Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Tuesday 24 October 2017

Kikombe Cha Asubuhi ;Yoshua 11...



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu katika yote..

Mtakatifu..Mtakatifu..Mtakatifu Baba wa Mbinguni..
Mungu wetu,Muumba wetu,Muumba wa Nchi na Mbingu
Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo,Baba wa Upendo
Baba wa amani, Muweza wa yote,Baba wa Yatima,Mume wa wajane
Utukuzwe ee Mungu wetu,Unastahili sifa,Unastahili kuabudiwa,
Unastahili kuhimidiwa,Unastahili ee Mungu wetu..
Unatosha Baba wa Mbinguni,Matendo yako ni ya ajabu,
Matendo yako ni makuu mno,Hakuna kama wewe Mungu wetu..




Mfalme Yehoshafati wa Yuda alirejea salama katika ikulu yake mjini Yerusalemu. Lakini mwonaji Yehu mwana wa Hanani, alikwenda kumlaki mfalme, akamwambia, “Je, unadhani ni vema kuwasaidia waovu na kuwapenda wamchukiao Mwenyezi-Mungu? Mambo uliyofanya yamekuletea ghadhabu ya Mwenyezi-Mungu. Walakini, kuna wema fulani ndani yako. Umekwisha ziondoa sanamu zote za Ashera, mungu wa kike, na umejitahidi sana kumtafuta Mungu kwa moyo wote.”
Asante kwa wema na fadhili zako kwetu..
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote..
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa kibali cha kuendelea
kuiona leo hii Mungu wetu..
Asante kwa pumzi/uzima,afya na tukiwa tayari kwa majukumu yetu..
Si kwamba sisi ni wema sana,si kwamba sisi ni wazuri mno,
si kwa nguvu/utashi wetu sisi kuwa hivi tulivvyo Mungu wetu..
Ni kwa Neema/rehema zako,ni kwa mapenzi yako Jehovah..
Sifa na utukufu tunakurudishia wewe Mungu wetu..





Mfalme Yehoshafati alikaa Yerusalemu, lakini hata hivyo, mara kwa mara aliwatembelea watu wa Beer-sheba kusini, mpaka milima ya Efraimu, upande wa kaskazini. Alifanya hivyo ili kuwavutia watu wamrudie Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zao. Aliteua waamuzi katika miji yote ya Yuda yenye ngome, akawaambia, “Muwe waangalifu sana wakati mnapoamua, kwa maana hukumu mtoayo hamwitoi kwa amri ya binadamu, bali kwa amri itokayo kwa Mwenyezi-Mungu, naye yu pamoja nanyi mnapotoa uamuzi. Basi, sasa mwogopeni Mwenyezi-Mungu, muwe waangalifu katika kila jambo mtakalotenda kwa sababu Mwenyezi-Mungu wetu hatavumilia upotoshaji wa haki, wala upendeleo wala ulaji rushwa.” Mjini Yerusalemu, Yehoshafati aliteua Walawi kadhaa, waamuzi na baadhi ya wakuu wa jamaa za Waisraeli wawe waamuzi wa magomvi yahusuyo uvunjaji wa sheria za Mwenyezi-Mungu, au ugomvi baina ya wakazi wa mji. Akawaamuru akisema; “Tekelezeni wajibu wenu mkimwogopa Mwenyezi-Mungu, kwa uaminifu na kwa moyo wote. Kila mara ndugu zenu kutoka katika mji wowote ule wanapowaletea shtaka lolote kuhusu uuaji, uvunjaji wa sheria, amri, kanuni au maagizo, washaurini vema ili wasije wakamkosea Mwenyezi-Mungu. Msipofanya hivyo, nyinyi pamoja na ndugu zenu mtapatwa na ghadhabu ya Mwenyezi-Mungu. Lakini mkiutekeleza wajibu wenu, hamtakuwa na hatia. Amaria, kuhani mkuu, ndiye atakayesimamia mambo yote yanayomhusu Mwenyezi-Mungu, naye Zebadia mwana wa Ishmaeli, gavana wa Yuda atasimamia mambo yote ya utawala, na Walawi watakuwa maofisa. Jipeni moyo muyatekeleze masharti haya, naye Mwenyezi-Mungu awe pamoja nao walio wema.”

Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,
tukijishusha na tukijiachilia mikononi mwako Yahweh..
Tunaomba utusamehe makosa yetu yote tuliyoyafanya
kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua..
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba utupe neema ya kuweza
kuwasamehe wale wote waliotukosea..
Mungu wetu tunaomba utuepushe katika majaribu
Baba utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote
Yahweh tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu
Baba wa Mbinguni utufunike kwa Damu ya Mwanao mpendwa
Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti..
Yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona..




Baada ya muda, majeshi ya Moabu na Amoni pamoja na baadhi ya Wameuni, waliivamia Yuda. Watu kadhaa walikuja wakamwambia mfalme Yehoshafati, “Jeshi kubwa limekuja kukushambulia kutoka Edomu, ngambo ya Bahari ya Chumvi. Tayari wamekwisha teka Hasason-tamari.” (Hili ni jina lingine la Engedi). Yehoshafati akashikwa na woga, akamwomba Mwenyezi-Mungu amwongoze. Akatangaza watu wote nchini Yuda wafunge. Watu wakaja Yerusalemu kutoka miji yote ya Yuda, wakakusanyika ili kumwomba Mwenyezi-Mungu awasaidie. Yehoshafati akasimama katikati ya kusanyiko la watu wa Yuda na Yerusalemu mbele ya ua mpya wa nyumba ya Mwenyezi-Mungu, akaomba kwa sauti akisema, “Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zetu, wewe ndiwe Mungu uliye mbinguni! Wewe unazitawala falme zote duniani; unao uwezo na nguvu, wala hakuna awezaye kukupinga.

Jehovah tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
vyote tunavyoenda kufanya/kutenda Mungu wetu tukatende
kama inavyokupendeza wewe..
Yahweh tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwabariki
wenye kuhitaji..
Jehovah tusipungukiwe katika mahitaji yetu,Yahweh ukatupe
sawasawa na mapenzi yako..

Mfalme wa amani tunaomba amani yako ikatawale katika
nyumba/ndoa zetu,watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na
wote wanotuzunguka,Mungu wetu tunaomba ulinzi wako
Baba tunaomba nuru yako ikaangaze katika maisha yetu
Yahweh upendo wetu ukadumu,Furaha,utuwema,fadhili...
Baba wa mbinguni tunaomba utupe neema ya kufuata njia zako
Yahweh tukasimamie Neno lako,Amri na sheria zako siku zote
za maisha yetu,Jehovah tukanene yaliyo yako,tukapate
kutambua/kujitambua na tukashirikiane katika shida na raha
ukatupe neema ya hekima,busara, kuchukuliana na kuonyana/kuelimishana kwa upendo,upole na amani..
Ukatufanye chombo chema Jehovah nasi tukatumike
sawasawa na mapenzi yako..
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi..



Ni wewe ee Mungu wetu, uliyewafukuza wenyeji wa nchi hii wakati watu wako Israeli walipoingia katika nchi hii, ukawapa wazawa wa Abrahamu rafiki yako, iwe yao milele. Nao wamekaa humu, na kukujengea hekalu kwa heshima ya jina lako, wakijua kwamba wakipatwa na maafa yoyote, vita, maradhi mabaya, au njaa, basi watakuja na kusimama mbele ya nyumba hii mbele yako, wakulilie katika shida zao, nawe utawasikiliza na kuwaokoa. Sasa watu wa Amoni, Moabu na wa mlima Seiri, ambao hukuwaruhusu babu zetu washambulie nchi zao walipotoka Misri, wakapitia kandokando wasiwaangamize, tazama, jinsi wanavyotulipa. Wanakuja kututoa katika nchi yako uliyotupa iwe mali yetu. Wewe ndiwe Mungu wetu! Waadhibu, kwani sisi hatuna uwezo wowote mbele ya jeshi kubwa kama hili linalotujia. Hatujui la kufanya ila tunatazamia msaada kutoka kwako.” Wanaume wote wa Yuda, pamoja na wake zao na watoto wao, walikuwa wamesimama hapo mbele ya Mwenyezi-Mungu. Ndipo Roho wa Mwenyezi-Mungu akamjia mmoja wa Walawi aliyekuwa hapo, jina lake Yahazieli mwana wa Zekaria, mwana wa Benaya, mwana wa Yeieli, mwana wa Matania, wa ukoo wa Asafu. Yahazieli akasema, “Sikilizeni watu wa Yuda na wakazi wa Yerusalemu na mfalme Yehoshafati, Mwenyezi-Mungu awaambia hivi: Msiogope wala msihangaike kwa sababu ya jeshi hili kubwa. Vita hivi si vyenu, bali ni vya Mungu. Kesho washambulieni wakati watakapokuwa wakipanda Bonde la Sisi. Mtawakuta mwisho wa bonde, mashariki mwa jangwa la Yerueli. Hamtahitaji kupigana vita hivi. Nyinyi jipangeni tu halafu mngojee, na mtaona Mwenyezi-Mungu akiwashinda kwa niaba yenu. Enyi watu wa Yuda na Yerusalemu, msiogope wala msifadhaike. Nendeni vitani, naye Mwenyezi-Mungu atakuwa pamoja nanyi!” Hapo mfalme Yehoshafati akasujudu pamoja na watu wote wa Yuda na wakazi wa Yerusalemu wakamsujudu na kumwabudu Mwenyezi-Mungu. Walawi wa ukoo wa Kohathi na Kora, wakasimama na kumsifu Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, kwa sauti kubwa sana. Kesho yake, wakaamka asubuhi na mapema, wakaenda mpaka katika jangwa la Tekoa. Walipokuwa wanaondoka, Yehoshafati alisimama, akawaambia, “Nisikilizeni, enyi watu wa Yuda na wakazi wa Yerusalemu! Mwaminini Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, nanyi mtakuwa imara. Muwe na imani na manabii wake, nanyi mtafaulu.” Baada ya kushauriana na watu, mfalme alichagua wanamuziki fulani, akawaagiza wajivike mavazi yao rasmi kisha watangulie mbele ya jeshi, wakiimba: “Mshukuruni Mwenyezi-Mungu, maana fadhili zake zadumu milele!” Wakati walipoanza kuimba na kusifu, Mwenyezi-Mungu aliwavuruga akili wanajeshi wa Amoni, Moabu na wa Mlima Seiri waliokuja kupigana na Yuda. Na wanajeshi hao wakashindwa. Watu wa Amoni na wa Moabu wakawashambulia wenyeji wa mlima Seiri, na kuwaangamiza kabisa. Baada ya kuwaangamiza wakazi wa mlima Seiri wakaanza kushambuliana wao kwa wao, wakaangamizana. Jeshi la Yuda lilipofika penye mnara wa ulinzi huko jangwani, waliangalia upande wa maadui, wakaona maiti zimetapakaa kila mahali. Hakuna mtu yeyote aliyenusurika. Yehoshafati na wanajeshi wake wakaenda kuchukua nyara wakakuta ng'ombe wengi, mali, nguo na vitu vingine vya thamani. Iliwachukua muda wa siku tatu kusomba nyara hizo, na hata hivyo, hawakuzimaliza kwani zilikuwa nyingi mno. Siku ya nne wakakusanyika katika Bonde la Sifa, na kumsifu Mwenyezi-Mungu kwa yote aliyowafanyia. Ndio maana bonde hilo linaitwa Bonde la Sifa hadi hivi leo. Kisha Yehoshafati akawaongoza wanajeshi wake mpaka Yerusalemu kwa shangwe, kwa sababu Mwenyezi-Mungu aliwashinda maadui zao. Walipofika Yerusalemu, walikwenda moja kwa moja hadi nyumba ya Mwenyezi-Mungu, wakipiga vinanda, vinubi na tarumbeta. Falme zote ziliingiwa na hofu ziliposikia jinsi Mwenyezi-Mungu alivyowashinda maadui za Israeli. Basi, Yehoshafati akatawala kwa amani, na Mungu akampa amani pande zote.

Tazama wenye shida/tabu,wagonjwa,wenye njaa,wote wanaopitia
magumu/majaribu,waliokata tamaa,walio katika vifungo vya
yule mwovu,waliopotea/walioanguka na wote wataabikao
na kuelemewa na mizigo,Mungu wetu tunaomba ukawape neema
ya kujiombea,wakapate kutambua Mungu muweza wa yote
upo na unayaweza yote, Mponyaji wa kweli upo, Baba wa Mbinguni
tunaomba ukawaponye kimwili na kiroho pia,Yahweh ukawaguse
kwa mkono wako wenye nguvu,Jehovah ukaonekane kwenye mapito
yao na ukasikie kulia kwao Mungu wetu ukawafute machozi yao
Baba wa Mbinguni ukawasimamshe na kuwasamehe

 wale wote walikwenda kinyume nawe,Mungu wetu ukapokee sala/maombi ya watoto wako
wote wanokutafuta na kukuomba kwa imani na bidii..
Baba ukawape amani ya moyo,mwanga katika maisha yao,
macho ya kuona na masikio ya kusikia sauti yako..


Tunayaweka haya yote mikononi mwako Mungu wetu
tukiamini Mungu wetu u pamoja nasi jana,leo na hata Milele..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Miele
Amina..!

Wapendwa katika Bwana asanteni sana kwakuwa nami
Baba wa upendo aendelee kuwatendea sawasawa na mapenzi yake
Nawapenda.

Yoshua anamshinda Yabini

1Mfalme Yabini wa mji wa Hazori alipopata habari hizo, alipeleka ujumbe kwa mfalme Yobabu wa Madoni, mfalme wa Shimroni na mfalme wa Akshafi, 2na kwa wafalme waliokuwa katika milima ya kaskazini, waliokuwa Araba ambayo ilikuwa kusini mwa Kinerethi, kwenye tambarare na waliokuwa Nafath-dori katika upande wa magharibi. 3Pia, alipeleka ujumbe kwa Wakanaani waliokuwa pande za mashariki na magharibi, kwa Waamori, Wahiti, Waperizi, Wayebusi ambao walikaa milimani na kwa Wahivi ambao walikaa chini ya mlima Hermoni katika nchi ya Mizpa. 4Basi, wakatoka wote na majeshi yao makubwa. Nao walikuwa wengi kama mchanga wa pwani pamoja na magari mengi na farasi wengi sana. 5Wafalme hawa wote wakaungana na kupiga kambi yao katika chemchemi ya Meromu ili wapigane na Waisraeli.
6Mwenyezi-Mungu akamwambia Yoshua, “Usiwaogope hao, maana kesho, wakati kama huu, nitawaangamiza wote kwa kuwatia mikononi mwa Waisraeli; nanyi mtakata mishipa ya farasi wao na kuteketeza magari yao kwa moto.” 7Basi, ghafla kwenye chemchemi ya Meromu Yoshua pamoja na jeshi lake lote akawatokea na kuwashambulia. 8Mwenyezi-Mungu akawatia mikononi mwa Waisraeli, nao wakawachapa na kuwafukuza mpaka Sidoni Kuu na Misrefoth-maimu, hadi upande wa mashariki katika bonde la Mizpa. Waisraeli wakawapiga na kuwaua wote. 9Yoshua aliwakatakata mishipa farasi wao wote na kuyateketeza magari yao kwa moto, kama Mwenyezi-Mungu alivyomwagiza.
10Yoshua alipokuwa anarudi, akauteka mji wa Hazori. Alimuua mfalme wake maana ndiye aliyekuwa kiongozi wa falme hizo zote. 11Kisha akauteketeza mji wa Hazori kwa moto na kuwaua wakazi wake wote, asimwache hata mtu mmoja. 12Pia aliiteketeza miji ile mingine yote kwa moto na kuwaua wafalme wao wote kama Mose, mtumishi wa Mwenyezi-Mungu, alivyomwamuru. 13Lakini Waisraeli hawakuiteketeza miji iliyokuwa vilimani, isipokuwa tu mji wa Hazori ambao Yoshua aliuteketeza. 14Waisraeli wakachukua vitu vyote walivyoteka nyara na wanyama wa miji hiyo; lakini waliwaua wakazi wake wote, wala hawakumwacha hata mtu mmoja. 15Amri hii alipewa Mose, mtumishi wa Mwenyezi-Mungu, naye Mose akamwamuru Yoshua ambaye aliitekeleza. Yoshua alitimiza kila jambo Mwenyezi-Mungu alilomwamuru Mose.

Nchi alizoteka Yoshua

16Yoshua aliiteka nchi nzima: Sehemu za milimani na sehemu zote za Negebu, eneo lote la Gosheni, nchi tambarare, nchi ya Araba, milima ya Israeli na sehemu zake zilizo tambarare; 17aliwateka na kuwaua wafalme wote wa nchi hizo kuanzia mlima uliokuwa mtupu wa Halaki karibu na Seiri mpaka Baal-gadi katika bonde la Lebanoni, kusini ya mlima Hermoni. 18Vita alivyopigana Yoshua na wafalme hawa wote vilichukua muda mrefu. 19Hakuna mji ambao ulifanya mapatano ya amani na Waisraeli, isipokuwa Gibeoni tu, ambamo waliishi Wahivi. Waisraeli waliiteka miji mingine yote kwa kupigana vita. 20Taz Kumb 7:16 Ilikuwa ni matakwa ya Mwenyezi-Mungu mwenyewe kuishupaza mioyo ya watu wa mataifa hayo ili wapigane. Alikusudia wasihurumiwe ila wateketezwe. Ndivyo Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose.
21Wakati huo, Yoshua alikwenda, akawaangamiza Waanaki waliokuwa wanaishi katika milima huko Hebroni, Debiri, Anabu, nchi yote ya milima ya Yuda na Israeli. Yoshua aliwaangamiza watu hao pamoja na miji yao. 22Hakuna mtu wa kabila la Anaki ambaye alibakia katika nchi ya Israeli; walibaki wachache tu katika miji ya Gaza, Gathi na Ashdodi.
23Basi, Yoshua akaitwaa nchi yote kulingana na yote yale Mwenyezi-Mungu aliyomwambia Mose. Yoshua akaikabidhi kwa Waisraeli iwe mali yao, wagawane kulingana na makabila yao. Kisha nchi nzima ikatulia, ikawa haina vita tena.



Yoshua 11;1-23

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

Monday 23 October 2017

Kikombe Cha Asubuhi ;Yoshua 10...





Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Haleluyah..!Mungu wetu yu mwema sana..
Ni wiki/siku nyingine tena Mungu wetu ametupa Kibali cha
kuendelea kuiona Leo hii..
Tumshukuru Mungu wetu kwa mema mengi aliyotutendea/anayotutendea

Asante Mungu wetu Baba yetu kwa wema na fadhili zako kwetu..
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote..
Asante kwa uzima/pumzi, afya na kutuamsha salama na
tukiwa tayari kwa majukumu yetu..




Shangilieni kwa sababu ya Mwenyezi-Mungu enyi waadilifu! Kumsifu Mungu ni wajibu wa watu wanyofu. Msifuni Mwenyezi-Mungu kwa zeze; mwimbieni kwa kinubi cha nyuzi kumi. Mwimbieni wimbo mpya; pigeni kinubi vizuri na kushangilia. Neno la Mwenyezi-Mungu ni la kweli; na matendo yake yote ni ya kuaminika. Mungu apenda uadilifu na haki, dunia imejaa fadhili za Mwenyezi-Mungu. Mbingu ziliumbwa kwa neno la Mwenyezi-Mungu, na vyote vilivyomo kwa pumzi ya mdomo wake. Alikusanya maji ya bahari kama katika chupa, vilindi vya bahari akavifunga ghalani. Dunia yote na imwogope Mwenyezi-Mungu! Wakazi wote duniani, wamche! Maana alisema na ulimwengu ukawako; alitoa amri nao ukajitokeza. Mwenyezi-Mungu hupangua mipango ya mataifa, na kuyatangua mawazo yao. Mpango wa Mwenyezi-Mungu hudumu milele; maazimio yake yadumu vizazi vyote. Heri taifa ambalo Mungu wake ni Mwenyezi-Mungu; heri wale aliowachagua kuwa watu wake mwenyewe! Mwenyezi-Mungu huangalia chini kutoka mbinguni, na kuwaona wanadamu wote. Kutoka kwenye kiti chake cha enzi, huwaangalia wakazi wote wa dunia. Yeye huunda mioyo ya watu wote, yeye ajua kila kitu wanachofanya. Mfalme hawezi kuokolewa kwa kuwa na jeshi kubwa; wala shujaa hapati ushindi kwa nguvu zake kubwa. Farasi wa vita hafai kitu kwa kupata ushindi; nguvu zake nyingi haziwezi kumwokoa mtu. Mwenyezi-Mungu huwaangalia wale wamchao, watu ambao wanatumainia fadhili zake. Yeye huwaokoa katika kifo, huwaweka hai wakati wa njaa. Mioyo yetu yamtumainia Mwenyezi-Mungu. Yeye ni msaada wetu na ngao yetu. Naam twafurahi kwa sababu yake; tuna matumaini katika jina lake takatifu. Fadhili zako zikae nasi, ee Mwenyezi-Mungu, kwani sisi tumekuwekea tumaini letu.
Utukuzwe ee Mungu wetu,Uhimidiwe Baba wa Mbinguni..
Unastahili sifa Jehovah,Unastahili kuabudiwa Yahweh..
Matendo yako ni ya ajabu mno,Matendo yako ni makuu sana..
Hakuna kama wewe ee Mungu wetu,Unatosha Jehovah..!

Tazama jana imepita Leo ni siku mpya na kesho ni siku nyingine
Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyeyekeza,
tukijishusha,tukijiachilia mikononi mwako Yahweh..
Tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizozifanya
kwakuwaza,wakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua..
Mfalme wa amani nasi tunaomba utupe neema ya kuweza
kuwasamehe wale wote waliotukosea..
Baba wa Mbinguni tunaomba utuepushe katika majaribu
Yahweh utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote..
Jehovah tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu
Mungu wetu utufunike kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
 wa Nazareti..
Yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona..





Manase alikuwa na umri wa miaka kumi na miwili alipoanza kutawala, akatawala kutoka Yerusalemu kwa muda wa miaka hamsini na mitano. Alitenda maovu mbele ya Mwenyezi-Mungu kwa kuiga mienendo miovu ya mataifa ambayo Mwenyezi-Mungu aliyafukuza wakati watu wake wa Israeli walipokuwa wanaingia nchini. Kwa maana alirekebisha mahali pa kuabudia miungu mingine palipokuwa pamebomolewa na Hezekia baba yake; akajenga madhabahu za kuabudia Mabaali, akatengeneza na sanamu za Maashera. Isitoshe, aliabudu vitu vyote vya mbinguni na kuvitumikia. Alijenga madhabahu katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu mahali ambapo Mwenyezi-Mungu alikuwa amesema, “Jina langu litaabudiwa milele katika Yerusalemu.” Alijenga madhabahu za kuabudia vitu vyote mbinguni kwenye nyua mbili za nyumba ya Mwenyezi-Mungu. Pia aliwatoa wanawe kama sadaka ya kuteketeza katika bonde la mwana wa Hinomu. Alipiga ramli, alibashiri na alitumia hirizi; hata alishirikiana na waaguzi wa mizimu na wachawi. Alitenda maovu mengi mbele ya Mwenyezi-Mungu, akamkasirisha. Nayo sanamu aliyoitengeneza, aliiweka katika nyumba ya Mungu mahali alipopazungumzia, mbele ya Daudi na Solomoni mwanawe: “Katika nyumba hii na katika Yerusalemu kati ya makabila kumi na mawili ya Israeli, ndipo mahali nitakapoabudiwa milele. Na iwapo watu wa Israeli watajali kutenda yote niliyowaamuru, wakatii sheria zote, masharti, na maagizo yaliyotolewa kwa mkono wa Mose, basi kamwe sitawaacha wafukuzwe kutoka katika nchi hii ambayo niliwapa babu zao.” Lakini Manase aliwapotosha watu wa Yuda na wakazi wa Yerusalemu, wakatenda maovu zaidi kuliko mataifa ambayo Mwenyezi-Mungu aliyaangamiza mbele ya watu wa Israeli.
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
vyote tunavyoenda kufanya/kutenda Mungu wetu tukatende
sawasawa na mapenzi yako..
Yahweh ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu tunaomba nasi utupe neema ya kuwabariki wenye kuhitaji
Jehovah tusipungukiwe katika mahitaji yetu Baba ukatupe kama
inavyokupendeza wewe..
Mfalme wa amani tunaomba amani yako ikatawale katika
nyumba/ndoa zetu,watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na
wote wanaotuzunguka..
Mungu wetu tunaomba ulinzi wako,Baraka,utuwema,fadhili
Baba ukatupe neema ya hekima,busara,heshima,upendo wa kweli
tukasaidiane,tukachukuliane na tukaonyane/kuelimishana kwa upendo
Baba wa Mbinguni pendo lako likadumu,Nuru ikaangaze katika maisha
yetu,tukawe na kiu/shauku ya kukutafuta wewe Mungu wetu..
Baba wa Mbinguni tunaomba utupe neema ya kusimamia Neno
lako Amri na Sheria zako siku zote za maisha yetu..



Mwenyezi-Mungu alimwonya Manase na watu wake, lakini hawakumsikia. Kwa hiyo, Mwenyezi-Mungu akawaleta makamanda wa jeshi la mfalme wa Ashuru. Hao makamanda walimkamata Manase kwa kulabu wakamfunga pingu za shaba, wakampeleka hadi Babuloni. Wakati alipokuwa taabuni, alimwomba Mwenyezi-Mungu, Mungu wake, akajinyenyekesha sana mbele ya Mungu wa babu zake. Alimsihi, naye Mungu akapokea ombi lake na sala yake akamrudisha Yerusalemu katika ufalme wake. Ndipo Manase akatambua kuwa Mwenyezi-Mungu ndiye Mungu.

Ukatufanye chombo chema Yahweh nasi tukatumike kama inavyokupendeza wewe..
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote,
tupate kutambua/kujitamnbu na tukawe na kiasi..

Tazama wenye shida/tabu Mungu wetu,wagonjwa,wenye njaa,
waliokatika vifungo vya yule mwovu,wanaopitia magumu/majaribu
mbalimbali,waliokata tamaa,waliokataliwa,wanaotafuta watoto,
wanaotafuta wenza mke/mume mwema na wote waliopotea/anguka
Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu..
Baba wa Mbinguni tunaomba ukawaponye kiroho na kimwili
Mfalme wa amani ukatawale kwenye maisha yao na mwanga wako
ukaangaze katika mapito yao,Jehovah nukawape neema ya kujiombea
na wakafuate njia zako nazo zikawaweke huru..
Baba wa Mbinguni ukawasamehe wale wote waliokwenda kinyume nawe
Yahweh ukawatendee wenye njaa,Baba ukawape maarifa na ubunifu
katika maisha yao,kazi,biashara,kilimo na wote wakutafutao kwa bidii
Baba ukaonekane katika shida zao,Mungu wetu ukasikie kulia kwao
Baba ukawafute machozi ya watoto wako,Mungu wetu ukapokee
Maombi/sala zetu,wafiwa ukawe mfarinji wao..




Baada ya haya, Manase alijenga ukuta mwingine upande wa nje wa mji wa Daudi, magharibi mwa Gihoni, bondeni, akauendeleza hadi Lango la Samaki, akauzungusha hadi Ofeli; akauinua juu sana. Pamoja na hayo, aliweka makamanda wa majeshi katika miji yote ya Yuda yenye ngome. Alitoa katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu miungu yote ya kigeni na sanamu pamoja na madhabahu zote alizokuwa amezijenga kwenye mlima wa nyumba ya Mwenyezi-Mungu na katika Yerusalemu; alivitupa nje ya mji. Alirudisha madhabahu ya kumwabudia Mwenyezi-Mungu, na juu yake akatoa tambiko za amani na za shukrani, akawaamuru watu wa Yuda wamwabudu Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli. Hata hivyo watu waliendelea kutoa sadaka mahali pa kufanyia ibada, lakini kwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wao tu.
Kwa imani tunayaweka haya yote mikononi mwako
tukiamini na kushukuru daima..
Sifa na utukufu ni wako Mungu wetu..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina...!


Asanteni sana wapendwa katika Bwana kwakuwa nami
Baba wa upendo aendelee kuwabariki na kuwatendea
sawasawa na mapenzi yake,Amani ya Kristo iwe nanyi daima
Nawapenda.

Waamori wanashindwa

1Mfalme Adoni-sedeki wa Yerusalemu10:1 Yerusalemu: Wakati huo mji huu ulikuwa wa Wayebusi. alipata habari juu ya jinsi Yoshua alivyouteka mji wa Ai na kuuharibu kabisa akiutendea mji huo na mfalme wake kama alivyoutendea Yeriko na mfalme wake. Pia alipata habari kwamba wakazi wa Gibeoni walikuwa wamefanya mkataba wa amani na Waisraeli na kwamba sasa wanaishi miongoni mwao. 2Habari hizo zilisababisha hofu kubwa huko Yerusalemu kwa sababu mji wa Gibeoni ulikuwa maarufu miongoni mwa miji ya kifalme. Isitoshe, mji huu ulikuwa maarufu kuliko Ai na wanaume wake wote walikuwa askari hodari mno. 3Basi, Mfalme Adoni-sedeki akapeleka ujumbe kwa mfalme Hohamu wa Hebroni, mfalme Piramu wa Yarmuthi, mfalme Yafia wa Lakishi na mfalme Debiri wa Egloni, akawaambia, 4“Njoni mnisaidie tuwaangamize Wagibeoni, maana wamefanya mkataba wa amani na Yoshua pamoja na Waisraeli.” 5Kisha wafalme hao watano wa Waamori: Mfalme wa Yerusalemu, mfalme wa Hebroni, mfalme wa Yarmuthi, mfalme wa Lakishi na mfalme wa Egloni, wakaunganisha majeshi yao, wakaenda nayo mpaka Gibeoni; wakapiga kambi kuuzingira mji huo, wakaushambulia.
6Wagibeoni wakapeleka ujumbe kwa Yoshua huko kambini Gilgali, wakamwambia, “Tafadhali, usitutupe sisi watumishi wako; njoo upesi utusaidie na kutuokoa kwa maana wafalme wote wa Waamori kutoka nchi ya milimani wamekuja kutushambulia.”
7Basi, Yoshua pamoja na jeshi lake lote na mashujaa wakaondoka Gilgali. 8Mwenyezi-Mungu akamwambia Yoshua, “Usiwaogope hata kidogo maana nimewatia mikononi mwako, wala hakuna hata mmoja atakayeweza kukukabili.” 9Baada ya kutembea kutoka Gilgali usiku kucha, Yoshua akawatokea ghafla. 10Naye Mwenyezi-Mungu akawatia hofu kuu mbele ya Waisraeli ambao waliwaua watu wengi huko Gibeoni wakiwakimbiza kwenye njia ya mteremko wa Beth-horoni mpaka Azeka na Makeda ambako pia waliwaua watu wengi sana. 11Walipokuwa wakiwakimbia Waisraeli kwenye mteremko wa Beth-horoni, Mwenyezi-Mungu akawanyeshea mvua ya mawe makubwa kutoka mbinguni wakiwa njiani mpaka Azeka hata waliouawa kwa mawe hayo wakawa wengi kuliko waliouawa kwa silaha za Waisraeli.
12Wakati Mwenyezi-Mungu alipowatia Waamori mikononi mwa Waisraeli, Yoshua alimwomba Mwenyezi-Mungu mbele ya Waisraeli wote, akasema,
“Wewe jua, simama kimya juu ya Gibeoni,
wewe mwezi, katika bonde la Aiyaloni.”
13 Taz 2Sam 1:18 Jua likasimama kimya na mwezi ukasimama mpaka taifa la Israeli lilipolipiza kisasi maadui wake. Kama alivyoandika katika kitabu cha Yashari, jua lilisimama kimya katikati ya mbingu, likakatiza safari yake ya kwenda kutua kwa siku nzima. 14Siku kama hiyo haijawahi kuwako kamwe wala haijapata kuonekana tena, siku ambayo Mwenyezi-Mungu amemwitikia binadamu kwa namna hiyo; maana Mwenyezi-Mungu mwenyewe aliwapigania Waisraeli.
15Kisha Yoshua akarudi kambini huko Gilgali pamoja na Waisraeli wote.

Yoshua anawaua wafalme watano wa Waamori

16Wale wafalme watano walikimbia na kujificha katika pango la Makeda. 17Yoshua akapata habari kwamba wafalme hao wamegunduliwa walikojificha katika pango la Makeda. 18Yoshua akasema, “Vingirisheni mawe makubwa mlangoni mwa pango na kuweka walinzi hapo. 19Lakini nyinyi msikae huko, bali muwafuatie adui zenu. Muwapige kutoka upande wa nyuma, wala musiwaache waingie mijini mwao, maana Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, amewatia mikononi mwenu.” 20Yoshua pamoja na Waisraeli waliwapiga na kuwaangamiza wote, na wachache wao walionusurika walikimbilia kwenye miji yao yenye ngome. 21Baada ya hayo Waisraeli wote walirudi salama kwa Yoshua huko kambini Makeda; na hakuna tena mtu aliyethubutu kusema lolote dhidi ya Waisraeli.
22Kisha Yoshua akasema, “Fungueni mlango wa pango mniletee kutoka humo wale wafalme watano.” 23Wakafanya hivyo, wakamletea Yoshua wale wafalme watano: Mfalme wa Yerusalemu, mfalme wa Hebroni, mfalme wa Yarmuthi, mfalme wa Lakishi na mfalme wa Egloni. 24Wafalme hao walipoletwa, Yoshua akawaita Waisraeli wote na wakuu wa majeshi waliokwenda naye vitani, akawaambia, “Njoni karibu mwakanyage wafalme hawa shingoni mwao.” Nao wakasogea na kuwakanyaga shingoni. 25Yoshua akawaambia “Msiogope, wala msiwe na wasiwasi, muwe imara na hodari, maana hivi ndivyo Mwenyezi-Mungu atakavyowatendea adui zenu ambao mtapigana nao. Kwa hiyo, muwe imara na hodari.” 26Baadaye, Yoshua aliwanyonga kwa kuwaangika kwenye miti mitano ambako walitundikwa mpaka jioni. 27Wakati jua lilipokuwa karibu kutua, Yoshua aliamuru waondolewe juu ya miti walipokuwa wameangikwa na kutupwa pangoni walimokuwa wamejificha. Kisha wakaweka mawe makubwa kwenye mlango wa pango, nayo mawe hayo yako huko mpaka leo.

Yoshua anateka miji ya kusini

28Siku hiyo Yoshua alipouteka mji wa Makeda, alimuua mfalme wake na wakazi wake wote bila kumbakiza hata mtu mmoja. Alimtendea mfalme wa Makeda kama vile alivyomtendea mfalme wa Yeriko.
29Kutoka Makeda, Yoshua pamoja na Waisraeli wote walikwenda Libna wakaushambulia. 30Mwenyezi-Mungu akautia mji huo pamoja na mfalme wao mikononi mwa Waisraeli, wakawaua wakazi wake bila kumbakiza hata mtu mmoja. Walimtendea mfalme wa Libna kama walivyomtendea mfalme wa Yeriko.
31Kisha kutoka Libna Yoshua na Waisraeli wote walikwenda Lakishi, wakauzingira na kuushambulia. 32Naye Mwenyezi-Mungu akautia mji huo mikononi mwa Waisraeli, wakauteka mnamo siku ya pili. Waliwaua wakazi wote wa mji huo kama walivyofanya kule Libna.
33Hapo, mfalme Horamu wa Gerezi akaamua kuja kuwasaidia watu wa Lakishi. Lakini Yoshua alimuua pamoja na watu wake wote, hakumbakiza hata mtu mmoja.
34Kisha kutoka Lakishi, Yoshua na Waisraeli wote walikwenda mpaka Egloni, wakauzingira na kuushambulia. 35Wakauteka siku hiyohiyo na kuwaua wakazi wake wote kama walivyofanya kule Lakishi.
36Halafu kutoka Egloni Yoshua na Waisraeli wote wakaenda mpaka Hebroni, wakaushambulia 37na kuuteka. Wakawaua wakazi wake wote pamoja na mfalme wao; waliiharibu kabisa miji mingine iliyouzunguka, wakawaua wakazi wake wote kama walivyofanya kule Egloni.
38Kisha, Yoshua na Waisraeli wote wakarudi Debiri, wakaushambulia. 39Waliuteka mji huo na mfalme wake pamoja na miji mingine yote iliyouzunguka na kuwaangamiza wote waliokuwamo bila kumbakiza hata mtu mmoja. Waliutendea mji huo kama walivyoutendea mji wa Hebroni na mji wa Libna na wafalme wao.
40Basi, Yoshua aliiteka nchi yote; aliwashinda wafalme wa sehemu za milimani, eneo la Negebu, na sehemu za nchi tambarare na miteremko. Hakuacha chochote chenye uhai ila aliangamiza kila kitu kama Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, alivyoamuru. 41Yoshua aliwashinda watu wote kutoka Kadesh-barnea mpaka Gaza, na kutoka Gosheni mpaka Gibeoni. 42Aliweza kuitwaa nchi hii yote kwa sababu Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, aliwapigania Waisraeli. 43Basi, Yoshua akarudi mpaka kambini huko Gilgali pamoja na Waisraeli wote.


Yoshua 10;1-43

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

Friday 20 October 2017

Kikombe Cha Asubuhi ;Yoshua 9...



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?
Ni siku nyingine tena Mungu wetu ametuchagua na kutupa kibali
cha kuiona leo hii,Si kwamba tumetenda mema sana,wala si kwamba
sisi ni wazuri mno,wala si kwa nguvu/utashi wetu sisi kuwa hivi tulivyo
ni kwa neema/rehema zake Mungu wetu..

Tumshukuru Mungu wetu kwa yote aliyotutendea/anayoendelea kututendea..





Siku ya Pentekoste ilipofika, waumini wote walikuwa wamekusanyika mahali pamoja. Ghafla, sauti ikasikika kutoka angani; sauti iliyokuwa kama ya upepo mkali, ikaijaza ile nyumba yote walimokuwa wamekaa. Kisha, vikatokea vitu vilivyoonekana kama ndimi za moto, vikagawanyika na kutua juu ya kila mmoja wao. Wote wakajazwa Roho Mtakatifu, wakaanza kusema lugha mbalimbali kadiri Roho alivyowawezesha. Na huko Yerusalemu walikuwako Wayahudi, watu wamchao Mungu, waliotoka katika kila nchi duniani. Waliposikia sauti hiyo, kundi kubwa la watu lilikusanyika. Wote walishtuka sana kwani kila mmoja wao aliwasikia hao waumini wakisema kwa lugha yake mwenyewe. Walistaajabu na kushangaa wakisema, “Je, hawa wote tunaowasikia wakisema hivi, si wenyeji wa Galilaya? Imekuwaje, basi, kwamba kila mmoja wetu anawasikia wakisema kwa lugha yake mwenyewe? Baadhi yetu ni Waparthi, Wamedi na Waelamu; wengine ni wenyeji wa Mesopotamia, Yudea, Kapadokia, Ponto na Asia, Frugia na Pamfulia, Misri na sehemu za Libia karibu na Kurene; wengine wetu ni wageni kutoka Roma, Wayahudi na watu walioongokea dini ya Kiyahudi; wengine wametoka Krete na Arabia. Sisi sote tunasikia wakisema kwa lugha zetu wenyewe mambo makuu ya Mungu.” Wote walishangaa na kufadhaika huku wakiulizana, “Hii ina maana gani?” Lakini wengine wakawadhihaki wakisema, “Watu hawa wamelewa divai mpya!”
Asante Mungu Baba kwa wema na fadhili zako kwetu..
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote..
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kwakuwa tayari kwa majukumu yetu
Utukuzwe Mungu wetu,Uhimidiwe Baba wa Mbingu,Usifiwe ee Baba,
Uabudiwe Jehovah,Matendo yako ni makuu sana,Matendo yako ni ya ajabu,hakuna kama wewe Mungu wetu,Unatosha Mfalme wa Amani..





Lakini Petro alisimama pamoja na wale kumi na mmoja akaanza kuwahutubia watu kwa sauti kubwa: “Ndugu Wayahudi nanyi nyote mnaokaa hapa Yerusalemu, sikilizeni kwa makini maneno yangu. Watu hawa hawakulewa kama mnavyodhani; mbona ni saa tatu tu asubuhi? Ukweli ni kwamba jambo hili ni lile alilosema nabii Yoeli: ‘Katika siku zile za mwisho, asema Bwana, nitawamiminia binadamu wote Roho wangu. Watoto wenu wa kiume na wa kike watatoa unabii, vijana wenu wataona maono, na wazee wenu wataota ndoto. Naam, hata watumishi wangu wa kiume na kike, nitawamiminia Roho wangu siku zile, nao watatoa unabii. Nitatenda miujiza juu angani, na ishara chini duniani; kutakuwa na damu, moto na moshi mzito; jua litatiwa giza, na mwezi utakuwa mwekundu kama damu, kabla ya kutokea ile siku kuu na tukufu ya Bwana. Hapo, yeyote atakayeomba kwa jina la Bwana, ataokolewa.’ “Wananchi wa Israeli, sikilizeni maneno haya! Yesu wa Nazareti alikuwa mtu ambaye mamlaka yake ya kimungu yalithibitishwa kwenu kwa miujiza, maajabu na ishara Mungu alizofanya kati yenu kwa njia yake, kama mnavyojua. Kufuatana na mpango wake mwenyewe Mungu alikwisha amua kwamba Yesu angetiwa mikononi mwenu; nanyi mkamuua kwa kuwaachia watu wabaya wamsulubishe. Lakini Mungu alimfufua kutoka kwa wafu, akamwokoa katika maumivu ya kifo kwa maana haingewezekana kabisa kifo kimfunge. Maana Daudi alisema juu yake hivi: ‘Nilimwona Bwana mbele yangu daima; yuko nami upande wangu wa kulia hata sitatikisika. Kwa hiyo, moyo wangu ulifurahi; tena nilipiga vigelegele vya furaha. Mwili wangu utakaa katika tumaini, maana hutaiacha roho yangu kuzimu, wala kumruhusu mtakatifu wako aoze. Umenionesha njia za uhai, umenijaza furaha kwa kuwako kwako!’


Tazama jana imepita Mungu wetu leo ni siku mpya na kesho ni siku
nyingine Jehovah..!
Tunakuja mbele zako Baba wa Mbinguni tukijinyenyekeza,tukijishusha
na tukijiachilia mikononi mwako Yahweh..
Baba tunaomba utusamehe makosa yetu yote tuliyoyafanya
kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua..
Jehovah nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe
wale wote waliotukosea..
Yahweh tunaomba utuepushe katika majaribu Baba wa Mbinguni
utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote..
Mungu wetu tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu kwa Damu
ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti...





“Ndugu zangu, napenda kuwaambieni waziwazi juu ya mambo yaliyompata Daudi, babu yetu. Yeye alikufa, akazikwa, tena kaburi lake liko papa hapa petu mpaka leo. Lakini kwa vile Daudi alikuwa nabii, alijua kuwa Mungu alimwapia kiapo kwamba atamtawaza mmoja wa uzawa wake kuwa mfalme mahali pake. Daudi aliona kabla mambo yatakayofanywa na Mungu na hivyo akasema juu ya ufufuo wa Kristo wakati aliposema: ‘Hakuachwa kuzimu, mwili wake haukuoza.’ Basi, Mungu alimfufua huyo Yesu na sisi sote ni mashahidi wa tukio hilo. Yesu alipokwisha pandishwa na kuwekwa na Mungu upande wake wa kulia, akapokea kutoka kwake Baba yule Roho Mtakatifu ambaye alituahidi, ametumiminia huyo Roho. Hicho ndicho mnachoona sasa na kusikia. Maana Daudi mwenyewe, hakupanda mpaka mbinguni; ila yeye alisema: ‘Bwana alimwambia Bwana wangu: Keti upande wangu wa kulia, hadi niwafanye adui zako kiti cha miguu yako.’ “Watu wote wa Israeli wanapaswa kufahamu kwa hakika kwamba huyo Yesu mliyemsulubisha, ndiye huyo ambaye Mungu amemfanya kuwa Bwana na Kristo.” Basi, watu waliposikia hayo, walichomwa moyo, wakawauliza Petro na wale mitume wenzake: “Ndugu zetu, tufanye nini?” Petro akajibu, “Tubuni na kila mmoja wenu abatizwe kwa jina la Yesu Kristo ili mpate kuondolewa dhambi zenu na kupokea ile ahadi ya Roho Mtakatifu. Maana, ahadi ile ilikuwa kwa ajili yenu, kwa ajili ya watoto wenu, kwa ajili ya wote wanaokaa mbali na kwa ajili ya kila mtu ambaye Bwana Mungu wetu atamwita kwake.” Kwa maneno mengine mengi, Petro alisisitiza na kuwahimiza watu akisema, “Jiokoeni katika kizazi hiki kiovu.” Wengi waliyakubali maneno yake, wakabatizwa. Watu wapatao 3,000 wakaongezeka katika kile kikundi siku hiyo. Hawa wote waliendelea kujifunza kutoka kwa mitume, kuishi pamoja kindugu, kumega mkate na kusali.


Yahweh tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Mungu wetu vyote tunavyoenda kufanya/kutenda na tukatende
sawasawa na mapenzi yako..
Mungu wetu tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Yahweh nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwabariki wengine..
Jehovah tusipungukiwe katika mahitaji yetu Baba wa Mbinguni ukatupe
sawasawa na mapenzi yako..

Mfalme wa Amani tunaomba amani yako ikatawale Nyumba/ndoa zetu
watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka..
Baba wa Mbingu uwepo wako uwe nasi,Baraka na furaha zitufuate,
utu wema na fadhili,unyenyekevu ,busara,hekima na upole kiasi
viwe nasi, huruma,kusaidia na kuonyana kwa upendo..
ukatupe neema ya kufuata njia zako,tukasimamie Neno lako
Amri na sheria zako siku zote za maisha yetu..
ukatufanye chombo chema nasi tukatumike kama inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi..





Miujiza na maajabu mengi yalifanyika kwa njia ya mitume hata kila mtu akajawa na hofu. Waumini wote waliendelea kuwa kitu kimoja na mali zao waligawiana. Walikuwa wakiuza mali na vitu vyao kisha wakagawana fedha kadiri ya mahitaji ya kila mmoja. Waliendelea kukutana pamoja kila siku hekaluni. Lakini wakati wa kumega mkate, walikutana katika nyumba zao na wakakishiriki chakula hicho kwa furaha na moyo mkunjufu. Walimtukuza Mungu, wakapendwa na watu wote. Kila siku Bwana aliwaongezea idadi ya watu waliokuwa wakiokolewa.
Baba wa Mbinguni tunawaweka mikononi mwako wote
wenye shida/tabu,wagonjwa,wenye njaa,wanaopitia magumu/majaribu
mbalimbali,waliokatika vifungo vya yule mwovu,walioanguka/potea
Mungu wetu tunaomba uwasamehe wale wote waliokwenda kinyume nawe
ukawaponye kimwili na kiroho,ukapokee maombi/sala za watoto wako
ukasikie kulia kwao na ukawafute machozi yao,ukawape neema ya kujiombea na kukutafuta wewe,Nuru/mwanga ukaangaze tena kwenye maisha yao,Imani yao kwako ikawaponye na kuwaweka huru..
Amani ya moyo,furaha na baraka ziwe nao..
ee Baba ukapokee sala/maombi yetu..
Tunakushukuru na kukusifu Daima..
tukiamini wewe ni Mungu wetu,Mungu wetu si kipofu unaona,Mungu wetu si kiziwi unasikia,Mungu wetu si bubu Unajibu na kutenda kama
inavyokupendeza wewe..


Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina..!!



Asanteni sana wapendwa katika Bwana kwa kuwa nami
Mungu muweza wa yote awe nanyi daima..
Amani ya Kristo iwe nanyi wakati wote..
Nawapenda.

Agano na watu wa Gibeoni

1Wafalme wote waliokuwa ngambo ya mto Yordani katika nchi ya milimani na kwenye tambarare na eneo lote la pwani ya bahari ya Mediteranea kuelekea Lebanoni, Wahiti, Waamori, Wakanaani, Waperizi, Wahivi na Wayebusi, waliposikia habari za Waisraeli, 2wakakusanyika pamoja kwa nia moja ili kupigana vita na Yoshua na Waisraeli.
3Lakini wakazi wa Gibeoni walipopata habari juu ya jinsi Yoshua alivyoitenda miji ya Yeriko na Ai, 4waliamua kutumia hila. Wakatayarisha vyakula, wakapakiza magunia yaliyochakaa juu ya punda wao, viriba vilivyochakaa na kushonwa; 5wakavaa viatu, nguo zilizochakaa na vyakula vyao vyote vilikuwa vikavu vilivyoota ukungu. 6Basi, wakamwendea Yoshua kambini Gilgali, wakamwambia yeye na Waisraeli, “Sisi tumetoka nchi ya mbali; tafadhali tunaomba mfanye agano nasi.”
7 Taz Kut 23:32; 34:12, Kumb 7:2 Lakini Waisraeli wakawajibu hao Wahivi, “Tunawezaje kufanya agano nanyi? Labda nyinyi mnaishi karibu nasi.” 8Nao wakamwambia Yoshua, “Sisi tu watumishi wako.” Naye Yoshua akawauliza, “Nyinyi ni akina nani, na mnatoka wapi?” 9Wakamjibu, “Sisi, watumishi wako, tumetoka nchi ya mbali na tumekuja kwa maana tumesikia sifa za jina la Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu; tulipata habari za umaarufu wake na yote aliyoyafanya nchini Misri. 10Taz Hes 21:21-35 Tumesikia yote aliyowatenda wafalme wawili wa Waamori waliokuwa ngambo ya mto Yordani, mfalme Sihoni wa Heshboni na mfalme Ogu wa Bashani aliyekaa huko Ashtarothi. 11Ndipo wazee wetu na wananchi wote wa nchi yetu, wakatuambia, tuchukue posho ya safari, tuje kukutana nanyi na kuwaambia kwamba sisi ni watumishi wenu; tafadhali fanyeni agano nasi. 12Tazama mikate yetu ambayo ilikuwa bado moto tulipoichukua wakati tulipoondoka kwetu, lakini sasa imekauka na kuota ukungu. 13Viriba hivi tulivijaza maji vikiwa vipya, lakini sasa vimepasukapasuka. Hata mavazi na viatu vyetu vimechakaa, kwani safari ilikuwa ndefu sana.”
14Hivyo, Waisraeli wakachukua vyakula vyao, bila ya kumwuliza shauri Mwenyezi-Mungu. 15Yoshua akafanya nao mkataba wa amani; akafanya agano kwamba atawaruhusu kuishi. Viongozi wa jumuiya ya Israeli wakawaapia kutekeleza mapatano hayo.
16Siku tatu baada ya kufanya agano nao, Waisraeli wakagundua kwamba watu hao walikuwa jirani zao na waliishi miongoni mwao. 17Basi, Waisraeli wakafunga safari, baada ya siku ya tatu wakafika katika miji yao. Miji hiyo ilikuwa Gibeoni, Kefira, Beerothi na Kiriath-yearimu. 18Lakini Waisraeli hawakuwaua, maana viongozi wa jumuiya ya Israeli walikuwa wamewaapia kwa jina la Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli. Hivyo basi, jumuiya yote ikawanungunikia viongozi wao. 19Lakini viongozi wa Waisraeli wakaiambia jumuiya ya watu wao, “Kwa vile tumewaapia kwa jina la Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, sasa hatuwezi kuwadhuru. 20Tutawaacha waishi, ili tusije tukaadhibiwa kwa sababu ya kiapo tulichokula. 21Waacheni waishi.” Hivyo Wagibeoni wakawa wanaitumikia jamii nzima ya Israeli, wakiwakatia kuni na kuwachotea maji, kama viongozi wa Waisraeli walivyosema.
22Yoshua akawaita Wagibeoni na kuwauliza, “Kwa nini mlitudanganya kwamba mlitoka nchi ya mbali na hali nyinyi mnaishi miongoni mwetu? 23Sasa, nyinyi mmelaaniwa na baadhi yenu daima mtakuwa watumwa wa kukata kuni na kuchota maji kwa ajili ya nyumba ya Mungu wangu.”
24Wakamjibu Yoshua, “Tuliambiwa kwamba kwa hakika Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, alimwamuru mtumishi wake Mose awaangamize wakazi wote wa nchi hii na kuwapa nyinyi nchi hii iwe mali yenu. Kwa hivyo, tulihofia maisha yetu na ndipo tukafanya jambo hili. 25Sasa sisi tumo mikononi mwako, ututendee kama unavyoona inafaa.” 26Basi, alilowatendea ni kuwaokoa mikononi mwa Waisraeli ili wasiangamizwe; hivyo hawakuwaua. 27Lakini kutoka siku hiyo, Yoshua aliwafanya hao kuwa wakata-kuni na wachota-maji kwa ajili ya jumuiya nzima ya Waisraeli na kwa ajili ya madhabahu ya Mwenyezi-Mungu, popote pale Mwenyezi-Mungu alipochagua mpaka hivi leo.



Yoshua 9;1-27

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

Thursday 19 October 2017

Kikombe Cha Asubuhi ;Yoshua 8...



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Haleluyah..!!Mungu wetu yu mwema sana.

Tumshukuru Mungu wetu katika yote..!
Mungu wetu Baba yetu,Muumba wetu,Muumba wa Mbingu na Nchi..
Muumba wa Vyote vilivyomo,Muumba wa vyote vinavyoonekana
 na visivyo onekana..
Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo,Mungu mwenye huruma..
Baba wa upendo,Baba wa faraja,Baba wa baraka,Baba wa Yatima..
Mume wa wajane,Mungu mwenye nguvu,Mungu mwenye uponyaji..
Muweza wa yote,Alfa na Omega,Hakuna kama wewe,Unatosha Mungu wetu
Utukuzwe Yahweh,Unastahili sifa,Unastahili kuabudiwa,Unastahili kuhimidiwa,Unastahili kuheshimiwa,Unastahili ee Baba....!


“Wastahili ee Bwana na Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu. Maana wewe uliumba vitu vyote, na kwa matakwa yako viliumbwa na vipo.”

Asante Mungu wetu kwa wema na fadhili zako kwetu..
Asante kwa ulinzi wako wakati wote..
Asante kwakutuchagua tena  na kutupa kibali cha kuendelea kuiona
leo hii..
Asante kwa afya,uzima/pumzi na tukiwa tayari kuendelea na majukumu yetu..

Mungu wetu tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha
na kujiachilia mikononi mwako  Jehovah..
Baba wa Mbinguni tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizozifanya
kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua..
Yahweh nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe
wale wote waliotukosea..



Enyi Waisraeli, mrudieni Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu. Mmejikwaa kwa sababu ya uovu wenu. Ombeni toba kwake, mrudieni na kumwambia: “Utusamehe uovu wote, upokee zawadi zetu, nasi tutakusifu kwa moyo. Ashuru haitatuokoa, hatutategemea tena farasi wa vita. Hatutaviita tena: ‘Mungu wetu’ hivyo vinyago tulivyochonga wenyewe. Kwako ee Mungu yatima hupata huruma.” Mwenyezi-Mungu asema, “Nitaponya utovu wao wa uaminifu; nitawapenda tena kwa hiari yangu, maana sitawakasirikia tena. Nitakuwa kama umande kwa Waisraeli nao watachanua kama yungiyungi, watakuwa na mizizi kama mwerezi wa Lebanoni. Chipukizi zao zitatanda na kuenea, uzuri wao utakuwa kama mizeituni, harufu yao nzuri kama maua ya Lebanoni. Watarudi na kuishi chini ya ulinzi wangu, watastawi kama bustani nzuri. Watachanua kama mzabibu, harufu yao nzuri kama ya divai ya Lebanoni. Enyi watu wa Efraimu, mna haja gani tena na sanamu? Mimi ndiye ninayesikiliza sala zenu, mimi ndiye ninayewatunzeni. Mimi nitawapa kivuli kama mberoshi, kutoka kwangu mtapata matunda yenu. Yeyote aliye na hekima ayaelewe mambo haya, mtu aliye na busara ayatambue. Maana njia za Mwenyezi-Mungu ni nyofu; watu wanyofu huzifuata, lakini wakosefu hujikwaa humo.”

Baba wa Mbinguni tunaomba utuepushe katika majaribu na utuokoe
na yule mwovu na kazi zake zote..
Yahweh tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu
Baba utufunike kwa damu ya Bwana wetu Yesu Kristo wa Nazareti


Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Yahweh tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji..


“Jihadharini msije mkafanya matendo yenu mema mbele ya watu kusudi mwonekane nao. La sivyo, Baba yenu aliye mbinguni hatawapeni tuzo. “Basi, unapomsaidia maskini, usijitangaze. Usifanye kama wanafiki wafanyavyo katika masunagogi na njiani ili watu wawasifu. Kweli nawaambieni, hao wamekwisha pata tuzo lao. Lakini wewe unapomsaidia maskini, fanya hivyo kwamba hata mwandani wako asijue ufanyalo. Toa msaada wako kwa siri, na Baba yako aonaye yaliyofichika, atakutuza.

Jehovah tunayakabidhi maisha yetu mikononi mwako..
Yahweh ukabariki Nyumba/ndoa zetu,watoto,wazazi wetu
familia/ndugu na wote wanaotuzunguka Mungu wetu tunaomba
Amani yako ikatawale,upendo wetu ukadumu,furaha na umoja ukawe
nasi,ukatupe neema ya kusimamia Neno lako Amri na Sheria zako
siku zote za maisha yetu.Tukawe na kiu/shauku ya kukutafuta Mungu
na kujifunza zaidi wema na fadhili zako,ukatupe macho ya kuona
na masikio ya kusikia sauti yako,tukanene yaliyo yako..
tukapate kutambua/kujitambua,tukasamehe na kusaidiana
tukaelimishane na kuelekezana kwa upendo na amani..
Ukatufanye chombo chema nasi tukatumike kama inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi..


Yesu alipokuwa akiongea, Mfarisayo mmoja alimkaribisha chakula nyumbani kwake, naye akaenda, akaketi kula chakula. Huyo Mfarisayo alistaajabu kuona kwamba alikula chakula bila kunawa kwanza. Bwana akamwambia, “Nyinyi Mafarisayo huosha kikombe na sahani kwa nje, lakini ndani mmejaa udhalimu na uovu. Wapumbavu nyinyi! Je, aliyetengeneza nje si ndiye aliyetengeneza ndani pia? Toeni kwa maskini vile vitu vilivyomo ndani, na vingine vyote vitakuwa halali kwenu. “Lakini ole wenu Mafarisayo, kwa sababu mnatoza watu zaka hata juu ya majani ya kukolezea chakula, mchicha na majani mengine, na huku hamjali juu ya haki na upendo kwa Mungu. Mambo haya iliwapasa muwe mmeyazingatia bila kuyasahau yale mengine. “Ole wenu nyinyi Mafarisayo, kwa sababu mnapenda kuketi mbele mahali pa heshima katika masunagogi, na kusalimiwa kwa heshima hadharani. Ole wenu, kwa sababu mko kama makaburi yaliyofichika; watu hutembea juu yake bila kufahamu.”

Mungu wetu ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu na ukawaponye
wote wanaotaabika,wagonjwa,waliokatika vifungo mbalimbali
waliokata tamaa Mungu wakapate tumaini,ukawape neema ya kujiombea
Mungu wetu ukawainue walioanguka,ukapokee sala/maombi yao..
Sifa na utukufu tunakurudishia Mungu wetu..

Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina..!

Wapendwa katika Bwana asanteni sana kwakuwa nami
Sina neno zuri la kusema zaidi ya kuwaombea Baraka,
Amani na yote yaliyomema yasiwapite..
Mungu aendelee kuwatunza na pendo lenu Imani yenu ikadumu
  tumshukuru Mungu kwa kila jambo..
Nawapenda.

Mji wa Ai unatekwa

1Mwenyezi-Mungu akamwambia Yoshua, “Usiogope, wala usiwe na wasiwasi wowote; wachukue wanajeshi wako wote uelekee mji wa Ai, kwani mfalme wa Ai nimemtia mikononi mwako, pamoja na watu wake, mji wake na nchi yake. 2Mtautendea mji wa Ai pamoja na mfalme wake kama vile mlivyoutendea mji wa Yeriko pamoja na mfalme wake. Mali zake pamoja na mifugo yake mtakayoteka itakuwa ni mali yenu. Nendeni mwuvamie mji kutoka upande wa nyuma.”
3Basi, Yoshua akaondoka, pamoja na wanajeshi wake wote kwenda Ai. Akawachagua watu hodari 30,000 na kuwaambia watangulie wakati wa usiku. 4Akawaamuru hivi: “Nyinyi mtauvizia mji kutoka upande wa nyuma. Msiende mbali na mji, bali muwe tayari wakati wote. 5Mimi, pamoja na watu wote walio pamoja nami, tutaukaribia mji. Watu watakapotoka nje kuja kutukabili kama hapo awali, sisi tutawakimbia. 6Nao wataendelea kutufuatia mpaka wawe mbali na mji wao, maana watafikiri wametutimua kama walivyofanya hapo awali. Sisi tutawaacha watufukuze. 7Hapo, nyinyi mtatokea kutoka huko mlikokuwa mnavizia na kuuteka mji, maana Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, atautia mji huo mikononi mwenu. 8Mkishauteka mji mtauteketeza kwa moto, kama vile Mwenyezi-Mungu alivyoamuru. Hayo ndiyo maagizo mtakayofuata.” 9Basi, Yoshua akawaambia waende mahali pao pa kuvizia; nao wakajiweka magharibi ya mji wa Ai kati ya mji wa Ai na Betheli. Lakini Yoshua alilala usiku huo katika kambi ya Waisraeli.
10Yoshua akaamka asubuhi na mapema, akawakusanya Waisraeli na kuelekea mjini Ai, akiwa pamoja na wazee. 11Wanajeshi wote waliofuatana naye walikaribia mji na kupiga kambi kaskazini yake, ngambo ya bonde mkabala wa mji wa Ai. 12Ndipo akachukua watu wengine 5,000 na kuwaweka wavizie kati ya mji wa Betheli na Ai, magharibi ya mji wa Ai. 13Kikosi kikubwa kiliwekwa kaskazini mwa mji na wale waliobaki waliwekwa magharibi ya mji. Lakini usiku huo, Yoshua akalala bondeni.
14Mfalme wa mji wa Ai alipoona hivyo, aliharakisha na kwenda kwenye mteremko wa kuelekea Araba ili akabiliane na Waisraeli vitani. Lakini hakujua kwamba mji wake ulikuwa umeviziwa kutoka nyuma. 15Kisha Yoshua pamoja na watu wake wakajifanya kana kwamba wanashindwa, wakaanza kukimbia kuelekea jangwani. 16Watu wote waliokuwa mjini waliitwa wawafuatie Waisraeli; na walipokuwa wanamfuatia Yoshua, walitoka na kwenda mbali na mji wao. 17Hakuna mtu yeyote aliyebaki mjini Ai,8:17 Ai: Kigiriki. Kiebrania: Ai na Betheli. waliuacha mji huo wazi wakaenda kuwafuatia Waisraeli.
18Halafu Mwenyezi-Mungu akamwambia Yoshua, “Elekeza mkuki wako huko mjini Ai maana nitautia mji huo mikononi mwako.” Yoshua akaelekeza mkuki wake mjini Ai. 19Mara Yoshua alipouelekeza mkuki wake kule Ai, kikosi kilichokuwa kikivizia upande mwingine kikatoka na kuingia mjini; kikauteka mji na kuuteketeza kwa moto. 20Watu wa Ai walipotazama nyuma, wakaona moshi kutoka mjini ukipanda mpaka mbinguni. Nao hawakuwa na uwezo wa kukimbia upande wowote, maana Waisraeli waliwageukia hao waliokuwa wanawafuatia. 21Yoshua na Waisraeli wote walipoona kuwa kikosi kilichokuwa kinavizia kimeuteka mji, na kwamba moshi ulikuwa unapanda juu, waliwageukia na kuanza kuwaua. 22Watu waliobaki mjini walitoka, lakini wote wakawa wamezingirwa na Waisraeli; nao wakauawa, asibaki hata mmoja wao. 23Lakini mfalme wa mji wa Ai walimteka akiwa hai na kumpeleka kwa Yoshua.
24Waisraeli walipomaliza kabisa kuwaua watu wote wa Ai huko nyikani ambako waliwafuatia wakarudi mjini Ai na kuwaua wote waliosalia humo. 25Jumla ya watu wa Ai waliouawa siku hiyo, wanaume kwa wanawake, walikuwa 12,000. 26Yoshua hakuushusha mkono wake aliokuwa ameushikilia mkuki wake kuelekea Ai mpaka alipowaua wakazi wote wa mji huo. 27Waisraeli waliteka tu wanyama na mali kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Yoshua. 28Basi, Yoshua aliuteketeza mji wa Ai kwa moto na kuufanya magofu hadi hivi leo. 29Kisha akamtundika mfalme wa Ai mtini mpaka jioni. Lakini jua lilipoanza kutua, Yoshua aliamuru maiti yake iondolewe mtini na kutupwa kwenye lango la mji kisha warundike rundo kubwa la mawe juu ya maiti hiyo; rundo hilo liko huko mpaka leo.

Sheria inasomwa mlimani Ebali

30 Taz Kumb 27:2-8 Kisha, Yoshua akamjengea Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, madhabahu mlimani Ebali, 31Taz Kut 20:25 kama Mose mtumishi wa Mwenyezi-Mungu alivyowaagiza Waisraeli, kadiri ilivyoandikwa katika kitabu cha sheria ya Mose kwamba itakuwa madhabahu iliyojengwa kwa mawe ambayo hayakuchongwa, wala kuguswa na chombo chochote cha chuma. Juu ya madhabahu hiyo walimtolea Mwenyezi-Mungu tambiko za kuteketezwa na sadaka za amani. 32Na huko, mbele ya umati wote wa Waisraeli, Yoshua aliandika nakala ya sheria ya Mose juu ya mawe. 33Taz Kumb 11:29; 27:11-14 Waisraeli wote pamoja na viongozi wao, wazee na waamuzi na wageni wote waliokuwa kati yao, wakasimama kila upande mkabala na sanduku la agano mbele ya makuhani Walawi waliokuwa wamelibeba sanduku la agano la Mwenyezi-Mungu. Nusu yao wakasimama mbele ya mlima Gerizimu na nusu nyingine wakasimama mbele ya mlima Ebali, kama vile Mose, mtumishi wa Mwenyezi-Mungu, alivyoagiza hapo awali kuhusu kubarikiwa kwa Waisraeli. 34Kisha, Yoshua akawasomea sheria zote, pamoja na baraka na laana kama ilivyoandikwa katika kitabu cha sheria. 35Hakuna neno lililoamriwa na Mose ambalo Yoshua hakulisoma mbele ya umati wa Waisraeli, wakiwemo miongoni mwao wanawake, watoto na wageni.


Yoshua 8;1-35

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

Wednesday 18 October 2017

Kikombe Cha Asubuhi ;Yoshua 7...




Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu kwa mema mengi 

aliyotutendea/anayoendelea kututendea..
Mungu wetu ,Baba yetu,Muumba wetu,Muumba wa Mbingu na Nchi..
Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo,Mungu mwenye huruma..
wewe ndiye Ndimi Mwenyezi-Mungu  Mungu wa wote wenye mwili
hakuna jambo lolote lililogumu linaloweza kukushinda Mungu wetu..
Utukuzwe Mungu wetu,Usifiwe Baba wa Mbingu,Uhimidiwe Jehovah
Uabudiwe Yahweh,Hakuna kama wewe Mungu wetu,Matendo yako
ni ya ajabu mno,Matendo yako ni makuu sana,Unatosha Baba wa Mbinguni


Mungu ni kimbilio letu na nguvu yetu; yeye ni msaada wetu daima wakati wa taabu. Kwa hiyo hatutaogopa chochote, dunia ijapoyeyuka na milima kutikisika kutoka baharini; hata kama bahari ikichafuka na kutisha, na milima ikatetemeka kwa machafuko yake. Kuna mto ambao maji yake hufurahisha mji wa Mungu, makao matakatifu ya Mungu Mkuu. Mungu yumo mjini humo, nao hauwezi kutikiswa; Mungu ataupa msaada alfajiri na mapema. Mataifa yaghadhibika na tawala zatikisika; Mungu anguruma nayo dunia yayeyuka. Mwenyezi-Mungu wa majeshi yu pamoja nasi, Mungu wa Yakobo ni kimbilio letu. Njoni mwone matendo ya Mwenyezi-Mungu; oneni maajabu aliyoyafanya duniani. Hukomesha vita popote duniani, huvunjavunja pinde na mikuki, nazo ngao huziteketeza. Asema: “Nyamazeni na kujua kuwa mimi ni Mungu! Mimi natukuka katika mataifa yote; mimi natukuzwa ulimwenguni kote!” Mwenyezi-Mungu wa majeshi yu pamoja nasi, Mungu wa Yakobo ni kimbilio letu.

Asante Mungu wetu Baba yetu kwa wema na fadhili zako kwetu

Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote..
Asante kwakutuchagua tena na kutupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii Mungu wetu..


Mwenyezi-Mungu asipoijenga nyumba, waijengao wanajisumbua bure. Mwenyezi-Mungu asipoulinda mji, waulindao wanakesha bure. Mnajisumbua bure kuamka mapema asubuhi na kuchelewa kwenda kupumzika jioni, mjipatie chakula kwa jasho lenu. Mungu huwaruzuku walio wake hata walalapo.
Tazama Jana imepita Jehovah Leo ni siku mpya Yahweh
na Kesho ni siku nyingine Mungu wetu..
Baba wa Mbinguni tukakuja mbele zako tukijinyenyekeza tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako..
Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizozifanya kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua..
Mungu wetu nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe
wale wote waliotukosea..
Baba wa Mbinguni tunaomba utuepushe katika majaribu na 
utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote..
Mungu wetu tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu
Baba tunaomba utufunike kwa Damu ya Bwana wetu
Yesu Kristo wa Nazareti,yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona..

Yahweh tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu,Biashara,masomo

na vyote tunavyoenda kufanya/kutenda Mungu wetu tukatende
sawasawa na mapenzi yako...
Mungu wetu tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Yahweh nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwabariki
wenye kuhitaji..
Mungu wetu tusipungukiwe katika mahitaji yetu Baba ukatupe 
sawasawa na mapenzi yako..

Mfalme wa Amani tunaomba amani yako ikatawale katika Nyumba/ndoa zetu,watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanotuzunguka..

Mungu wetu tunaomba ukatupe neema ya hekima,busara,kutambua/kujitambu katika yote,tukanene yaliyo yako tukachukuliane,tukapendane na pendo letu likawe la kweli nasi  kwa unafiki,tukaonyane na kuelemishana kwa upendo,tukasameheane,tukawe wanyeyekevu kwa watu wote,na Mungu wetu ukaonekane popote tupitapo/tuendapo,tukasimamie Neno lako Amri na Sheria zako siku zote za maisha yetu..
Ukatufanye chombo chema nasi tukatumike kama inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi..


Heri wote wamchao Mwenyezi-Mungu, wanaoishi kufuatana na amri zake. Utapata matunda ya jasho lako, utafurahi na kupata fanaka. Mkeo atakuwa kama mzabibu wa matunda mengi nyumbani mwako; watoto wako kama chipukizi za mzeituni kuzunguka meza yako. Naam, ndivyo atakavyobarikiwa mtu amchaye Mwenyezi-Mungu. Mwenyezi-Mungu akubariki kutoka Siyoni! Uione fanaka ya Yerusalemu, siku zote za maisha yako. Uishi na hata uwaone wajukuu zako! Amani iwe na Israeli!

Mungu wetu ukawakuguse na mkono wako wenye nguvu wote 

wenye shida/tabu,wagonjwa,wenye njaa,waliokatika vifungo
vya yule mwovu,wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali..
Yahweh ukawaponye kimwili na kiroho pia,Baba ukawasimamishe
wale wote walioanguka,Mungu wetu ukawasamehe wale wote
waliokwenda kinyume nawe,Mungu wetu ukawape neema ya kujiombea
Baba ukapokee sala/maombi ya watoto wako wote wakuombao
kwa imani na wafiwa ukawape nguvu,uvumilivu ,Baba ukawafariji..


Ee Mwenyezi-Mungu, sina moyo wa kiburi; mimi si mtu wa majivuno. Sijishughulishi na mambo makuu, au yaliyo ya ajabu mno kwangu. Ila nafsi yangu imetulia na kuwa na amani, kama mtoto mchanga alivyotulia na mama yake; ndivyo nafsi yangu ilivyo tulivu. Ee Israeli, umtumainie Mwenyezi-Mungu, tangu sasa na hata milele.
Asante Mungu wetu sifa na utukufu tunakurudishia wewe
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina..!!
Asanteni sana wapendwa kwa kuwa nami
UPendo Wenu Ukadumu Daima..
Mungu wetu aendelee kuwabariki na kuwatendea katika yote
Baraka,Amani na furaha viwe nanyi daima..
Nawapenda.



Kosa na adhabu ya Akani

1Lakini Waisraeli hawakuwa waaminifu kuhusu vile vitu vilivyotolewa viangamizwe kwani Akani mwana wa Karmi, mwana wa Zabdi, mwana wa Zera, wa kabila la Yuda, alichukua baadhi ya vitu vilivyoamriwa viteketezwe. Kwa hiyo hasira ya Mwenyezi-Mungu ikawaka dhidi ya Waisraeli.
2Yoshua akawatuma watu kutoka Yeriko kwenda mji wa Ai, ulio karibu ya Beth-aveni, mashariki ya Betheli, akawaambia, “Nendeni mkaipeleleze nchi.” Nao wakaenda na kuupeleleza mji wa Ai. 3Waliporudi, wakamwambia Yoshua, “Hakuna haja kupeleka watu wote kuushambulia mji wa Ai, maana wakazi wake ni wachache tu. Watu elfu mbili au tatu watatosha.” 4Basi, watu kama elfu tatu hivi wakaenda kuushambulia mji wa Ai, lakini wakakimbizwa na wakazi wa mji huo. 5Watu wa Ai wakawaua Waisraeli thelathini na sita na kuwafukuza wengine kutoka lango la mji mpaka Shebarimu, wakawaua kwenye mteremko. Waisraeli wakafa moyo na kulegea kama maji.
6Yoshua akayararua mavazi yake, yeye pamoja na wazee wa Israeli. Wakajitupa chini mbele ya sanduku la Mwenyezi-Mungu mpaka jioni; wakajitia mavumbi vichwani mwao. 7Yoshua akasema, “Ole wetu, ee Bwana Mungu! Kwa nini umetuvusha mto Yordani ili kututia mikononi mwa Waamori watuangamize? Tungaliridhika kubaki ngambo ya mto Yordani! 8Ee Bwana, niseme nini hali Waisraeli wamewakimbia adui zao? 9Basi, Wakanaani pamoja na wakazi wote wa nchi hii watakapopata habari hiyo watatuzingira na kutufuta kabisa duniani. Sasa utafanya nini kuonesha ukuu wa jina lako?”
10Mwenyezi-Mungu akamwambia Yoshua, “Simama! Mbona umejitupa chini hivyo? 11Waisraeli wametenda dhambi, maana wamelivunja agano langu nililowaamuru washike; wamevichukua baadhi ya vitu vilivyowekwa wakfu viangamizwe; wameviiba na kudanganya, wakaviweka pamoja na vitu vyao. 12Kwa hiyo Waisraeli hawawezi kuwakabili maadui zao; wanawakimbia adui zao kwa sababu wamejifanya wenyewe kuwa kitu cha kuangamizwa! Sitakuwa pamoja nao tena msipoharibu vitu vilivyomo kati yenu vilivyotolewa viangamizwe. 13Basi, inuka uwatakase watu, waambie wajitakase na kujitayarisha kwa siku ya kesho, maana mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, nasema hivi: ‘Miongoni mwenu kuna vitu vilivyotolewa viangamizwe; hamwezi kuwakabili adui zenu mpaka vitu hivyo vimeondolewa kati yenu! 14Kwa hiyo kesho asubuhi wote mtakuja mbele yangu, kabila baada ya kabila. Kabila nitakalolichagua litakwenda mbele, ukoo baada ya ukoo. Ukoo nitakaouchagua utakwenda mbele, jamaa baada ya jamaa. Na jamaa nitakayoichagua itakwenda mbele, mtu mmojammoja. 15Mtu yeyote atakayepatikana akiwa na vitu vilivyotolewa viangamizwe atateketezwa kwa moto, yeye pamoja na kila kitu chake maana ameliasi agano langu mimi Mwenyezi-Mungu, akatenda jambo la aibu katika Israeli.’”
16Basi, Yoshua akaamka asubuhi na mapema, akawaleta Waisraeli wote karibu, kabila baada ya kabila; kabila la Yuda likachaguliwa. 17Akazileta karibu koo za Yuda, ukoo baada ya ukoo; na ukoo wa Zerahi ukachaguliwa. Akazileta karibu jamaa za ukoo wa Zerahi, jamaa baada ya jamaa; na jamaa ya Zabdi ikachaguliwa. 18Yoshua akaileta jamaa ya Zabdi karibu, nyumba baada ya nyumba; na nyumba ya Akani mwana wa Karmi, mwana wa Zabdi, mwana wa Zera, wa kabila la Yuda, ikachaguliwa. 19Yoshua akamwambia Akani, “Mwanangu, mtukuze Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, msifu na kisha uniambie yale uliyotenda, wala usinifiche.” 20Akani akamjibu; “Ni kweli nimetenda dhambi mbele ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli. Na hivi ndivyo nilivyofanya: 21Nilipoona vazi moja zuri kutoka Shinari kati ya nyara, shekeli 200 za fedha na mchi wa dhahabu wenye uzito wa shekeli 50, nikavitamani na kuvichukua; nimevificha ardhini ndani ya hema langu; na fedha iko chini ya vitu hivyo.”
22Basi, Yoshua akawatuma wajumbe, nao wakakimbia hemani kwa Akani. Na kumbe, vilikuwa vimefichwa hemani na fedha ikiwa chini yake. 23Wakavichukua hemani na kuvipeleka kwa Yoshua na watu wote wa Israeli; nao wakaviweka chini, mbele ya Mwenyezi-Mungu. 24Yoshua pamoja na Waisraeli wote, wakamchukua Akani, mwana wa Zera, pamoja na fedha, vazi, dhahabu, watoto wake wa kiume na binti zake, ng'ombe, punda na kondoo wake, hema lake na kila kitu alichokuwa nacho na kuwapeleka kwenye bonde la Akori. 25Yoshua akamwuliza Akani, “Kwa nini umetuletea taabu? Mwenyezi-Mungu atakuletea taabu wewe mwenyewe leo.” Waisraeli wote wakampiga Akani kwa mawe mpaka akafa. Kisha wakawapiga jamaa yake yote kwa mawe mpaka wakafa, wakawateketeza wote kwa moto. 26Halafu wakarundika mawe mengi juu yake, ambayo yako hadi leo. Hapo hasira ya Mwenyezi-Mungu ikapoa; na mahali hapo pakaitwa Bonde la Akori7:26 Akori: Maana yake “taabu”. mpaka hivi leo.


Yoshua 7;1-26

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.