Tuesday 20 June 2017
Kikombe Cha Asubuhi;Mambo Ya Walawi..18...
Matendo maovu ya ndoa
1Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose, 2“Waambie watu wa Israeli hivi: Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu. 3Kamwe msifanye kama wafanyavyo watu wa nchi ya Misri ambako mlikaa; wala msifanye kama wafanyavyo watu wa nchi ya Kanaani ambako nawapeleka. Kamwe msifuate mitindo yao. 4Nyinyi mtafuata maagizo yangu na kuyashika masharti yangu. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu. 5#Taz Neh 9:29; Eze 18:9; 20:11-13; Luka 10:28; Roma 10:5; Gal 3:12 Kwa hiyo, ili mtu apate kuyaokoa maisha, mnapaswa kuyashika masharti yangu na maagizo yangu. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.
6“Mtu yeyote wa Israeli haruhusiwi kumkaribia mtu wa jamaa yake wa karibu ili kulala naye. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu. 7Kamwe usimvunjie heshima baba yako kwa kulala na mama yako aliyekuzaa. Usimwaibishe; yeye ni mama yako. 8Kamwe usimvunjie heshima baba yako kwa kulala na mmoja wa wake zake. Hao ni mama zako. 9Kamwe usilale na dada yako, awe ni dada yako halisi au dada yako wa kambo. 10Kamwe usilale na mjukuu wako, mtoto wa mwanao au binti yako; maana sehemu zao za siri ni kama zako mwenyewe. 11Kamwe usilale na msichana aliyezaliwa na mama yako wa kambo aliyeolewa na baba yako; msichana huyo ni dada yako. 12Kamwe usilale na shangazi yako; kwani huyo ni dada wa baba yako. 13Kamwe usilale na dada wa mama yako; kwani huyo ni mama yako mkubwa au mdogo. 14Kamwe usilale na mke wa baba yako mkubwa au mdogo; huyo ni mama yako. 15Kamwe usilale na mke wa mwanao; huyo ni mkewe mwanao. Kamwe usilale naye. 16Kamwe usilale na mke wa ndugu yako; huyo ni shemeji yako. 17Ukilala na mwanamke, basi, kamwe usilale naye na binti yake, wala wajukuu zake. Hao ni ndugu. Kuwachanganya ni kufanya uovu. 18Kamwe usimwoe dada wa mkeo wakati mke wako yungali hai; hiyo itasababisha ushindani.
19 # Taz Neh 9:29; Eze 18:9; 20:11-13; Luka 10:28; Roma 10:5; Gal 3:12 “Kamwe usilale na mwanamke awapo mwezini. 20#Taz Lawi 20:10 Kamwe usilale na mke wa jirani yako na hivyo kujitia mwenyewe najisi naye.
21 # Taz Lawi 20:1-5 “Kamwe usimtoe mtoto wako yeyote kuwa sadaka kwa mungu Moleki maana kufanya hivyo utalikufuru jina langu mimi Mungu wako. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.
22 # Taz Lawi 20:13 “Kamwe usilale na mwanamume mwenzio kana kwamba ni mwanamke. Hilo ni chukizo. 23#Taz Kut 22:19; Lawi 15-16; Kumb 27:21 Kamwe usilale na mnyama ili usijitie najisi; mwanamume au mwanamke yeyote kamwe asifanye hivyo; kufanya hivyo ni upotovu.
24“Msijitie najisi kwa kufanya mambo hayo kwani kwa sababu ya mambo hayo nayafukuza mataifa yaliyo mbele yenu kwa vile wao hufanya hayo na kujitia najisi. 25Nchi yao ilitiwa unajisi nami nikaiadhibu, nayo ikawakataa wakazi wake. 26Lakini nyinyi na wageni wanaokaa kati yenu ni lazima kuyashika masharti na maagizo yangu na wala msifanye machukizo hayo. 27Machukizo hayo waliyafanya watu waliokaa katika nchi ya Kanaani kabla yenu, nao wakaitia nchi unajisi. 28Basi, nyinyi msifanye mambo hayo, la sivyo nchi hiyo itawatapika kama ilivyolitapika taifa lililokuwa kabla yenu. 29Watu wote watakaofanya mambo hayo ya kuchukiza ni lazima watengwe mbali na watu wao. 30Kwa hiyo shikeni kikamilifu yote ninayowaagiza; msifuate mazoea yoyote ya kuchukiza yaliyofanywa na wale walioishi nchini kabla yenu, msije mkajitia unajisi kwayo. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.”
Mambo Ya Walawi18;1-30
Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)
"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.
Monday 19 June 2017
Kikombe Cha Asubuhi;Mambo Ya Walawi..17...
Mwongozo kuhusu damu
1Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose, 2“Mwambie Aroni, wanawe na watu wote wa Israeli amri zifuatazo: 3Kama mtu yeyote miongoni mwa Waisraeli akichinja ng'ombe au mwanakondoo au mbuzi ndani au nje ya kambi, 4badala ya kumleta mnyama huyo kwenye mlango wa hema la mkutano ili kumtolea Mwenyezi-Mungu mbele ya maskani yake takatifu, mtu huyo atakuwa na hatia ya kumwaga damu; amemwaga damu na atatengwa na watu wake. 5Kusudi la sheria hii ni kwamba Waisraeli wanapaswa kuleta wanyama ambao wangewachinjia mashambani ili wawalete kwa Mwenyezi-Mungu kwa kuhani kwenye mlango wa hema la mkutano, naye atawachinja na kumtolea Mwenyezi-Mungu sadaka za amani. 6Basi, kuhani atainyunyizia damu madhabahu ya Mwenyezi-Mungu iliyoko mlangoni mwa hema la mkutano na kuyateketeza yale mafuta yawe harufu nzuri ya kumpendeza Mwenyezi-Mungu. 7Kwa hiyo Waisraeli watakoma kabisa kutambikia yale majini, jambo ambalo limewafanya wakose uaminifu kwangu. Sharti hili ni la kudumu milele katika vizazi vyao vyote.
8“Waambie kwamba mtu yeyote miongoni mwa Waisraeli au mgeni anayeishi kati yao, anayetoa sadaka ya kuteketezwa au tambiko, 9lakini haileti mbele ya mlango wa hema la mkutano ili kumtolea Mwenyezi-Mungu, mtu huyo atatengwa na watu wake.
10 # Taz Mwa 9:4; Lawi 7:26-27; l9:26; Kumb 12:16,23; 15:23 “Kama mtu yeyote wa jumuiya ya Israeli au mgeni anayeishi kati yao anakula damu yoyote, mimi nitamwandama mtu huyo aliyekula damu na kumtenga mbali na watu wake. 11#Taz Ebr 9:22 Itakuwa hivyo kwa sababu uhai wa kiumbe umo katika damu. Nimewaagiza kuitolea damu madhabahuni ili kufanya ibada ya upatanisho kwa ajili ya roho zenu; kwa sababu damu hufanya upatanisho maana uhai umo katika damu. 12Ndiyo maana nimewaagiza Waisraeli hivi: Mtu yeyote miongoni mwenu wala mgeni anayeishi kati yenu kamwe asile damu.
13“Mtu yeyote miongoni mwa Waisraeli au mgeni anayekaa miongoni mwao akienda kuwinda mnyama au ndege, ni lazima aimwage damu chini na kuifunika kwa udongo. 14Maana, uhai wa kila kiumbe umo katika damu. Ndiyo maana nimewaagiza Waisraeli, kamwe wasile damu ya kiumbe chochote kwani uhai wa kiumbe chochote ni damu yake. Yeyote atakayekula damu atatengwa.
15“Mtu yeyote awe ni mwenyeji au mgeni, anayekula chochote kilichokufa chenyewe au kilichouawa na mnyama wa porini, lazima ayafue mavazi yake na kuoga; naye atakuwa najisi mpaka jioni. Baada ya hapo atakuwa safi. 16Lakini asipoyafua mavazi yake na kuoga, ni lazima mtu huyo awajibike kwa uovu wake.”
Mambo Ya Walawi17;1-16
Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)
"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.
Sunday 18 June 2017
Natumaini Jumapili ilikuwa njema/inaendelea vyema;Happy Father's Day..Burudani-Phil Wickham - This Is Amazing Grace,At Your Name (Yahweh Yahweh)
Enyi watoto, watiini wazazi wenu Kikristo maana hili ni jambo jema. “Waheshimu Baba na mama yako,” hii ndiyo amri ya kwanza ambayo imeongezewa ahadi, yaani, “Upate fanaka na kuishi miaka mingi duniani.” Nanyi akina baba, msiwachukize watoto wenu ila waleeni katika nidhamu na mafundisho ya Kikristo.
Siandiki mambo haya kwa ajili ya kuwaaibisha nyinyi, bali kwa ajili ya kuwafundisheni watoto wangu wapenzi. Maana hata kama mnao maelfu ya walezi katika maisha yenu ya Kikristo, baba yenu ni mmoja tu, kwani katika kuungana na Kristo mimi ndiye niliyewazaeni kwa kuihubiri Habari Njema. Kwa hiyo, nawasihi: Fuateni mfano wangu. Ndiyo maana nimemtuma Timotheo kwenu. Yeye ni mtoto wangu mpenzi na mwaminifu katika kuungana na Bwana. Atawakumbusheni njia ninayofuata katika kuungana na Kristo; njia ninayofundisha kila mahali katika makanisa yote.
"Swahili Na Waswahili"Pamoja Daima.
Friday 16 June 2017
Kikombe Cha Asubuhi;Mambo Ya Walawi..16...
Siku ya msamaha wa dhambi
1Mwenyezi-Mungu alizungumza na Mose, baada ya wana wawili wa Aroni kufa wakati ule walipomkaribia. 2#Taz Ebr 6:19 Alimwambia, “Mwambie ndugu yako Aroni asiingie mahali patakatifu nyuma ya pazia wakati usiokubaliwa. Asiingie mahali hapo kwani ndipo nitakapotokea katika wingu juu ya kiti cha rehema. Asipotii, atakufa. 3#Taz Ebr 9:7 Aroni ataingia mahali patakatifu sana akiwa na fahali mchanga kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi na kondoo dume kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa. 4Ataoga mwili wote katika maji, kisha atavaa mavazi matakatifu. Ataingia mahali hapo akiwa amevaa mavazi matakatifu: Joho la kitani baada ya nguo ya ndani ya suruali ya kitani na akiwa amevaa kanzu ya kitani na kujifunga mkanda wa kitani. 5Atatwaa kutoka jumuiya ya watu wa Israeli beberu wawili kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi na kondoo dume mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa.
6“Aroni atamtoa huyo fahali sadaka ya kuondoa dhambi kwa ajili yake mwenyewe, na kufanya ibada ya upatanisho kwa ajili yake mwenyewe na jamaa yake. 7Kisha, wale beberu wawili atawaweka kwenye mlango wa hema la mkutano. 8Atawapigia kura hao beberu wawili, kura moja kwa ajili ya Mwenyezi-Mungu na nyingine kwa ajili ya Azazeli. 9Atamleta yule beberu ambaye kura ilimtaka kwa ajili ya Mwenyezi-Mungu na kumtolea sadaka ya kuondoa dhambi. 10Lakini yule beberu aliyetakiwa na kura kwa ajili ya Azazeli atatolewa mbele ya Mwenyezi-Mungu akiwa hai ili kufanya ibada ya upatanisho kuhani atamwacha aende jangwani kwa Azazeli, ili kuondoa dhambi za jumuiya.
11“Aroni atamtoa fahali wa sadaka ya kuondoa dhambi kwa ajili yake mwenyewe, na kufanya ibada ya upatanisho kwa ajili yake mwenyewe na kwa ajili ya jamaa yake, kisha atamchinja fahali huyo sadaka ya kuondoa dhambi. 12Halafu atachukua chetezo na kutwaa makaa madhabahuni mbele ya Mwenyezi-Mungu na ubani konzi mbili uliosagwa vizuri sana. 13Ili asije akafa, atauleta ubani huo mbele ya Mwenyezi-Mungu na kuutia katika moto ili moshi wa ubani huo ukifunike kifuniko cha sanduku la agano. 14Atachukua kiasi cha damu ya yule fahali na kunyunyiza kwa kidole chake upande wa mashariki juu ya kiti cha rehema kisha atainyunyizia mbele ya sanduku la agano mara saba kwa kidole chake.
15 # Taz Ebr 9:12 “Halafu atamchinja yule beberu wa sadaka ya kuondoa dhambi kwa ajili ya watu wote. Damu ya mbuzi huyo ataileta ndani mahali patakatifu sana na kufanya kama alivyofanya na damu ya yule fahali; atainyunyiza juu ya kiti cha rehema, upande wake wa mbele. 16Hivyo atafanya ibada ya upatanisho kwa ajili ya mahali patakatifu kwa sababu ya unajisi, makosa na dhambi zote za Waisraeli. Ndivyo atakavyofanya pia kwa ajili ya hema la mkutano lililo miongoni mwa watu hao walio najisi. 17Wakati Aroni anafanya ibada ya upatanisho kwa ajili yake mwenyewe, jamaa yake na jamii nzima ya Israeli, kamwe asiwepo mtu yeyote ndani ya hema la mkutano hadi atakapokuwa amemaliza na kutoka nje. 18Kisha atatoka na kwenda kwenye madhabahu iliyo mbele ya Mwenyezi-Mungu na kuifanyia ibada ya upatanisho. Atachukua kiasi cha damu ya yule fahali na ya yule mbuzi na kuzipaka pembe za madhabahu pande zote. 19Atainyunyizia madhabahu hiyo damu kwa kidole chake mara saba na hivyo kuiweka wakfu na kuitakasa unajisi wote wa watu wa Israeli.
20“Baada ya Aroni kumaliza kupatakasa mahali patakatifu, hema la mkutano na madhabahu, ndipo atamtoa yule beberu kwa ajili ya Azazeli,#16:20 Azazeli: Taz Lawi 16:8. akiwa hai. 21Aroni ataweka mikono yake juu ya kichwa cha huyo beberu hai na kuuungama juu yake dhambi zote za watu wa Israeli, makosa yao yote na dhambi zao zote, ili kumwajibisha huyo. Kisha atamwacha huyo beberu aende jangwani akipelekwa huko na mtu yeyote anayejitoa kwa hiari. 22Atamwacha huyo beberu aende jangwani, mahali pasipokuwa na watu, akiwa ameyachukua maovu yao yote.
23 # Taz Eze 44:19 “Kisha Aroni atarudi ndani ya hema la mkutano, atavua yale mavazi aliyovaa alipoingia mahali patakatifu sana na kuyaacha humo. 24Ataoga humo ndani katika mahali patakatifu na kuvaa mavazi yake. Atatoka na kutoa sadaka yake ya kuteketezwa, na sadaka ya kuteketezwa ya watu wa Israeli, ili kufanya ibada ya upatanisho kwa ajili yake mwenyewe na kwa ajili ya watu wote. 25Mafuta ya sadaka ya kuondoa dhambi atayateketeza juu ya madhabahu. 26Yule mtu aliyempeleka yule beberu kwa Azazeli kwanza atayafua mavazi yake na kuoga ndipo atakapoweza kuingia kambini. 27#Taz Ebr 13:11 Yule fahali na mbuzi waliotolewa sadaka ya kuondoa dhambi ambao damu yao ilipelekwa mahali patakatifu sana ili kufanya ibada ya upatanisho, watapelekwa nje ya kambi na kuteketezwa. Ngozi zao, nyama na mavi yao, vyote vitateketezwa. 28Yule mtu atakayewateketeza atayafua mavazi yake na kuoga, ndipo atakapoweza kuingia kambini.
29 # Taz Lawi 23:26-32; Hes 29:7-11 “Hili ni sharti ambalo mnapaswa kulifuata milele: Siku ya kumi ya mwezi wa saba, nyinyi wenyewe na hata wageni wanaoishi miongoni mwenu, ni lazima mfunge siku hiyo na kuacha kufanya kazi. 30Mtafanya hivyo kwa sababu siku hiyo ndiyo siku ambayo mtafanyiwa ibada ya upatanisho, msafishwe dhambi zenu, nanyi mtakuwa safi mbele ya Mwenyezi-Mungu. 31Siku hiyo ni siku ya mapumziko kamili nanyi mtafunga. Kanuni hiyo ni ya kudumu milele. 32Kuhani aliyepakwa mafuta na kuwekwa wakfu ashike nafasi ya baba yake, ndiye atakayefanya ibada ya upatanisho akiwa amevaa mavazi matakatifu ya kitani. 33Atafanya ibada ya upatanisho kwa ajili ya mahali patakatifu sana, kwa ajili ya hema la mkutano, madhabahu, makuhani na kwa ajili ya jumuiya nzima ya Israeli. 34Hili, basi ni sharti la kudumu milele; ni lazima mlifuate ili kufanya ibada ya upatanisho kwa ajili ya watu wa Israeli mara moja kila mwaka na kusamehewa dhambi zao.” Mose akafanya yote kama alivyoamriwa na Mwenyezi-Mungu.
Mambo Ya Walawi16;1-34
Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)
"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.
Thursday 15 June 2017
Kikombe Cha Asubuhi;Mambo Ya Walawi..15...
Vitu najisi vya mwili
1Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose na Aroni, 2“Waambieni Waisraeli hivi: Mwanamume yeyote akitokwa na usaha, usaha huo wamfanya kuwa najisi. 3Na ufuatao ni mwongozo kuhusu najisi hiyo: Muda wote anapotokwa na usaha au usaha unapokuwa umezuiwa ndani yake, mtu huyo ni najisi. 4Kitanda chochote atakacholalia au atakachokalia, kitakuwa najisi. 5Mtu yeyote atakayegusa kitanda chake mtu huyo ni lazima ayafue mavazi yake, na kuoga; naye atakuwa najisi mpaka jioni. 6Mtu yeyote atakayekalia kitu chochote alichokalia huyo mtu mwenye kutokwa na usaha, ni lazima ayafue mavazi na kuoga; na atakuwa najisi hadi jioni. 7Mtu yeyote atakayemgusa mtu atokwaye na usaha, lazima afue mavazi yake na kuoga; naye atakuwa najisi mpaka jioni. 8Mtu yeyote akitemewa mate na mtu anayetokwa usaha ni lazima mtu huyo aliyetemewa mate ayafue mavazi yake, na kuoga; naye atakuwa najisi mpaka jioni. 9Tandiko lolote la mnyama aliloketia mtu anayetokwa na usaha litakuwa najisi. 10Mtu yeyote atakayegusa kitu chochote alichokalia mtu huyo, atakuwa najisi mpaka jioni. Mtu yeyote anayebeba kitu chochote kilichokuwa cha mtu huyo ni lazima ayafue mavazi yake, na kuoga; naye atakuwa najisi mpaka jioni. 11Mtu yeyote anayetokwa na usaha akimgusa mtu bila kusafisha kwanza mikono yake na kuoga, aliyeguswa atakuwa najisi mpaka jioni. 12Chombo chochote cha udongo kilichoguswa na mtu anayetokwa na usaha ni lazima kivunjwe. Lakini chombo chochote cha mbao ni lazima kisafishwe kwa maji.
13“Mwanamume yeyote anayetokwa na usaha akiponywa ugonjwa wake, ni lazima huyo mtu angoje siku saba kabla ya kuondolewa unajisi wake. Atayafua mavazi yake na kuoga kwa maji ya mtoni; naye atakuwa safi. 14Siku ya nane, ni lazima alete hua wawili au makinda mawili ya njiwa mbele ya Mwenyezi-Mungu mlangoni mwa hema la mkutano na kumkabidhi kuhani. 15Kuhani atawatoa hao, mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi na mwingine kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa; naye kuhani atamfanyia huyo mtu ibada ya upatanisho mbele ya Mwenyezi-Mungu na kumwondolea unajisi wake wa kutokwa na usaha.
16“Kama mwanamume yeyote akitokwa na shahawa yake, ni lazima aoge mwili mzima kwa maji, naye atakuwa najisi mpaka jioni. 17Vazi lolote lililodondokewa shahawa au ngozi yoyote iliyoguswa na shahawa hiyo ni lazima ioshwe kwa maji, na itakuwa najisi mpaka jioni. 18Kama mwanamume akilala na mwanamke, akatokwa na shahawa, basi, ni lazima wote wawili waoge kwa maji, nao watakuwa najisi mpaka jioni.
19“Mwanamke yeyote anapokuwa mwezini, atakuwa najisi kwa muda wa siku saba. Mtu yeyote atakayemgusa mwanamke huyo atakuwa najisi mpaka jioni. 20Kitu chochote anacholalia au kukalia wakati yu najisi, kitakuwa najisi. 21Mtu yeyote atakayegusa kitanda cha huyo mwanamke ni lazima ayafue mavazi yake na kuoga kwa maji; naye atakuwa najisi mpaka jioni. 22Mtu yeyote atakayegusa kitu chochote anachokalia mwanamke huyo ni lazima ayafue mavazi yake na kuoga kwa maji, naye atakuwa najisi mpaka jioni. 23Mwanamume yeyote atakayegusa kitu chochote alicholalia au kukalia huyo mwanamke, atakuwa najisi mpaka jioni. 24Kama mwanamume akilala na mwanamke huyo na damu ya huyo mwanamke ikamdondokea huyo mwanamume, basi, mwanamume huyo atakuwa najisi kwa muda wa siku saba. Kitanda chochote atakacholalia huyo mwanamume kitakuwa najisi.
25“Kama mwanamke anatokwa na damu kwa muda wa siku nyingi kuliko ilivyo kawaida au anatokwa damu wakati usio wa majira yake ya kutokwa damu, basi, ataendelea kuwa najisi muda wote damu inapomtoka. 26Kitanda chochote anacholalia wakati huo au kiti chochote anachokalia, kitakuwa najisi sawa kama wakati wa unajisi wake wa kutokwa damu. 27Mtu yeyote atakayegusa vitu hivyo, atakuwa najisi na ni lazima ayafue mavazi yake na kuoga; naye atakuwa najisi mpaka jioni. 28Baada ya kukauka damu yake mwanamke huyo atangoja hadi siku saba ili kuwa safi; na baada ya muda huo atakuwa safi. 29Siku ya nane atachukua hua wawili au makinda mawili ya njiwa na kumletea kuhani mlangoni mwa hema la mkutano. 30Kuhani atamtoa mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi na mwingine kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa. Hivyo kuhani atamfanyia huyo mwanamke ibada ya upatanisho mbele ya Mwenyezi-Mungu na kumwondolea unajisi wake wa kutokwa damu.
31“Ndivyo mtakavyowatahadharisha Waisraeli na unajisi wao, wasije wakaikufuru maskani yangu takatifu iliyo miongoni mwao wakiingia humo na unajisi wao; wakifanya hivyo watauawa.”
32Hiyo ndiyo sheria kuhusu mwanamume anayetokwa na usaha na anayetokwa na shahawa na kuwa najisi. 33Sheria hiyo yamhusu pia mwanamke anayetokwa damu na kuwa najisi. Sheria hiyo yamhusu mwanamume au mwanamke yeyote anayetokwa na chochote na pia yahusu mwanamume anayelala na mwanamke ambaye ni najisi.
Mambo Ya Walawi15;1-33
Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)
"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.
Wednesday 14 June 2017
Kikombe Cha Asubuhi;Mambo Ya Walawi..14...
Utakaso baada ya kuugua magonjwa ya ngozi
1Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose, 2“Ifuatayo ni sheria kumhusu mwenye ukoma katika siku ya kutakaswa kwake. Baada ya kupona ataletwa kwa kuhani. 3Kuhani atakwenda kumwangalia huyo mtu nje ya kambi. Ikiwa ukoma huo umepona, 4basi, kuhani ataamuru watu walete ndege wawili safi walio hai, kipande cha mwerezi, sufu ya rangi nyekundu na tawi la husopo kwa ajili ya huyo mtu atakayetakaswa. 5Kuhani atawaamuru wamchinje ndege mmoja katika chungu chenye maji safi ya chemchemi. 6Kuhani atamchukua yule ndege mwingine hai, kipande kile cha mwerezi, sufu ya rangi nyekundu na lile tawi la husopo na kuvitumbukiza vyote katika damu ya yule ndege aliyechinjwa. 7Kisha, atamnyunyizia huyo mwenye kutakaswa ile damu mara saba, halafu atamtangaza mtu huyo kuwa safi. Yule ndege hai atamwacha aende zake mashambani nje ya mji. 8Huyo mtu atayafua mavazi yake, atanyoa nywele zake, na kuoga; naye atakuwa safi. Baada ya hayo atarudi kambini, lakini atakaa nje ya hema lake kwa muda wa siku saba. 9Siku ya saba atanyoa nywele zake zote, ndevu na kope za macho yake. Kisha atafua mavazi yake na kuoga, ataoga kwa maji; naye atakuwa safi.
10“Siku ya nane ataleta wanakondoo madume wawili wasio na dosari, kondoo jike wa mwaka mmoja asiye na dosari, kilo tatu za unga laini uliochanganywa na mafuta kwa ajili ya sadaka ya nafaka pamoja na mafuta theluthi moja ya lita. 11Kuhani atakayemtakasa mtu huyo atamleta mbele ya Mwenyezi-Mungu karibu na mlango wa hema la mkutano pamoja na vitu alivyoleta. 12Kuhani atachukua mwanakondoo dume mmoja na kumtolea sadaka ya kuondoa hatia pamoja na yale mafuta theluthi moja ya lita. Atafanya ishara ya kuvitolea mbele ya Mwenyezi-Mungu. 13Kisha atamchinja huyo mwanakondoo katika mahali patakatifu, wanapochinjia wanyama wa sadaka ya kuondoa dhambi na sadaka ya kuteketezwa. Sadaka hii ya kuondoa hatia, kama ilivyo sadaka ya kuondoa dhambi, ni mali yake kuhani; ni sadaka takatifu kabisa. 14Kuhani atachukua kiasi cha damu ya sadaka ya kuondoa hatia na kumpaka mtu anayetakaswa katika ncha ya sikio lake la kulia na kidole gumba cha mkono wake wa kulia na kidole gumba cha mguu wake wa kulia. 15Kisha, kuhani atachukua kiasi cha ile theluthi moja ya mafuta na kuyatia katika kiganja cha mkono wake wa kushoto. 16Atachovya kidole cha mkono wake wa kulia katika mafuta hayo na kumnyunyizia huyo mtu anayetakaswa mara saba mbele ya Mwenyezi-Mungu. 17Kiasi cha mafuta yanayobaki katika kiganja chake atampaka huyo mtu anayetakaswa katika ncha ya sikio lake la kulia na kidole gumba cha mkono wake wa kulia na kidole gumba cha mguu wake wa kulia, mahali palepale alipompaka damu ya sadaka ya kuondoa hatia. 18Yale mafuta yaliyobaki atampaka huyo mtu kichwani. Hivyo kuhani atamfanyia ibada ya upatanisho mbele ya Mwenyezi-Mungu. 19Kuhani atatolea sadaka ya kuondoa dhambi na kumfanyia huyo mtu anayetakaswa ibada ya upatanisho ili kumwondolea unajisi wake. Kisha atamchinja mwanakondoo wa sadaka ya kuteketezwa. 20Kuhani atatolea ile sadaka ya kuteketezwa na sadaka ya nafaka juu ya madhabahu. Hivyo kuhani atamfanyia huyo mtu ibada ya upatanisho, naye atakuwa safi.
21“Lakini ikiwa mtu huyo ni maskini, hana uwezo wa kutoa vitu hivyo, basi ataleta mwanakondoo dume mmoja kuwa fidia ya sadaka ya kuondoa hatia ambaye atafanyiwa ishara ya kutoa sadaka ili kumfanyia huyo mtu ibada ya upatanisho. Ataleta pia kilo moja ya unga laini uliochanganywa na mafuta kwa ajili ya sadaka ya nafaka na mafuta theluthi moja ya lita. 22Ataleta pia hua wawili au makinda mawili ya njiwa kadiri anavyoweza mmoja atakuwa kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi na mwingine kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa. 23Siku ya nane atamletea kuhani vitu hivyo mbele ya mlango wa hema la mkutano kwa ajili ya utakaso wake mbele ya Mwenyezi-Mungu. 24Kuhani atamchukua huyo mwanakondoo dume wa sadaka ya kuondoa hatia pamoja na yale mafuta theluthi moja ya lita na kufanya ishara ya kuvitolea mbele ya Mwenyezi-Mungu. 25Atamchinja huyo mwanakondoo dume wa sadaka ya kuondoa hatia. Kuhani atachukua kiasi cha damu na kumpaka huyo mtu anayetakaswa katika ncha ya sikio lake la kulia, katika kidole gumba cha mkono wake wa kulia na kidole gumba cha mguu wake wa kulia. 26Kuhani atatia kiasi cha mafuta hayo katika kiganja cha mkono wake wa kushoto. 27Kisha atamnyunyizia huyo mtu kwa kidole chake cha kulia kiasi cha hayo mafuta yaliyomo katika kiganja chake cha kushoto mara saba mbele ya Mwenyezi-Mungu. 28Kuhani atampaka huyo mtu anayetakaswa mafuta katika ncha ya sikio lake la kulia, katika kidole gumba cha mkono wake wa kulia, na kidole gumba cha mguu wake wa kulia. Atampaka mahali pale ambapo alimpaka ile damu ya sadaka ya kuondoa hatia. 29Mafuta yanayosalia mkononi mwake atampaka huyo mtu kichwani, ili kumfanyia ibada ya upatanisho mbele ya Mwenyezi-Mungu. 30Kisha kuhani atamchukua mmoja wa wale hua au njiwa wawili kadiri mtu huyo anavyoweza kuleta. 31Hua atakuwa kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi na mwingine kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa. Pamoja na hao, atatoa sadaka ya nafaka; naye kuhani atamfanyia huyo mtu ibada ya upatanisho mbele ya Mwenyezi-Mungu. 32Huo ndio mwongozo kuhusu mtu mwenye ukoma asiyeweza kutoa sadaka za kumtakasa.”
Upele katika nyumba
33Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose na Aroni, 34“Mtakapoingia katika nchi ya Kanaani ambayo ninawapa kuwa milki yenu, nami nikafanya namna ya upele wa ukoma uote katika ukuta wa nyumba fulani katika nchi mtakayoimiliki, 35basi, mwenye nyumba hiyo ni lazima amwambie kuhani kwamba namna ya upele wa ukoma umeonekana katika nyumba yake. 36Kuhani ataamuru vitu vyote ndani ya nyumba hiyo vitolewe kabla yeye mwenyewe hajaanza uchunguzi wake; visije vyote kutangazwa kuwa najisi. Kisha kuhani ataingia kuiangalia nyumba hiyo. 37Atauchunguza upele huo; kama upele huo umeonekana ukutani na umesababisha madoa ya rangi ya kijani kibichi au nyekundu na kuonekana kuwa yamepenya ndani ya kuta, 38basi, kuhani atatoka nje mlangoni na kuifunga nyumba hiyo kwa muda wa siku saba. 39Siku ya saba kuhani atarudi na kuiangalia tena nyumba hiyo. Ikiwa upele huo umeenea katika kuta za nyumba hiyo, 40kuhani ataamuru mawe yaliyoko kwenye sehemu zenye upele yatolewe na kutupwa mahali najisi nje ya mji. 41Lipu ya nyumba hiyo itabanduliwa na kifusi chake kutupwa mahali najisi nje ya mji. 42Kisha watachukua mawe mapya na kujenga mahali walipobomoa; nao wataipiga nyumba hiyo lipu upya.
43“Ikiwa upele huo utatokea tena baada ya kutoa mawe hayo na kukwangua lipu na kuipiga lipu upya, 44yapasa kuhani aje kuichunguza. Ikiwa upele umeenea katika nyumba hiyo, basi huo ni upele wa kufisha; nyumba hiyo ni najisi. 45Nyumba hiyo ni lazima ibomolewe na mawe yake, miti yake na lipu vipelekwe mahali najisi nje ya mji. 46Zaidi ya hayo, yeyote atakayeingia ndani ya nyumba hiyo wakati itakapokuwa imefungwa, atakuwa najisi mpaka jioni. 47Yeyote anayelala katika nyumba hiyo au kulia chakula ndani yake, lazima ayafue mavazi yake.
48“Lakini ikiwa baada ya kuikagua nyumba hiyo, kuhani ataona kuwa upele haujaenea baada ya kupigwa lipu, basi, kuhani atatangaza kuwa nyumba hiyo ni safi kwani upele umekwisha. 49Ili kuitakasa nyumba hiyo, mwenye nyumba ataleta ndege wawili pamoja na kipande cha mwerezi, sufu nyekundu na tawi la husopo. 50Atamchinja ndege mmoja katika chungu chenye maji safi ya chemchemi. 51Atachukua kipande cha mwerezi, tawi la husopo na ile sufu nyekundu pamoja na yule ndege mwingine aliye hai na kuvitumbukiza vyote katika damu ya yule ndege aliyechinjwa. Kisha atainyunyizia nyumba hiyo damu mara saba. 52Hivyo ndivyo atakavyoitakasa nyumba hiyo kwa damu ya ndege, maji safi ya chemchemi, ndege hai, kipande cha mwerezi, tawi la husopo na ile sufu nyekundu. 53Yule ndege hai atamwacha aende zake mashambani nje ya mji. Hivyo ndivyo atakavyoitakasa nyumba hiyo, nayo itakuwa safi.”
54Hii ndiyo sheria kuhusu aina yoyote ya namna ya upele wa ukoma; 55upele katika nguo au nyumba, 56uvimbe, jipu au kipaku, 57ili kuonesha ni kitu gani kilicho najisi na kisicho najisi. Hiyo ndiyo sheria kuhusu namna ya upele wa ukoma.
Mambo Ya Walawi14;1-57
Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)
"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.
Subscribe to:
Posts (Atom)