Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Monday 30 January 2017

Kikombe Cha Asubuhi;Mwanzo 8....

Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje Wapendwa/Waungwana?
Ni wiki nyingine tena kwa uwezo,Neema/Rehema za Mungu ametujaalia kuiona tena Siku hii..
Tumrudishie Sifa/Utukufu kwa Muumba wa Yote,Yeye akisema atakubariki na hufanyika hivyo,
Yeye akisema ndiyo hakuna wa kupinga,
Tuanze wiki/siku hii na Mungu wetu akawe Mwanzo wa yote na mwisho wa yote.
Akabariki Kazi,Biashara,Masomo,Familia,Ndugu,Jamaa na Marafiki...
Wenye Shida/Tabu Mungu baba akawaguse,Yatima/Wajane baba ukawe nao..
Akatupe sawasawa na mapenzi yake.
Mungu wetu yu Mwema sana...!!!!
Tuanzena Mungu.


Mwisho wa gharika

1Kisha Mungu akamkumbuka Noa na wanyama wote wa porini na wa kufugwa waliokuwa pamoja naye ndani ya safina. Basi, Mungu akavumisha upepo juu ya nchi, maji yakaanza kupungua. 2Chemchemi za maji ya vilindi na madirisha ya mbinguni yakafungwa. Mvua ikazuiwa, 3maji yakaendelea kupungua polepole katika nchi. Baada ya siku 150, maji yakawa yamepungua sana. 4Mnamo siku ya kumi na saba ya mwezi wa saba, safina ikatua juu ya milima ya Ararati. 5Maji yakaendelea kupungua polepole, na siku ya kwanza ya mwezi wa kumi, vilele vya milima vikaonekana.
6Baada ya siku arubaini, Noa alifungua dirisha alilokuwa ametengeneza katika hiyo safina, 7akamtoa kunguru nje, naye hakurudi bali aliruka huko na huko mpaka maji yalipokauka nchini. 8Kisha Noa akamtoa njiwa apate kuona kama maji yalikuwa yamepungua juu ya nchi. 9Lakini, kwa vile maji yalikuwa bado yameifunika nchi yote, huyo njiwa hakupata mahali pa kutua, akamrudia Noa katika safina. Noa akanyosha mkono, akamtwaa na kumrudisha ndani ya safina. 10Noa akangoja siku nyingine saba, kisha akamtoa tena huyo njiwa. 11Njiwa huyo akamrudia Noa saa za jioni akiwa na tawi bichi la mzeituni mdomoni mwake. Kwa hiyo Noa akajua kwamba maji yalikuwa yamepungua katika nchi. 12Kisha akangoja siku nyingine saba, akamtoa tena yule njiwa; safari hii njiwa hakurudi kabisa.
13Noa alipokuwa na umri wa miaka 601, siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza, maji yalikuwa yamekauka katika nchi. Noa akafunua kifuniko cha safina na alipotazama, akaona kwamba nchi ilikuwa imekauka. 14Siku ya 27 ya mwezi wa pili, nchi ilikuwa imekauka kabisa.
15Hapo, Mungu akamwambia Noa, 16“Toka katika safina, wewe pamoja na mkeo, wanao na wake zao. 17Toa pia viumbe wote hai wa kila aina waliokuwa pamoja nawe, ndege na wanyama na kila kiumbe kitambaacho, wapate kuzaa kwa wingi duniani, waongezeke na kuenea kila mahali duniani.” 18Basi, Noa akatoka katika safina pamoja na wanawe na mkewe pamoja na wake za wanawe. 19Wakatoka kufuatana na jamii zao, wanyama wote wa porini, viumbe wote watambaao, ndege wote na wanyama wote hai duniani.

Noa anamtolea Mungu tambiko

20Noa akamjengea Mwenyezi-Mungu madhabahu, akatwaa mmoja katika kila aina ya wanyama walio safi na ndege walio safi, akamtolea Mungu sadaka za kuteketezwa. 21Harufu nzuri ya tambiko hiyo ikampendeza Mwenyezi-Mungu, naye akasema moyoni mwake, “Kamwe sitailaani tena nchi kwa sababu ya binadamu; najua kwamba mawazo yake ni maovu tangu utoto wake. Wala sitaangamiza tena viumbe wote kama nilivyofanya. 22Kadiri itakavyodumu nchi majira ya kupanda na kuvuna, ya baridi na joto, ya masika na kiangazi, usiku na mchana, hayatakoma.”
Mwanzo 8;1-22

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (BHN):
Jifunze zaidi


"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

Sunday 29 January 2017

Natumaini Mlikuwa/Mnaendelea na Jumapili hii Vjema

Natumaini Jumapili Ilikuwa njema/Inaendela vyema,
Mungu yu mwema na andelee kuwabariki katika yote..
hapa kwetu ni baridi inataka moyo kuamka Asubuhi na kwenda kwenye Ibada,
Basi tujitahidi kama tuwezavyo kwenda kutafuta mkate wetu..Mungu atusaidi na tushinde
Jaribu hili....
Tukumbushane kwa Amani na Upendo..




““Mimi ni mzabibu wa kweli, na Baba yangu ndiye mkulima. Kila tawi ndani yangu lisilozaa matunda yeye huliondoa, na kila tawi lizaalo hulisafisha lipate kuzaa zaidi. Nyinyi mmekwisha kuwa safi kwa sababu ya ule ujumbe niliowaambieni. Kaeni ndani yangu, nami nikae ndani yenu. Kama vile tawi haliwezi peke yake kuzaa matunda lisipobaki katika mzabibu, hali kadhalika nanyi hamwezi kuzaa matunda msipokaa ndani yangu. “Mimi ni mzabibu, nanyi ni matawi. Akaaye ndani yangu, nami nikiwa ndani yake, huyo huzaa matunda mengi, maana bila mimi hamwezi kufanya chochote. Mtu yeyote asipokaa ndani yangu hutupwa nje kama tawi litupwalo nje hata likakauka. Watu huliokota tawi la namna hiyo na kulitupa motoni liungue. Mkikaa ndani yangu na maneno yangu yakikaa ndani yenu, basi, ombeni chochote mtakacho nanyi mtapewa. Baba yangu hutukuzwa kama mkizaa matunda mengi na kuwa wanafunzi wangu. Mimi nimewapenda nyinyi kama vile Baba alivyonipenda mimi. Kaeni katika pendo langu. Mkizishika amri zangu mtakaa katika pendo langu, kama vile nami nilivyozishika amri za Baba yangu na kukaa katika pendo lake. Nimewaambieni mambo haya ili furaha yangu ikae ndani yenu, na furaha yenu ikamilike. Hii ndiyo amri yangu: Pendaneni; pendaneni kama nilivyowapenda nyinyi. Hakuna upendo mkuu zaidi kuliko upendo wa mtu atoaye uhai wake kwa ajili ya rafiki zake. Nyinyi ni rafiki zangu mkifanya ninayowaamuru. Nyinyi siwaiti tena watumishi, maana mtumishi hajui anachofanya bwana wake. Lakini mimi nimewaita nyinyi rafiki, kwa sababu nimewajulisha yote ambayo nimeyasikia kutoka kwa Baba yangu. Nyinyi hamkunichagua mimi; mimi niliwachagueni na kuwatuma mwende mkazae matunda, matunda yadumuyo, naye Baba apate kuwapeni chochote mnachomwomba kwa jina langu. Basi, amri yangu kwenu ndiyo hii: Pendaneni.”
‭‭Yohane‬ ‭15:1-17‬ ‭BHND‬‬
http://bible.com/393/jhn.15.1-17.bhnd














"Swahili Na Waswahili"Muwe na wakati mwema.

Friday 27 January 2017

Kikombe Cha Asubuhi;Mwanzo 7....


Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,mmeamkaje Wapendwa/Waungwana?
Nimatumaini yangu wengi mmeamka salama na wenye afya..
walio Wagonjwa,Wenye Shida/Tabu,Kufiwa na wanopitia kwenye Magumu/Majaribu Mungu kamwe hajawaacha.
Tuzidi kumuomba Baba wa yote,Mfalme wa Amani,Mwenye-enzi,Muumba wa Vyote,Mume wa Wajane,Baba wa Yatima,Yeye asiyechoka,Yeye asiye lala,Mwingi wa Rehema/Neema,Kimbilio letu,Baba wa Uzima,Yeye husamehe,
Sifa na Utukufu ni kwake daima...!!!!!
Akatubariki Tuingiapo/Tutokapo,Vilaji/Vinywaji,Masomoni,Biashara,Kazi
na tumtangulize kwa kila jambo.
Muwe na wakati mwema.

Gharika kuu

1Mwenyezi-Mungu akamwambia Noa, “Ingia ndani ya safina wewe pamoja na jamaa yako yote, kwa maana, kati ya watu wote wanaoishi nyakati hizi zako, nimekuona wewe peke yako kuwa mwadilifu mbele yangu. 2Chukua pamoja nawe wanyama wote walio safi, dume na jike, saba saba; lakini wanyama walio najisi, chukua dume na jike, wawiliwawili. 3Vilevile chukua ndege wa angani dume na jike, saba saba, ili kuzihifadhi hai aina zao duniani. 4Baada ya siku saba, nitanyesha mvua nchini siku arubaini mchana na usiku, na kila kiumbe hai nilichokiumba duniani nitakiangamiza.” 5Noa akafanya yote kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru.
6Noa alikuwa na umri wa miaka 600 wakati gharika ilipotokea nchini. 7Noa, mkewe, wanawe na wake zao wakaingia ndani ya safina ili kuiepa gharika. 8Wanyama walio safi, wanyama walio najisi, ndege na viumbe vyote vitambaavyo, 9wawiliwawili, dume na jike, wakaingia ndani ya safina pamoja na Noa kama Mungu alivyomwamuru. 10Baada ya siku saba, maji ya gharika yakaanza kuifunika nchi.
11Noa alipokuwa na umri wa miaka 600, mnamo siku ya kumi na saba ya mwezi wa pili, siku hiyo chemchemi zote za vilindi vya nchi zikabubujika maji, na madirisha ya mbinguni yakafunguka. 12Mvua ikanyesha nchini siku arubaini mchana na usiku. 13Siku hiyohiyo mvua ilipoanza kunyesha, Noa, mkewe na wanawe, Shemu, Hamu na Yafethi, pamoja na wake zao, waliingia ndani ya safina. 14Waliingia wao wenyewe pamoja na aina zote za wanyama wa porini, wanyama wafugwao, wanyama watambaao na ndege wa kila aina. 15Waliingia ndani ya safina pamoja na Noa wiliwawili wa kila aina ya viumbe hai. 16Kila aina yao waliingia, dume na jike, kama Mungu alivyomwamuru Noa. Kisha, Mwenyezi-Mungu akaufunga mlango wa safina nyuma yake Noa.
17Gharika ilidumu nchini kwa muda wa siku arubaini. Maji yakaongezeka na kuiinua safina, ikaelea juu ya ardhi. 18Maji yakaendelea kuongezeka zaidi nchini na safina ikaelea juu yake. 19Maji hayo yakawa mengi sana juu ya nchi, yakaifunika milima yote mirefu katika nchi. 20Yaliongezeka hata kuifunika milima kiasi cha mita saba na nusu. 21Viumbe wote hai katika nchi wakafa. Ndege, wanyama wa kufugwa, wanyama wa porini, makundi ya viumbe wote katika nchi kavu na wanadamu wote; 22naam, kila kiumbe hai katika nchi kavu kilikufa. 23Mungu akaangamiza kila kiumbe kilichokuwa hai duniani: Binadamu, wanyama, viumbe vitambaavyo na ndege wa angani. Vyote viliangamizwa duniani. Noa tu ndiye aliyesalimika na wale waliokuwa pamoja naye ndani ya safina. 24Maji hayo yalidumu katika nchi siku 150.
Mwanzo 7;1-24
Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN):
Jifunze zaidi


"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

Thursday 26 January 2017

Kikombe Cha Asubuhi;Mwanzo 6....

Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje Wapendwa/Waungwana?
Ni kwa Neema  ya Mungu tuu wala si kwa uwezo wetu kuiona tena siku hii...
sisi tumempa nini Mungu kwa Neema hii?Kipi hata kidogo umemfanyia,Unamfanyia Mungu
kwa kukupatia Neema hii ukiwa Hai, mwenye Afya njema,Nguvu,Akili timamu?
Wangapi wametamani kuendelea kuwepo na kupata hayo niliyoyasema na zaidi au hata kimoja wapo
lakini wameshindwa Asubuhi/siku ya leo?
Basi Wapendwa/Waungwana tutumie nafasi hii ya Neema ya Mungu vyema..
Popote tulipo Mungu wetu yupo..
Mungu akawabariki katika yote... Na akatuepushe na kila Ovu...
Awe nasi katika kazi zetu,Masomo, biashara, Vyombo vya usafiri,tutembee naye,Tuingiapo na Tutokapo,
Akawaguse wanaopitia Magumu,Wenye Shida/Tabu, Yatima na Wajane, Wagonjwa mahospitalini,Majumbani,Walio Magerezani pasipo na Hatia Mungu wetu akaonekane.
Tuendelee kukumbushana vyema..!!!!!!
Muwe na wakati mzuri.




Uovu wa binadamu

1Binadamu walipozidi kuongezeka duniani na kuzaa wasichana, 2watoto wa kiume wa Mungu waliwaona hao wasichana wa watu kuwa ni wazuri, wakawachukua wale waliowapenda kuwa wake zao. 3Hapo Mwenyezi-Mungu akasema, “Roho yangu haitakaa ndani ya binadamu milele, maana yeye ni wa kufa tu. Basi, hataishi zaidi ya miaka 120.” 4Nyakati hizo na hata baadaye, kulikuwa na majitu duniani ambao walikuwa wazawa wa watoto wa kiume wa Mungu na wasichana wa watu. Hao ndio watu waliokuwa mashujaa na wenye sifa enzi hizo, nao waliitwa Wanefili.
5Mwenyezi-Mungu alipoona wingi wa uovu wa binadamu duniani, na kwamba kila analokusudia binadamu moyoni mwake ni ovu daima, 6Mwenyezi-Mungu alisikitika sana kwa kumuumba binadamu duniani. Mwenyezi-Mungu alihuzunika sana moyoni mwake, 7hivyo akasema, “Nitamfuta kabisa duniani binadamu niliyemuumba; nitafutilia mbali pia wanyama wa porini, viumbe vitambaavyo na ndege wa angani. Ninasikitika kwamba niliwaumba duniani.” 8Lakini Noa alipata fadhili mbele ya Mwenyezi-Mungu.

Noa

9Ifuatayo ni habari juu ya Noa ambaye alikuwa ndiye mwadilifu pekee na ambaye hakuwa na lawama nyakati zake. Alikuwa mcha Mungu. 10Noa alikuwa na watoto watatu wa kiume: Shemu, Hamu na Yafethi. 11Mungu aliiona dunia kuwa imeharibika na kujaa ukatili. 12Naam, Mungu aliiangalia dunia, akaona kuwa imeharibika kabisa, kwa maana kila mtu alifuata njia yake mbovu.
13Mungu akamwambia Noa, “Nimeamua kuwaangamiza binadamu wote kwa sababu wameijaza dunia ukatili. Naam, nitawaangamiza kabisa pamoja na dunia! 14Kwa hiyo, jitengenezee safina kwa mbao za mpingo. Gawa vyumba ndani yake na ipake lami ndani na nje. 15Utaitengeneza hivi: Urefu wake mita 139, upana wake mita 25 na kimo chake mita 15. 16Safina hiyo iwe ya ghorofa tatu na yenye mlango pembeni. Itengenezee paa, kisha acha nafasi ipatayo nusu mita kati ya paa na dari. 17Nitaleta gharika ili kuangamiza viumbe vyote hai duniani. Kila kiumbe hai duniani kitakufa. 18Lakini nitafanya agano nawe. Utaingia katika safina, wewe pamoja na mkeo, wanao na wake zao. 19Nawe utaingiza katika safina jozi ya kila aina ya viumbe, wa kiume na wa kike, ili kuwahifadhi hai pamoja nawe.
20“Utaingiza kila aina ya ndege wa angani, kila aina ya mnyama, kila aina ya kiumbe kitambaacho, wawiliwawili, ili kuwahifadhi hai. 21Pia chukua aina zote za vyakula vinavyolika, uvihifadhi kwa ajili ya chakula chenu na viumbe hao.” 22Noa akafanya yote kama Mungu alivyomwamuru.

Mwanzo6;1-22


Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (BHN): 
Jifunze zaidi

Wednesday 25 January 2017

Kikombe Cha Asubuhi Mwanzo.5...



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje Wapendwa/Waungwana?
Tumshukuru Mungu kwa kutuamsha salama na kuiona tena Leo hii..
Walio Wagonjwa,wenye Shida/Tabu,Majaribu na kukata Tamaa Mungu akawaguse na kuwaponya katika yote.
 Mungu yu mwema sana na anawapenda,
Tumaini la kweli,Uponyaji na Faraja vyote vinapatikana kwakwe.
Yeye ni mwanzo na yeye ni mwisho,
Mungu wetu si kiziwi,Si kipofu,si Bubu,Ukimuomba,Ukiabudu,Ukiamini
kamwe hawezi kukuacha yeye anatosha..
Mungu aendelee kutubariki katika Kazi zetu,Shule,Biashara , Tuingiapo na Tutokapo,Vilaji na Vinyaji na katika yote sawasawa na Mapenzi Yake...
Yeye ni Mkuu katika yote..!!!
Muwe na wakati Mwema.


Wazawa wa Adamu

(1Nya 1:1-4)

1Ifuatayo ni orodha ya wazawa wa Adamu. Wakati Mungu alipomuumba binadamu, alimuumba kwa mfano wake. 2Aliwaumba mwanamume na mwanamke, kisha akawabariki na kuwapa jina “Binadamu.”
3Adamu alipokuwa na umri wa miaka 130, alipata mtoto aliyefanana naye, na mwenye sura kama yake; akamwita Sethi. 4Baada ya kumzaa Sethi, Adamu aliishi miaka 800, na kupata watoto wengine wa kiume na wa kike. 5Adamu alifariki akiwa na umri wa miaka 930.
6Sethi alipokuwa na umri wa miaka 105, alimzaa Enoshi. 7Baada ya kumzaa Enoshi, Sethi aliishi miaka 807, na kupata watoto wengine wa kiume na wa kike. 8Sethi alifariki akiwa na umri wa miaka 912.
9Enoshi alipokuwa na umri wa miaka 90, alimzaa Kenani. 10Baada ya kumzaa Kenani, Enoshi aliishi miaka 815 na kupata watoto wengine wa kiume na wa kike. 11Enoshi alifariki akiwa na umri wa miaka 905.
12Kenani alipokuwa na umri wa miaka 70, alimzaa Mahalaleli. 13Baada ya kumzaa Mahalaleli, Kenani aliishi miaka 840 na kupata watoto wengine wa kiume na wa kike. 14Kenani alifariki akiwa na umri wa miaka 910.
15Mahalaleli alipokuwa na umri wa miaka 65, alimzaa Yaredi. 16Baada ya kumzaa Yaredi, Mahalaleli aliishi miaka 830 na kupata watoto wengine wa kiume na wa kike. 17Mahalaleli alifariki akiwa na umri wa miaka 895.
18Yaredi alipokuwa na umri wa miaka 162, alimzaa Henoki. 19Baada ya kumzaa Henoki, Yaredi aliishi miaka 800 na kupata watoto wengine wa kiume na wa kike. 20Yaredi alifariki akiwa na umri wa miaka 962.
21Henoki alipokuwa na umri wa miaka 65, alimzaa Methusela. 22Henoki alikuwa mcha Mungu. Baada ya kumzaa Methusela, Henoki aliishi miaka 300 na kupata watoto wengine wa kiume na wa kike. 23Henoki aliishi miaka 365. 24Alikuwa mcha Mungu, akatoweka, kwa maana Mungu alimchukua.
25Wakati Methusela alipokuwa na umri wa miaka 187, alimzaa Lameki. 26Baada ya kumzaa Lameki, Methusela aliishi miaka 782, na kupata watoto wengine wa kiume na wa kike. 27Methusela alifariki akiwa na umri wa miaka 969.
28Wakati Lameki alipokuwa na umri wa miaka 182, alimzaa mtoto wa kiume. 29Alimwita mtoto huyo Noa, akisema, “Mtoto huyu ndiye atakayetufariji kutokana na kazi yetu ngumu tunayofanya kwa mikono yetu katika ardhi aliyoilaani Mwenyezi-Mungu.” 30Baada ya kumzaa Noa, Lameki aliishi miaka 595 na kupata watoto wengine wa kiume na wa kike. 31Lameki alifariki akiwa na umri wa miaka 777.
32Noa alipokuwa na umri wa miaka 500, alimzaa Shemu na Hamu na Yafethi.
Mwanzo5;1-32

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN): 
Jifunze zaidi

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

Tuesday 24 January 2017

Kikombe Cha Asubuhi;Mwanzo 4....



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje Wapendwa/Waungwana..?
Nimatumaini yangu mmeamka salama,Tunamshukuru Mungu  ametupa Neema ya Kuiona siku nyingine..
Tunaomba Mungu aendelee Kuwabariki,Kuwalinda,Kuwaongoza kwenye Vyombo vya usafiri na watembeao,
Akabriki kazi zetu ,Wanafunzi shuleni akawape ufahamu,Kukumbuka na kuelewa katika masomo yao..
Akabariki Vilaji/Vinywaji,Tuingiapo/Tutokapo...Akawe nasi katika yote na akatupe sawasawa na Mapenzi yake.
Akawabariki Yatima,Wajane,Wenye Shida/Tabu.
Wajawazito na Watafutao watoto Mfalme wa Amani akawaguse..
Sifa na Utukufu ni kwa Mungu muumba wetu...!!!!
Mkawe na wakati mwema.


Kaini na Abeli
1Adamu akalala na Hawa mkewe, naye akapata mimba, akamzaa Kaini. Hawa akasema, “Nimepata mtoto wa kiume kwa msaada wa Mwenyezi-Mungu!” 2Halafu akamzaa Abeli nduguye. Abeli alikuwa mfugaji kondoo na Kaini alikuwa mkulima. 3Baada ya muda fulani, Kaini alimtolea Mwenyezi-Mungu sadaka kutokana na mazao ya shambani, 4naye Abeli akamtolea Mungu sadaka ya wazawa wa kwanza wa kondoo wake na nyama nono. Mwenyezi-Mungu akapendezwa na Abeli na tambiko yake, 5lakini hakupendezwa na Kaini wala na tambiko yake. Basi, Kaini akakasirika sana na uso wake ukakunjamana. 6Mwenyezi-Mungu akamwambia Kaini, “Kwa nini umekasirika, na kwa nini uso wako umekunjamana? 7Je, ukitenda vyema hutakubaliwa? Na usipotenda vyema, basi, dhambi inakuvizia mlangoni; inakutamani, lakini unapaswa kuishinda.”
8Baadaye, Kaini akamwambia Abeli nduguye, “Twende nje shambani” Basi, walipokuwa shambani, Kaini akamvamia Abeli nduguye, akamuua. 9Mwenyezi-Mungu akamwuliza Kaini, “Ndugu yako Abeli yuko wapi?” Kaini akamjibu, “Mimi sijui! Je, mimi ni mlinzi wa ndugu yangu?” 10Mwenyezi-Mungu akasema, “Umefanya nini? Damu ya ndugu yako yanililia kutoka udongoni. 11Sasa wewe umelaaniwa! Hutailima tena ardhi yenye rutuba ambayo kama kinywa imeipokea damu ya nduguyo uliyemuua. 12Ukiilima ardhi haitakupatia tena mazao yake. Utakuwa mtu wa kutangatanga, asiye na makao maalumu duniani.”
13Kaini akamwambia Mwenyezi-Mungu, “Adhabu yangu ni kubwa mno; siwezi kuistahimili. 14Leo umenifukuza kutoka ardhi yenye rutuba na mbali nawe. Basi, nitakuwa mtu wa kutangatanga, asiye na makao maalumu duniani, na yeyote atakayeniona ataniua.” 15Lakini Mwenyezi-Mungu akamjibu, “Sivyo! Atakayekuua wewe Kaini atalipizwa mara saba.” Basi, Mwenyezi-Mungu akamtia Kaini alama ya tahadhari, ili yeyote atakayemwona asimuue. 16Kisha Kaini akaondoka mbele ya Mwenyezi-Mungu, akawa anaishi katika nchi ya Nodi, upande wa mashariki wa Edeni.
Wazawa wa Kaini
17Kaini akalala na mkewe, naye akapata mimba, akamzaa Henoki. Kaini akajenga mji akauita kwa jina la Henoki mwanawe. 18Henoki akamzaa Iradi, naye Iradi akamzaa Mehuyaeli; Mehuyaeli akamzaa Methushaeli, naye Methushaeli akamzaa Lameki. 19Lameki alioa wanawake wawili, mmoja aliitwa Ada na mwingine Sila. 20Ada alimzaa Yabali ambaye alikuwa baba yao wafugaji waishio mahemani. 21Ndugu yake alikuwa Yubali; huyo alikuwa baba yao wanamuziki wote wapigao zeze na filimbi. 22Sila naye alimzaa Tubal-kaini, ambaye alikuwa mhunzi wa vyombo vyote vya shaba na chuma. Dada yake Tubal-kaini alikuwa Naama.
23Lameki akawaambia wake zake,
“Ada na Sila sikieni sauti yangu!
Sikilizeni nisemayo enyi wake za Lameki.
Mimi niliua mtu kwa kunijeruhi,
naam, nilimuua kijana kwa kuniumiza.
24Ikiwa Kaini atalipizwa mara saba,
kweli Lameki atalipizwa mara sabini na saba.”

 Sethi na Enoshi
25Adamu akalala tena na Hawa mkewe, naye akazaa mtoto wa kiume, akamwita Sethi akisema, “Mungu amenijalia mtoto mahali pa Abeli aliyeuawa na Kaini.” 26Sethi naye alipata mtoto wa kiume, akamwita Enoshi. Hapo ndipo watu walipoanza kumwomba Mwenyezi-Mungu kwa jina lake.
Mwanzo 4;1-26

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN): 
Jifunze zaidi

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

Monday 23 January 2017

Kikombe Cha Asubuhi;Mwanzo 3...


Shalom,Habari za Asubuhi/Leo,Hamjambo,Mmeamkaje Wapendwa/Waungwana?
Nimatumaini yangu mnandelea vyema na Mungu anaendelea kuwatendea sawasawa na Mapenzi yake.
Ni wiki nyingine tena Mungu ametupa kibali cha kuiona tena,Tuanze wiki hii vyema na Mungu azidi
kuonekana katika maisha yetu,
Tuzidi kumsifu/Kumuabudu,Kumshukuru,Kumuomba na kumtafuta kwa bidii...
Akawe kiongozi wetu katika Kazi zetu,Shuleni,Nyumbani,Njiani na popote tulipo naye awepo...
Akatubariki tuingiapo na Tutokapo..
Akawe mfariji wa wote waliopatwa na misiba,Akawaguse wenye Shida/Tabu.
Alipo MUNGU yote yanawezekana..!!!
Muwe na siku njema.



Uasi wa binadamu
1Nyoka alikuwa mwerevu kuliko wanyama wote wa porini walioumbwa na Mwenyezi-Mungu. Basi, nyoka akamwambia huyo mwanamke, “Ati Mungu alisema msile matunda ya mti wowote bustanini?” 2Mwanamke akamjibu huyo nyoka, “Twaweza kula matunda ya mti wowote bustanini; 3lakini Mungu alisema, ‘Msile matunda ya mti ulio katikati ya bustani, wala msiuguse, msije mkafa.’” 4Nyoka akamwambia mwanamke, “Hamtakufa! 5Mungu alisema hivyo kwa sababu anajua kwamba mkila matunda ya mti huo mtafumbuliwa macho, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.”
6Basi, mwanamke alipoona kuwa mti huo ni mzuri kwa chakula, wavutia macho, na kwamba wafaa kwa kupata hekima, akachuma tunda lake, akala, akampa na mumewe, naye pia akala. 7Mara macho yao yakafumbuliwa, wakatambua kwamba wako uchi; hivyo wakajishonea majani ya mtini, wakajifanyia mavazi ya kiunoni.
8Jioni, wakati wa kupunga upepo, huyo mwanamume na mkewe wakasikia hatua za Mwenyezi-Mungu akitembea bustanini, nao wakajificha kati ya miti ya bustani, Mwenyezi-Mungu asipate kuwaona. 9Lakini Mwenyezi-Mungu akamwita huyo mwanamume, “Uko wapi?” 10Naye akamjibu, “Nimesikia hatua zako bustanini, nikaogopa na kujificha, maana nilikuwa uchi.” 11Mwenyezi-Mungu akamwuliza, “Nani aliyekuambia kwamba uko uchi? Je, umekula tunda la mti nililokuamuru usile?” 12Huyo mwanamume akajibu, “Mwanamke uliyenipa akae pamoja nami ndiye aliyenipa tunda la mti huo, nami nikala.”
13Hapo Mwenyezi-Mungu akamwuliza huyo mwanamke, “Umefanya nini wewe?” Mwanamke akamjibu, “Nyoka alinidanganya, nami nikala.”

Adhabu
14Kisha Mwenyezi-Mungu akamwambia nyoka,
“Kwa kuwa umefanya hivyo,
umelaaniwa kuliko wanyama wote wa kufugwa,
na kuliko wanyama wote wa porini.
Kwa tumbo lako utatambaa,
na kula vumbi siku zote za maisha yako.
15Nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke,
kati ya uzawa wako na uzawa wake;
yeye atakiponda kichwa chako,
nawe utamwuma kisigino chake.”
16Kisha akamwambia mwanamke,
“Nitakuzidishia uchungu wa kuzaa,
kwa uchungu utazaa watoto.
Hata hivyo utakuwa na hamu na mumeo,
naye atakutawala.”
17Kisha akamwambia huyo mwanamume,
“Kwa kuwa wewe umemsikiliza mkeo,
ukala matunda ya mti ambayo nilikuamuru usile;
kwa hiyo, kwa kosa lako ardhi imelaaniwa.
Kwa jasho utajipatia humo riziki yako,
siku zote za maisha yako.
18Ardhi itakuzalia michongoma na magugu,
nawe itakubidi kula majani ya shambani.
19Kwa jasho lako utajipatia chakula
mpaka utakaporudi udongoni ulimotwaliwa;
maana wewe ni mavumbi, na mavumbini utarudi.”
20Adamu akampa mkewe jina “Hawa”, kwani alikuwa mama wa binadamu wote. 21Mwenyezi-Mungu akawatengenezea Adamu na mkewe mavazi ya ngozi, akawavika.

Adamu na Hawa wanafukuzwa bustanini
22Kisha Mwenyezi-Mungu akasema, “Sasa, binadamu amekuwa kama mmoja wetu, anajua mema na mabaya. Lazima kumzuia kula lile tunda la mti wa uhai, kwani akilila ataishi milele!” 23Basi, Mwenyezi-Mungu akamfukuza Adamu nje ya bustani ya Edeni, ili akailime ardhi ambamo alitwaliwa. 24Alimfukuza nje, na kuweka mlinzi upande wa mashariki wa bustani ya Edeni na upanga wa moto uliogeuka huko na huko, kuilinda njia iendayo kwenye mti wa uhai.
Mwanzo 3;1-24

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (BHN): 
Jifunze zaidi

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.