Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Thursday 28 November 2019

Kikombe Cha Asubuhi;Isaya 65....



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu katika yote....

Mungu wetu Baba yetu,Muumba wetu Muumba wa Mbingu na Nchi
Muumba wa vyote vilivyomo vinavyoonekana na visivyoonekana
Mungu wa walio hai,Mungu  mwenye huruma,Mungu wa upendo
Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo...
Asante kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwatayari kwa majukumu yetu

Neema yako yatutosha ee Mungu wetu....!!

“Sikiliza! Kilio kinasikika kutoka Babuloni! Kishindo cha maangamizi makubwa kutoka nchi ya Wakaldayo! Maana mimi Mwenyezi-Mungu naiangamiza Babuloni, na kuikomesha kelele yake kubwa. Adui ananguruma kama mawimbi ya maji mengi, sauti ya kishindo chao inaongezeka.
Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,
tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako

Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote 
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba ukatupe neema
ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea
Usitutie majaribuni Mungu wetu tunaomba utuepushe
na yule mwovu na kazi zake zote
Jehovah ututakase miili yetu na akili zetu
Baba wa Mbinguni tunaomba utufunike kwa Damu
ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti
yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona....

Naam, mwangamizi anaijia Babuloni; askari wake wametekwa, pinde zao zimevunjwavunjwa. Mimi Mwenyezi-Mungu ni Mungu mwenye kuadhibu, hakika mimi nitalipiza kisasi kamili.
Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa katika utendaji
Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Yahweh tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomna ukatupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji
Tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe kama inavyokupendeza wewe...


Yahweh tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyovimiliki
Yahweh tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia
Baba wa Mbinguni tukawe salama rohoni
Yahwe ukatupe akili ya kutambua mema na mabaya
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu ukatupe macho ya kuona,masikio ya kusikia sauti yako na kuitii..
Baba wa Mbinguni  tunaomba ukatupe neema ya kufuata
njia zako,tukasimamie Neno lako,amri na sheria zako
siku zote za maisha yetu...
Ukatuguse kwa mkono wako wenye nguvu,ukatufanye chombo chema
ee Mungu wetu nasi tukatumike kama inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi....


Nitawalewesha wakuu na wenye hekima wake, watawala wake, madiwani na askari wake; watalala usingizi wa milele wasiinuke tena. Nasema mimi mfalme ambaye jina langu ni Mwenyezi-Mungu wa Majeshi. “Mimi Mwenyezi-Mungu wa Majeshi nasema: Ukuta mpana wa Babuloni utabomolewa mpaka chini, na malango yake marefu yatateketezwa kwa moto. Watu wanafanya juhudi za bure, mataifa yanajichosha maana mwisho wao ni motoni!”
Tazama watoto wako wenye shida/tabu,wote wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali
Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu
kila mmoja na mahitaji yake
Mungu wetu tunaomba ukawasamehe pale walipo kwenda kinyume nawe
Yahweh tunaomba ukawape neema ya kuweza kujiombea,kufuata njia zako nazo zikawaweke huru...
Baba wa Mbinguni tunayaweka haya yote mikononi mwako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele...
Amina...!!


Asanteni sana wapendwa katika Kristo Yesu kwakuwa nami,Baba wa Mbinguni aendelee kuwatendea sawasawa na mapenzi yake...
Nawapenda.


Mungu huwaadhibu waasi
1Mwenyezi-Mungu asema;
“Nilikuwa tayari kujionesha
kwao wasiouliza habari zangu.
Nilikuwa tayari kuwapokea
wale wasionitafuta.
Nililiambia taifa ambalo halikuomba kwa jina langu:
‘Nipo hapa! Nipo hapa!’
2 65:2 Taz Rom 10:21 Mchana kutwa niliwanyoshea mikono watu waasi,
watu ambao hufuata njia zisizo sawa,
watu ambao hufuata fikira zao wenyewe.
3Ni watu ambao daima hunichokoza waziwazi;
hutambikia miungu yao katika bustani,
na kuifukizia ubani juu ya matofali.
4Huketi makaburini na kukaa mafichoni usiku.
Hula nyama ya nguruwe na mchuzi wa wanyama haramu.
5Huwaambia wale wanaokutana nao:
‘Kaeni mbali nami;
msinikaribie kwani mimi ni mtakatifu!’
Watu hao wananikasirisha mno,
hasira yangu ni kama moto usiozimika.
6“Jueni kuwa nimelitia jambo hilo moyoni,
sitanyamaza bali nitawafanya walipe;
nitawafanya walipe kwa wingi.
7Mimi Mwenyezi-Mungu, nitawalipiza maovu yao
wayalipie na maovu ya wazee wao.
Wao waliifukizia ubani miungu yao milimani,
wakanitukana mimi huko vilimani.
Nitawafanya walipe kwa wingi,
watayalipia matendo yao ya awali.”
8Mwenyezi-Mungu asema hivi:
“Mtu akikuta kishada cha zabibu nzuri,
watu husema: ‘Tusikiharibu; kina baraka.’
Ndivyo nitakavyofanya kwa ajili ya watumishi wangu;
sitawaangamiza wote.
9Nitawajalia watu wa Yakobo,
na Yuda nitamjalia warithi wa milima yangu;
watumishi wangu watakaa huko.
10Nchi tambarare ya Sharoni itakuwa malisho,
bonde la Akori65:10 Akori: Maana yake Taabu. litakuwa mapumziko ya mifugo
kwa ajili ya watu wangu walionitafuta.
11“Lakini nitafanya nini na nyinyi
mnaoniacha mimi Mwenyezi-Mungu,
msioujali Siyoni, mlima wangu mtakatifu,
nyinyi mnaoabudu mungu ‘Gadi’,
na kumtolea tambiko ya divai mungu ‘Meni’?65:11 Gadi, yaani bahati na Meni, yaani ajali ni majina ya miungu.
12Nimewapangia kifo kwa upanga,
nyote mtaangukia machinjoni!
Maana, nilipowaita, hamkuniitikia;
niliponena, hamkunisikiliza.
Mlitenda yaliyo maovu mbele yangu,
mkachagua yale nisiyoyapenda.
13Basi, mimi Mwenyezi-Mungu nasema,
watumishi wangu watakula,
lakini nyinyi mtaona njaa;
watumishi wangu watakunywa,
lakini nyinyi mtaona kiu;
watumishi wangu watafurahi,
lakini nyinyi mtafedheheka.
14Watumishi wangu wataimba kwa furaha moyoni,
lakini nyinyi mtalia kwa uchungu moyoni
na kupiga kelele kwa uchungu mkubwa rohoni.
15Wale niliowachagua nitawapa jina jipya.
Lakini nyinyi jina lenu watalitumia kulaania;
‘Watasema: Bwana Mungu awaue kama hao.’
16Basi, mwenye kujitakia baraka nchini,
atajitakia baraka kwa Mungu wa kweli.
Mwenye kuapa katika nchi hii,
ataapa kwa Mungu wa kweli.
Maana taabu za zamani zimepita
zimetoweka kabisa mbele yangu.
Ulimwengu mpya
17“Sasa, naumba mbingu mpya na dunia mpya.
mambo ya zamani hayatakumbukwa tena.
18Furahini, mkashangilie milele,
kwa ajili ya vitu hivi ninavyoumba.
Yerusalemu nitaufanya mji wa shangwe,
na watu wake watu wenye furaha.
19 65:19 Taz Ufu 21:4 Nami nitaufurahia mji wa Yerusalemu,
nitawafurahia watu wangu.
Sauti ya kilio haitasikika tena,
kilio cha taabu hakitakuwako.
20Hakutakuwa tena na vifo vya watoto wachanga,
wazee nao hawatakufa kabla ya wakati wao.
Akifa mtu wa miaka 100 amekufa akiwa kijana;
na akifa kabla ya miaka 100 ni balaa.
21Watu watajenga nyumba na kuishi humo;
watalima mizabibu na kula matunda yake.
22Hawatajenga nyumba zikaliwe na watu wengine,
wala kulima chakula kiliwe na watu wengine.
Maana watu wangu niliowachagua
wataishi maisha marefu kama miti;
wateule wangu watafurahia matunda ya jasho lao.
23Kazi zao hazitakuwa bure,
wala hawatazaa watoto wa kupata maafa;
maana watakuwa waliobarikiwa na Mwenyezi-Mungu,
wamebarikiwa wao pamoja na wazawa wao.
24Hata kabla hawajaniita, mimi nitawaitikia;
kabla hawajamaliza kusema, nitakuwa nimewajibu.
25Mbwamwitu na kondoo watakula pamoja,
simba watakula nyasi kama ng'ombe,
nao nyoka chakula chao kitakuwa vumbi.
Katika mlima wangu wote mtakatifu,
hakuna atakayeumiza au kuharibu kitu.
Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”


Isaya65;1-25

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: