Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Wednesday 21 June 2017

Kikombe Cha Asubuhi;Mambo Ya Walawi..19...


Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje Wapendwa/Waungwana?

Tumshukuru Mungu katika yote..
Asante Mungu wetu kwa wema na fadhili zako..
Asante kwa ulinzi wako wakati wote..

Asante kwakutuchagua tena na kutupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii..
Asante kwa pumzi na kutuasha wenye afya njema..

Tunakuja mbele zako Mungu wetu tukijinyenyekeza, tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako Mfalme wa Amani tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizofanya kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua..
Mungu wetu tunaomba nasi utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale waliotukosea..
Utuepushe katika majaribu,utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote, Ututakase Miili yetu na Akili zetu na utufunike kwa Damu ya mwanao Mpendwa Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo..
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi..

Mfalme wa Amani tunaomba ukatamalaki na kutuatamia katika nyumba zetu/maisha yetu..

Ukabariki kazi zetu,Biashara,Masomo na ukatuongoze katika utendaji na ukatupe ubunifu na maarifa katika kazi /biashara zetu..
Pale tunapokosea Baba ukatuonyeshe njia,ukatupe mwanga  katika kuendeleza/kuanzisha na tukafanye kama itavyokupendeza wewe..
Mungu wetu ukatupe kutambua na kuelewa nini tunatakiwa kufanya  tukafanye nini wapi na wakati gani katika mazingira tunalinayo..
Mungu wetu ukaonekane katika maisha yetu na tusipungukiwe katika mahitaji yetu..na ukatupe sawasawa na mapenzi yako..
Ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo nasi ukatupe neema ya kuwabariki wanaohitaji..
Mungu wetu ukaonekane popote tunapopita, tukawe chombo chema na tukatumike sawasawa na mapenzi yako..

Tazama waliokata tamaa,waliokwama,wenye hofu/mashaka,waliokataliwa,waliokatika vifungo mbalimbali,wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali,wenye shida/tabu..Mungu wetu ukawaguse na mkono wako wenye nguvu,ukawaponye kiroho na kimwili pia..Mungu wetu ukawainue na kuwabariki,Ukaonekane katika mahitaji yao..Mungu wetu ukasikie kulia kwao,ukajibu maombi yao,ukawatendee na kuwafadhili..Ukawape sawasawa na mapenzi yako..


Mungu wetu tunakwenda kinyume  na adui yule mwovu, na nguvu zote za giza,Nguvu za mapepo,nguvu za mizimu,za mpinga Kristo.Maagano yote ya mwovu,yeyote anayetunenea mabaya,tunavunja kwa Jina la YESU na tunajifunika kwa Damu ya Bwana wetu YESU Kristo wa Nazareti yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona...


Hatimaye, nawatakeni muwe imara katika kuungana na Bwana na kwa msaada wa nguvu yake kuu. Vaeni silaha anazowapeni Mungu mpate kuzipinga mbinu mbaya za Ibilisi. Maana vita vyetu si vita kati yetu na binadamu, bali ni vita dhidi ya jeshi ovu la ulimwengu wa roho; tunapigana na watawala, wakuu na wenye nguvu, wanaomiliki ulimwengu huu wa giza. Kwa sababu hiyo, vaeni silaha za Mungu ili siku ile itakapofika mweze kuyapinga mashambulio ya adui; na mkisha pigana mpaka mwisho, mtakuwa bado imara. Basi, kaeni tayari. Ukweli na uwe kama mkanda kiunoni mwenu, uadilifu uwe kama vazi la kujikinga kifuani, na hamu ya kutangaza Habari Njema ya amani iwe kama viatu miguuni mwenu. Zaidi ya hayo yote, imani iwe daima kama ngao mikononi mwenu, iwawezeshe kuizima mishale ya moto ya yule Mwovu. Upokeeni wokovu kama kofia yenu ya chuma, na neno la Mungu kama upanga mnaopewa na Roho Mtakatifu. Salini daima, mkiomba msaada wa Mungu. Salini kila wakati kwa nguvu ya Roho. Kesheni bila kuchoka mkisali kwa ajili ya watu wote wa Mungu. Niombeeni nami pia ili niongeapo Mungu anijalie cha kusema, niweze kuwajulisha watu fumbo la Injili kwa uthabiti. Mimi ni balozi kwa ajili ya Injili hiyo ingawa sasa niko kifungoni. Ombeni, basi, ili niweze kuwa hodari katika kuitangaza kama inipasavyo.
Asante Mungu wetu tunapokwenda kupokea katika Jina la YESU..
Amani ikatawale moyoni mwetu,Upendo na udumu,Tuendelee kusaidiana na kuhurumiana,tuchukuliane na tusameheane,Tuijue kweli yako nayo ituweke huru..

Tunayaweka haya yote mikononi mwako..
Tunashukuru na kukusifu daima..


kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina..!


Asante sana kwakunisoma/kuwa pamoja..
tuendelee kumuomba Mungu pasipo kuchoka..
Munguaendelee kuwabariki katika maisha yetu..
Nawapenda.


Kutenda mema

1Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose, 2#Taz Lawi 11:44-45; 1Pet 1:16 “Iambie jumuiya yote ya watu wa Israeli hivi: Ni lazima muwe watakatifu kwani mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, ni mtakatifu. 3Kila mmoja wenu ni lazima amheshimu mama yake na baba yake, na kuzishika Sabato zangu. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu. 4Msizigeukie sanamu za miungu, wala msijitengenezee sanamu za kusubu za miungu. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.
5“Mnaponitolea mimi Mwenyezi-Mungu sadaka za amani, mtanitolea kama itakiwavyo ili mpate kukubaliwa. 6Sadaka hiyo ni lazima iliwe siku hiyohiyo inapotolewa au kesho yake. Chochote kinachobaki hadi siku ya tatu ni lazima kiteketezwe kwa moto. 7Kama sehemu ya nyama yake italiwa siku ya tatu, tendo hilo ni chukizo; na sadaka hiyo haitakubaliwa, 8naye atakayekula nyama hiyo ni lazima awajibike kwa uovu wake kwa sababu amekitia unajisi kitu kitakatifu cha Mwenyezi-Mungu. Mtu huyo atatengwa na watu wake.
9 # Taz Lawi 23:22; Kumb 24:19-22 “Utakapovuna mavuno ya nchi yako, usivune kabisa hadi mpakani mwa shamba wala usirudi nyuma kukusanya mabaki. 10Msirudie kukusanya kila kitu katika shamba la mizabibu, wala usiokote zabibu zilizoanguka chini; utawaachia maskini na wageni. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.
11 # Taz Kut 20:15-16; Kumb 5:19-20; Kut 20:7; Kumb 5:11; Mat 5:33 “Msiibe, msidanganye wala kuambiana uongo. 12Msiape uongo kwa jina langu hata kulikufuru jina la Mungu wenu. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.
13 # Taz Kumb 24:14-15 “Usimdhulumu jirani yako wala kumwibia. Mshahara wa mtu aliyeajiriwa usikae kwako usiku kucha hadi asubuhi. 14#Taz Kumb 27:18 Usimlaani kiziwi wala kuweka kizuizi mbele ya kipofu, bali umche Mungu wako. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.
15 # Taz Kut 23:6-8; Kumb 16:19 “Unapotoa hukumu uamue kwa haki; usimpendelee maskini wala kumwogopa mwenye cheo. Bali ni lazima kumwamua jirani kwa haki. 16Kamwe usipitepite ukiwachongea watu wa jamaa yako. Usiyatie maisha ya jirani yako katika hatari ya kifo kwa maneno yako. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.
17 # Taz Mat 18:15 “Usimwekee kisasi ndugu yako moyoni mwako, bali upatane daima na jirani yako ili usije ukatenda dhambi. 18#Taz Mat 5:43 Usijilipize kisasi au kuwa na kinyongo dhidi ya wazawa wa watu wako bali umpende jirani yako kama unavyojipenda wewe mwenyewe. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.
19 # Taz Kumb 22:9-11 “Yakupasa kuyashika masharti yangu. Usiiache mifugo yako ipandwe na wanyama wa aina nyingine. Shambani mwako usipande mbegu za aina mbili. Usivae vazi lililofumwa kwa aina mbili za nguo.
20“Mwanamume akilala na mwanamke mtumwa ambaye ameposwa na mwanamume mwingine, lakini bado hajakombolewa wala kupewa uhuru, uchunguzi ufanywe. Lakini wasiuawe kwa sababu mwanamke huyo hakuwa bado huru. 21Mwanamume huyo ataleta mbele ya hema la mkutano sadaka yake ya kondoo dume ya kuondoa hatia na kunitolea mimi Mwenyezi-Mungu. 22Kuhani atamfanyia ibada ya upatanisho kwa kutumia kondoo huyo mbele ya Mwenyezi-Mungu kwa ajili ya dhambi aliyotenda; naye atasamehewa dhambi hiyo aliyotenda.
23“Mtakapofika katika nchi ya Kanaani na kupanda aina zote za miti ya matunda, matunda hayo hamtayala; hamtaruhusiwa kuyala kwa muda wa miaka mitatu. 24Mnamo mwaka wa nne matunda yake yote yatakuwa matakatifu, yatatolewa kuwa sadaka ya sifa,#19:24 sifa: Au shukrani. kwa Mwenyezi-Mungu. 25Lakini matunda ya kuanzia mwaka wa tano hayo mnaweza kula, na mavuno yenu yataongezeka. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.
26 # Taz Mwa 9:4; Lawi 7:26-27; 17:10-14; Kumb 12:16,23; 15:23; 18:10 “Msile nyama yoyote yenye damu. Msipige bao wala kufanya uchawi. 27#Taz Lawi 2:5; Kumb 14;1 Nywele zenu msizikate pembeni wala kunyoa ndevu zenu. 28Msijitie alama zozote mwilini mwenu kwa ajili ya kuomboleza au kujikatakata mwilini au kujichanja chale. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.
29 # Taz Kumb 23:17 “Usimchafue binti yako kwa kumfanya kahaba, nchi nzima isije ikaangukia katika ukahaba na hivyo kujaa uovu. 30#Taz Lawi 26:2 Mtazishika Sabato zangu na kupaheshimu mahali pangu patakatifu. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.
31 # Taz Kumb 18:11; 1Sam 28:3; 2Fal 23:4; Isa 8:19 “Msiwaendee waaguzi wa mizimu wala wachawi ili kuwaomba wawaagulie na hivyo mkajitia najisi. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.
32“Uwapo mbele ya mzee ni lazima usimame ili kumpa heshima yake; nawe umche Mungu wako. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.
33“Kama kuna mgeni katika nchi yako usimtendee vibaya. 34Huyo mgeni anayekaa nawe atakuwa kwako kama mwenyeji nawe utampenda kama unavyojipenda mwenyewe, kwa kuwa nawe ulikuwa mgeni katika nchi ya Misri. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.
35 # Taz Kut 22:21; Kumb 24:14-18; 27:19 “Usikose kamwe kuamua kwa haki kuhusu vipimo vya urefu, uzito na ujazo. 36Ni lazima mtumie mizani halali, na vipimo vilivyo halali. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, niliyewatoa katika nchi ya Misri. 37Ni lazima kuyashika na kuyatekeleza masharti yangu na maagizo yangu. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.”

Mambo Ya Walawi19;1-37


Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: