Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Wednesday 29 August 2018

Kikombe Cha Asubuhi ; Nehemia 5...



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Haleluyah Mungu wetu yu mwema sana
Tumshukuru Mungu wetu kila wakati
Asante Mungu wetu kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwatayari kwa majukumu yetu

Utukuzwe ee Mungu wetu,usifiwe Baba wa Mbinguni
Uabudiwe Jehovah,Uhimidiwe Yahweh,Matendo yako ni makuu mno,
Matendo yako ni ya ajabu,Matendo yako yanatisha
Hakuna kama wewe ee Mungu wetu..

Neema yako yatutosha Baba wa Mbinguni...!!


Nimefanya mambo mema na adili; usiniache makuchani mwa maadui zangu. Uahidi kunisaidia mimi mtumishi wako; usikubali wenye kiburi wanidhulumu. Macho yangu yanafifia nikingojea uniokoe, nikingojea utimize uliyoahidi. Unitendee mimi mtumishi wako kadiri ya wema wako, unifundishe masharti yako. Mimi ni mtumishi wako, unipe maarifa, nipate kujua maamuzi yako. Ee Mwenyezi-Mungu, sasa ni wakati wa kufanya kitu, kwa maana watu wanavunja sheria yako. Mimi, nazipenda amri zako, kuliko hata dhahabu safi kabisa. Kwa hiyo, nafuata kanuni zako zote; kila njia potovu naichukia.


Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha
na kujiachilia mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizo zifanya
Kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba ukatupe neema
ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea
Usitutie majaribu Mungu wetu tunaomba utuepushe
na yule mwovu na kazi zake zote
Jehovah ututakase miili yetu na akili zetu
Baba wa Mbinguni tunaomba utufunike kwa Damu
ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti
yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona

Kwakupigwa kwake sisi tumepata kupona...




Maamuzi yako ni ya ajabu; kwa hiyo nayashika kwa moyo wote. Maelezo ya mafundisho yako huleta mwanga; huwapa akili watu wasiojua kitu. Nafungua kinywa kwa hamu kubwa, maana ninatamani sana amri zako. Unigeukie na kunionea huruma, kama uwatendeavyo wanaokupenda. Uniimarishie hatua zangu kama ulivyoahidi; usikubali mimi nitawaliwe na uovu. Unikomboe kutoka udhalimu wa binadamu, ili nipate kuzishika kanuni zako. Uniangazie uso wako kwa wema, unifundishe masharti yako. Macho yangu yabubujika machozi kama mto, kwa sababu watu hawaishiki sheria yako.


Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa 
katika utendaji
Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki ridhiki zetu
ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba ukatupe neema ya kuweza
kuwabariki wenye kuhitaji
Yahweh tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Mungu wetu ukatupe kama inavyokupendeza wewe

Baba wa Mbinguni tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyo vimiliki
Yahweh tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia
Baba wa Mbinguni tukawe salama rohoni
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia 
sauti yako na kuitii

 Mungu wetu ukatupe akili ya kutambua mema na mabaya
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe neema ya kufuata njia zako
Yahweh tukasimamie Neno lako amri na sheria zako siku zote 
za maisha yetu
Mungu wetu ukaonekane katika maisha yetu
Neema zako zikawe nasi Nuru yako ikaangaze katika maisha yetu
ukatuguse kwa mkono wako wenye nguvu
Ukatufanye barua  njema ee Mungu wetu nasi tukasomeke kama
inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi...



Ee Mwenyezi-Mungu, wewe ni mwadilifu; na hukumu zako ni za haki. Umetoa maamuzi yako, kwa haki na uthabiti. Upendo wangu kwako wanifanya niwake hasira, maana maadui zangu hawajali maneno yako. Ahadi yako ni hakika kabisa, nami mtumishi wako naipenda. Mimi ni mdogo na ninadharauliwa; hata hivyo sisahau kanuni zako. Uadilifu wako ni wa haki milele; sheria yako ni ya kweli. Taabu na huzuni vimenipata, lakini amri zako ndizo furaha yangu. Maamuzi yako ni ya haki daima; unijalie maarifa nipate kuishi.


Baba wa Mbinguni tunawaweka mikononi mwako wenye shida/tabu
wote wanaopotia magumu/majaribu mbalimbali
watoto wako wanaokuomba kwa bidii na imani
Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu
 kila mmoja na mahitaji yake 
Yahweh tunaomba ukaonekane katika maisha yao
Jehovah tunaomba ukawaokoe,ukawavushe salama na  kuwalinda
Mungu wetu tunaomba ukawasamehe pale walipokwenda kinyume nawe
Baba wa Mbinguni ukawape neema ya kujiombea,kufuata njia zako
wakasimaie Neno lako nalo likaweke huru
Mungu wetu tunaomba ukasikie kuomba kwetu
Baba wa Mbinguni ukapokee sala/maombi yetu
Mungu wetu ukawatendee  kama inavyokupendeza wewe
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina...!!

Asanteni sana wapendwa katika Kristo Yesu kwakuwa nami
Mungu Baba aendelee kuwabariki na kuwatendea 
sawasawa na mapenzi yake....

Amani ya Bwana wetu Yesu Kristo na Upendo 
wa Mungu Baba ukae nanyi daima....
Nawapenda.


Maskini wanadhulumiwa

1Baada ya muda kulitokea malalamiko miongoni mwa watu, wanaume kwa wanawake, wakiwalalamikia ndugu zao Wayahudi. 2Kulitokea waliosema, “Tafadhali tupatie nafaka tule ili tuweze kuishi kwa kuwa sisi, wana wetu na binti zetu tu wengi.” 3Na wengine wakalalamika, “Tumeweka rehani mashamba yetu, mizabibu yetu hata na nyumba zetu ili kupata nafaka kwa sababu ya njaa.” 4Tena kukawa na hata wale, waliolalamika, wakisema, “Ili kulipa kodi ya mfalme juu ya mashamba na mizabibu yetu, ilitubidi tukope fedha. 5Lakini sisi ni sawa na Wayahudi wengine; watoto wetu ni sawa na watoto wao. Hata hivyo, tunawalazimisha watoto wetu kuwa watumwa. Baadhi ya binti zetu tayari ni watumwa. Hatuna uwezo wa kuzuia jambo hili kwani mashamba yetu na mizabibu yetu yameporwa na watu wengine.”
6Niliposikia malalamiko yao, nilikasirika sana. 7Nikaamua kuchukua hatua. Nikawashutumu wakuu na maofisa, nikawaambia, “Mnawatoza riba ndugu zenu.” 8Nikasema, “Kulingana na uwezo tulio nao, tumekuwa tukiwanunua tena ndugu zetu Wayahudi waliokuwa wameuzwa kwa watu wa mataifa mengine. Lakini sasa hata mnawauza ndugu zenu, nasi tunalazimika kuwanunua!” Basi walinyamaza kimya, bila kuwa na la kujibu.
9Kisha nikawaambia, “Mnalolifanya ni baya. Je, haiwapasi kumcha Mungu wetu ili kuzuia mataifa mengine yaliyo adui zetu yasitusute? 10Zaidi ya hayo, mimi mwenyewe, ndugu zangu na watumishi wangu tumewaazima ndugu zetu fedha na nafaka. Na hatutadai riba yoyote. 11Leo hii na muwarudishie mashamba yao, mashamba ya mizabibu, mashamba ya mizeituni na nyumba zao, hata na riba ya fedha, nafaka, divai, na mafuta ambayo nilikuwa ninawatoza.” 12Wao wakaitikia na kusema, “Tutawarudishia na hatutawadai chochote. Tutafanya kama ulivyosema.” Nikawaita makuhani mbele, na viongozi wote wakaapa mbele ya makuhani kufanya kama walivyoahidi. 13Nilikunguta kibindo changu na kusema, “Kila mmoja asiyetimiza ahadi hii Mungu na amkungute, amtoe katika nyumba yake na katika kazi yake. Basi, akungutike na kubaki mikono mitupu.” Mkutano mzima ukaitikia, na kusema, “Amina” wakamsifu Mwenyezi-Mungu. Watu wakafanya kama walivyokuwa wameahidi.

Tabia ya Nehemia

14Tangu wakati nilipoteuliwa kuwa mtawala wa nchi ya Yuda kwa miaka kumi na miwili yaani tangu mwaka wa ishirini mpaka mwaka wa thelathini na mbili wa kutawala kwa mfalme Artashasta, sikula chakula kinachostahili kuliwa na mtawala, wala ndugu zangu hawakufanya hivyo. 15Watawala walionitangulia walikuwa mzigo mzito kwa watu wakiwadai chakula na divai, mbali na kuwadai kuwalipa sarafu za uzito wa shekeli arubaini za fedha. Hata watumishi wao waliwadhulumu watu. Bali, mimi sikufanya hivyo, kwani nilimcha Mungu. 16Nilikuwa na juhudi nyingi katika ujenzi mpya wa ukuta huu na kamwe sikujipatia hata shamba. Hata watumishi wangu wote walifanya kazi hii kwa bidii. 17Zaidi ya hayo, kila siku niliwalisha watu 150, wakiwamo Wayahudi na maofisa, mbali na wale watu waliotujia toka mataifa jirani. 18Kila siku, ili kuwalisha watu hao, nilichinjiwa dume mmoja na kondoo safi sita na kuku. Kila baada ya siku kumi nilitoa kwa wingi viriba vya divai. Lakini licha ya haya yote, kwa kuwa watu walikuwa na mzigo mzito wa kubeba kila siku, sikutaka posho ya ziada.
19Sasa, ee Mungu wangu, kumbuka wema wangu wote niliowatendea watu hawa.



Nehemia5;1-19

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: