Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Thursday 2 February 2017

Kikombe Cha Asubuhi;Mwanzo 11....

Shalom,habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje Wapendwa/Waungwana?
Nimatumaini yangu mmeamka salama na mnaendelea/mmeanza na Mungu.
Mungu aendelee kutulinda,Kutubariki,Kututendea...
Katika Kazi,Biashara,Masomo,
Kwenye vyombo vya usafiri, Tuingiapo/Tutokapo,Vilaji/Vinywaji,Familia na katika yote
tumtangulize yeye Atoshaye,Ikawe siku njema yenye Amani,Furaha,Upendo,Faraja na shukrani...
Akawaguse wote Wanaopitia Magumu/Majaribu,Shida/Tabu Mungu hajawaacha Muite naye Ataitika
Mungu wetu yu mwema sana...!!!!!
Muwe na wakati mwema.


Mnara wa Babeli

1Kwanza, watu wote duniani walikuwa na lugha moja na walitumia maneno yaleyale. 2Basi, ikawa watu waliposafirisafiri kutoka mashariki, walifika katika nchi tambarare huko Shinari, wakakaa. 3Kisha wakaambiana, “Haya! Na tufyatue matofali, tuyachome moto vizuri.” Walikuwa na matofali badala ya mawe, na lami badala ya chokaa. 4Wakasema, “Na tujijengee mji na mnara ambao kilele chake kitafika mbinguni ili tujipatie jina, tusije tukatawanyika duniani kote.”
5Ndipo Mwenyezi-Mungu akashuka chini kuuona mji huo na mnara walioujenga binadamu. 6Mwenyezi-Mungu akasema, “Tazama, watu hawa ni taifa moja na wote wana lugha moja; huu ni mwanzo tu wa yale watakayoyafanya. Lolote wanalokusudia kulifanya watafanikiwa. 7Haya, na tushuke chini na kuivuruga lugha yao ili wasielewane wao kwa wao.” 8Hivyo, Mwenyezi-Mungu akawatawanya mahali pote duniani, nao wakaacha kuujenga ule mji. 9Mji huo ukaitwa Babeli, kwa sababu huko ndiko Mwenyezi-Mungu alikoivuruga lugha ya dunia yote, na kutoka huko akawatawanya watu kila mahali duniani.

Wazawa wa Shemu

10Wafuatao ni wazawa wa Shemu. Miaka miwili baada ya ile gharika, Shemu akiwa na umri wa miaka 100, alimzaa Arfaksadi. 11Baada ya kumzaa Arfaksadi, Shemu aliishi miaka 500 na kupata watoto wengine wa kiume na wa kike.
12Arfaksadi alipokuwa na umri wa miaka 35, alimzaa Shela. 13Baada ya kumzaa Shela, Arfaksadi aliishi miaka 403 na kupata watoto wengine wa kiume na wa kike.
14Shela alipokuwa na umri wa miaka 30, alimzaa Eberi. 15Baada ya kumzaa Eberi, Shela aliishi miaka 403 na kupata watoto wengine wa kiume na wa kike.
16Eberi alipokuwa na umri wa miaka 34, alimzaa Pelegi. 17Baada ya kumzaa Pelegi, Eberi aliishi miaka 430 na kupata watoto wengine wa kiume na wa kike.
18Pelegi alipokuwa na umri wa miaka 30, alimzaa Reu. 19Baada ya kumzaa Reu, Pelegi aliishi miaka 209 na kupata watoto wengine wa kiume na wa kike.
20Reu alipokuwa na umri wa miaka 32, alimzaa Serugi. 21Baada ya kumzaa Serugi, Reu aliishi miaka 207 na kupata watoto wengine wa kiume na wa kike.
22Serugi alipokuwa na umri wa miaka 30, alimzaa Nahori. 23Baada ya kumzaa Nahori, Serugi aliishi miaka 200 na kupata watoto wengine wa kiume na wa kike.
24Nahori alipokuwa na umri wa miaka 29, alimzaa Tera. 25Baada ya kumzaa Tera, Nahori aliishi miaka 119, na kupata watoto wengine wa kiume na wa kike.
26Tera alipokuwa na umri wa miaka 70, alimzaa Abramu na Nahori na Harani.

Wazawa wa Tera

27Wafuatao ni wazawa wa Tera, baba yao Abramu, Nahori na Harani. Harani alikuwa baba yake Loti. 28Huyo Harani alifariki wakati Tera baba yake alikuwa anaishi huko Uri alikokuwa amezaliwa. 29Abramu na Nahori walioa. Mke wa Abramu aliitwa Sarai. Mke wa Nahori aliitwa Milka, binti Harani ambaye pia alikuwa baba yake Iska. 30Sarai hakuwa na mtoto kwa sababu alikuwa tasa.
31Tera akamchukua Abramu mwanawe, Loti mjukuu wake aliyekuwa mwanawe Harani, na Sarai mkewe Abramu, wakaondoka wote pamoja toka Uri, mji wa Wakaldayo, wakaenda katika nchi ya Kanaani. Lakini walipofika Harani, wakakaa. 32Tera alifariki huko Harani akiwa na umri wa miaka 205.
Mwanzo11;1-32

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (BHN):
Jifunze zaidi

"Swahili Na Waswahili" Mbarikiwe sana.

Wednesday 1 February 2017

Kikombe Cha Asubuhi;Mwanzo 10....

Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje Wapendwa/Waungwana?
Ni mwezi/Siku mpya tena kwa mapenzi ya Muumba wa vyote ametupa Neema/Rehema ya kuiona tena..
Shukrani na Utukufu daima ni kwake Mungu,
Yeye awezaye yote,Yeye aponyae,
Yeye hutengeneza njia pasipo na njia,Yeye Abarikiae, Yeyeagawae ridhiki,Yeye ni mkuu wa vyote,
Yeye ni mwanzo na Yeye ni mwisho..
Jina lake na Litukuzwe milele na Milele.
Akawabariki wenye Shida/Tabu,Yatima/Wajane,Wagonjwa walio mahospitalini/Majumbani,Wafungwa wasio na Hatia
Waliopatwa na misiba akawe mfariji wao...
Wenye kutafuta watoto baba akawaguse...Wenye kukata tamaa wamgeukie Mungu yeye anaweza,
Tua mizigo uliyonayo Mungu anaponya....
Abariki Kazi zetu,Biashara Watoto wetu/Familia,Wanafunzi Mungu akawaongoze wapate kuelewa na kukumbuka wanayo fundishwa..Muombe kwa Kumaani sha,Kumtukuza na Kumsifu yeye Anatosha.!!!!
Mungu atuongoze vyema..


Wazawa wa Noa

1Baada ya gharika, watoto wa Noa, Shemu, Hamu na Yafethi, walipata watoto wa kiume na wa kike. Hii ndiyo orodha ya wazawa wao:
2Watoto wa kiume wa Yafethi walikuwa Gomeri, Magogu, Madai, Yavani, Tubali, Mesheki na Tirasi. 3Watoto wa kiume wa Gomeri walikuwa Ashkenazi, Rifathi na Togama. 4Watoto wa kiume wa Yavani walikuwa Elisha, Tarshishi, Kitimu na Dodanimu. 5Hawa ndio asili ya watu walioenea sehemu za pwani, kila watu kwa lugha yao, kwa jamaa zao na kufuata mataifa yao.
6Watoto wa kiume wa Hamu walikuwa Kushi, Misri, Puti na Kanaani. 7Watoto wa kiume wa Kushi walikuwa Seba, Hawila, Sabta, Raama na Sabteka. Watoto wa kiume wa Raama walikuwa Sheba na Dedani. 8Kushi alikuwa baba yake Nimrodi ambaye alikuwa shujaa wa kwanza duniani. 9Alikuwa mwindaji shujaa mbele ya Mwenyezi-Mungu, ndiyo maana kuna msemo usemao, “Kama Nimrodi mwindaji shujaa mbele ya Mwenyezi-Mungu.” 10Miji ya kwanza ya utawala wake ilikuwa Babuloni, Ereki na Akadi, katika nchi ya Shinari. 11Kutoka huko, Nimrodi alikwenda Ashuru, akajenga miji ya Ninewi, Rehoboth-iri, Kala na 12Reseni ulioko kati ya Ninewi na mji mkubwa wa Kala.
13Misri alikuwa babu wa Waludi, Waanamu, Walehabi, Wanaftuhi, 14Wapathrusi, Wakasluhi (ambao ndio asili ya Wafilisti), na Wakaftori.
15Kanaani alikuwa babu yake Sidoni, mzaliwa wake wa kwanza, na Hethi, 16na pia babu yao Wayebusi, Waamori, Wagirgashi, 17Wahivi, Waarki, Wasini, 18Waarvadi, Wasemari na Wahamathi. Baadaye watu wa jamii mbalimbali za Kanaani walitawanyika, 19hata eneo la nchi yao likawa toka Sidoni kuelekea kusini, hadi Gerari mpaka Gaza, na kuelekea mashariki hadi Sodoma na Gomora, Adma na Seboimu hadi Lasha. 20Hao ndio wazawa wa Hamu kadiri ya makabila yao, lugha zao, nchi zao na mataifa yao.
21Shemu, mkubwa wa Yafethi, alikuwa baba yao Waebrania wote. 22Watoto wa kiume wa Shemu walikuwa Elamu, Ashuru, Arfaksadi, Ludi na Aramu. 23Watoto wa kiume wa Aramu walikuwa Usi, Huli, Getheri na Mashi. 24Arfaksadi alimzaa Shela, Shela akamzaa Eberi. 25Eberi alikuwa na watoto wa kiume wawili; wa kwanza akamwita Pelegi kwa sababu wakati huo watu duniani waligawanyika, na wa pili akamwita Yoktani. 26Yoktani alikuwa baba wa Almodadi, Shelefu, Hasarmawethi, Yera, 27Hadoramu, Uzali, Dikla, 28Obali, Abimaeli, Sheba, 29Ofiri, Hawila na Yobabu. Hao wote walikuwa watoto wa Yoktani. 30Nchi walimokaa ilienea toka Mesha mpaka Sefari katika nyanda za juu za mashariki. 31Hao ndio wazawa wa Shemu, kadiri ya makabila yao, lugha zao, nchi zao na mataifa yao.
32Hao ndio jamaa za watoto wa Noa, kadiri ya vizazi vyao na mataifa yao. Kutokana nao mataifa yote yalienea duniani baada ya gharika.
Mwanzo10;1-32

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN):
Jifunze zaidi

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

Tuesday 31 January 2017

Kikombe Cha Asubuhi Mwanzo 9..

Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje Wapendwa/Waungwana?
Tumshukuru Mungu kwa kutuamsha tena siku hii iliyompendeza Mungu..
Ikawe yenye Baraka,Amani,Upendo na Furaha..
Abariki Kutoka/Kuingia kwetu,Katika Kazi zetu,Masomo,Biashara na yote..
Akatuongoze kwenye Kunena,Kusikia na Kutenda..
Akawaponye na kuwagusa wote wanaopitia katika Magumu/majaribu Shida/Tabu.
Sifa na Utukufu ni kwakwe Daima!!!!
Mbarikiwe sana.


Mungu anafanya agano na Noa

1Mungu akambariki Noa na wanawe, akiwaambia, “Zaeni, muongezeke, mkaijaze nchi. 2Wanyama wote, ndege wote wa angani, viumbe wote watambaao juu ya nchi na samaki wote wa baharini watakuwa na hofu na kuwaogopa nyinyi. Wote wamewekwa chini ya mamlaka yenu. 3Wanyama wote hai watakuwa chakula chenu kama vile nilivyowapa mimea kuwa chakula chenu. 4Lakini msile nyama yenye damu, kwani uhai uko katika damu. 5Damu ya uhai wenu nitaidai; nitaidai kutoka kwa kila mnyama na binadamu. Atakayemuua binadamu mwenzake, nitamdai uhai wake.
6Amwagaye damu ya binadamu,
damu yake itamwagwa na binadamu;
maana binadamu aliumbwa kwa mfano wa Mungu.
7Nanyi zaeni, mkaongezeke;
zaeni kwa wingi, mkaongezeke nchini.”

Upinde wa mvua

8Kisha Mungu akamwambia Noa na wanawe, 9“Ninaweka agano langu nanyi na wazawa wenu 10na viumbe vyote hai: Ndege, wanyama wa kufugwa na wanyama wa porini, wote waliotoka katika safina pamoja nanyi. 11Nathibitisha agano langu nanyi, kwamba, kamwe viumbe vyote hai havitaangamizwa kwa gharika, wala haitatokea tena gharika kuiharibu nchi.” 12Tena Mungu akasema, “Hii ndiyo alama ya agano ninalofanya kati yangu nanyi na kila kiumbe hai kilicho pamoja nanyi kwa vizazi vyote vijavyo. 13Naweka upinde wangu mawinguni, nao utakuwa ishara ya agano kati yangu na dunia. 14Kila nitakapoifunika dunia kwa mawingu, na huo upinde wa mvua utakapoonekana katika mawingu, 15nitalikumbuka agano langu nanyi na viumbe vyote hai. Kamwe maji hayatageuka kuwa gharika ya kuviangamiza viumbe vyote hai. 16Huo upinde utakapotokea mawinguni, nitauona na kulikumbuka agano hilo la milele kati yangu na viumbe vyote hai duniani.” 17Mungu akamwambia Noa, “Hii ndiyo ishara ya agano ambalo nimefanya na viumbe vyote hai duniani.”

Noa na wanawe

18Watoto wa Noa waliotoka katika safina walikuwa Shemu, Hamu na Yafethi. Hamu alikuwa baba yake Kanaani. 19Hao ndio watoto watatu wa Noa, na kutokana nao watu walienea duniani kote.
20Noa alikuwa mkulima wa kwanza. Alilima shamba la mizabibu, 21akanywa divai, akalewa, kisha akalala uchi hemani mwake. 22Hamu, baba yake Kanaani, aliuona uchi wa baba yake, akatoka nje na kuwaambia ndugu zake wawili. 23Lakini Shemu na Yafethi wakatwaa nguo, wakaitanda mabegani mwao, wakaenda kinyumenyume na kuufunika uchi wa baba yao. Waliangalia pembeni, wala hawakuuona uchi wa baba yao. 24Noa alipolevuka na kujua alivyotendewa na mwanawe mdogo, 25akasema,
“Kanaani na alaaniwe!
Atakuwa mtumwa wa watumwa kwa ndugu zake.”
26Tena akasema,
“Shemu na abarikiwe na Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu!
Kanaani na awe mtumwa wake.
27Mungu na amkuze Yafethi,
aishi katika hema za Shemu;
Kanaani na awe mtumwa wake.”
28Baada ya gharika, Noa aliishi miaka 350, 29kisha akafariki akiwa na umri wa miaka 950.
Mwanzo 9;1-28
Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (BHN):
Jifunze zaidi

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

Monday 30 January 2017

Kikombe Cha Asubuhi;Mwanzo 8....

Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje Wapendwa/Waungwana?
Ni wiki nyingine tena kwa uwezo,Neema/Rehema za Mungu ametujaalia kuiona tena Siku hii..
Tumrudishie Sifa/Utukufu kwa Muumba wa Yote,Yeye akisema atakubariki na hufanyika hivyo,
Yeye akisema ndiyo hakuna wa kupinga,
Tuanze wiki/siku hii na Mungu wetu akawe Mwanzo wa yote na mwisho wa yote.
Akabariki Kazi,Biashara,Masomo,Familia,Ndugu,Jamaa na Marafiki...
Wenye Shida/Tabu Mungu baba akawaguse,Yatima/Wajane baba ukawe nao..
Akatupe sawasawa na mapenzi yake.
Mungu wetu yu Mwema sana...!!!!
Tuanzena Mungu.


Mwisho wa gharika

1Kisha Mungu akamkumbuka Noa na wanyama wote wa porini na wa kufugwa waliokuwa pamoja naye ndani ya safina. Basi, Mungu akavumisha upepo juu ya nchi, maji yakaanza kupungua. 2Chemchemi za maji ya vilindi na madirisha ya mbinguni yakafungwa. Mvua ikazuiwa, 3maji yakaendelea kupungua polepole katika nchi. Baada ya siku 150, maji yakawa yamepungua sana. 4Mnamo siku ya kumi na saba ya mwezi wa saba, safina ikatua juu ya milima ya Ararati. 5Maji yakaendelea kupungua polepole, na siku ya kwanza ya mwezi wa kumi, vilele vya milima vikaonekana.
6Baada ya siku arubaini, Noa alifungua dirisha alilokuwa ametengeneza katika hiyo safina, 7akamtoa kunguru nje, naye hakurudi bali aliruka huko na huko mpaka maji yalipokauka nchini. 8Kisha Noa akamtoa njiwa apate kuona kama maji yalikuwa yamepungua juu ya nchi. 9Lakini, kwa vile maji yalikuwa bado yameifunika nchi yote, huyo njiwa hakupata mahali pa kutua, akamrudia Noa katika safina. Noa akanyosha mkono, akamtwaa na kumrudisha ndani ya safina. 10Noa akangoja siku nyingine saba, kisha akamtoa tena huyo njiwa. 11Njiwa huyo akamrudia Noa saa za jioni akiwa na tawi bichi la mzeituni mdomoni mwake. Kwa hiyo Noa akajua kwamba maji yalikuwa yamepungua katika nchi. 12Kisha akangoja siku nyingine saba, akamtoa tena yule njiwa; safari hii njiwa hakurudi kabisa.
13Noa alipokuwa na umri wa miaka 601, siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza, maji yalikuwa yamekauka katika nchi. Noa akafunua kifuniko cha safina na alipotazama, akaona kwamba nchi ilikuwa imekauka. 14Siku ya 27 ya mwezi wa pili, nchi ilikuwa imekauka kabisa.
15Hapo, Mungu akamwambia Noa, 16“Toka katika safina, wewe pamoja na mkeo, wanao na wake zao. 17Toa pia viumbe wote hai wa kila aina waliokuwa pamoja nawe, ndege na wanyama na kila kiumbe kitambaacho, wapate kuzaa kwa wingi duniani, waongezeke na kuenea kila mahali duniani.” 18Basi, Noa akatoka katika safina pamoja na wanawe na mkewe pamoja na wake za wanawe. 19Wakatoka kufuatana na jamii zao, wanyama wote wa porini, viumbe wote watambaao, ndege wote na wanyama wote hai duniani.

Noa anamtolea Mungu tambiko

20Noa akamjengea Mwenyezi-Mungu madhabahu, akatwaa mmoja katika kila aina ya wanyama walio safi na ndege walio safi, akamtolea Mungu sadaka za kuteketezwa. 21Harufu nzuri ya tambiko hiyo ikampendeza Mwenyezi-Mungu, naye akasema moyoni mwake, “Kamwe sitailaani tena nchi kwa sababu ya binadamu; najua kwamba mawazo yake ni maovu tangu utoto wake. Wala sitaangamiza tena viumbe wote kama nilivyofanya. 22Kadiri itakavyodumu nchi majira ya kupanda na kuvuna, ya baridi na joto, ya masika na kiangazi, usiku na mchana, hayatakoma.”
Mwanzo 8;1-22

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (BHN):
Jifunze zaidi


"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

Sunday 29 January 2017

Natumaini Mlikuwa/Mnaendelea na Jumapili hii Vjema

Natumaini Jumapili Ilikuwa njema/Inaendela vyema,
Mungu yu mwema na andelee kuwabariki katika yote..
hapa kwetu ni baridi inataka moyo kuamka Asubuhi na kwenda kwenye Ibada,
Basi tujitahidi kama tuwezavyo kwenda kutafuta mkate wetu..Mungu atusaidi na tushinde
Jaribu hili....
Tukumbushane kwa Amani na Upendo..




““Mimi ni mzabibu wa kweli, na Baba yangu ndiye mkulima. Kila tawi ndani yangu lisilozaa matunda yeye huliondoa, na kila tawi lizaalo hulisafisha lipate kuzaa zaidi. Nyinyi mmekwisha kuwa safi kwa sababu ya ule ujumbe niliowaambieni. Kaeni ndani yangu, nami nikae ndani yenu. Kama vile tawi haliwezi peke yake kuzaa matunda lisipobaki katika mzabibu, hali kadhalika nanyi hamwezi kuzaa matunda msipokaa ndani yangu. “Mimi ni mzabibu, nanyi ni matawi. Akaaye ndani yangu, nami nikiwa ndani yake, huyo huzaa matunda mengi, maana bila mimi hamwezi kufanya chochote. Mtu yeyote asipokaa ndani yangu hutupwa nje kama tawi litupwalo nje hata likakauka. Watu huliokota tawi la namna hiyo na kulitupa motoni liungue. Mkikaa ndani yangu na maneno yangu yakikaa ndani yenu, basi, ombeni chochote mtakacho nanyi mtapewa. Baba yangu hutukuzwa kama mkizaa matunda mengi na kuwa wanafunzi wangu. Mimi nimewapenda nyinyi kama vile Baba alivyonipenda mimi. Kaeni katika pendo langu. Mkizishika amri zangu mtakaa katika pendo langu, kama vile nami nilivyozishika amri za Baba yangu na kukaa katika pendo lake. Nimewaambieni mambo haya ili furaha yangu ikae ndani yenu, na furaha yenu ikamilike. Hii ndiyo amri yangu: Pendaneni; pendaneni kama nilivyowapenda nyinyi. Hakuna upendo mkuu zaidi kuliko upendo wa mtu atoaye uhai wake kwa ajili ya rafiki zake. Nyinyi ni rafiki zangu mkifanya ninayowaamuru. Nyinyi siwaiti tena watumishi, maana mtumishi hajui anachofanya bwana wake. Lakini mimi nimewaita nyinyi rafiki, kwa sababu nimewajulisha yote ambayo nimeyasikia kutoka kwa Baba yangu. Nyinyi hamkunichagua mimi; mimi niliwachagueni na kuwatuma mwende mkazae matunda, matunda yadumuyo, naye Baba apate kuwapeni chochote mnachomwomba kwa jina langu. Basi, amri yangu kwenu ndiyo hii: Pendaneni.”
‭‭Yohane‬ ‭15:1-17‬ ‭BHND‬‬
http://bible.com/393/jhn.15.1-17.bhnd














"Swahili Na Waswahili"Muwe na wakati mwema.

Friday 27 January 2017

Kikombe Cha Asubuhi;Mwanzo 7....


Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,mmeamkaje Wapendwa/Waungwana?
Nimatumaini yangu wengi mmeamka salama na wenye afya..
walio Wagonjwa,Wenye Shida/Tabu,Kufiwa na wanopitia kwenye Magumu/Majaribu Mungu kamwe hajawaacha.
Tuzidi kumuomba Baba wa yote,Mfalme wa Amani,Mwenye-enzi,Muumba wa Vyote,Mume wa Wajane,Baba wa Yatima,Yeye asiyechoka,Yeye asiye lala,Mwingi wa Rehema/Neema,Kimbilio letu,Baba wa Uzima,Yeye husamehe,
Sifa na Utukufu ni kwake daima...!!!!!
Akatubariki Tuingiapo/Tutokapo,Vilaji/Vinywaji,Masomoni,Biashara,Kazi
na tumtangulize kwa kila jambo.
Muwe na wakati mwema.

Gharika kuu

1Mwenyezi-Mungu akamwambia Noa, “Ingia ndani ya safina wewe pamoja na jamaa yako yote, kwa maana, kati ya watu wote wanaoishi nyakati hizi zako, nimekuona wewe peke yako kuwa mwadilifu mbele yangu. 2Chukua pamoja nawe wanyama wote walio safi, dume na jike, saba saba; lakini wanyama walio najisi, chukua dume na jike, wawiliwawili. 3Vilevile chukua ndege wa angani dume na jike, saba saba, ili kuzihifadhi hai aina zao duniani. 4Baada ya siku saba, nitanyesha mvua nchini siku arubaini mchana na usiku, na kila kiumbe hai nilichokiumba duniani nitakiangamiza.” 5Noa akafanya yote kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru.
6Noa alikuwa na umri wa miaka 600 wakati gharika ilipotokea nchini. 7Noa, mkewe, wanawe na wake zao wakaingia ndani ya safina ili kuiepa gharika. 8Wanyama walio safi, wanyama walio najisi, ndege na viumbe vyote vitambaavyo, 9wawiliwawili, dume na jike, wakaingia ndani ya safina pamoja na Noa kama Mungu alivyomwamuru. 10Baada ya siku saba, maji ya gharika yakaanza kuifunika nchi.
11Noa alipokuwa na umri wa miaka 600, mnamo siku ya kumi na saba ya mwezi wa pili, siku hiyo chemchemi zote za vilindi vya nchi zikabubujika maji, na madirisha ya mbinguni yakafunguka. 12Mvua ikanyesha nchini siku arubaini mchana na usiku. 13Siku hiyohiyo mvua ilipoanza kunyesha, Noa, mkewe na wanawe, Shemu, Hamu na Yafethi, pamoja na wake zao, waliingia ndani ya safina. 14Waliingia wao wenyewe pamoja na aina zote za wanyama wa porini, wanyama wafugwao, wanyama watambaao na ndege wa kila aina. 15Waliingia ndani ya safina pamoja na Noa wiliwawili wa kila aina ya viumbe hai. 16Kila aina yao waliingia, dume na jike, kama Mungu alivyomwamuru Noa. Kisha, Mwenyezi-Mungu akaufunga mlango wa safina nyuma yake Noa.
17Gharika ilidumu nchini kwa muda wa siku arubaini. Maji yakaongezeka na kuiinua safina, ikaelea juu ya ardhi. 18Maji yakaendelea kuongezeka zaidi nchini na safina ikaelea juu yake. 19Maji hayo yakawa mengi sana juu ya nchi, yakaifunika milima yote mirefu katika nchi. 20Yaliongezeka hata kuifunika milima kiasi cha mita saba na nusu. 21Viumbe wote hai katika nchi wakafa. Ndege, wanyama wa kufugwa, wanyama wa porini, makundi ya viumbe wote katika nchi kavu na wanadamu wote; 22naam, kila kiumbe hai katika nchi kavu kilikufa. 23Mungu akaangamiza kila kiumbe kilichokuwa hai duniani: Binadamu, wanyama, viumbe vitambaavyo na ndege wa angani. Vyote viliangamizwa duniani. Noa tu ndiye aliyesalimika na wale waliokuwa pamoja naye ndani ya safina. 24Maji hayo yalidumu katika nchi siku 150.
Mwanzo 7;1-24
Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN):
Jifunze zaidi


"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

Thursday 26 January 2017

Kikombe Cha Asubuhi;Mwanzo 6....

Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje Wapendwa/Waungwana?
Ni kwa Neema  ya Mungu tuu wala si kwa uwezo wetu kuiona tena siku hii...
sisi tumempa nini Mungu kwa Neema hii?Kipi hata kidogo umemfanyia,Unamfanyia Mungu
kwa kukupatia Neema hii ukiwa Hai, mwenye Afya njema,Nguvu,Akili timamu?
Wangapi wametamani kuendelea kuwepo na kupata hayo niliyoyasema na zaidi au hata kimoja wapo
lakini wameshindwa Asubuhi/siku ya leo?
Basi Wapendwa/Waungwana tutumie nafasi hii ya Neema ya Mungu vyema..
Popote tulipo Mungu wetu yupo..
Mungu akawabariki katika yote... Na akatuepushe na kila Ovu...
Awe nasi katika kazi zetu,Masomo, biashara, Vyombo vya usafiri,tutembee naye,Tuingiapo na Tutokapo,
Akawaguse wanaopitia Magumu,Wenye Shida/Tabu, Yatima na Wajane, Wagonjwa mahospitalini,Majumbani,Walio Magerezani pasipo na Hatia Mungu wetu akaonekane.
Tuendelee kukumbushana vyema..!!!!!!
Muwe na wakati mzuri.




Uovu wa binadamu

1Binadamu walipozidi kuongezeka duniani na kuzaa wasichana, 2watoto wa kiume wa Mungu waliwaona hao wasichana wa watu kuwa ni wazuri, wakawachukua wale waliowapenda kuwa wake zao. 3Hapo Mwenyezi-Mungu akasema, “Roho yangu haitakaa ndani ya binadamu milele, maana yeye ni wa kufa tu. Basi, hataishi zaidi ya miaka 120.” 4Nyakati hizo na hata baadaye, kulikuwa na majitu duniani ambao walikuwa wazawa wa watoto wa kiume wa Mungu na wasichana wa watu. Hao ndio watu waliokuwa mashujaa na wenye sifa enzi hizo, nao waliitwa Wanefili.
5Mwenyezi-Mungu alipoona wingi wa uovu wa binadamu duniani, na kwamba kila analokusudia binadamu moyoni mwake ni ovu daima, 6Mwenyezi-Mungu alisikitika sana kwa kumuumba binadamu duniani. Mwenyezi-Mungu alihuzunika sana moyoni mwake, 7hivyo akasema, “Nitamfuta kabisa duniani binadamu niliyemuumba; nitafutilia mbali pia wanyama wa porini, viumbe vitambaavyo na ndege wa angani. Ninasikitika kwamba niliwaumba duniani.” 8Lakini Noa alipata fadhili mbele ya Mwenyezi-Mungu.

Noa

9Ifuatayo ni habari juu ya Noa ambaye alikuwa ndiye mwadilifu pekee na ambaye hakuwa na lawama nyakati zake. Alikuwa mcha Mungu. 10Noa alikuwa na watoto watatu wa kiume: Shemu, Hamu na Yafethi. 11Mungu aliiona dunia kuwa imeharibika na kujaa ukatili. 12Naam, Mungu aliiangalia dunia, akaona kuwa imeharibika kabisa, kwa maana kila mtu alifuata njia yake mbovu.
13Mungu akamwambia Noa, “Nimeamua kuwaangamiza binadamu wote kwa sababu wameijaza dunia ukatili. Naam, nitawaangamiza kabisa pamoja na dunia! 14Kwa hiyo, jitengenezee safina kwa mbao za mpingo. Gawa vyumba ndani yake na ipake lami ndani na nje. 15Utaitengeneza hivi: Urefu wake mita 139, upana wake mita 25 na kimo chake mita 15. 16Safina hiyo iwe ya ghorofa tatu na yenye mlango pembeni. Itengenezee paa, kisha acha nafasi ipatayo nusu mita kati ya paa na dari. 17Nitaleta gharika ili kuangamiza viumbe vyote hai duniani. Kila kiumbe hai duniani kitakufa. 18Lakini nitafanya agano nawe. Utaingia katika safina, wewe pamoja na mkeo, wanao na wake zao. 19Nawe utaingiza katika safina jozi ya kila aina ya viumbe, wa kiume na wa kike, ili kuwahifadhi hai pamoja nawe.
20“Utaingiza kila aina ya ndege wa angani, kila aina ya mnyama, kila aina ya kiumbe kitambaacho, wawiliwawili, ili kuwahifadhi hai. 21Pia chukua aina zote za vyakula vinavyolika, uvihifadhi kwa ajili ya chakula chenu na viumbe hao.” 22Noa akafanya yote kama Mungu alivyomwamuru.

Mwanzo6;1-22


Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (BHN): 
Jifunze zaidi