Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Wednesday 6 December 2017

Kikombe Cha Asubuhi ;Waamuzi 18...




Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Mungu wetu yu mwema sana tumshukuru katika yote..
Asante Baba wa Mbinguni kwa wema na fadhili zako kwetu..
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote..
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwa tayari kwa majukumu yetu..
Asante kwakutuchagua tena na kutupa kibali cha kuiona leo hii..
Utukuzwe ee Mungu wetu,Usifiwe Baba wa Mbinguni,Uhimidiwe Yahweh
Uabudiwe daima Jehovah Jireh..!Unatosha Jehovah Nissi..!Hakuna kama wewe Jehovah Shammah..!Matendo yako ni makuu mno Jehovah Rapha..!
Matendo yako ni ya ajabu Jehovah Raah..!Utukufu una wewe Jehovah
Shalom,Asante Emanuel-Mungu pamoja nasi...!!


Kwake Mwenyezi-Mungu nakimbilia usalama; mnawezaje basi kuniambia: “Ruka kama ndege, mpaka milimani, maana waovu wanavuta pinde; wameweka mishale tayari juu ya uta, wawapige mshale watu wema gizani! Kama misingi ikiharibiwa, mtu mwadilifu atafanya nini?” Mwenyezi-Mungu yumo katika hekalu lake takatifu; kiti cha enzi cha Mwenyezi-Mungu kiko mbinguni. Kwa macho yake huwachungulia wanadamu, na kujua kila kitu wanachofanya. Mwenyezi-Mungu huwapima waadilifu na waovu; huwachukia kabisa watu wakatili. Atawanyeshea waovu makaa ya moto na madini ya kiberiti; upepo wa hari utakuwa ndio adhabu yao. Mwenyezi-Mungu ni mwadilifu na apenda uadilifu; watu wanyofu watakaa pamoja naye.


Tunakuja mbele zako Mungu wetu tukijinyenyekeza,tukijishusha na 
kujiachilia mikononi mwako Baba wa Mbinguni..
Yahweh tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizozifanya kwakuwaza,
kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua..
Mungu wetu nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale
wote waliotukosea..
Baba wa Mbinguni tunaomba utuepushe katika majaribu Yahweh tunaomba utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote..
Jehovah tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu Baba utufunike
kwa Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti
yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona..




Nani ee Mwenyezi-Mungu atakayekaa hemani mwako? Nani atakayeishi juu ya mlima wako mtakatifu? Ni mtu aishiye bila lawama, atendaye daima yaliyo mema, asemaye ukweli kutoka moyoni; ni mtu asiyesengenya watu, asiyemtendea uovu rafiki yake, wala kumfitini jirani yake; ni mtu anayewadharau wafisadi, lakini huwaheshimu wamchao Mwenyezi-Mungu; ni mtu asiyegeuza kiapo chake hata kikimtia hasara; asiyekopesha fedha yake kwa riba, wala kupokea rushwa kumdhulumu asiye na hatia. Mtu atendaye hayo, kamwe hatatikisika.

Yahweh tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu Mungu wetu tunaomba
ukatupe ubunifu,maarifa katika ufanyaji/utendaji Jehovah tukatende
kama inavyokupendeza wewe..
Mungu wetu tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo Yahweh
nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji..
Baba wa Mbinguni tunaomba tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Jehovah ukatupe sawasawa na mapenzi yako..

Mfalme wa Amani tuyaweka maisha yetu mikononi mwako Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,watoto ,wazazi 
wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka..
Yahweh tunaomba amani yako ikatawale Baba wa Mbinguni tunaomba
Ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyovimiliki,Mungu wetu tunaomba
ukatamalaki na kutuatamia Jehovah ukatuguse kwa mkono wako wenye nguvu Yahweh ukatupe uponyaji moyoni,tukanene yaliyoyako,tukapate
kutambua/kujitambua BABA tunaomba ukatupe neema ya kufuata njia
zako,kusimamia Neno lako amri na sheria zako siku zote za maisha yetu
Baba wa Mbinguni ukaonekane katika maisha yetu na popote tupitapo
na ijulikane kama Upo Mungu wetu..
Yahweh ukatufanye chombo chema nasi tukatumike kama inavyokupendeza wewe..
Roho matakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi..


Unilinde ee Mungu; maana kwako nakimbilia usalama. Namwambia Mungu: “Wewe u Bwana wangu; sina jema lolote ila wewe.” Ni bora sana hao watakatifu walioko nchini, kukaa nao ndiyo furaha yangu. Lakini wanaoabudu miungu mingine, watapata mateso mengi. Tambiko ya damu sitaitolea kamwe, na majina ya miungu hiyo sitayataja. Wewe ee Mwenyezi-Mungu ndiwe riziki yangu kuu, majaliwa yangu yamo mikononi mwako. Umenipimia sehemu nzuri sana; naam, urithi wangu ni wa kupendeza. Namsifu Mwenyezi-Mungu kwa kuniongoza, usiku dhamiri yangu yanionya. Namweka Mwenyezi-Mungu mbele yangu daima; yuko pamoja nami, wala sitatikisika. Kwa hiyo nitafurahi kwa moyo wote na kushangilia, nami nitakaa salama salimini. Naam wewe hutaiacha nafsi yangu kuzimu, hutaniacha mimi mwaminifu wako nipate kuoza. Wanionesha njia ya kufikia uhai; kuwako kwako kwanijaza furaha kamili, katika mkono wako wa nguvu mna mema ya milele.

Mungu wetu tazama wenye shida/tabu,wagonjwa,wenye njaa,wanaotaabika na kuelemewa na mizigo,wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali,waliokatika vifungo vya yule mwovu,
waliokata tamaa,waliokataliwa,wenye hofu na mashaka,waliopoteza
matumaini,wajane,yatima,Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu,Yahweh ukawaponye kimwili na kiroho pia,Mungu wetu ukawafungue na kuwaweka huru,Jehovah ukawavushe salama na amani
yako ikawe nao,Baba wa Mbinguni ukawapatie chakula na ukabariki mashamba,kazi zao,Yahweh ukawasamehe wale wote waliokwenda kinyume nawe Mungu wetu ukaonekane katika maisha yao,Baba wa Mbinguni ukawape neema ya kujiombea,kufuata njia zako..
Yahweh Nuru yako ikaangaze katika maisha yao..
Mungu wetu tunaomba ukasikie,ukapokee na ukajibu sala/maombi yetu
Mungu wetu tunaomba ukawatendee sawasawa na mapenzi yako..
Wafiwa ukawe mfariji wao..



Lakini wewe wawaona wenye dhiki na shida; nawe daima uko tayari kuwasaidia. Mnyonge anakutegemea wewe, ee Mungu, wewe umekuwa daima msaada wa yatima. Uzivunje nguvu za mtu mwovu; ukomeshe uovu wake wote, usiwepo tena. Mwenyezi-Mungu ni mfalme milele na milele! Mataifa yasiyomjua yatatoweka nchini mwake. Ee Mwenyezi-Mungu, wapokea dua za mnyonge; wampa moyo na kumtegea sikio. Utawatendea haki yatima na wanaodhulumiwa, binadamu aliye udongo asiweze tena kuleta hofu.
Sifa na Utukufu tunakurudishia Mungu Baba..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina..!

Asanteni sana wapendwa katika Bwana kwakuwa nami
Mungu aendelee kuwabariki,amani ya Kristo Yesu iwe nanyi daima
Baba wa Mbinguni akawatendee kama inavyompendeza yeye..
Nawapenda.

Mika na kabila la Dani

1Siku hizo hakukuwa na mfalme katika Israeli. Basi kabila la Dani lilikuwa linatafuta eneo lake lenyewe la kuishi humo, kwani mpaka wakati huo, halikuwa limegawiwa sehemu yake lenyewe miongoni mwa makabila ya Israeli. 2Hivyo watu wa kabila la Dani walichagua miongoni mwao watu hodari wakawatuma kutoka huko Eshtaoli na Sora wakawaamuru waende kuipeleleza nchi. Basi watu hao wakafika katika nchi ya milima ya Efraimu, nyumbani kwa Mika, wakakaa humo. 3Walipokuwa nyumbani kwa Mika, waliitambua sauti ya yule kijana Mlawi. Wakamgeukia na kumwuliza, “Nani amekuleta huku? Una shughuli gani hapa?” 4Yeye akawajibu, “Mika amefanya nami mpango; ameniajiri nami nimekuwa kuhani wake.” 5Nao wakamwambia, “Tafadhali utuulizie kwa Mwenyezi-Mungu kama tutafanikiwa katika safari yetu.” 6Yule kuhani akawaambia, “Nendeni kwa amani. Mwenyezi-Mungu anaichunga safari yenu.”
7Basi, watu hao watano wakaondoka, wakaenda Laishi. Waliwaona watu walioishi huko, na jinsi walivyokaa kwa usalama kama vile watu wa Sidoni. Walikuwa watu watulivu wasio na wasiwasi na hawakupungukiwa18:7 hawakupungukiwa: Linganisha na 18:10; maana katika Kiebrania si dhahiri. mahitaji yoyote nchini. Walikuwa mbali na watu wa Sidoni, na hawakuwa na shughuli yoyote na watu wengine.
8Basi hao wapelelezi walirudi kwa ndugu zao huko Sora na Eshtaoli, nao wakawauliza, “Mmetuletea taarifa gani?” 9Wao wakasema, “Inukeni twende na kuishambulia nchi hiyo. Tumeiona nchi hiyo, na kweli ni nchi yenye rutuba. Je, mtakaa hapa tu bila kufanya kitu? Msikawie kwenda kuimiliki nchi hiyo. 10Mtakapofika huko mtakuta watu wasio na wasiwasi wowote. Nchi hiyo ni kubwa, haikupungukiwa chochote na Mungu ameitia mikononi mwetu.”
11Basi, watu 600 wa kabila la Dani wakiwa na silaha zao za vita wakaondoka kutoka Sora na Eshtaoli 12wakaenda kupiga kambi yao huko Kiriath-yearimu katika nchi ya Yuda. Ndiyo maana mahali hapo, upande wa magharibi wa Kiriath-yearimu pameitwa Mahane-dani18:12 Mahane-dani: Maana yake ni Kambi ya Dani. mpaka leo. 13Kutoka huko wakaelekea nchi ya milima ya Efraimu, wakafika nyumbani kwa Mika.
14Watu wale watano waliokwenda kuipeleleza nchi ya Laishi wakawaambia ndugu zao, “Je, mnajua kwamba katika nyumba mojawapo ya hizi kuna kizibao, kinyago na sanamu ya kusubu? Basi, fikirini namna ya kufanya.” 15Basi wale wapelelezi wakaelekea kwenye nyumba ya Mika, wakaingia ndani na kumwuliza habari zake yule kijana Mlawi. 16Wakati huo, wale watu 600 wa kabila la Dani wakiwa na silaha zao za vita walisimama mlangoni. 17Wale watu watano waliokwenda kuipeleleza nchi waliingia ndani, wakachukua ile sanamu mungu ya kusubu, kile kizibao na kinyago cha ibada. Wakati huo yule kuhani alikuwa amesimama mlangoni pamoja na wale watu 600 wenye silaha. Basi, alipowaona wale wapelelezi 18wameingia nyumbani mwa Mika wakachukua sanamu ya kuchonga, kifuko cha kauli, kinyago na sanamu ile ya kusubu, akawauliza, “Mnafanya nini?” 19Nao wakamwambia, “Nyamaza, funga mdomo wako, uje pamoja nasi, uwe kuhani wetu na kama baba yetu. Au waonaje? Je, yafaa kwako zaidi kuwa kuhani wa mtu mmoja ama kuwa kuhani wa kabila moja la Israeli?” 20Yule kuhani akafurahi sana akachukua kile kifuko, kile kinyago cha ibada, na ile sanamu ya mungu ya kusubu, akafuatana nao.
21Basi, wakaanza safari yao, huku wametanguliwa na watoto wao na mifugo na mali zao. 22Walipokuwa wamefika mbali na nyumbani kwa Mika, watu waliokuwa jirani na Mika wakaitwa, wakawafuatia watu wa kabila la Dani wakawafikia. 23Kisha wakawapigia kelele, nao watu wa kabila la Dani wakageuka, wakamwuliza Mika, “Una shida gani hata umetufuatia pamoja na kundi hili lote?”
24Mika akasema, “Nyinyi mmechukua miungu yangu niliyojitengenezea, mkamchukua na kuhani wangu, mkaniacha bila chochote. Mnawezaje basi kuniuliza nina shida gani?” 25Watu wa kabila la Dani wakamwambia, “Afadhali uache kelele zako, la sivyo wengine wetu wenye hasira wanaweza wakakuvamia, nawe ukapoteza maisha yako na maisha ya jamaa yako.” 26Mika alipoona kwamba wamemzidi nguvu, akageuka, akarudi nyumbani; nao watu wa kabila la Dani wakaenda zao.
27Hao watu wa kabila la Dani walivichukua vitu vile ambavyo Mika alikuwa amevitengeneza, wakamchukua na yule kuhani aliyemhudumia. Basi wakaenda kushambulia Laishi wakawaua wakazi wake ambao waliishi humo kwa utulivu na bila wasiwasi, wakauteketeza mji huo. 28Wakazi wa mji huo hawakuwa na mtu wa kuwaokoa kwa sababu walikuwa mbali na mji wa Sidoni, tena hawakuwa na uhusiano na watu wengine. Mji huo ulikuwa kwenye bonde la Beth-rehobu. Watu wa kabila la Dani wakaujenga upya, wakaishi humo. 29Walibadilisha jina la mji huo, wakauita Dani, kufuata jina la babu yao aliyekuwa mwana wa Israeli. Lakini mji huo hapo awali uliitwa Laishi. 30Watu wa kabila la Dani wakaisimika ile sanamu ya kuchonga, naye Yonathani, mwana wa Gershomu, mwana wa Mose, akawa kuhani wao. Wazawa wake pia walikuwa makuhani wa kabila la Dani mpaka wananchi wa nchi hiyo walipopelekwa uhamishoni. 31Wakati wote nyumba ya Mungu ilipokuwa huko Shilo, watu wa kabila la Dani waliiabudu sanamu ya kuchonga ambayo Mika aliitengeneza.


Waamuzi 18;1-31


Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: