naye atawatawala watu wa mataifa; nao watamtumainia.” Basi, Mungu aliye msingi wa matumaini, awajazeni furaha yote na amani kutokana na imani yenu; tumaini lenu lipate kuongezeka kwa nguvu ya Roho Mtakatifu.

Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Mungu wetu tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa katika utendaji
Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Mungu wetu tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Yahweh nasi tunaomba ukatupe neema ya kuweza kuwabariki
wenye kuhitaji
Mungu wetu tusipungukiwe katika mahitaji yetu Baba wa Mbinguni
ukatupe kama inavyokupendeza wewe...

Mfalme wa amani tunaomba amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,watoto,wazazi wetu
Familia/ndugu na wote wanaotuzunguka
Yahweh tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyovimiliki
Mungu wetu tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Jehovah ukavitakase na kuvifunika kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu tunaomba ukatamalaki na kutuatamia
Yahweh tukawe salama rohoni Baba wa Mbinguni ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia sauti yako na kuitii
Jehovah tunaomba ukatupe neema ya kufuata njia zako Yahweh tukasimamie Neno lako amri na sheria zako siku zote za maisha yetu
Mungu wetu ukatupe neema ya kutambua mema na mabaya
Baba wa Mbinguni ukaonekane katika maisha yetu neema yako na Nuru
yako ikaangaze katika maisha yetu,hekima,busara vikawe nasi  upendo
ukadumu kati yetu....
Ukatufanye chombo chema Mungu wetu nasi tukatumike kama 
inavyokupendeza wewe..
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi....


Ndugu zangu, mimi binafsi nina hakika kwamba nyinyi pia mmejaa wema, elimu yote, na mnaweza kushauriana nyinyi kwa nyinyi. Lakini nimewaandikia hapa na pale katika barua hii bila woga, nipate kuwakumbusheni juu ya mambo fulani. Nimefanya hivyo kwa sababu ya neema aliyonijalia Mungu ya kuwa mtumishi wa Yesu Kristo kwa watu wa mataifa. Ni jukumu langu la kikuhani kuihubiri Habari Njema ya Mungu ili watu wa mataifa mengine wapate kuwa tambiko inayokubaliwa na Mungu, tambiko iliyotakaswa na Roho Mtakatifu. Kwa hiyo, nikiwa nimeungana na Kristo Yesu, naweza kujivunia huduma yangu kwa ajili ya Mungu. Sithubutu kusema kitu kingine chochote isipokuwa tu kile ambacho Kristo Yesu amekifanya kwa kunitumia mimi ili watu wa mataifa wapate kutii. Amefanya hivyo kwa maneno na vitendo, kwa nguvu ya miujiza na maajabu, na kwa nguvu ya Roho wa Mungu. Basi, kwa kusafiri kila mahali, tangu kule Yerusalemu mpaka Iluriko, nimeihubiri kikamilifu Habari Njema ya Kristo. Nia yangu imekuwa daima kuihubiri Habari Njema popote pale ambapo jina la Kristo halijapata kusikika, nisije nikajenga juu ya msingi wa mtu mwingine. Kama yasemavyo Maandiko Matakatifu: “Watu wote ambao hawakuambiwa habari zake wataona; nao wale ambao hawajapata kusikia, wataelewa.”

Baba wa Mbinguni tazama wenye shida/tabu,wagonjwa,wenye njaa,
wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali,waliokatika vifungo vya
yule mwovu,walio magerezani pasipo na hatia,walio kataliwa,
walio kata tamaa,wenye hofu na mashaka,walioumizwa rohoni,
waliokwama kibiashara,waliokwama kielimu...
Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu
kila mmoja na mahitaji yake
Jehovah tunaomba ukawaponye na kuwaokoa,Mungu wetu ukawaweke huru na haki ikatendeke ,Baba wa Mbinguni ukabariki mashamba,biashara na kazi  zao
Yahweh tunaomba ukawasamehe pale walipokwenda kinyume nawe
Jehovah tunaomba ukawape neema ya kujiombea na kufuata njiza zako
nazo zikawaweke huru
Neema na nuru yako ikaangaze katika maisha yao
Ee Mungu wetu tunaomba ukasikie na ukapokee sala/maombi yetu
Mungu wetu ukawatendee sawasawa na mapenzi yako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina..!!!

Asanteni sana wapendwa katika Kristo Yesu kwakuwa nami/
kunisoma Mungu aendelee kuwabariki na kuwatendea kama inavyompendeza yeye,Amani ya Bwana wetu Yesu Kristo na Upendo
wa Mungu Baba vikawe nanyi daima....
Nawapenda. 
  

Yehu atawazwa kuwa mfalme wa Israeli

1Wakati huohuo nabii Elisha alimwita mmoja wa wanafunzi wa manabii, akamwambia, “Jitayarishe kwenda Ramothi katika Gileadi. Chukua chupa hii ya mafuta 2na utakapofika huko, mtafute Yehu mwana wa Yehoshafati na mjukuu wa Nimshi. Mchukue kando chumbani mbali na wenzake, 3kisha chukua chupa hii ya mafuta, ummiminie kichwani na kumwambia, ‘Mwenyezi-Mungu asema hivi: Nimekupaka mafuta kuwa mfalme wa Israeli.’ Kisha fungua mlango na kuondoka upesi utakavyoweza.”
4Basi, Nabii huyo kijana akaenda Ramothi Gileadi. 5Alipofika aliwakuta makamanda wa jeshi mkutanoni. Akasema “Nina ujumbe wako, kamanda.”
Yehu akamwuliza, “Ni nani kati yetu unayemwambia?” Akamjibu, “Wewe, kamanda.” 6Ndipo wote wawili wakaingia chumba cha ndani na huko nabii akamtia Yehu mafuta kichwani na kumwambia, “Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, asema, ‘Nakupaka mafuta uwe mfalme juu ya watu wangu Israeli. 7Nawe utaipiga jamaa ya bwana wako Ahabu ili nimlipize kisasi Yezebeli damu ya watumishi wangu manabii na ya watumishi wangu wote. 8Utafanya hivyo kwa sababu jamaa yote ya Ahabu itaangamia; pia nitamkatilia mbali kila mwanamume wa jamaa ya Ahabu awe mtumwa au mtu huru. 9Jamaa yake itakuwa kama jamaa ya Yeroboamu mwana wa Nebati na ya Baasha mwana wa Ahiya. 10Yezebeli hatazikwa na mtu, maiti yake italiwa na mbwa katika nchi ya Yezreeli.’” Baada ya kusema hayo, nabii akaondoka chumbani na kukimbia.
11Yehu aliporudi kwa wenzake, mmoja wao alimwuliza, “Kuna shida yoyote? Mwendawazimu huyu alitaka nini kwako?” Yehu akawajibu, “Mnajua alichotaka.” 12Nao wakamwambia, “Hiyo si kweli! Tuambie alilosema!” Akawaambia, “Aliniambia kwamba Mwenyezi-Mungu amesema, ‘Nimekutawaza kuwa mfalme wa Israeli.’”
13Mara moja makamanda wenzake wakavua mavazi yao, wakayarundika pamoja kwenye ngazi ili asimame juu yake, wakapiga tarumbeta na kupaza sauti, “Yehu ni mfalme!”

Mfalme Yoramu wa Israeli auawa

14Yehu mwana wa Yehoshafati, ambaye pia alikuwa mjukuu wa Nimshi, alikula njama dhidi ya Yoramu. Yoramu na watu wote wa Israeli walikuwa Ramoth-gileadi kulinda zamu dhidi ya mfalme Hazaeli wa Aramu. 15Lakini mfalme Yoramu alikuwa amerudi Yezreeli ili apone majeraha aliyopata wakati wa kupigana vitani na mfalme Hazaeli wa Aramu. Yehu aliwaambia maofisa wenzake; “Ikiwa mtakubaliana nami, mtu yeyote asitoke Ramothi kwenda Yezreeli kupeleka habari hizi.” 16Ndipo akapanda gari lake na kuelekea Yezreeli. Yoramu alikuwa bado hajapona, na Ahazia mfalme wa Yuda alikuwa amemtembelea.
17Mlinzi aliyekuwa kwa zamu juu ya mnara wa Yezreeli akasema, “Naona watu wakija na gari!” Yoramu akajibu, “Chagua mpandafarasi mmoja, umtume ili akutane nao, awaulize ‘Kuna amani?’” 18Basi, mjumbe huyo alipokwenda alikutana na Yehu na kumwambia, “Mfalme anauliza: Kuna amani?” Yehu akajibu, “Kwa nini unauliza kuhusu amani? Wewe geuka ufuatane nami!” Mlinzi juu ya mnara akasema, “Mjumbe amewafikia, lakini harudi.” 19Ndipo mjumbe wa pili akatumwa, ambaye pia alimwuliza Yehu swali hilohilo. Yehu akamwambia vivyo hivyo, “Kwa nini unauliza kuhusu amani? Wewe geuka ufuatane nami!” 20Kwa mara nyingine tena mlinzi akasema “Mjumbe amewafikia lakini harudi.” Halafu akaongeza, “Uendeshaji wa gari ni kama wa Yehu mwana wa Nimshi; kwa sababu yeye huendesha kwa kasi.”
21Basi, Yoramu mfalme wa Israeli akaamuru akisema, “Tayarisha gari.” Nao walitayarisha gari lake. Kisha Yoramu mfalme wa Israeli na Ahazia mfalme wa Yuda waliondoka kila mmoja akipanda gari lake, wakaenda kukutana na Yehu. Walimkuta katika uwanja wa Nabothi Myezreeli. 22Ikawa Yoramu, alipomwona Yehu, alimwuliza, “Je, kuna amani, Yehu?” Yehu akamjibu, “Amani gani, wakati makahaba na wachawi wa Yezebeli ni wengi?” 23Yoramu aligeuza gari lake na kuondoka, huku akimwambia Ahazia, “Huu ni uhaini Ahazia!” 24Yehu akatwaa upinde wake na kutupa mshale ambao ulipenya mabega ya Yoramu na kuchoma moyo wake, naye akafa papo hapo garini mwake. 25Yehu akamwambia msaidizi wake Bidkari, “Chukua hiyo maiti yake uitupe katika shamba hilo la Nabothi Myezreeli. Kwa maana, kumbuka wewe na mimi tulipokuwa tumepanda farasi wetu nyuma ya baba yake Ahabu, jinsi Mwenyezi-Mungu alivyonena maneno haya dhidi yake. 26Mwenyezi-Mungu alisema, ‘Kwa ile damu ya Nabothi na kwa damu ya wanawe niliyoona jana naapa kwamba nitakulipiza kisasi katika shamba hilo.’ Kwa hiyo, chukua maiti ya Yoramu uitupe katika shamba la Nabothi kama alivyosema Mwenyezi-Mungu.”

Mfalme Ahazia wa Yuda auawa

27Ahazia mfalme wa Yuda alipoona yaliyotukia alikimbia akielekea Nyumba ya Bustani, huku akifuatwa na Yehu. Yehu akawaamuru watu wake, “Muueni naye pia!” Nao wakampiga mshale akiwa garini kwenye njia ya kupanda Guri karibu na mji wa Ibleamu. Halafu alikimbilia Megido na kufia huko. 28Maofisa wake wakaichukua maiti yake ndani ya gari lake na kuipeleka Yerusalemu; na huko akazikwa katika makaburi ya kifalme katika mji wa Daudi.
29Ahazia alianza kutawala juu ya Yuda katika mwaka wa kumi na moja wa enzi ya Yoramu mwana wa Ahabu.

Malkia Yezebeli auawa

30Yehu alipofika Yezreeli, Yezebeli alikuwa amekwisha pata habari za mambo yaliyotokea. Alijipaka rangi machoni na kupanga nywele zake, ndipo akaenda dirishani na kuangalia chini. 31Yehu alipokuwa akiingia langoni Yezebeli alisema, “Unakuja kwa amani, ewe Zimri! Wewe unayewaua mabwana zako?” 32Yehu akaangalia juu na kusema “Ni nani aliye upande wangu?” Maofisa wawili au watatu wakatokeza vichwa vyao kumwangalia kutoka dirishani, 33naye Yehu akawaambia, “Mtupe chini!” Wakamtupa chini na damu yake ikatapakaa juu ya ukuta na kwenye farasi. Yehu akapitisha farasi na gari lake juu ya maiti yake 34na kuingia katika jumba la kifalme, na huko akala na kunywa. Halafu akaamuru: “Mzikeni mwanamke huyo aliyelaaniwa; kwa kuwa ni binti mfalme.” 35Ndipo walipokwenda kumzika; lakini hawakuona chochote isipokuwa fuvu la kichwa, mifupa ya mikono na miguu. 36Kisha walirudi na kumpasha Yehu habari hizi, naye akasema, “Hivi ndivyo Mwenyezi-Mungu alivyotabiri kupitia kwa mtumishi wake Elia Mtishbi akisema, ‘Mbwa wataula mwili wa Yezebeli katika nchi ya Yezreeli. 37Maiti yake Yezebeli itakuwa kama mavi shambani katika nchi ya Yezreeli, hivyo kwamba hakuna atakayeweza kumtambua.’”




2Wafalme9;1-37


Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

Monday 16 April 2018

Kikombe Cha Asubuhi ; 2 Wafalme 8......




Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Haleluyah Mungu wetu yu mwema sana..
Ni siku/wiki nyingine tena Mungu wetu ametuchagua
na kutupa kibali cha kuendelea kuina leo hii...

Tumshukuru Mungu wetu katika yote....

Asante Mungu wetu kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa uwepo,pumzi/uzima na kuwa tayari kwa majukumu yetu
Utukuzwe ee Mungu wetu,Unastahili sifa Baba wa Mbinguni,
Unastahili kuabudiwa Yahweh,Unastahili kuhimidiwa Jehovah..
Matendo yako ni makuu mno,Matendo yako niya ajabu,Matendo yako yanatisha...
Neema yako yatutosha ee Mungun wetu...!!


Usihangaike kwa sababu ya waovu; usiwaonee wivu watendao mabaya. Maana hao watatoweka mara kama nyasi; watanyauka kama mimea mibichi. Mtumainie Mwenyezi-Mungu na kutenda mema, upate kuishi katika nchi na kuwa salama. Uitafute furaha yako kwa Mwenyezi-Mungu, naye atakujalia unayotamani moyoni. Mkabidhi Mwenyezi-Mungu maisha yako; mtumainie yeye naye atafanya kitu. Ataufanya wema wako ungae kama mwanga, na uadilifu wako kama jua la adhuhuri. Tulia mbele ya Mwenyezi-Mungu, mngojee kwa saburi; usihangaike juu ya wale wanaofanikiwa, watu wanaofaulu katika mipango yao mibaya.


Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha
na kujiachilia mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizozifanya
Kwakuwaza,Kwakunena,Kwakutenda,kwakujua/Kutojua
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe
wale wote waliotukosea
Jehovah usitutie katika majaribu Baba wa Mbinguni tunaomba utuokoe
na yule mwovu na kazi zake zote
Yahweh tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu Baba wa mbinguni
utufunike kwa Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti
yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona...


Epuka hasira wala usiwe na ghadhabu; usihangaike maana hiyo huzidisha ubaya. Watu watendao mabaya wataangamizwa, bali wanaomtumaini Mwenyezi-Mungu wataimiliki nchi. Bado kitambo kidogo, naye mwovu atatoweka; utamtafuta pale alipokuwa, wala hutamwona. Lakini wapole wataimiliki nchi, hao watafurahia wingi wa fanaka. Mwovu hula njama dhidi ya mwadilifu, na kumsagia meno kwa chuki. Lakini Mwenyezi-Mungu humcheka mwovu, kwani ajua mwisho wake u karibu. Waovu huchomoa panga na kuvuta pinde zao, wapate kuwaua maskini na fukara; wawachinje watu waishio kwa unyofu. Lakini panga zao zitawapenya wao wenyewe, na pinde zao zitavunjwavunjwa. Afadhali mali kidogo ya mtu mwadilifu kuliko utajiri wa watu waovu wengi. Maana nguvu za waovu zitavunjwa, lakini Mwenyezi-Mungu huwategemeza waadilifu. Mwenyezi-Mungu hutunza maisha ya watu waaminifu, na urithi wao utadumu milele. Hawataaibika zikifika nyakati mbaya; siku za njaa watakuwa na chakula tele. Lakini waovu wataangamia, maadui za Mwenyezi-Mungu watanyauka kama maua nyikani; naam, watatoweka kama moshi.


Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa katika
utendaji Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Yahweh tunomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba ukatupe neema ya kuweza kuwabariki
wenye kuhitaji,Jehovah tusipungukiwe katika mahitaji yetu Mungu 
wetu ukatupe kama inavyokupendeza wewe...


Baba wa Mbinguni tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,watoto,wazazi wetu
Familia/ndugu na wote wanaotuzunguka
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyovimiliki
Mungu wetu tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Yahweh tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Jehovah ukavifunike kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo...
Baba wa Mbinguni ukatamalaki na kutuatamia Mungu wetu tukawe salama
rohoni Yahweh ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia sauti yako
na kuitii,Mungu wetu tunaomba ukatupe neema ya kutamnbua mema na mabaya,Yahweh ukatupe neema ya kufuata njia zako Mungu wetu
tukasimamie Neno lako amri na sheria zako siku zotye za maisha yetu..
Jehovah ukaonekane katika maisha yetu Mungu wetu popote
tupitapo na ikajulikane kwamba upo Baba wa Mbinguni...
Ukatufanye chombo chema Jehovah nasi tukatumike kama inavyokupendeza wewe...
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi....


Mtu mwovu hukopa bila kurudisha; lakini mwadilifu hutoa kwa ukarimu. Waliobarikiwa na Mwenyezi-Mungu wataimiliki nchi, lakini waliolaaniwa naye watafutiliwa mbali. Mwenyezi-Mungu huziongoza nyayo za mtu, humlinda yule ampendezaye. Ajapoanguka, haanguki akabaki chini, kwa sababu Mwenyezi-Mungu humtegemeza. Nilikuwa kijana na sasa ni mzee; kamwe sijaona mwadilifu ameachwa na Mungu, au watoto wake wakiombaomba chakula. Daima huwapa wengine kwa furaha na kukopesha, na watoto wake ni baraka. Achana na uovu, utende mema, nawe utaishi nchini daima; maana Mwenyezi-Mungu hupenda uadilifu, wala hawaachi waaminifu wake. Huwalinda hao milele; lakini wazawa wa waovu wataangamizwa. Waadilifu wataimiliki nchi, na wataishi humo milele. Mtu mwadilifu husema maneno ya hekima, kwa ulimi wake hunena yaliyo ya haki. Huizingatia moyoni mwake sheria ya Mungu wake; naye hatetereki katika mwenendo wake. Mtu mwovu humvizia mtu mwema na kujaribu kumuua; lakini Mwenyezi-Mungu hatamtia mtu mwema makuchani mwake, wala kumwacha apatilizwe akishtakiwa. Mtumainie Mwenyezi-Mungu na kushika njia yake, naye atakukuza uimiliki nchi, na kuwaona waovu wakiangamizwa. Nilimwona mwovu mdhalimu sana, alijiweka juu ya wote kama mierezi ya Lebanoni! Baadaye nikapita hapo, naye hakuwapo tena; nikamtafuta, lakini hakuonekana tena. Mwangalie mtu mwema, mtu mwadilifu; mtu anayependa amani hujaliwa wazawa. Lakini wakosefu wote wataangamizwa; na wazawa wao watafutiliwa mbali. Mwenyezi-Mungu huwaokoa waadilifu, na kuwalinda wakati wa taabu. Mwenyezi-Mungu huwasaidia na kuwaokoa; huwatoa makuchani mwa waovu na kuwaokoa, maana wanakimbilia usalama kwake.

Yahweh tazama watoto wako wanaokutafuta kwa bidii na imani
Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu
Jehovah tunaomba ukawaponye na kuwatendea kila mmoja na 
mahitaji yake Baba wa Mbinguni ukaonekane katika maisha yao
Jehovah ukawasamehe pale walipokwenda kinyume nawe
Mungu wetu tunaomba ukawape neema ya kujiombea,kufuata
njia zako wakasimamie Neno lako nalo likawaweke huru
Yahweh nuru yako ikaangaze katika maisha yao Baba wa Mbinguni
ukasikie kulia kwao Mungu wetu tunaomba ukawafute machozi yao
Jehovah tunaomba ukasikie na ukapokee sala/maombi yetu
Mungu wetu tunaomba ukawatendee sawasawa na mapenzi yako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina....!!!

Asanteni sana wapendwa katika Kristo Yesu kwakuwa nami/kunisoma
Mungu Baba aendelee kuwabariki na kuwatendea sawasawa na mapenzi
yake,Amani ya Bwana wetu Yesu Kristo na upendo wa Mungu Baba ukawe nanyi Daima....
Nawapenda.

Mwanamke wa Shunemu arudi

1Elisha alikuwa amemwambia mwanamke aliyeishi Shunemu ambaye alikuwa amemfufua mwanawe, “Ondoka, na jamaa yako, uhamie ugenini kwa sababu Mwenyezi-Mungu ameleta njaa itakayokuwamo nchini kwa muda wa miaka saba.” Akamshauri ahame aende mahali pengine. 2Huyo mwanamke akaondoka akafanya kama mtu wa Mungu alivyosema akaenda pamoja na jamaa yake na kukaa kama mgeni katika nchi ya Filistia kwa miaka saba.
3Miaka saba ilipokwisha, alitoka Filistia akarudi Israeli na kwenda kwa mfalme kuomba arudishiwe nyumba yake na shamba lake. 4Akamkuta mfalme anaongea na Gehazi, akisema, “Tafadhali nieleze miujiza ambayo hutendwa na Elisha.” 5Gehazi alipokuwa anamweleza mfalme jinsi Elisha alivyofufua mtu aliyekufa, mwanamke huyo alitoa ombi lake kwa mfalme. Gehazi akasema, “Ee mfalme; huyu ndiye mwanamke ambaye Elisha alimfufua mwanawe!” 6Mfalme alipomwuliza mwanamke huyo, yeye alimweleza. Mfalme akamwita ofisa wake na kumwamuru amrudishie mwanamke huyo mali yake yote, pamoja na mapato yote ya mashamba yake katika muda huo wote wa miaka saba.

Elisha na mfalme Ben-hadadi wa Aramu

7Baadaye Elisha alikwenda Damasko. Wakati huo mfalme Ben-hadadi alikuwa mgonjwa na alipoambiwa kwamba Elisha alikuwa Damasko, 8alimwambia ofisa wake Hazaeli, “Mpelekee mtu wa Mungu zawadi umwambie atafute shauri kwa Mwenyezi-Mungu kama nitapona au la.” 9Hazaeli akapakia zawadi za kila aina ya mazao ya Damasko kiasi cha mizigo ya ngamia arubaini na kumpelekea Elisha. Alipofika kwa Elisha alimwambia, “Mtumishi wako, Ben-hadadi, mfalme wa Aramu amenituma kwako; yeye anauliza, ‘Nitapona ugonjwa huu?’” 10Basi Elisha akamjibu, “Atapona; lakini Mwenyezi-Mungu amenionesha kwamba atakufa.” 11Ndipo Elisha akamkazia macho akiwa na hofu hata Hazaeli akashikwa na wasiwasi. Ghafla, Elisha mtu wa Mungu, akaanza kulia. 12Hazaeli akamwuliza, “Bwana wangu, mbona unalia?” Elisha akamjibu, “Kwa sababu ninajua maovu ambayo utawatendea watu wa Israeli. Utateketeza ngome zao kwa moto, na kuwaua vijana wao, utawapondaponda watoto wao na kuwararua wanawake waja wazito.” 13Hazaeli akauliza, “Lakini mimi mtumishi wako ni kitu kweli? Mimi niliye mbwa tu nitawezaje kutenda mambo hayo makubwa?” Elisha akamjibu, “Mwenyezi-Mungu amenionesha kwamba utakuwa mfalme wa Aramu.” 14Ndipo Hazaeli alipotoka kwa Elisha, akarudi kwa bwana wake. Mfalme Ben-hadadi akamwuliza, “Elisha alikuambia nini?” Hazaeli akamjibu, “Aliniambia ya kwamba hakika utapona.” 15Lakini kesho yake Hazaeli akachukua blanketi akalilowesha majini, kisha akamfunika nalo usoni mpaka akafa. Hazaeli akatawala Aramu mahali pake.

Mfalme Yehoramu wa Yuda

(2Nya 21:1-20)

16Mnamo mwaka wa tano wa utawala wa Yoramu mwana wa Ahabu, mfalme wa Israeli,8:16 Israeli: Makala ya Kiebrania: Israeli Yehoshafati alipokuwa mfalme wa Yuda. Yehoramu mwana wa Yehoshafati, mfalme wa Yuda alianza kutawala. 17Alianza kutawala akiwa na umri wa miaka thelathini na miwili. Alitawala huko Yerusalemu miaka minane. 18Alizifuata njia mbaya za wafalme wengine wa Israeli, kama jamaa ya Ahabu ilivyofanya, kwa sababu mkewe alikuwa binti Ahabu. Akatenda maovu mbele ya Mwenyezi-Mungu, 19lakini Mwenyezi-Mungu hakutaka kuangamiza Yuda, kwa sababu ya Daudi mtumishi wake, kwani aliahidi kwamba wazawa wake wataendelea kutawala milele. 20Wakati wa enzi ya Yehoramu, watu wa Edomu waliasi utawala wa Yuda, wakamtawaza mfalme wao.
21Kwa hiyo Yoramu aliondoka na magari yake yote kwenda Zairi. Wakati wa usiku alitoka na makamanda wake wa magari akawashambulia Waedomu waliokuwa wamemzunguka; lakini jeshi lake lilikimbia nyumbani. 22Hivyo watu wa Edomu wakauasi utawala wa Yuda mpaka sasa. Wakati huohuo, wakazi wa Libna nao wakaasi.
23Matendo mengine yote ya mfalme Yehoramu yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Nyakati za Wafalme wa Yuda. 24Yehoramu akafa na kuzikwa katika makaburi ya kifalme katika mji wa Daudi, naye Ahazi, mwanawe Yehoramu, akatawala mahali pake.

Mfalme Ahazia wa Yuda

(2Nya 22:1-6)

25Katika mwaka wa kumi na mbili wa utawala wa Yoramu mwana wa Ahabu mfalme wa Israeli, Ahazia mwana wa Yehoramu mfalme wa Yuda, alianza kutawala. 26Ahazia alianza kutawala akiwa na umri wa miaka ishirini na miwili, akatawala kutoka Yerusalemu kwa muda wa mwaka mmoja. Mama yake aliitwa Athalia, mjukuu wa mfalme Omri mfalme wa Israeli. 27Kwa sababu Ahazia alikuwa mkwe wa jamaa ya Ahabu, naye alifuata mwenendo wa jamaa hiyo ya Ahabu, alitenda maovu mbele ya Mwenyezi-Mungu, kama vile jamaa ya Ahabu walivyofanya.
28Mfalme Ahazia akaenda na Yoramu mwana wa Ahabu kupigana vita dhidi ya Hazaeli mfalme wa Aramu huko Ramoth-gileadi mahali Waaramu walipomjeruhi Yoramu. 29Kisha mfalme Yoramu akarudi mjini Yezreeli ili apate kutibiwa majeraha aliyoyapata huko Rama, alipopigana na Hazaeli mfalme wa Aramu. Naye Ahazia mwana wa Yehoramu mfalme wa Yuda alimwendea Yoramu mwana wa Ahabu huko Yezreeli, kwa sababu alikuwa mgonjwa.



2Wafalme8;1-29


Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

Saturday 14 April 2018

Wanawake na Urembo,Kucha..

Habari za Jumamosi wapendwa//waungwana..?
weekend yako inakwendaje ?
Jumamosi hii umeamua kufanya nini tofauti?
Na kila jumamosi utaratibu wako ukoje?
Ni kufanya usafi mkubwa wa nyumba?
Kufanya usafi wa nywele,kucha,nyusi au?
najua usafi wa mwili na hivyo vyote ni vya kawaida lakini kuna
vile vya kuongezea na si lazima....

Mimi leo nimekuletea usafi na urembo wa kucha
Jee wewe ni mpenzi wa kuweka kucha bandia?
Jee kama ndiyo huwa unaziacha/kubadili baada ya muda gani?
usipo fanya hivyo unajisikiaje ?
kazi yako inaruhusu uwe na kucha ndefu au kucha za bandia?
jee kama ndiyo vipi ukipata kazi isiyoruhusu urembo huu?
Asanteni karibuni tena.....

"Swahili Na Waswahili"Pamoja Sana.

Friday 13 April 2018

Kikombe Cha Asubuhi ; 2 Wafalme 7......



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Ni siku nyingine tena Mungu wetu ametuchagua na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Si kwa nguvu zetu wala si kwa uwezo wetu si kwamba sisi
tumetenda mema sana wala si kwa akili zetu wala utashi wetu
sisi kuwa hivi tulivyo leo hii
Ni kwa rehema/neema zake Mungu ni kwa mapenzi yake Mungu wetu
sisi kuwa hivi tulivyo...
Asante Mungu wetu kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati  wote
Asante kwa uwepo wako,pumzi,uzima,afya na kuwa tayari kwa 
majukumu yetu...
Utukuzwe ee Mungu wetu,Neema yako yatutosha Baba wa Mbinguni
wewe ni mwanzo na wewe ni mwisho ni Alfa na Omega...!
Sifa na Utukufu tunakurudishia wewe Mungu wetu....!!


Basi, ueni chochote kilicho ndani yenu ambacho ni cha kidunia: Uasherati, uchafu, shauku, tamaa mbaya na uchu (ambao ni sawa na kuabudu sanamu). Kwa sababu ya mambo hayo hasira ya Mungu huwajia wote wanaomwasi. Wakati mmoja nyinyi pia mliishi kufuatana na mambo hayo, mlipotawaliwa nayo. Lakini sasa mnapaswa kuachana na mambo haya yote: Hasira, tamaa na uovu; kufuru au maneno yasiyofaa yasitoke kamwe vinywani mwenu. Msiambiane uongo, kwani nyinyi mmekwisha vua ule utu wa kale pamoja na matendo yake yote, mkavaa utu mpya. Huu unaendelea kurekebishwa na Mungu, Muumba wake, kadiri ya mfano wake, ili mpate kumjua Mungu kwa ukamilifu. Katika hali hii, hakuna tena tofauti kati ya Mgiriki na Myahudi, aliyetahiriwa na asiyetahiriwa, msomi na asiye msomi, mtumwa na mtu aliye huru. Kristo ni kila kitu, na yumo katika yote.


Tazama jana imepita Mungu wetu Leo ni siku mpya Baba wa Mbinguni
na Kesho ni nyingine Jehovah...
Yahweh tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha na kujiachilia
mikononi mwako..
Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizozifanya
Kwakuwaza,kwakutenda,kwakunena,kwakujua/kutojua
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe
wale wote waliotukosea
Jehovah usitutie katika majaribu Yahweh tunaomba utuokoe na yule
mwovu na kazi zake zote
Mungu wetu tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu
Baba wa Mbinguni tunaomba utufunike kwa Damu ya Bwana na Mwokozi
wetu Yesu Kristo wa Nazareti yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona


Nyinyi ni watu wake Mungu; yeye aliwapenda na kuwateua. Kwa hiyo, basi, vaeni moyo wa huruma, wema, unyenyekevu, upole na uvumilivu. Vumilianeni na kusameheana iwapo mmoja wenu analo jambo lolote dhidi ya mwenzake. Mnapaswa kusameheana kama Bwana alivyowasamehe nyinyi. Zaidi ya hayo yote, zingatieni upendo, kwani upendo huunganisha kila kitu katika umoja ulio kamili. Nayo amani ya Kristo itawale mioyoni mwenu; maana kwa ajili hiyo nyinyi mmeitwa katika mwili huo mmoja. Tena muwe na shukrani! Ujumbe wa Kristo na ukae ndani yenu pamoja na utajiri wake wote. Fundishaneni na kushauriana kwa hekima yote. Imbeni Zaburi, nyimbo na tenzi za kiroho; mwimbieni Mungu mioyoni mwenu kwa shukrani. Na, kila mfanyacho kwa neno au tendo, fanyeni vyote kwa jina la Bwana Yesu na kumshukuru Mungu Baba kwa njia yake.

Jehovah tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Mungu wetu tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa katika utendaji
Yahweh tunaomba nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Baba wa Mbinguni tunomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba ukatupe neema ya kuweza kuwabariki 
wenye kuhitaji
Jehovah tunaomba tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe kama inavyokupendeza wewe....

Mungu wetu tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Baba wa Mbinguni tunomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka
Jehovah tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo Mungu wetu
tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Yahweh tunaomba ulinzi wako kwetu na vyote tunavyovimiliki
Jehovah ukatamalaki na kutuatamia Mungu wetu tukawe salama
rohoni,Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe macho ya kuona  Yahwweh
ukatupe masikio ya kusikia sauti yako na kuitii
Mungu wetu tunaomba ukatupe neema ya kufuata njia zako Baba wa Mbinguni tukasimamie Neno lako amri na sheria zako siku zote za 
maisha yetu,Jehovah ukaonekane katika maisha yetu popote
tupitapo na ikajulikane kwamba upo Baba wa Mbinguni
Yahweh ukatupe neema ya kutambua mema na mabaya
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika miasha yetu
Hekima,busara, utu wema ukawe nasi na upendo ukadumu kati yetu
Yahweh ukatufanye barua njema nasi tukasomeke kama inavyokupendeza wewe....
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi....


Enyi wake, watiini waume zenu, kwani ndivyo apendavyo Bwana. Nanyi waume, wapendeni wake zenu, na msiwe wakali kwao. Enyi watoto, watiini wazazi wenu daima maana hiyo humpendeza Bwana. Nanyi wazazi, msiwachukize watoto wenu, la sivyo watakata tamaa. Enyi watumwa, watiini wakuu wenu wa kidunia katika mambo yote, na si tu wakati wanapowatazama kwa kuwa mnataka kujipendekeza kwao; ila fanyeni hivyo kwa moyo wote, kwa sababu ya kumcha Bwana. Kila mfanyacho, fanyeni kwa moyo wote, kwa sababu ya Bwana na si kwa ajili ya mtu. Kumbukeni kwamba atawapeni tuzo lile alilowawekea watu wake. Mtumikieni Kristo Bwana! Atendaye mabaya atalipwa kufuatana na ubaya wake; Mungu hana ubaguzi.

Yahweh tunawaweka mikononi mwako wote 
wanaokutafuta/kukuomba kwa bidii na imani,Mungu wetu tuomba
ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu kila mmoja na hitaji lake
Jehovah tunaomba ukawape neema ya kujiombea,kufuata njia zako,
kusimamia Neno lako nalo likawaweke huru
Mungu wetu tunaomba ukawasamehe pale walipokwenda kinyume nawe
Baba wa Mbinguni tunaomba ukasikie kulia kwao Mungu wetu tunaomba
ukawafute machozi yao
Jehovah ukaonekane katika maisha yao Yahweh tunaomba ukasikie,
ukapokee sala/maombi yetu Mungu wetu  ukawatendee sawasawa na
mapenzi yako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina...!!

Wapendwa katika Kristo Yesu asanteni sana kwakuwanami/kunisoma
Mungu Baba aendelee kuwabariki na kuwatendea sawasawa na
mapenzi yake pendo lenu likadumu amani ya Kristo Yesu ikawe nanyi daima ....
Nawapenda.

1Elisha akamjibu, “Sikiliza neno la Mwenyezi-Mungu: Kesho wakati kama huu, humu Samaria kilo tatu za unga bora wa ngano zitagharimu fedha shekeli moja ya fedha, na kilo sita za shayiri kadhalika zitagharimu fedha shekeli moja.” 2Kapteni mwaminifu wa mfalme akamwambia Elisha, “Kama Mwenyezi-Mungu mwenyewe angefanya madirisha mbinguni, je, jambo hilo litawezekana!” Elisha akamjibu, “Utaona kwa macho yako mwenyewe, lakini wewe hutakula.”

Jeshi la Aramu laondoka

3Kulikuwa na watu wanne wenye ugonjwa wa ukoma waliokuwa nje ya milango ya mji wa Samaria ambao walisemezana, wao kwa wao, “Mbona tunakaa hapa tukifa njaa? 4Hakuna maana ya kuingia mjini kwa sababu huko tutakufa. Kwa hiyo hebu twende kwenye kambi ya Waaramu; inawezekana wakatuua, au wasituue.” 5Hivyo, giza lilipoanza kuingia, wakaenda kwenye kambi ya Waaramu, lakini walipofika huko, hapakuwa na mtu. 6Maana Mwenyezi-Mungu alilifanya jeshi la Waaramu lisikie sauti kama ya jeshi kubwa lililokuwa na magari na farasi. Waaramu wakadhani kuwa mfalme wa Israeli amekodisha majeshi ya Wahiti na Wamisri kuja kuwashambulia. 7Basi, katika usiku huo, Waaramu walikimbia wote ili kuyaokoa maisha yao wakiacha mahema yao, farasi na punda wao, na hata kambi yao jinsi ilivyokuwa.
8Wakoma wale wanne walipofika pembeni mwa kambi, waliingia ndani ya hema moja, wakala na kunywa vile walivyopata humo, wakachukua fedha, dhahabu na nguo, wakaenda kuzificha. Wakaingia katika hema nyingine na kufanya vivyo hivyo. 9Lakini wakaambiana, “Tunalofanya si sawa! Hii ni habari njema tuliyo nayo leo, na ikiwa tutangoja mpaka asubuhi, bila shaka tutaadhibiwa. Twende mara moja tukawaambie watu wa nyumba ya mfalme!” 10Hivyo, wakaondoka katika kambi ya Waaramu na kuwaita mabawabu wa mji na kuwaambia: “Tulikwenda katika kambi ya Waaramu na hatukuweza kumwona wala kumsikia mtu yeyote. Farasi na punda wangali wamefungwa, na mahema yako kama walivyoyaacha.”
11Walinda malango wakaeneza habari hizi mpaka zikafika nyumbani kwa mfalme. 12Ingawa kulikuwa bado giza, mfalme aliamka na kuwaambia maofisa wake, “Mimi najua mpango wa Waaramu! Wanajua tuna njaa mjini, sasa wameacha kambi yao kwenda kujificha ili tutakapokwenda kutafuta chakula, watukamate sote hai na kuuteka mji.”
13Mmoja kati ya maofisa wake akasema, “Watu wengi tayari wameangamia kama vile wale ambao wamekwisha fariki. Tafadhali utume watu wachache na farasi watano wa wale waliobaki ili waende kuona kumetokea nini.” 14Wakachagua watu na kuwapa magari mawili. Mfalme akawatuma kuwafuata Waaramu, akisema, “Nendeni mkaone.” 15Watu hao wakaenda mpaka Yordani na njiani waliona nguo na vifaa vingine Waaramu walivyoacha walipokuwa wanakimbia. Wakarudi na kumpasha mfalme habari. 16Watu wa Samaria wakatoka na kuteka nyara kambi ya Waaramu. Kama vile Mwenyezi-Mungu alivyosema: Kilo tano za unga safi wa ngano au kilo kumi za shayiri ziliuzwa kwa kipande kimoja cha fedha.
17Naye mfalme alikuwa amemweka ofisa mlinzi wake kulinda lango la mji. Ofisa huyo alikanyagwa papo hapo langoni na kuuawa na watu, kama vile Elisha mtu wa Mungu alivyotabiri wakati mfalme alipokwenda kumwona. 18Elisha alikuwa amemwambia mfalme kwamba wakati kama huo siku iliyofuata, kilo tano za unga mzuri wa ngano au kilo kumi za shayiri zingeuzwa kwa kipande kimoja cha fedha; lakini hapo awali 19kapteni alikuwa amembishia Elisha, akisema, “Kama Mwenyezi-Mungu mwenyewe angefanya madirisha mbinguni, je, jambo hili lingewezekana?” Naye Elisha alikuwa amemjibu, “Utaona yakitendeka, lakini chakula chenyewe hutakila.” 20Na hivyo ndivyo ilivyotokea – kapteni akafa kwa kukanyagwa na watu kwenye lango la mji.



2Wafalme7;1-20


Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.