Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Thursday 5 October 2017

Kikombe Cha Asubuhi Kumbukumbu la Sheria 32 (Kumbukumbu la Torati katika tafsiri nyingine)



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu katika yote..
Mungu wetu,Baba yetu,Muumba wetu na Muumba wa vyote...
Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo..
Baba wa upendo,Baba wa Baraka,Mfalme wa Amani..
Yahweh,Jehovah,El shaddai,Elo him,El Olam,El Qanna,Emanuel..
Mungu pamoja nasi..!!
Utukuzwe Jehovah,Uhimidiwe Yahweh,Usifiwe Mungu wetu..
Uabudiwe Baba wa Mbinguni,Hakuna kama wewe..
wewe ni mwanzo na wewe ni mwisho,Alfa na Omega..
Unatosha Mungu wetu,Matendo yako ni ya ajabu...
Matendo yako ni makuu mno...!!



Sasa, ndugu, napenda kuwakumbusha ile Habari Njema niliyowahubirieni, nanyi mkaipokea na kusimama imara ndani yake. Kwa njia yake mnaokolewa, ikiwa mnayazingatia maneno niliyowahubirieni, na kama kuamini kwenu hakukuwa bure. Mimi niliwakabidhi nyinyi mambo muhimu sana ambayo mimi niliyapokea: Kwamba Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu kufuatana na Maandiko Matakatifu; kwamba alizikwa, akafufuka siku ya tatu kufuatana na Maandiko Matakatifu; kwamba alimtokea Kefa, na baadaye aliwatokea wale kumi na wawili. Kisha aliwatokea ndugu zaidi ya 500 kwa mara moja; wengi wao wanaishi bado, lakini baadhi yao wamekwisha kufa. Baadaye alimtokea Yakobo kisha akawatokea mitume wote. Baada ya wote, akanitokea hata mimi, mimi niliyekuwa kama mtu aliyezaliwa kabla ya wakati. Maana mimi ni mdogo kabisa miongoni mwa mitume, na wala sistahili kuitwa mtume, kwa sababu nililidhulumu kanisa la Mungu. Lakini, kwa neema yake Mungu, nimekuwa kama nilivyo, na neema yake kwangu haikuwa bure. Mimi nimefanya kazi kuliko wote; si mimi hasa, ila ni neema ya Mungu ifanyayo kazi pamoja nami. Lakini hata hivyo, iwe wao ndio wahubirio au mimi nihubiriye, haidhuru, hiki ndicho tunachohubiri, na hiki ndicho mnachoamini.

Asante Baba wa Mbinguni kwa wema na fadhili zako kwetu..
Asante kwa ulinzi wako wakati wote..
Asante kwakutuchagua tena na kutupa kibali cha kuendelea
kuiona leo hii..
Si kwamba sisi ni wema sana,wala si kwamba sisi ni wazuri mno
Si kwa nguvu zetu wala uwezo wetu sisi kuwa hivi tulivyo..
Ni kwa mapenzi yako,nikwa Neema na rehema zako Mungu wetu

Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha
na tukijiachilia mikononi mwako Mungu wetu..
Baba tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizozifanya..
kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua..
Jehovah nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe
wale wote waliotukosea..
Baba wa Mbinguni tunaomba utuepushe katika majaribu
 na utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote...
Mungu wetu tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu
na utufunike kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo wa Nazareti..
Yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona..




Sasa, maadamu inahubiriwa kwamba Kristo amefufuliwa kutoka kwa wafu, baadhi yenu wanawezaje kusema kwamba hakuna ufufuo wa wafu? Kama hakuna ufufuo wa wafu, basi, Kristo naye hakufufuka; na kama Kristo hakufufuka, basi mahubiri yetu hayana maana na imani yenu haina maana. Zaidi ya hayo sisi tungekuwa mashahidi wa uongo mbele ya Mungu, maana tulisema kwamba Mungu alimfufua Kristo kutoka kwa wafu na kumbe yeye hakumfufua – kama ni kweli kwamba wafu hawafufuliwi. Maana, ikiwa ni kweli kwamba wafu hawafufuki, basi naye Kristo hakufufuka. Na kama Kristo hakufufuliwa, basi, imani yenu ni ya bure; mngali bado katika dhambi zenu. Zaidi ya hayo, wale wote waliokufa wakiwa wameungana na Kristo wamepotea kabisa. Kama matumaini yetu katika Kristo yanahusu tu maisha haya ya sasa, basi, sisi ni watu wa kusikitikiwa zaidi kuliko wengine wote duniani. Lakini ukweli ni kwamba Kristo amefufuliwa kutoka kwa wafu, wa kwanza wa wale waliolala katika kifo. Maana kama vile kifo kilivyoletwa duniani na mtu mmoja, vivyo hivyo nako kufufuka kutoka kwa wafu kumesababishwa na mtu mmoja. Kama vile watu wote wanavyokufa kwa kujiunga na Adamu, vivyo hivyo wote watafufuliwa kwa kuungana na Kristo. Lakini kila mmoja kwa mpango wake: Kristo kwanza; halafu wale walio wake Kristo wakati Kristo atakapokuja. Baada ya hayo, mwisho utafika wakati ambapo Kristo atamkabidhi Mungu Baba ufalme, baada ya kufutilia mbali kila tawala na mamlaka na nguvu. Maana Kristo sharti atawale mpaka Mungu atakapowashinda maadui zake wote na kuwaweka chini ya miguu yake. Adui wa mwisho atakayeangamizwa ni kifo. Maana, Maandiko yasema: “Mungu ameweka vitu vyote chini ya miguu yake.” Lakini, Maandiko yanaposema: “Vitu vyote vimewekwa chini ya miguu yake avitawale” ni dhahiri kwamba Mungu haingii katika kundi hilo la vitu, maana yeye ndiye anayeviweka vitu hivyo chini ya Kristo. Lakini vitu vyote vitakapowekwa chini ya utawala wa Kristo, ndipo naye Mwana atakapojiweka chini ya Mungu, aliyeweka vyote chini ya utawala wake; ili Mungu atawale juu ya vyote. Kama hakuna ufufuo, je watu wale wanaobatizwa kwa ajili ya wafu wanatumainia kupata nini? Kama wafu hawafufuliwi, ya nini kubatizwa kwa ajili yao? Na sisi, ya nini kujitia hatarini kila saa? Ndugu, mimi nakikabili kifo kila siku! Fahari niliyo nayo juu yenu katika kuungana na Kristo Yesu Bwana wetu inanifanya nitangaze jambo hili. Kama kusudi langu lingalikuwa la kibinadamu tu, kule kupigana kwangu na wanyama wakali hapa Efeso kungalinifaa kitu gani? Kama wafu hawafufuki, basi, “Tule na tunywe, maana kesho tutakufa.” Msidanganyike! Urafiki mbaya huharibu tabia njema. Amkeni! Anzeni kuishi vema, na acheni kutenda dhambi. Baadhi yenu hawamjui Mungu kabisa. Hii nawaambieni, ni aibu kubwa kwenu!



Yahweh tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu,Biashara,
Masomo na yote tunayoenda kufanya/kutenda tukatende
sawasawa na mapenzi yako..
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki ridhiki zetu
ziingiazo/zitokazo,Mungu wetu nasi tunaomba utupe neema
ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji..
Jehovah tusipungukiwe katika mahitaji yetu..
Yahweh ukatupe sawasawa na mapenzi yako..

Mfalme wa Amani tuyaweka maisha yetu mikononi mwako..
Nyumba/Ndoa zetu,watoto,wazazi,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka..
Mungu wetu tunaomba ulinzi wako,Furaha,Amani yako ikatawale..
Upendo ulio wako,hekima,busara na tukanene yaliyo yako..
Tukasimamie Neno lako Amri na Sheria zako siku zote za maisha yetu
Ukatufanye chombo chema nasi tukatumike kama inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi..



Lakini mtu anaweza kuuliza: “Wafu watafufuliwaje? Watakuwa na mwili wa namna gani?” Hayo ni maswali ya kijinga! Ukipanda mbegu, isipokufa kwanza haitaota. Unachopanda ni mbegu tu, labda ya ngano au nafaka nyingine, na si mmea mzima ambao hutokea baadaye. Mungu huipa hiyo mbegu mwili anaoutaka mwenyewe; kila mbegu hupata mwili wake wa pekee. Miili ya viumbe vyote si sawa. Miili ya binadamu ni ya namna moja, ya wanyama ni ya namna nyingine, ya ndege ni ya namna nyingine na miili ya samaki pia ni ya namna nyingine. Iko miili ya mbinguni na miili ya duniani; uzuri wa miili ya mbinguni ni mwingine, na uzuri wa miili ya duniani ni mwingine. Uko uzuri wa jua, wa mwezi na wa nyota; hata nyota nazo huhitilafiana kwa uzuri. Ndivyo ilivyo kuhusu ufufuo wa wafu. Kama vile mbegu, mwili huzikwa ardhini ukiwa katika hali ya kuharibika, lakini hufufuliwa katika hali ya kutoharibika. Huzikwa katika hali duni, hufufuliwa katika hali tukufu; huzikwa katika hali dhaifu, hufufuliwa ukiwa wenye nguvu. Unapozikwa ni mwili wa kawaida, unapofufuliwa ni mwili wa kiroho. Kuna mwili wa kawaida na kutakuwa na mwili wa kiroho. Maana Maandiko yasema: “Mtu wa kwanza, Adamu, alikuwa kiumbe mwenye uhai;” lakini Adamu wa mwisho ni Roho awapaye watu uhai. Lakini unaotangulia kuwako si ule mwili wa kiroho, ila ule mwili wa kawaida, kisha ule mwili wa kiroho. Adamu wa kwanza aliumbwa kwa udongo, alitoka ardhini; mtu wa pili alitoka mbinguni. Wote walio wa dunia wako kama huyo mtu aliyeumbwa kwa udongo; wale walio wa mbinguni wako kama yule aliyetoka mbinguni. Kama vile tulivyofanana na yule aliyeumbwa kwa udongo, vivyo hivyo tutafanana na huyo aliyetoka mbinguni.

Yahweh tazama wenye shida/tabu,wagonjwa,wenye njaa..
waliokata tamaa,waliokataliwa,wenye mashaka/hofu..
walioanguka na kuelemewa na mizigo,walio katika vifungo vya 
yule mwovu na wote wenye kuhitaji..
Mungu wetu tunaomba unyooshe mkono wako wenye nguvu...
ukawaguse na kuwaponya kimwili na kiroho pia..
Baba wa Mbinguni ukawafungue na wakapate kuwa huru..
Yahweh ukawasimamishe na kuwasamehe wale waliokwenda kinyume nawe..
Baba wa Mbimnguni ukawape neema ya kujiombea ,Mfalme wa Amani Nuru yako ikaangaze katika maisha ya watoto wako..
Baba ukasikie kulia kwao Jehovah ukawafute machozi yao
Baba wa Mbinguni ukapokee sala/maombi yao..
Yahweh ukawape neema ya kukujua wewe na kusimamia
Neno lako na wakafuate njia zako nao wakapate kuwa huru..
Wafiwa ukawe mfariji wao..



Basi, ndugu, nasema hivi: Kile kilichofanywa kwa mwili na damu hakiwezi kuushiriki ufalme wa Mungu; na chenye kuharibika hakiwezi kuwa na hali ya kutoharibika. Sikilizeni, nawaambieni siri: Sisi hatutakufa sote, ila sote tutageuzwa, wakati wa mbiu ya mwisho, kwa nukta moja, kufumba na kufumbua. Maana tarumbeta ya mwisho itakapolia, wafu watafufuliwa katika hali ya kutoweza kufa tena, na sisi tutageuzwa. Maana ni lazima kila kiharibikacho kijivalie hali ya kutoharibika, mwili uwezao kufa ujivalie hali ya kutokufa. Basi, mwili huu wenye kuharibika utakapojivalia hali ya kutoharibika, na kile chenye kufa kitakapojivalia hali ya kutokufa, hapo ndipo litakapotimia lile neno lililoandikwa: “Kifo kimeangamizwa; ushindi umekamilika!” “Kifo, ushindi wako uko wapi? Uwezo wako wa kuumiza uko wapi?” Kifo hupata sumu yake katika dhambi, nayo dhambi hupata nguvu yake katika sheria. Lakini tumshukuru Mungu anayetupatia ushindi kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristo. Basi, ndugu zangu wapenzi, simameni imara na thabiti. Endeleeni daima kuwa na bidii katika kazi ya Bwana, mkijua kwamba kazi mnayofanya katika utumishi wa Bwana haitapotea bure.

Jehovah tunayaweka haya yote mikononi mwako..
Tukishukuru na kuamini wewe ndiye Mungu wetu..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina..!!
Wapendwa/waungwana asanteni sana kwakuwa nami..
Baba wa faraja,upendo,Amani awe nanyi 
Nuru yake ikaangaze katika maisha yenu..
Nawapenda.


1“Tegeni masikio enyi mbingu:
Sikiliza, ee dunia, maneno ninayosema.
2Mafundisho yangu na yatone kama mvua,
maneno yangu yadondoke kama umande,
kama manyunyu kwenye mimea michanga,
kama mvua nyepesi katika majani mabichi.
3Maana nitalitangaza jina la Mwenyezi-Mungu,
nanyi mseme, ‘Mungu wetu ni Mkuu’.
4“Mwenyezi-Mungu ni Mwamba wa usalama;
kazi zake ni kamilifu,
njia zake zote ni za haki.
Yeye ni Mungu mwaminifu asiye na kosa,
yeye hufanya mambo ya uadilifu na ya haki.
5Lakini nyinyi mmekosa uaminifu kwake,
nyinyi sio watoto wake tena kwa sababu ya uovu,
nyinyi ni kizazi kiovu na kipotovu.
6Mnawezaje kumlipa hivyo Mwenyezi-Mungu,
enyi watu wapumbavu na msio na akili?
Je, yeye siye Baba yenu aliyewaumba,
aliyewafanya na kuwaimarisha?
7Kumbukeni siku zilizopita,
fikirieni miaka ya vizazi vingi;
waulizeni baba zenu nao watawajulisha,
waulizeni wakubwa wenu nao watawaeleza.
8Mungu Mkuu alipoyagawia mataifa mali yao,
alipowagawa wanadamu,
kila taifa alilipatia mipaka yake,
9kulingana na idadi ya watoto wa Mungu,32:9 watoto wa Mungu: Tafsiri kadiri ya hati ya Kumrani. Kiebrania: Watoto wa Israeli.
lakini alijiwekea watu wa Yakobo kuwa wake,
hao alijichagulia kuwa mali yake.
10Aliwakuta katika nchi ya jangwa,
nyika tupu zenye upepo mkali.
Aliwalinda na kuwatunza,
aliwafanya kama mboni ya jicho lake.
11Kama tai alindaye kiota chake,
na kurukaruka juu ya makinda yake,
akitandaza mabawa yake ili kuwashikilia,
na kuwabeba juu ya mabawa yake.
12Yeye Mwenyezi-Mungu mwenyewe aliwaongoza
na hapakuwa na mungu mwingine wa kumsaidia.
13Aliwapitisha katika nyanda za juu za nchi,
nao wakala mazao ya mashambani.
Akawapa asali miambani waonje
na mafuta kutoka mwamba mgumu.
14Aliwapa siagi na maziwa ya mifugo,
mafuta ya wanakondoo na kondoo madume,
makundi ya mifugo ya Bashani na mbuzi.
Aliwapa ngano nzuri kabisa na divai mpya wakanywa.
15Watu wa Israeli walinona na kupiga mateke;
walinenepa, wakawa na kitambi na kunawiri;
kisha wakamwacha Mungu aliyewaumba,
wakamdharau Mwamba wa wokovu wao.
16Walimfanya aone wivu mkali kwa miungu yao,
walimchochea akasirike kwa matendo yao ya kuchukiza.
17Walitambikia majini ambayo hayakuwa miungu,
waliiendea miungu ambayo hawakuijua kamwe,
miungu mipya iliyotokea siku za karibuni,
ambayo wazee wao hawakuiheshimu kamwe.
18Hamkumjali Mwamba aliyewapa uhai,
mlimsahau Mungu aliyewazaa nyinyi.
19Mwenyezi-Mungu aliona jambo hilo akawaacha;
aliwakataa watoto wake, waume kwa wake.
20Akasema, ‘Nitawaficha uso wangu
nione mwisho wao utakuwaje!
Maana wao ni kizazi kipotovu,
watoto wasio na uaminifu wowote.
21Wamenichochea kuona wivu kwa kitu kisicho mungu,
wamenikasirisha kwa sanamu zao.
Hivyo nitawafanya waone wivu kwa kisicho watu,
nitawakasirisha kwa kutumia taifa la wapumbavu.
22Hasira yangu imewaka moto,
inachoma mpaka chini kuzimu,
itateketeza dunia na vilivyomo,
itaunguza misingi ya milima.
23Nitarundika maafa chungu nzima juu yao,
nitawamalizia mishale yangu.
24Watakonda kwa njaa,
wataangamizwa kwa homa kali.
Nitapeleka wanyama wenye meno makali kuwashambulia,
na nyoka wenye sumu wanaotambaa mavumbini.
25Vita vitasababisha vifo vingi nje
na majumbani hofu itawatawala,
vijana wa kiume na wa kike watauawa
hata wanyonyao na wazee wenye mvi.
26Nilisema, ningaliwaangamiza kabisa
na kuwafanya wasikumbukwe tena na mtu yeyote,
27ila tu kwa sababu ya majivuno ya maadui zao
ili maadui zao wasije wakafikiria vingine;
wasije wakasema, wamefaulu kuwaangamiza,
nami Mwenyezi-Mungu sihusiki katika mambo haya!’
28“Israeli ni taifa lisilo na akili,
watu wake hawana busara ndani yao.
29Wangekuwa na hekima wangejua kwa nini walishindwa,
wangeweza kuelewa mwisho wao utakuwaje.
30Mtu mmoja anawezaje kuwashinda watu 1,000,
au watu wawili wanawezaje kuwashinda watu 10,000,
isipokuwa kama Mwamba wao amewatupa,
Mwenyezi-Mungu wao amewaacha?
31Hata adui zetu wenyewe wamekiri wazi,
mwamba wao hauna nguvu kama mwamba wetu.
32Maana mizabibu yao ni miche ya Sodoma
zimetoka katika konde za Gomora;
zabibu zake ni zabibu zenye sumu,
vishada vyake ni vichungu.
33Divai yao ni kama sumu ya nyoka,
ina sumu kali ya majoka.
34“Je sina njia ya kuwaadhibu?
Silaha zangu ninazo mkononi.
35Kisasi ni juu yangu,
mimi nitalipiza,
wakati miguu yao itakapoteleza;
maana siku yao ya maafa imewadia,
mwisho wao u karibu sana.
36Mwenyezi-Mungu atawatetea watu wake,
na kuwahurumia watumishi wake,
wakati atakapoona nguvu zao zimeishia,
wala hakuna aliyebaki, mfungwa au mtu huru.
37Ndipo Mwenyezi-Mungu atakapowauliza watu wake,
‘Iko wapi ile miungu yenu,
mwamba mlioukimbilia usalama?’
38Iko wapi hiyo miungu iliyokula matoleo yenu
na kunywa divai na tambiko zenu za kinywaji?
Basi na iinuke, iwasaidieni;
acheni hiyo iwe kinga yenu sasa!
39Oneni kuwa mimi ndimi Mungu
na wala hakuna mwingine ila mimi.
Mimi huua na kuweka hai;
hujeruhi na kuponya,
na hakuna awezaye kumwokoa yeyote mikononi mwangu.
40Nanyosha mkono wangu mbinguni,
na kuapa, kwa uhai wangu wa milele,
41kama mkiuona upanga wangu umeremetao,
na kunyosha mkono kutoa hukumu,
nitawalipiza kisasi maadui zangu,
nitawaadhibu wale wanaonichukia.
42Mishale yangu nitailevya kwa damu,
upanga wangu utashiba nyama,
utalowa damu ya majeruhi na mateka
na adui wenye nywele ndefu.
43“Enyi mataifa washangilieni watu wake,
maana yeye hulipiza kisasi damu ya watumishi wake,
huwalipiza kisasi wapinzani wake,
na kuitakasa nchi ya watu wake.”
44Mose alikuja mbele ya Yoshua, mwana wa Nuni, wakakariri maneno ya wimbo huu, ili Waisraeli wote wausikie.

Wosia wa Mose

45Mose alipomaliza kuwaambia watu wa Israeli maneno haya yote, 46aliwaambia, “Yawekeni mioyoni mwenu maneno yote ambayo ninawapeni leo. Lazima muwaamuru watoto wenu ili wafuate kwa uaminifu maneno yote ya sheria hii. 47Maana sheria hii si maneno matupu bali ni uhai wenu; kwa sheria hii mtaishi maisha marefu katika nchi mnayokwenda kuimiliki, ngambo ya mto Yordani.”
48Siku hiyohiyo, Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose, 49“Panda mlima huu wa Abarimu, mlima Nebo katika nchi ya Moabu, mkabala wa mji Yeriko, ukaiangalie nchi ya Kanaani ninayowapa Waisraeli waimiliki. 50Kisha ufariki hukohuko mlimani kama kaka yako Aroni alivyofariki katika mlima Hori, 51kwa sababu nyote wawili mlivunja uaminifu wenu kwangu mbele ya Waisraeli mlipokuwa kwenye maji ya Meriba, karibu na mji wa Kadeshi, katika jangwa la Sini, mkakosa kuuthibitisha utakatifu wangu kati ya Waisraeli. 52Utaiona nchi iliyo mbele yako, lakini hutaingia katika nchi hiyo ninayowapa Waisraeli.”



Kumbukumbu la Sheria 32:1-52

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

Wednesday 4 October 2017

Kikombe Cha Asubuhi Kumbukumbu la Sheria 31 (Kumbukumbu la Torati katika tafsiri nyingine)




Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Mungu wetu yu mwema sana tumshukuru katika yote..
Asante Mungu wetu Baba yetu kwa wema na fadhili zako kwetu..
Asante kwakutuchagua tena na kutupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa ulinzi wako wakati wote..
Utukuzwe Mungu wetu,Unastahili sifa,Unastahili kuabudiwa..
Baba wa yatima,Mume wa wajane,Mfalme wa Amani Muweza wa yote
Alfa na Omega,Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo..
Kimbilio letu,Faraja yetu,Baba wa Huruma hakuna kama wewe
Matendo yako ni ya ajabu,Matendo yako ni makuu mno..



Ni vema kukushukuru, ee Mwenyezi-Mungu, kuliimbia sifa jina lako, ee Mungu Mkuu. Ni vema kutangaza fadhili zako asubuhi, na uaminifu wako nyakati za usiku, kwa muziki wa zeze na kinubi, kwa sauti tamu ya zeze. Ee Mwenyezi-Mungu, matendo yako yanifurahisha; nitashangilia kwa sababu ya mambo yote uliyotenda. Matendo yako, ee Mwenyezi-Mungu, ni makuu mno! Mawazo yako ni mazito mno! Mtu mpumbavu hawezi kufahamu, wala mjinga hajui jambo hili:

Tunakuja mbele zako Baba wa Mbinguni tukijinyenyekeza,
tujikishusha na kujiachilia mikononi mwako Mungu wetu..
Jehovah tunaomba utusamehe makosa yetu yote tuliyoyafanya..
Kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwajua/kutojua..
Yahweh nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe
wale wote waliotukosea..
Baba wa Mbinguni tunaomba utuepushe katika majaribu
 na utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote..
Mungu wetu tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu
Baba utufunike kwa Damu ya mwanao mpendwa Bwana na 
Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti..
Yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona..
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Biashara,masomo na vyote tunavyoenda kufanya/kutenda
tukatende sawasawa na mapenzi yako..
ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo Yahweh nasi 
tunaomba utupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji..
Tusipungukiwe katika mahitaji yetu 
Jehovah ukatupe sawasawa na mapenzi yako..

Mfalme wa Amani tunaomba ukatawale katika maisha yetu..
Amani ikawe nasi katika nyumba/ndoa zetu,watoto,wazazi wetu
familia/ndugu na wote wanaotuzunguka Mungu wetu ukawe
Mlinzi mkuu,ukatamalaki na kutuatamia,ukatubariki na 
ukatupe macho ya rohoni na masikio ya kusikia sauti yako
ukatupe neema ya kusimamia Neno lako Amri na Sheria zako
Ukatufanye chombo chema nasi tukatumike kama inavyo kupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi




Kumbuka kwamba, katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za taabu. Watu watakuwa na ubinafsi, wenye tamaa ya fedha, wenye majivuno, wenye kujiona, wenye kumtukana Mungu, wasiowatii wazazi wao, wasio na shukrani na waovu; watatokea watu wasio na upendo moyoni, wasio na huruma, wachongezi, walafi na wakali; watachukia chochote kilicho chema; watakuwa wahaini, wakaidi na waliojaa kiburi; watapenda anasa kuliko kumpenda Mungu. Kwa nje wataonekana kama watu wenye kumcha Mungu, lakini wataikana nguvu yake. Jiepushe kabisa na watu wa namna hiyo. Baadhi yao huenda katika nyumba za watu na huwateka wanawake dhaifu waliolemewa mizigo ya dhambi na ambao wanaongozwa na tamaa za kila aina; wanawake ambao wanajaribu daima kujifunza lakini hawawezi kuufikia ujuzi wa huo ukweli. Watu hao huupinga ukweli kama vile Yane na Yambre walivyompinga Mose. Hao ni watu wa akili potovu na imani ya uongo. Lakini hawataweza kuendelea zaidi kwa maana upumbavu wao utaonekana wazi kwa wote. Ndivyo ilivyokuwa kwa akina Yane na Yambre. Wewe, lakini, umeyafuata mafundisho yangu, mwenendo wangu, makusudi yangu katika maisha, imani yangu, uvumilivu wangu, upendo wangu, subira yangu, udhalimu na mateso. Unayajua mambo yaliyonipata huko Antiokia, Ikonio na Lustra. Nilivumilia udhalimu mkubwa mno! Lakini Bwana aliniokoa katika mambo hayo yote. Kila mtu anayetaka kuishi maisha ya kumcha Mungu katika kuungana na Kristo Yesu lazima adhulumiwe. Watu waovu na wadanganyifu wataendelea kuwa wabaya, wakidanganya wengine, na wao wenyewe wakidanganywa. Lakini wewe dumu katika ukweli ule uliofundishwa ukaukubali kabisa. Wawajua wale waliokuwa waalimu wako, wakumbuka kwamba tangu utoto wako umejua Maandiko Matakatifu ambayo yaweza kukupatia hekima iletayo wokovu kwa njia ya imani kwa Kristo Yesu. Maandiko yote Matakatifu yameandikwa kwa uongozi wa Mungu, na yanafaa katika kufundishia ukweli, kuonya, kusahihisha makosa, na kuwaongoza watu waishi maisha adili, ili mtu wa Mungu awe mkamilifu, na tayari kabisa kufanya kila kazi njema.

Baba wa Mbinguni ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu wote
wataabikao,wagonjwa,wenye njaa,shida/tabu,wali katika
vifungo vya yule mwovu,waliokata taama na wote walioanguka
Baba wa Mbinguni ukawaiunue na kuwapa uponyaji wa mwili
na roho,ukawasamehe pale walipokwenda kinyume nawe
ukawape neema ya kukujua wewe na kufuata njia zako
wakapate neema ya kujiombea Baba na ukapokee sala/maombi yao
ukasikie kulia kwao na ukawafute machozi yao..
eeh Baba tunaomba upokee sala/maombi ya watoto wako..



Kwa sababu hiyo, nampigia magoti Baba, aliye asili ya jamaa zote duniani na mbinguni. Namwomba Mungu, kadiri ya utajiri wa utukufu wake, awajalieni kwa uwezo wa Roho wake, nguvu ya kuwa imara ndani yenu, naye Kristo akae mioyoni mwenu kwa imani. Namwomba mpate kuwa na mzizi na msingi katika mapendo kusudi muweze kufahamu pamoja na watu wote wa Mungu jinsi upendo wa Kristo ueneavyo kwa mapana na marefu, kwa kimo na kina. Naam, mpate kujua upendo wa Kristo upitao elimu yote, mjazwe kabisa utimilifu wote wa Mungu. Kwake yeye ambaye kwa nguvu yake ifanyayo kazi ndani yetu aweza kufanya mambo makuu zaidi ya yale tuwezayo kuomba au kufikiria; kwake Mungu uwe utukufu katika kanisa na katika Kristo Yesu, nyakati zote, milele na milele! Amina.
Sifa na utukufu tunakurudishia Mungu wetu..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina..!!
Asanteni sana wapendwa katika Bwana kwa kuwa nami
Baraka,Amani,Furaha na upendo visipungue katika maisha yenu
Mungu aendelee kuwabariki na kuwafadhili..
Nawapenda.

Yoshua anachukua mahali pa Mose

(Hes 27:12-23)

1Mose aliendelea kuongea na Waisraeli wote, 2akawaambia, “Mimi sasa nina umri wa miaka 120, na sina nguvu ya kufanya kazi zaidi. Tena Mwenyezi-Mungu, ameniambia kuwa sitavuka mto Yordani. 3Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, atawatangulia na kuyaangamiza mataifa yanayoishi huko, ili muimiliki nchi yao. Yoshua atakuwa kiongozi wenu kama alivyosema Mwenyezi-Mungu. 4Mwenyezi-Mungu atayaangamiza mataifa hayo kama vile alivyowaangamiza Sihoni na Ogu, wafalme wa Waamori, na nchi yao. 5Mwenyezi-Mungu atawapeni ushindi juu yao nanyi mtawatendea kama nilivyowaamuru. 6Muwe imara na hodari, wala msiwaogope au kutishwa nao, maana Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu ndiye anayekwenda pamoja nanyi. Yeye hataacha kuwasaidia na hatawatupa.”
7Kisha Mose akamwita Yoshua, akamwambia mbele ya watu wote wa Israeli, “Uwe Imara na hodari, maana wewe utawaongoza watu hawa kwenda kuimiliki nchi ambayo Mwenyezi-Mungu aliwaahidi babu zao; nawe utawakabidhi waimiliki. 8Mwenyezi-Mungu ndiye anayewaongoza; yeye atakuwa pamoja nanyi; yeye hataacha kuwasaidia na hatawatupa. Hivyo, msiogope wala msifadhaike.”

Kukumbuka sheria kila mwaka wa saba

9Basi, Mose aliandika sheria hiyo, akawapa makuhani wa ukoo wa Lawi ambao walikuwa na jukumu la kubeba agano la Mwenyezi-Mungu, na wazee wote wa Israeli. 10Kisha akawaamuru akasema, “Kila mwaka wa saba utakuwa mwaka wa mafungulio. Katika sikukuu ya vibanda, mwaka huo, 11wakati watu wa Israeli wanapokuja mbele ya Mwenyezi-Mungu mahali pale atakapochagua mtawasomea watu wote wa Israeli sheria hii. 12Wakusanye watu: Wanaume, wanawake, watoto na wageni wanaoishi katika miji yenu, ili kila mmoja asikie maneno haya ya kujifunza kumcha Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, na kuwa waangalifu kutekeleza maneno ya sheria hii. 13Nao wazawa wao ambao hawajasikia sheria ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, wapate kuisikia na kujifunza kumcha Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, muda wote mtakaoishi katika nchi ambayo mnakwenda kuimiliki ngambo ya mto Yordani.”
14Basi, Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose, “Siku yako ya kuaga dunia imekaribia. Mwite Yoshua, mje pamoja katika hema la mkutano ili nimpe maagizo.” Basi, Mose na Yoshua wakaenda katika hema la mkutano, 15naye Mwenyezi-Mungu akawatokea humo katika nguzo ya wingu ambayo ilisimama kwenye mlango wa hema.
16Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose, “Umekaribia sasa kuaga dunia, na baada ya kufariki, watu wataanza kuniacha na kuiendea miungu mingine ya nchi hiyo ambamo watakwenda kuishi; wataniacha na kuvunja agano nililoagana nao. 17Hapo hasira yangu itawawakia siku hiyo, nami nitawaacha na kuuficha uso wangu mbali nao, wataangamizwa. Maovu mengi na taabu zitawavamia hata watambue kwamba maovu hayo yamewapata kwa kuwa Mungu wao hayupo miongoni mwao. 18Hakika nitawaficha uso wangu kwa sababu wamefanya mambo maovu na kuigeukia miungu mingine.
19“Sasa, andika wimbo huu, uwafundishe watu wa Israeli ili uwe ushahidi wangu juu yao. 20Nitakapowapeleka katika nchi inayotiririka maziwa na asali, kama nilivyowaapia babu zao, nao wakala wakashiba na kunenepa, wataigeukia miungu mingine na kuitumikia; watanidharau na kulivunja agano langu. 21Watakapovamiwa na maafa mengi na taabu, wimbo huu utawakabili kama ushahidi kwani hautasahauliwa na wazawa wao. Na hata sasa, kabla sijawapeleka katika nchi niliyoapa kuwapa, naijua mipango ambayo wanapanga.”
22Basi, Mose aliandika wimbo huo siku hiyohiyo, akawafundisha Waisraeli.
23Kisha Mwenyezi-Mungu akamwagiza Yoshua, mwana wa Nuni, akamwambia, “Uwe imara na hodari, maana utawaongoza Waisraeli katika nchi ambayo nimewaapia kuwapa, nami nitakuwa pamoja nawe.”
24Mose alipomaliza kuandika maneno ya sheria hiyo tangu mwanzo mpaka mwisho, 25aliwaambia Walawi, waliokuwa na jukumu la kubeba lile sanduku la agano la Mwenyezi-Mungu, 26“Chukueni kitabu hiki cha sheria, mkiweke karibu na sanduku la agano la Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, ili kiwe ushahidi dhidi yenu. 27Maana najua mlivyo waasi na wakaidi. Ikiwa mmemwasi Mwenyezi-Mungu wakati niko hai pamoja nanyi, itakuwaje baada ya kifo changu? 28Wakusanye mbele yangu wazee wote wa makabila yenu na maofisa wenu nipate kusema maneno haya wasikie, nazo mbingu na dunia zishuhudie juu yao. 29Maana ninajua kuwa baada ya kifo changu hakika mtakuwa waovu na kuiacha ile njia niliyowaamuru mwifuate. Na katika siku zijazo mtakumbwa na maafa kwa kuwa mtafanya maovu mbele ya Bwana na kumkasirisha kwa matendo yenu.”

Wimbo wa Mose

30Halafu, Mose akakariri maneno ya wimbo huu mbele ya kusanyiko lote la Waisraeli.



Kumbukumbu la Sheria 31:1-30


Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

Tuesday 3 October 2017

Kikombe Cha Asubuhi Kumbukumbu la Sheria 30 (Kumbukumbu la Torati katika tafsiri nyingine)



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu katika yote..
Mtakatifu..!Mtakatifu..!Mtakatifu..! Baba wa Mbinguni..
Mungu wetu,Muumba wetu,Muumba wa Mbingu na Nchi na vyote
vilivyomo vinavyoonekana na visivyoonekana..
Mfalme wa Amani,Baba wa Upendo,Baba wa Baraka..
Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo..!
Muweza wa yote,hakuna lisilowezekana juu yako..
Unatosha Baba wa Mbinguni,Hakuna kama wewe.
Alfa na Omega,Matendo yako ni makuu sana,Matendo yako ni ya Ajabu..



Yahusu sasa vyakula vilivyotambikiwa sanamu: Tunajua kwamba sisi sote tuna ujuzi, lakini ujuzi huo huwafanya watu wawe na majivuno; lakini mapendo hujenga. Anayefikiri kwamba anajua kitu, kwa kweli hajui chochote kama inavyompasa. Lakini anayempenda Mungu, huyo anajulikana naye. Kwa hiyo, kuhusu vyakula vilivyotambikiwa sanamu, twajua kwamba sanamu si kitu duniani; twajua kwamba Mungu ni mmoja tu. Hata kama viko vitu viitwavyo miungu duniani au mbinguni, na hata kama wako miungu na mabwana wengi, hata hivyo, kwetu sisi yuko Mungu mmoja tu; Baba, Muumba wa vyote, ambaye kwa ajili yake sisi tuko. Pia yuko Bwana mmoja tu, Yesu Kristo, ambaye kwa njia yake vitu vyote viliumbwa, na sisi twaishi kwa njia yake.


Asante Mungu wetu kwa wema na fadhili zako kwetu..
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii..
Tazama jana imepita Baba wa Mbinguni Leo ni siku mpya Jehovah Kesho ni siku nyingine..
Mungu wetu tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza, tukijishusha na tukijiachilia mikononi mwako Baba wa Mbinguni..
Tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizozifanya..
Kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua..
Jehovah nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea..
Baba wa Mbinguni tunaomba utuepushe katika majaribu na utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote..
Nguvu za giza,nguvu za mizimu,Nguvu za mapepo,nguvu za mpinga Kristo
Zishindwe katika jina lililokuu kupita majina yote 
jina la Bwana wetu Yesu Kristo wa Nazareti..
Yahweh tunaomba ututakase na utufunike kwa Damu ya 
Mwanao mpendwa Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo..
kwakupigwa kwakwe sisi tumepona..


Nani aliyeamini mambo tuliyosikia? Nani aliyetambua kuwa mkono wa Mwenyezi-Mungu ulihusika? Maana, mbele yake Mwenyezi-Mungu, mtumishi wake alikua kama mti mchanga, kama mzizi katika nchi kavu. Hakuwa na umbo wala sura ya kutupendeza, wala hakuwa na uzuri wowote wa kutuvutia. Alidharauliwa na kukataliwa na watu, alikuwa mtu wa uchungu na huzuni. Alikuwa kama mtu kinyaa kwa watu; alidharauliwa na tukamwona si kitu. Hata hivyo alivumilia majonzi yetu, na kubeba huzuni zetu. Sisi tulifikiri amepata adhabu, amepigwa na Mungu na kuteswa. Lakini alijeruhiwa kwa sababu ya dhambi zetu, aliumizwa kwa sababu ya maovu yetu. Kwa kuadhibiwa kwake sisi tumepata uhai; kwa kupigwa kwake sisi tumepona.

Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu..
Jehovah ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo..
Mfalme wa Amani nasi tunaomba utupe neema ya kuweza
kuwabariki wenye kuhitaji..
Baba wa Mbinguni ukabariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Mungu wetu ukavitakase na Ukavifunike kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo...

Yahweh tunayaweka maisha yetu mikononi mwako..
Amani na upendo vikatawale katika Nyumba/Ndoa zetu
Watoto/wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanao tuzunguka
Mungu wetu tunaomba ulinzi wako wakati wote..
Baba wa Mbinguni ukatamalaki na kutuatamia..
Jehovah ukatupe hekima,busara na tukawe baraka kwa wengine..
Tukanene yaliyo yako,tukasikie sauti yako na ukatupe macho ya rohoni
tukapate kutambua na kujitambua..
Tukasaidiane na kuhurumiana,tukaelimishane kwa upendo na tukachuliane...
Ukatupe neema ya kusimamia Neno lako Amri na Sheria zako siku zote za maisha yetu..
Tukawe barua njema popote tupitato na tukasomeke kama inavyokupendeza wewe..


Basi, nasema hivi: Mwenendo wenu na uongozwe na Roho, nanyi hamtafuata tena tamaa za kidunia. Maana, tamaa za kidunia hupingana na matakwa ya roho; na matakwa ya Roho hupingana na tamaa za kidunia. Mambo hayo mawili hayaafikiani; kwa sababu hiyo hamwezi kufanya yale mnayotaka nyinyi wenyewe. Kama mkiongozwa na Roho, basi, hamko tena chini ya sheria. Basi, matendo ya kidunia yanajulikana: Uzinzi, uasherati, ufisadi; kuabudu sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, choyo, mabishano, mafarakano; husuda, ulevi, ulafi na mambo mengine kama hayo. Nawaambieni tena kama nilivyokwisha sema: Watu wanaotenda mambo hayo hawataupata ufalme wa Mungu uwe wao. Lakini matokeo ya kuongozwa na Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, wema, fadhili, uaminifu, upole na kiasi. Hakuna sheria inayoweza kupinga mambo hayo. Wale walio na Kristo wameisulubisha hali yao ya kidunia pamoja na mawazo yake mabaya na tamaa zake. Tukiishi kwa msaada wa Roho, na tuufuate mwongozo wake. Basi, tusijivune, tusichokozane wala kuoneana wivu.
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi..

Sifa na Utukufu tunakurudishia Mungu wetu..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na
 Utukufu hata Milele..
Amina...!
Asanteni sana wapendwa katika Bwana kwakuwa nami..
Baba wa Baraka na upendo awe nanyi daima..
Mkono wake wenye nguvu ukawaguse na Amani ya
Kristo iwe nanyi daima..
Nawapenda. 


Matumaini mema kwa siku zijazo

1Mose akaendelea kusema, “Nimewapeni uchaguzi kati ya baraka na laana. Mambo hayo yote yakiwapata nanyi mkiyatafakari popote mlipo miongoni mwa mataifa ambamo Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu atakuwa amewatawanya, 2mkamrudia Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, nyinyi na watoto wenu, mkatii kwa moyo wote na roho yote neno lake ninalowaamuru leo, 3hapo Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, atawarudishieni mema yenu na kuwahurumia na kuwakusanya tena kutoka katika mataifa ambamo atakuwa amewatawanya. 4Na hata kama mmetawanywa katika sehemu mbali kabisa duniani, Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, atawakusanya na kuwarudisheni, 5ili muimiliki tena nchi ambamo waliishi wazee wenu. Naye atawafanya mfanikiwe zaidi na kuwa wengi kuliko wazee wenu. 6Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, atawafanyeni nyinyi na wazawa wenu muwe na moyo wa utii ili mumpende yeye kwa moyo wenu wote na roho yenu yote, mpate kuishi. 7Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, atazifanya laana hizi zote ziwapate adui zenu ambao waliwatesa. 8Nanyi mtaitii sauti ya Mwenyezi-Mungu na kuzishika amri zake zote ninazowapeni leo. 9Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu atawafanya mfanikiwe katika kila mtakalofanya; mtakuwa na watoto wengi na ng'ombe wengi na mashamba yenu yatatoa mazao. Maana atapenda tena kuwafanya mfanikiwe kama vile alivyopenda kuwafanikisha wazee wenu, 10ikiwa mtiatii sauti yake na kushika amri na masharti yake yaliyoandikwa katika kitabu hiki cha sheria na kumrudia Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, kwa moyo wote na roho yote.
11“Amri ninazowapa leo si ngumu mno kwenu, wala haziko mbali nanyi. 12Haziko mbinguni hata mseme, ‘Nani atakayepanda juu mbinguni kutuletea ili tupate kuzisikia na kuzitii?’ 13Wala haziko ngambo ya bahari, hata mseme, ‘Nani atakayevuka bahari atuletee ili tuzisikie na kuzitii.’ 14Sivyo, ila zipo karibu nanyi, vinywani mwenu na mioyoni mwenu, mpate kuzitekeleza.
15“Leo hii nawapeni uchaguzi kati ya mema na mabaya; kati ya uhai na kifo. 16Kama mkitii amri za Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, ambazo ninawapa leo, mkampenda Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, na kufuata njia zake na kushika masharti na maagizo yake, basi, mtaishi na kuongezeka; naye Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu,30:16 mkitii amri za Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu: Kiebrania hakina maneno hayo. atawabariki katika nchi ambayo mnakwenda kuimiliki. 17Lakini mkipotoshwa na kukataa kumsikiliza, mkavutwa kuabudu miungu mingine na kuitumikia, 18mimi nawatangazieni leo hii kwamba mtaangamia. Hamtaishi kwa muda mrefu katika nchi mnayokwenda kuimiliki, ngambo ya mto wa Yordani. 19Naziita mbingu na dunia zishuhudie juu yenu leo hii, kwamba nimewapeni uchaguzi kati ya uhai na kifo, kati ya baraka na laana. Basi, chagueni uhai nyinyi na wazawa wenu mpate kuishi, 20mkimpenda Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, mkiitii sauti yake na kuambatana naye. Maana kufanya hivyo kunamaanisha kwamba mtapata maisha marefu na kuishi katika nchi ambayo Mwenyezi-Mungu aliwaahidi wazee wenu, Abrahamu, Isaka na Yakobo, kwamba atawapeni.”


Kumbukumbu la Sheria 30:1-20

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

Monday 2 October 2017

Kikombe Cha Asubuhi Kumbukumbu la Sheria 29 (Kumbukumbu la Torati katika tafsiri nyingine)




Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Haleluyah..!Haleluyah..!Mungu wetu yu mwema sana..
Tumshukuru Mungu wetu katika yote..
Ni Mwezi/wiki/siku nyingine tena Baba wa Mbinguni umetuchagua na kutupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii...
Asante kwa wema na fadhili zako kwetu..
Asante kwa Ulinzi wako wakati wote..



Basi, tukiwa wafanyakazi pamoja na Mungu, tunawasihi msikubali ile neema mliyopokea kutoka kwa Mungu ipotee bure. Mungu asema hivi: “Wakati wa kufaa nimekusikiliza, wakati wa wokovu nikakusaidia.” Basi, sasa ndio wakati wa kufaa; sasa ndiyo siku ya wokovu! Kusudi tusiwe na lawama yoyote katika utumishi wetu, hatupendi kumwekea mtu yeyote kizuizi chochote. Badala yake, tunajionesha kuwa kweli watumishi wa Mungu kwa kila kitu: Kwa uvumilivu mwingi wakati wa mateso, shida na taabu. Tumepigwa, tumetiwa gerezani na kuzomewa hadharani; tumefanya kazi tukachoka; tumekesha na kukaa bila kula. Tunajionesha kuwa watumishi wa Mungu kwa usafi wa moyo, elimu, uvumilivu na wema; kwa Roho Mtakatifu, kwa upendo usio na unafiki, kwa ujumbe wa kweli na kwa nguvu ya Mungu. Uadilifu ndiyo silaha yetu kila upande. Tuko tayari kupata heshima na kudharauliwa, kulaumiwa na kusifiwa. Twadhaniwa kuwa waongo, kumbe twasema kweli; kama wasiojulikana, kumbe twajulikana kwa wote; kama waliokufa, lakini mwonavyo, sisi ni hai kabisa. Ingawa tumeadhibiwa, hatukuuawa; ingawa tunayo huzuni, twafurahi daima; ingawa tu maskini, twatajirisha watu wengi; twaonekana kuwa watu tusio na chochote, kumbe tuna kila kitu. Ndugu Wakorintho, tumezungumza nanyi kwa unyofu; mioyo yetu iko wazi kabisa. Kama mnaona kuna kizuizi chochote kile, kizuizi hicho kiko kwenu nyinyi wenyewe, na si kwa upande wetu. Sasa nasema nanyi kama watoto wangu: Wekeni mioyo yenu wazi kama nasi tulivyofanya.
Mungu wetu Baba yetu,Muumba wetu,Muumba  wa Nchi na Mbingu
Muumba wa vyote vinavyoonekana na visivyoonekana..
Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo..
Muweza wa yote,wewe ni mwanzo na wewe ni mwisho..
Hakuna kama wewe Mungu wetu,Matendo yako ni ya ajabu..
Unatosha Mungu wetu,Unastahili kuwabudiwa,Unastahili sifa..
Uhimidiwe Baba wa Mbinguni,Utukuzwe Jehovah..

Yahweh tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza, tukijishusha na tukijiachilia mikononi mwako Mungu wetu..
Tunaomba utusamehe makosa yetu tuliyoyafanya
kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua.
Jehovah nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe
wale wote waliotukosea..
Mungu wetu tunaomba utuepushe katika majaribu utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote..



Msiambatane na watu wasioamini. Je, wema na uovu vyapatana kweli? Mwanga na giza vyawezaje kukaa pamoja? Kristo anawezaje kupatana na Shetani? Mwaamini ana uhusiano gani na asiyeamini? Hekalu la Mungu lina uhusiano gani na sanamu za uongo? Maana sisi ni hekalu la Mungu aliye hai. Kama Mungu mwenyewe alivyosema: “Nitafanya makao yangu kwao, na kuishi kati yao. Nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.” Kwa hiyo Bwana asema pia: “Ondokeni kati yao, mkajitenge nao; msiguse kitu najisi, nami nitawapokea. Mimi nitakuwa Baba yenu, nanyi mtakuwa wanangu, waume kwa wake, asema Bwana Mwenye Nguvu.”
Baba wa Mbinguni tumaomba ututakase miili yetu na akili zetu
Yahweh utufunike kwa Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo
wa Nazareti,yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona..




Namshukuru Bwana wetu Yesu Kristo aliyenipa nguvu kwa ajili ya kazi yangu. Namshukuru kwa kuniona mimi kuwa ni mwaminifu, akaniteua nimtumikie, ingawa pale awali mimi nilimtukana na kumtesa na kumdhulumu. Lakini Mungu alinionea huruma, kwa sababu sikuwa na imani bado, na hivyo sikujua nilichokuwa ninafanya. Lakini Bwana wetu alinijalia neema yake kwa wingi, akanipa imani na upendo katika kuungana na Kristo Yesu. Usemi huu ni wa kuaminika, na tena unafaa kukubaliwa kabisa: Kristo Yesu alikuja ulimwenguni kuwaokoa wenye dhambi. Nami ni mkosefu zaidi kuliko hao wote, lakini Mungu alinionea huruma, ili Kristo aoneshe uvumilivu wake wote kwangu mimi, kama mfano kwa wale wote ambao baadaye watamwamini na kupokea uhai wa milele. Kwake yeye aliye Mfalme wa milele, asiyekufa, asiyeonekana na aliye Mungu pekee – kwake viwe heshima na utukufu milele na milele! Amina. Mwanangu Timotheo, nakukabidhi amri hii kufuatana na maneno ya unabii yaliyosemwa zamani juu yako. Yatumie maneno hayo yawe silaha yako katika kupigana vita vizuri, na ushike imani yako na dhamiri njema. Watu wengine hawakusikiliza dhamiri zao na hivyo wakaiharibu imani yao. Miongoni mwao ni Humenayo na Aleksanda ambao nimewakabidhi kwa Shetani, ili wafundishwe wasimtukane Mungu.
Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo..
Jehovah nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji..
Tusipungukiwe katika mahita yetu Mungu wetu ukatupe
 sawasawa na mapenzi yako..


Mungu wetu tunayaweka maisha yetu mikononi mwako..
Tunaomba ukabariki Nyumba/Ndoa zetu,watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka..
Mungu wetu tunaomba ulinzi wako,Amani ikatawale,
ukatamalaki na kutuatamia,ukatuguse kwa mkono wako
baraka,Furaha,upendo,utuwema na fadhili ziwe nasi..
Ukatupe neema ya kusimamia Neno lako Amri na Sheria zako
siku zote za maisha yetu..
Ukatufanye chombo chema nasi tukatumike kama 
inavyokupendeza wewe..




Basi, ueni chochote kilicho ndani yenu ambacho ni cha kidunia: Uasherati, uchafu, shauku, tamaa mbaya na uchu (ambao ni sawa na kuabudu sanamu). Kwa sababu ya mambo hayo hasira ya Mungu huwajia wote wanaomwasi. Wakati mmoja nyinyi pia mliishi kufuatana na mambo hayo, mlipotawaliwa nayo. Lakini sasa mnapaswa kuachana na mambo haya yote: Hasira, tamaa na uovu; kufuru au maneno yasiyofaa yasitoke kamwe vinywani mwenu. Msiambiane uongo, kwani nyinyi mmekwisha vua ule utu wa kale pamoja na matendo yake yote, mkavaa utu mpya. Huu unaendelea kurekebishwa na Mungu, Muumba wake, kadiri ya mfano wake, ili mpate kumjua Mungu kwa ukamilifu. Katika hali hii, hakuna tena tofauti kati ya Mgiriki na Myahudi, aliyetahiriwa na asiyetahiriwa, msomi na asiye msomi, mtumwa na mtu aliye huru. Kristo ni kila kitu, na yumo katika yote. Nyinyi ni watu wake Mungu; yeye aliwapenda na kuwateua. Kwa hiyo, basi, vaeni moyo wa huruma, wema, unyenyekevu, upole na uvumilivu. Vumilianeni na kusameheana iwapo mmoja wenu analo jambo lolote dhidi ya mwenzake. Mnapaswa kusameheana kama Bwana alivyowasamehe nyinyi. Zaidi ya hayo yote, zingatieni upendo, kwani upendo huunganisha kila kitu katika umoja ulio kamili. Nayo amani ya Kristo itawale mioyoni mwenu; maana kwa ajili hiyo nyinyi mmeitwa katika mwili huo mmoja. Tena muwe na shukrani! Ujumbe wa Kristo na ukae ndani yenu pamoja na utajiri wake wote. Fundishaneni na kushauriana kwa hekima yote. Imbeni Zaburi, nyimbo na tenzi za kiroho; mwimbieni Mungu mioyoni mwenu kwa shukrani. Na, kila mfanyacho kwa neno au tendo, fanyeni vyote kwa jina la Bwana Yesu na kumshukuru Mungu Baba kwa njia yake.


Roho Mtakatifu akatuongoze na tukapate kutambua/kujitambua
tukanene yaliyo yako Mungu wetu na tukawe na kiasi..


Yahweh tazama wenye shida/tabu,wagonjwa na wenye njaa
wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali,walio katika vifungo vya 
yule mwovu na waliokata tamaa..
Mungu wetu ukawaguse na mkono wako wenye wenye nguvu..
ukawaponye kimwili na kiroho pia,Ukawape neema ya kujua njia zako
waweze kujiombea na kukutafuta wewe Mungu,ukasikie kulia kwao na ukawafute machozi yao,Ukapokee sala/maombi yao na ukawatendee
kama inavyokupendeza wewe..


Dumuni katika sala, na mnaposali muwe waangalifu, mkimshukuru Mungu. Vilevile, mtuombee sisi pia ili Mungu atupe fursa ya kuuhubiri ujumbe wake kuhusu siri ya Kristo. Kwa ajili hiyo mimi niko sasa kifungoni. Basi, ombeni ili niweze kusema kama inavyonipasa na kwa namna itakayodhihirisha siri hiyo. Muwe na hekima katika uhusiano wenu na watu wasioamini, mkitumia vizuri wakati mlio nao. Mazungumzo yenu yanapaswa kuwa daima mema na yaliyokolezwa kwa chumvi na ya kuvutia, na mnapaswa kujua jinsi ya kumjibu vizuri kila mmoja.


Sifa na Utukufu tunakurudishia Mungu Baba..

Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina..!!

Asanteni sana wapendwa/waungwana kwa kuwa nami..
Mungu wetu aendelee kutubariki katika yote yampendezayo
Amani na Upendo ukatawale katika maisha yenu..
Nawapenda.


Agano la Mwenyezi-Mungu na Waisraeli nchini Moabu

1Haya ni maneno ya agano ambalo Mwenyezi-Mungu aliwaamuru Mose kufanya na Waisraeli katika nchi ya Moabu, licha ya agano Mwenyezi-Mungu alilofanya nao mlimani Horebu. 2Mose aliwaita pamoja Waisraeli wote akawaambia, “Mliona nyinyi wenyewe jinsi Mwenyezi-Mungu alivyomtendea mfalme wa Misri, maofisa, watumishi wake na nchi yake yote. 3Mliona maafa makubwa, ishara na maajabu aliyotenda. 4Lakini mpaka leo Mwenyezi-Mungu hajawapa akili ya kuelewa, macho ya kuona, wala masikio ya kusikia!
5“Kwa muda wa miaka arubaini, mimi niliwaongoza jangwani, nguo zenu mlizovaa hazikuchakaa wala viatu vyenu havikuchakaa miguuni mwenu. 6Hamkula mkate wala kunywa divai au kileo chochote kile, mpate kujua kwamba Mwenyezi-Mungu ni Mungu wenu.
7“Na mlipofika mahali hapa, mfalme Sihoni wa Heshboni na mfalme Ogu wa Bashani walikuja kupigana nasi; lakini tukawashinda, 8tukaichukua nchi yao, tukayagawia makabila ya Reubeni na Gadi na nusu kabila la Manase iwe mali yao. 9Kwa hiyo muwe waangalifu kushika maneno yote ya agano hili ili mpate kufanikiwa katika kazi zenu zote.
10“Leo, mmesimama mbele ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, nyinyi nyote viongozi wa makabila, wazee wenu, maofisa wenu, 11watoto wenu na wake zenu, wageni wanaoishi miongoni mwenu ambao hukata kuni na kuwatekea maji. 12Mko hapa leo ili kufanya agano hili ambalo Bwana Mungu wenu anafanya leo, 13kwamba atawathibitisha leo kuwa watu wake naye atakuwa Mungu wenu, kama alivyowaapia nyinyi na babu zenu: Abrahamu, Isaka na Yakobo. 14Wala sifanyi agano hili leo kwa niaba yenu tu na kutamka laana zake; sifanyi kwa niaba ya wale tu walio pamoja nasi leo mbele ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, 15bali pia kwa niaba ya wale ambao hawapo pamoja nasi leo.
16“Mnajua jinsi tulivyoishi nchini Misri na jinsi tulivyosafiri katika nchi za mataifa mengine. 17Mliona sanamu zao za kuchukiza, miungu ya miti na mawe, ya fedha na dhahabu. 18Chukueni hadhari kwamba hakuna mwanamume, mwanamke, jamaa au kabila lolote linalosimama hapa leo litakalomwacha Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, kwenda kutumikia miungu ya mataifa mengine. Jambo hili litakuwa kama mzizi utakaomea na kuzaa matunda machungu yenye sumu. 19Kama baada ya kusikia maneno ya agano hili ambayo mmeapishwa, halafu mtu akajiamini mwenyewe moyoni mwake na kusema atakuwa salama, hata kama atafuata ukaidi wake mwenyewe, hiyo itawaangamiza wote, wabaya na wema. 20Mwenyezi-Mungu hatasamehe mtu huyo, nayo hasira ya Mwenyezi-Mungu na wivu wake vitamwakia mtu huyo; laana zote zilizoandikwa katika kitabu hiki zitamjia, naye Mwenyezi-Mungu atalifuta kabisa jina la mtu huyo kutoka duniani. 21Mwenyezi-Mungu atamtenga kutoka miongoni mwa makabila yote ya Israeli apatwe na maafa kufuatana na laana zote za agano zilizoandikwa katika kitabu hiki. 22Katika vizazi vijavyo, wazawa wenu na wageni kutoka nchi ya mbali wataona jinsi Mwenyezi-Mungu alivyoiletea nchi hii maafa na mateso: 23Imejaa madini ya kiberiti na chumvi, imeteketea na kuwa tupu, haikupandwa mbegu na haioti chochote. Ni kama ilivyokuwa wakati Mwenyezi-Mungu alipoangamiza Sodoma na Gomora, Adma na Seboimu, kwa hasira yake kali. 24Naam, mataifa yote yatasema: ‘Kwa nini Mwenyezi-Mungu ameitendea hivyo nchi hii? Hasira hii kubwa inamaanisha nini?’ 25Na jibu litatolewa: ‘Ni kwa sababu walivunja agano la Mwenyezi-Mungu, Mungu wa wazee wao ambalo alifanya nao alipowatoa katika nchi ya Misri, 26wakaenda kuitumikia na kuiabudu miungu mingine, ambayo hawakuijua hapo awali, wala Mwenyezi-Mungu hakuwa amewapa. 27Kwa hiyo hasira ya Mwenyezi-Mungu iliwaka dhidi ya nchi hii, na kuiletea laana zote zilizoandikwa katika kitabu hiki. 28Naye Mwenyezi-Mungu, akawangoa kutoka katika nchi yao kwa hasira na ghadhabu kubwa, akawatupa katika nchi nyingine kama ilivyo leo.’
29“Mambo ya siri ni ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, lakini yale ambayo ameyafunua ni yetu na wazawa wetu milele, ili tutekeleze maneno yote ya sheria hii.”



Kumbukumbu la Sheria 29:1-29


Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.