Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Tuesday 19 September 2017

Kikombe Cha Asubuhi Kumbukumbu la Sheria 20 (Kumbukumbu la Torati katika tafsiri nyingine)


Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?


Tumshukuru Mungu wetu katika yote..
Mungu wetu,Baba yetu,Baba wa Mbinguni..
Muumba wetu,Muumba wa Mbingu na Nchi..
Mungu wa Abrahamu Isaka na Yakobo..
Utukuzwe Yahweh,Uhimidiwe Jehovah..
Usifiwe Baba wa Mbinguni,Uabudiwe Mungu wetu..
Unatosha Baba, Hakuna kama wewe Mungu wetu..
Matendo yako ni ya Ajabu..!!


“Hakuna aliye mtakatifu kama Mwenyezi-Mungu; hakuna yeyote aliye kama yeye; hakuna aliye mwamba kama Mungu wetu. Acheni kujisifu, acheni kusema ufidhuli. Maana ajuaye ni Mwenyezi-Mungu. Yeye huyapima matendo yote. Pinde za wenye nguvu zimevunjika. Lakini wadhaifu wanaendelea kupata nguvu. Wale ambao zamani walikuwa na chakula tele, sasa wanaajiriwa ili wapate chakula. Lakini waliokuwa na njaa, sasa hawana njaa tena. Mwanamke tasa amejifungua watoto saba. Lakini mama mwenye watoto wengi, sasa ameachwa bila mtoto. Mwenyezi-Mungu huua na hufufua; yeye huwashusha chini kuzimu naye huwarudisha tena. Mwenyezi-Mungu huwafanya baadhi wawe maskini, na baadhi wawe matajiri. Wengine huwashusha, na wengine huwakweza. Huwainua maskini toka mavumbini; huwanyanyua wahitaji toka majivuni, akawaketisha pamoja na wakuu, na kuwarithisha viti vya heshima. Maana, minara ya dunia ni ya Mwenyezi-Mungu; yeye ameisimika dunia juu ya minara yake. “Maisha ya waaminifu wake huyalinda, lakini maisha ya waovu huyakatilia mbali gizani. Maana, binadamu hapati ushindi kwa nguvu zake.

Asante Baba wa Mbinguni kwa wema na fadhili zako kwetu..
Asante kwa ulinzi wako wakati wote..
Asante kwakutuchagua tena na kutupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii..


Tazama jana imepita Mungu wetu Leo ni siku mpya na Kesho ni siku nyingine Jehovah..
Tunakuja mbele zako Mungu wetu tukijinyenyekeza,tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako Baba wa Mbinguni..
Tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizozifanya..
Kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua..
Mfalme wa Amani tunaomba nasi utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukoasea..
Baba wa Mbinguni utuepushe katika majaribu na utuoke na yule mwovu na kazi zake zote..
Yahweh tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu na utufunike kwa Damu ya mwanao Mpendwa Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti..

Yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona..

Lakini sasa, njia ya Mungu ya kuwakubali watu kuwa waadilifu imekwisha dhihirishwa, tena bila kutegemea sheria. Sheria na manabii hushuhudia jambo hili. Mungu huwakubali watu kuwa waadilifu kwa njia ya imani yao kwa Yesu Kristo; Mungu hufanya hivyo kwa wote wanaoamini; hakuna ubaguzi wowote. Watu wote wametenda dhambi na wametindikiwa utukufu wa Mungu. Lakini kwa zawadi ya neema ya Mungu, watu wote hukubaliwa kuwa waadilifu kwa njia ya Yesu Kristo anayewakomboa. Mungu alimtoa Yesu kusudi, kwa damu yake, awe njia ya kuwaondolea watu dhambi zao kwa imani yao kwake. Alifanya hivyo ili apate kuonesha kwamba yeye ni mwadilifu. Hapo zamani Mungu alikuwa mvumilivu bila kuzijali dhambi za watu; sasa, wakati huu, anazikabili dhambi za watu apate kuonesha uadilifu wake. Kwa namna hiyo Mungu mwenyewe huonesha kwamba yeye ni mwadilifu na kwamba humfanya kuwa mwadilifu mtu yeyote anayemwamini Yesu. Basi, tunaweza kujivunia nini? Hakuna! Kwa nini? Je, kwa sababu ya kutimiza sheria? La! Bali kwa sababu tunaamini. Maana Mungu humkubali mtu kuwa mwadilifu kwa imani, wala si kwa kutimiza matakwa ya sheria. Au je, Mungu ni Mungu wa Wayahudi tu, ama pia wa watu wa mataifa mengine? Naam, wa watu wa mataifa mengine pia. Mungu ni mmoja, naye atawafanya Wayahudi kuwa waadilifu kwa imani yao, na watu wa mataifa mengine pia kwa imani yao. Je, tunaitumia imani kuibatilisha sheria? Hata kidogo; bali tunaipa sheria thamani yake kamili.

Baba wa Mbinguni tunaomba utubariki na ukabariki kazi za mikono yetu..
Ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo..
Yahweh nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji..
Tusipungukiwe katika mahitaji yetu Mungu wetu ukatupe sawasawa na mapenzi yako...
Mfalme wa Amani tunaomba Amani ikatawale katika Nyumba/Ndoa zetu..
Ukatupe hekima na Busara katika kuendesha nyumba zetu/malezi yetu..
Ukatupe ulinzi wako na ukatamalaki na kutuatamia..
Ukatufunike kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo na Ukatupe neema ya kusimamia Neno lako Amri na Sheria zako..
Ukawabariki wazazi/wazee wetu Familia/Ndugu na wote wanaotuzunguka..
Mungu wetu ukatufanye chombo chema nasi tukatumike kama inavyokupendeza wewe..


Basi, inueni mikono yenu inayolegea na kuimarisha magoti yenu yaliyo dhaifu. Endeleeni kutembea katika njia iliyonyoka, ili kile kilicholemaa kisiumizwe, bali kiponywe. Jitahidini kuishi kwa amani na watu wote. Ishini maisha ya utakatifu, kwa sababu hakuna mtu atakayemwona Bwana bila ya maisha kama hayo. Jitahidini sana mtu yeyote asije akapoteza neema ya Mungu. Muwe waangalifu ili mti mchungu usizuke kati yenu na kuwaua wengi kwa sumu yake. Jihadharini ili miongoni mwenu pasiwe na mtu mwasherati au mtu asiyemcha Mungu kama Esau, aliyeuza haki yake ya mzaliwa wa kwanza kwa mlo mmoja. Nyinyi mnafahamu kwamba hata alipotaka kuipata tena ile baraka iliyokuwa yake, alikataliwa, maana hakupata tena nafasi ya kutubu, ingawa aliitafuta kwa machozi. Nyinyi hamkuwasili mlimani Sinai, ambao unaweza kushikika kama walivyofanya watu wa Israeli; hamkufika kwenye moto uwakao, penye giza, tufani, mvumo wa tarumbeta na sauti ya maneno. Wale waliosikia sauti hiyo waliomba wasisikie tena neno lingine, kwani hawakuweza kustahimili amri iliyotolewa: “Atakayegusa mlima huu, hata kama ni mnyama, atapigwa mawe.” Hayo yote yalionekana ya kutisha mno, hata Mose akasema, “Naogopa na kutetemeka.” Lakini nyinyi mmefika katika mlima wa Siyoni, kwenye mji wa Mungu aliye hai. Mmefika Yerusalemu, mji wa mbinguni, ambapo wamekusanyika malaika kwa maelfu. Mmefika kwenye kusanyiko kubwa la wazaliwa wa kwanza wa Mungu, ambao majina yao yameandikwa mbinguni. Mnasimama mbele ya Mungu aliye hakimu wa wote, na mbele ya roho za watu waadilifu waliofanywa wakamilifu. Mmefika kwa Yesu ambaye ni mpatanishi katika agano jipya, na ambaye damu yake iliyomwagika inasema mambo mema kuliko ile ya Abeli. Basi, jihadharini msije mkakataa kumsikiliza huyo anayesema nanyi. Kama wale waliokataa kumsikiliza yule aliyewaonya hapa duniani hawakuokoka, sisi tutawezaje kuokoka kama tukikataa kumsikiliza yule anayetuonya kutoka mbinguni? Wakati ule sauti ilitetemesha nchi, lakini sasa ameahidi: “Nitatetemesha nchi tena, lakini si nchi tu bali pia mbingu.” Neno hili: “Tena” linatuonesha kwamba vitu vyote vilivyoumbwa vitatetemeshwa na kutoweka ili vibaki vile visivyotetemeshwa. Sisi basi, na tushukuru, kwani tunapokea ufalme usiotikisika. Tuwe na shukrani na kumwabudu Mungu kwa namna itakayompendeza, kwa ibada na hofu; maana Mungu wetu kweli ni moto mkali unaoteketeza.

Roho Mtakatifu akatuongoze na tukawe na kiasi..

Baba wa Mbinguni ukawaguse na mkono wako wenye nguvu wote wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali..
Ukawape uponyaji wa mwili na roho pia..
Asante Mungu wetu yote tutaweka mikononi mwako..


Sifa na Utukufu tunakurudishia Mungu wetu..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina..!!

Asanteni sana wapendwa/Waungwana kwakuwa nami..
Baraka na Amani visiwapungukie katika maisha yenu..
Nawapenda.



Kuhusu vita

1“Mkienda vitani kupigana na adui zenu, mkaona farasi, magari na jeshi kubwa zaidi kuliko lenu msiwaogope. Maana Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu aliyewatoa Misri, atakuwa nanyi. 2Kabla ya kuanza mapigano, kuhani atajitokeza mbele na kuwaambia watu, 3‘Watu wa Israeli sikilizeni! Leo mnakaribia kupigana dhidi ya adui zenu. Msife moyo, au kuogopa, au kutishika, au kuwaogopa adui; 4maana Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, ndiye atakayekwenda pamoja nanyi kupigana kwa niaba yenu dhidi ya adui zenu na kuwapa ushindi.’
5“Kisha maofisa watawaambia watu: ‘Kuna mtu yeyote hapa aliyejenga nyumba mpya lakini hajaizindua? Arudi nyumbani, asije akafia vitani na mtu mwingine akaizindua. 6Kuna mtu yeyote hapa aliyepanda mizabibu na ambaye hajafurahia matunda yake ya kwanza? Arudi nyumbani asije akafia vitani na mtu mwingine akafurahia matunda yake. 7Kuna mwanamume yeyote hapa aliyeposa na yuko karibu kuoa? Arudi nyumbani, asije akafia vitani, na mwanamume mwingine akaoa mchumba wake.’ 8Maofisa wataendelea kuwaambia watu, ‘Je, yupo hapa mtu aliyekufa moyo? Arudi nyumbani, asije akasababisha wenzake kufa moyo kama yeye.’ 9Maofisa wakisha sema na watu, basi makamanda watawaongoza watu.
10“Mnapokaribia mji kuushambulia, kwanza wapeni wakazi wake masharti ya amani. 11Wakazi wa mji huo wakitaka amani na kujisalimisha kwenu, basi watu wote waliomo humo watawatumikieni na kufanya kazi za kulazimishwa. 12Lakini wakazi wa mji huo wasipofanya amani nanyi, lakini wakapigana vita nanyi, basi, mtauzingira mji wao; 13naye Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu akiutia mikononi mwenu, mtawaua kwa upanga wanaume wote; 14lakini wanawake na watoto, ng'ombe, na vyote vilivyomo mjini, nyara zake zote mwaweza kuchukua mateka kwa ajili yenu wenyewe; mnaweza kufurahia nyara za adui zenu, ambazo Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, amewapa. 15Ndivyo mtakavyoitendea miji yote ambayo iko mbali na nchi mtakayoimiliki. 16Lakini katika miji ya nchi ambayo Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, anawapeni, msisalimishe chochote. 17Mtawaangamiza watu wote: Wahiti, Waamori, Wakanaani, Waperizi, Wahivi na Wayebusi kama Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, alivyoamuru, 18wasije wakawafundisha desturi zao za kuchukiza ambazo waliifanyia miungu yao, nanyi mkatenda dhambi dhidi ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.
19“Mkiuzingira mji kwa muda mrefu, mkapigana kuuteka, msiiharibu miti ya matunda kwa mashoka. Je, miti ni watu hata muishambulie? Mnaweza kula matunda ya miti hiyo, lakini msiikate. 20Mnaweza kukata tu miti mingine kuitumia kuuzingira mji mpaka muuteke.


Kumbukumbu la Sheria 20:1-20

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: